Habari za Punde

WAKAZI WA KILAMBO MKOANI MTWARA WAOMBA KIWANDA CHA KUSINDIKA MAZAO YA KILIMO

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (wa pili kushoto), akitoka kukagua Kituo cha Forodha na Ushuru cha Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA katika Mpaka wa Tanzania na Msumbiji (Kilambo), alipofanya ziara na kuzungumza na wafanyakazi wa Kituo hicho, mkoani Mtwara.

Na Benny Mwaipaja, WFM, Mtwara
WAKAZI wa Kijiji cha Kilambo, Wilaya ya Mtwara, mkoani 
Mtwara, wameiomba Serikali iwasaidie kuwatafutia 
mwekezaji atakayejenga kiwanda cha kusindika matunda na 
mazao ya kilimo katika kijiji chao kutokana na kijiji hicho 
kuwa na matunda na mazao mbalimbali yanayokosa soko na 
kuwasababishia umasikini.
Wakazi hao wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha 
Kilambo Bw. Mohamed Mkama, wametoa ombi hilo mbele 
yaWaziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, 
aliyefanya ziara ya kikazi katika Kituo cha Forodha cha 
Kilambo, kilichoko mpakani mwa Tanzania na Msumbiji, 
mkoani Mtwara,  kwamba kijiji chao kina fursa nyingi za 
kilimo zinazohitaji viwanda vya kuongeza thamani ya mazao 
yao na kutoa ajira kwa vijana.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kilambo Bw. Mohamed Mkama, 
alisema kuwa Kijiji chao kinapakana na nchi ya Msumbiji 
ambako kuna mwingiliano mkubwa wa watu katika masuala 
ya biashara na uhusiano wa kijamii ikiwemo pande mbili za 
nchi kuoleana hivyo kuwafanya wananchi wa Msumbiji 
waishio mpakani kutegemea bidhaa kwa wingi kutoka katika 
kijiji chao.

"Watu kutoka Msumbiji wananunua sana chakula na bidhaa 
nyingine kutoka kwetu lakini tunawauzia bidhaa bila 
kuongeza thamani hivyo uwepo wa kiwanda utakuza uchumi 
wa kijiji chetu na tunakuomba Mhe. Waziri wa Fedha na 
Mipango, utusaidie kupata kiwanda ili nasi tuweze 
kunufaika" alisisitiza Mwenyekiti huyo wa Kijiji

Mkazi mwingine wa Kijiji hicho  Bw. Selemani Kumamba, 
alimweleza Waziri wa Fedha na Mipango kwamba Kijiji chao 
ni maarufu kwa kilimo cha matunda hivyo wanapendekeza 
kujengwa kwa kiwanda cha kusindika matunda ili juisi 
itakayozalishwa katika kijiji chao iwe na soko.

"Mhe. Waziri sisi ni wakulima wazuri wa matunda lakini 
matunda yetu wakati wa msimu yanakosa soka, yanaoza  na 
tunayatupa jambo linalotulazimu tukuombe utusaidie 
kuhamasisha wawezezaji waje wajenge kiwanda cha 
kusindika juisi katika kijiji chetu ili nasi tuondokane na 
umasikini" alisema mzee Selemani Kumamba

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, 
aliwaambia wakazi hao kwamba inabidi ufanyike utafiti wa 
kutosha ili kubaini wingi wa mazao yanayozalishwa na 
wakulima katika kijiji hicho na vijiji jirani ili kupata takwimu 
sahihi za uzalishaji wa mazao hayo yakiwemo matunda ili 
kuiwezesha Serikali kuwashawishi wawekezaji kujenga 
kiwanda katika eneo hilo na kuwapongeza wakulima hao 
kwakufanya kazi kwa bidii na mawazo yao ya kujiletea 
maendeleo.

"Tukiwa na uhakika huo hata mwekezaji anayekuja 
tutamwambia kwa mwaka mmoja, kwa wastani, kijiji hiki na 
vijiji jirani vinazalisha maenbe kiasi fulani, kwa hiyo wazo la 
kutaka kuwa ni kiwanda ni  zuri lakini linahitaji kufanyiwa 
kazi zaidi" alisema Dkt. Mpango aliyeambatana na Mkuu wa 
Wilaya ya Mtwara, Bw. Evod Mmanda

Aliwasahauri wanakijiji hao kuanzisha mashamba mapya ya 
matunda na kupanda mbegu za kisasa zinazozaa kwa wingi 
na kuushauri uongozi wa wilaya kuwasaidia wananchi hao 
kupata miche ya kisasa inayozaa kwa muda mfupi ili waweze 
kushawishi zaidi kupatikana kwa kiwanda kijijini hapo.

Dokta Philip Mpango, yuko mkoani Mtwara kwa ziara ya 
kikazi ambapo pamoja na mambo mengine amekutana na 
wafanyabiashara wa mkoa wa Kigoma pamoja na 
Kutembelea taasisi zilizochini ya Wizara hiyo. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.