Habari za Punde

Mashindano ya Fainali ya Vilabu Vya Kodi Yafana.

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Charles Kichere akiwakabidhi zawadi wanafunzi wa St. Joseph wakati wa fainali za mashindano ya vilabu vya kodi kwa Shule za Sekondari za Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zilizofanyika katika Chuo cha Usimamizi wa Kodi (ITA) Jijini Dar es Salaam.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Charles Kichere akimkabidhi zawadi mwanafunzi mwenye umri wa mika 12 wa Shule ya Sekondari Mbezi Inn, Charles Denis wakati wa fainali za mashindano ya vilabu vya kodi kwa Shule za Sekondari za Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zilizofanyika katika Chuo cha Usimamizi wa Kodi (ITA) Jijini Dar es Salaam.
 Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Charles Kichere akimkabidhi zawadi mwanafunzi bora wa mwaka 2018 Runi David kutoka Shule ya Sekondari Tumbi wakati wa fainali za mashindano ya vilabu vya kodi kwa Shule za Sekondari za Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zilizofanyika katika Chuo cha Usimamizi wa Kodi (ITA) Jijini Dar es Salaam.

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Charles Kichere akimvisha mmoja wa wanafunzi ambaye shule yake iliibuka mshindi wakati wa fainali za mashindano ya vilabu vya kodi kwa Shule za Sekondari za Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zilizofanyika katika Chuo cha Usimamizi wa Kodi (ITA) Jijini Dar es Salaam.
 (Picha na TRA)


Na. Veronica Kazimoto. Dar es Salaam.21 Oktoba, 2018
Fainali za mashindano ya vilabu vya kodi zilizoandaliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zimefanyika kwa mafanikio makubwa ambapo zawadi mbalimbali zimetolewa kwa Shule za Sekondari zilizoibuka na ushindi na baadhi ya wanafunzi waliofanya vizuri katika mashindano hayo.
Fainali hizo zilizofunguliwa na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) zilifanyika jana katika Chuo cha Usimamizi wa Kodi (ITA) kilichopo Mikocheni jijini Dar es Salaam.
Katika mashindano hayo, Shule ya Sekondari St. Joseph iliibuka mshindi wa kwanza kati ya shule 28 za Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani na kuzawadiwa runinga, kompyuta ya mezani, printa, saa ya ukutani, medali, ngao, na cheti.

Shule ya Sekondari Tumbi imeshika nafasi ya pili ambayo ilijinyakulia kompyuta ya mezani, printa, saa ya ukutani, medali, ngao, na cheti ikifuatiwa na Shule ya Sekondari Dar es Salaam ambayo ilipata  ngao, kompyuta ya mezani, saa ya ukutani na cheti.

Kwa upande wa uwasilishaji mada zinazohusu masuala ya kodi, Shule ya Sekondari Zanaki iliongoza na kuzawadiwa kompyuta ya mezani, printa, saa ya ukutani, medali na cheti ikifuatiwa na Kerege ambayo ilijibebea printa, saa ya ukutani na cheti huku Shule ya Sekondari Misitu ikishika nafasi ya tatu na kuondoka na kompyuta ya mezani, ngao, na cheti.

Kwenye kipengele cha Ukusanyaji wa Risiti za Kielektroniki za EFD, walioibuka washindi ni Shule ya Sekondari Gerezani ambayo ilizawadiwa runinga, fedha taslimu shilingi 1,000,000, cheti na medali. Mshindi wa pili ni St. Joseph iliyojitwalia ngao, cheti na fedha taslimu shilingi 750,000 ikifuatiwa na Shule ya Sekondari Benjamini iliyopata ngao, cheti na fedha taslimu shilingi 500,000.

Aidha, Mwanafunzi Bora wa Mwaka huu katika fainali hizo, alikuwa ni Runi David kutoka Shule ya Sekondari Tumbi ambaye alijinyakulia laptop, ngao, medali na cheti.

Kilichofurahisha zaidi katika mashindano hayo ni ushiriki wa mwanafunzi mdogo kuliko wote mwenye umri wa miaka 12 Charles Denis kutoka Shule ya Sekondari Mbezi Inn ambaye alizawadiwa laptop, medali na kikombe cha chai kama motisha kwa wanafunzi wengine wenye umri kama wake kushiriki mashindano ya vilabu vya kodi.

Kwa upande wa jambo ambalo halikuwa la furaha lakini baadaye likageuka kuwa la shangwe ni pale mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Zawadi,  Mariam Hussein aliyebubujikwa na machozi wakati akisimulia kukatazwa kushiriki mashindano hayo na mama yake mzazi, suala lililopelekea Mamlaka ya Mapato Tanzania kuahidi kumlipia gharama zote za kidato cha nne ikiwemo ada, jambo lililoibua furaha isiyo ya kifani kwa washiriki wa fainali hizo.

Fainali hizo zilizoshuhudiwa na Kamishna Mkuu wa TRA Charles Kichere ambaye ndiye aliyekabidhi zawadi mbalimbali kwa washindi, zilifungwa na Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi Richard Kayombo kwa kuwashukuru walimu, wanafunzi, majaji na kamati ya maandalizi kwa kufanikisha mashindano hayo.

"Napenda kuchukua fursa hii kumshukuru kila mtu aliyefanikisha mashindano haya wakiwemo wanafunzi, walimu, majaji na kamati nzima ya maandalizi ambayo imejituma kufanya kazi mpaka usiku ili kuhakikisha kuwa fainali hizi zinafanikiwa," alisema Kayombo.

Vilabu vya Kodi vilianzishwa na TRA mwaka 2008 na mpaka sasa kuna jumla ya vilabu 226 Tanzania Bara vikiwa na jumla ya wanafunzi 27,250 ambao ni wanachama hai wa vilabu hivyo.
Mashindano ya mwaka huu ni ya 11 kufanyika ambapo jumla ya shule 50 kutoka Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani zilishindanishwa na hatimaye shule 28 kati ya hizo zikafaulu kuingia kwenye fainali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.