Tume ya Taifa
ya Uchaguzi imewasihi wapiga kura wote waliojiandikisha kwenye Daftari la
Kudumu la Wapiga Kura na wanaoishi kwenye kata Sita za Tanzania Bara,
kujitokeza kwa wingi kupiga kura siku ya Jumapili Desemba 2 mwaka huu ili kuwachagua viongozi wanaowataka
wawaongoze kwa kipindi cha takribani miaka miwili ijayo.
Wito huo
umetolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Semistocles Kaijage
wakati akisoma risala ya uchaguzi mdogo wa Udiwani unaohusisha kata za Miteja,
Kivinje au Sigino , Somanga na Mitole katika Halmashauri ya Kilwa, kata ya Muhinda katika Halmashauri ya Wilaya ya
Buhigwe na Kata ya Nkoanekoli katika
Halmashauri ya wilaya ya Meru.
“Wapiga
Kura wapatao 31,818 wanatarajiwa kupiga Kura kuwachagua Madiwani katika Kata 6
za Tanzania Bara na uchaguzi huo utafanyika katika Vituo 91 vya Kupigia Kura
ambako ndipo Wapiga kura walijiandikishia kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa
Rais,Wabunge na Madiwani wa Mwaka 2015.
Aliwataka
kwenda kupiga kura bila hofu, woga, wasiwasi au ushawishi kwani chini ya Kanuni
ya 3.1 (b) ya Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2015,
Serikali imepewa wajibu wa kuhakikisha kuwa kuna hali ya usalama, amani na
utulivu katika kipindi chote cha Uchaguzi.
Mbali na wito
huo, Jaji Kaijage aliwataka wananchi, vyama vya Siasa na wadau wote wa uchaguzi
kushirikiana ili kuhakikisha kuwa viashiria vya kuvunjika kwa amani na utulivu
vinaepukwa ili uchaguzi utakaofanyika uwe huru, wazi na wa haki.
Jaji Kaijage
alivisisitiza vyama vya siasa kufanya mikutano ya kampeni inatakiwa kufikia mwisho
leo Jumamosi saa kumi na mbili kamili
(12:00) jioni na baada ya muda huo, vyama, wagombea na mashabiki waache kufanya
kampeni za aina yoyote, kama vile kutumia alama za vyama zinazoashiria kampeni,
vipeperushi, bendera, mavazi na vitu vingine visivyokubalika katika siku ya
Uchaguzi.
“Aidha,
wananchi waheshimu Sheria za Nchi wakati wote wa upigaji, kuhesabu, kujumlisha
kura na kutangaza matokeo. Pale panapokuwa na malalamiko yoyote ya ukiukwaji wa
Sheria na Taratibu za Uchaguzi, malalamiko hayo yafikishwe kwenye mamlaka
inayohusika kwa utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa Sheria.”, alisema Jaji
Kaijage na kuongeza kuwa:
“Vivyo hivyo,
Viongozi wa Vyama vya Siasa, Wagombea au wafuasi wao na wananchi kwa ujumla
wajiepushe na vitendo vinavyoweza kusababisha fujo au vurugu katika vituo vya
Kupigia, Kuhesabia na Kujumlishia Kura.”
Jaji Kaijage
aliwataka wapiga kura kuondoka kwenye maeneo ya kituo cha kupigia kura mara
baada ya kupiga kura na kujiepusha na mikusanyiko au mikutano katika maeneo ya
vituo vya kupigia kura kwani vyama vya siasa vimeweka mawakala vituoni ambao
watalinda maslahi ya vyama husika na wagombea wao.
Mwenyekiti
huyo wa NEC, alivikumbusha vyama vya siasa, wagombea, wananchi na watendaji wa
uchaguzi kwa ujumla kuzingatia na kuheshimu matakwa na masharti ya Sheria za
Uchaguzi, Sheria za Nchi, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi wakati wa Upigaji Kura,
Kuhesabu, Kujumlisha Kura, na Kutangaza matokeo.
Alisema
upigaji kura utafanyika kuanzia saa moja kamili asubuhi na kumalizika saa kumi
kamili jioni katika vituo vilivyotumika wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015
na kwamba watakaokuwepo kwenye mstari kwenye vituo vya kupigia kura kuanzia saa
kumi kamili jioni wataruhusiwa kupiga kura.
Hata hivyo,
alibainisha kuwa watakaoruhusiwa kupiga kura ni wale tu waliomo kwenye Daftari
la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Kata husika na wana kadi ya mpiga kura na wale
waliopoteza kadi zao za kupigia kura au zimeharibika au zimechakaa wataruhusiwa
kupiga kura kutumia Pasi ya Kusafiria, Leseni ya Udereva au Kitambulisho cha
Uraia kinachotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kwa sharti kuwa
majina yaliyomo kwenye vitambulisho hivyo yafanane na yale yaliyomo kwenye
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
“Ni wajibu wa
vyama vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi kuweka mawakala katika vituo
vyote vya Kupigia na Kujumlishia Kura kwa utaratibu ambao tulikubaliana na
umekuwa ukitumika katika chaguzi za hivi karibuni wakati wa Mkutano wa Tume na
Vyama vya Siasa tarehe 10/07/2018 uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa
Mikutano wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam, na maelekezo kuhusiana na utaratibu
huo kutumwa kwa Wasimamizi wa Uchaguzi.”, alikumbusha Jaji Kaijage.
Hata hivyo,
alisema mawakala hao wanaruhusiwa kuwepo katika Vituo vya Kupigia Kura na
wanatakiwa kufuata na kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu zinazoongoza
Uchaguzi katika kipindi chote cha kupiga, kuhesabu, kujumlisha kura na
kutangaza matokeo.
MWISHO.
No comments:
Post a Comment