Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya
Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Balozi Joseph Sokoine akiwa katika picha
ya pamoja na wadau wa mazingira walioshiriki kikao kazi cha siku moja cha kujadili
fursa zilizopo katika uzalishaji wa mifuko mbadala wa plastiki Jijini Mwanza,
washiriki wakiwa ni wamiliki wa viwanda vinavyozalisha bidhaa za karatasi na
plastiki, wawakilishi wa sekta binafsi, baadhi ya Wizara na Taasisi za
Serikali.
Bw. Mangabe Mnilago Afisa
Mazingira kutoka Mkoa wa
Mwanza akaichangia jambo katika kikao cha kujadili na kuhimiza wadau kuwekeza
katika uzalishaji wa mifuko mbadala wa plastiki
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya
Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Balozi Joseph Sokoine (wa pili kulia)
akimsikiliza mmoja wa wadau wa mazingira ambae amebadili changamoto kuwa fursa
kwa kuzalisha mifuko mbadala rafiki wa mazingira. Wa pili kutoka kushoto ni
Prof. William Mwegoha Mkurugenzi wa mazingira na Bi. Magdalena Mtenga Mkurugenzi Msaidizi
Ofisi ya Makamu wa Rais.
Na.lulu mussa
Imebainika kuwa Mto
Nile, ambao chanzo chake ni Ziwa Victoria, ni mto wa tano miongoni mwa mito
kumi duniani iliyoorodheshwa kwa kusafirisha kiwango kikubwa cha taka za
plastiki kwenda baharini kutoa nchi kavu ikiwa ni takriban tani 85,000 kwa
mwaka kwa mujibu wa tafiti za Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira.
Akifungua kikao
cha siku moja cha wadau kujadili fursa zilizopo katika uzalishaji wa mifuko mbadala
wa plastiki Jijini Mwanza, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano
na Mazingira Balozi Joseph Sokoine amesema kuwa Takwimu zinaonesha kuwa
takriban nusu ya taka za plastiki zinazozalishwa zinajumuisha vifungashio na
mifuko ya plastiki.
Balozi Sokoine
amesema kuwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira linakadiria kuwa hali ya
sasa ya uzalishaji na matumizi ya mifuko na vifungashio vya plastiki
ikiendelea, ifikapo mwaka 2050 takataka za plastiki zitakuwa nyingi kuliko
samaki baharini, na kusisitiza kuwa changamoto za taka za plastiki si suala la
afya ya jamii na hifadhi ya mazingira tu bali linagusa uchumi na mustakabali wa
maisha yetu ya sasa na ya vizazi vijavyo.
“Uchafuzi wa
taka za plastiki baharini ni changamoto ya Dunia inayohitaji hatua za haraka.
Hivyo, ni muhimu kama Taifa tukashirikiana na Jumuiya ya Kimataifa kwa kuchukua
hatua madhubuti ili kuinusuru Dunia dhidi ya janga hili” Balozi Sokoine
alisisitiza.
Kwa upande
mwingine Afisa Mazingira kutoka Mkoa wa Mwanza Bw. Mangabe Mnilago amesema ni
vema jamii ikafahamu kuwa uzalishaji wa mifuko mbadala wa plastiki ni fursa kwa
wananchi na kuwasihi kuwekeza katika sekta hiyo.
Serikali kwa
muda sasa imekuwa ikifanyia kazi suala la kuzuia uzalishaji na matumizi ya
mifuko ya plastiki ya kubebea bidhaa nchini. Dhamira ambayo inafanyiwa kazi na kikao
cha leo ni moja ya hatua za kimkakati katika kufikia azma hiyo.
Kikao cha leo
kimelenga kupata mwelekeo wa hatua muafaka ili kudhibiti uchafuzi wa mazingira
unaochangiwa na mifuko ya plastiki ikiwa ni moja ya hatua za kuhamasisha
uzalishaji na matumizi ya mifuko mbadala iliyo rafiki kwa mazingira
inayotengenezwa kwa karatasi, vitambaa vya nguo na hata vikapu vya asili na kimejumuisha
wamiliki wa viwanda vinavyozalisha bidhaa za karatasi na plastiki, wawakilishi
wa sekta binafsi, baadhi ya Wizara na Taasisi za Serikali na kimefanyika Katika
Ukumbi wa Chuo cha Benki Kuu Mwanza.
No comments:
Post a Comment