Habari za Punde

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Balozi Seif Ali Iddi Afungua Ijitimai ya Kimataifa Kidoti Zanzibar leo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akilakiwa na Viongozi wa Dini ya Kiislamu alipowasili Kidoti kwa ajili ya kuifungua Ijitimai ya Kimataifa kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al – Hajj Dr. Ali Mohamed Shein.

Balozi Seif akiifungua Ijitimai ya Kimataifa kwa niaba ya Rais wa Zanzibar hapo katika Msikiti Mkuu wa eneo la ijitimai hiyo Kidoti Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Fiysabilillah Tablih Markaz Amir Ali Khamis Mwinyi akitoa Taarifa ya Ijitimai katika hafla ya ufunguzi wake uliofanywa na Balozi Seif kwa niaba ya Rais wa Zanzibar.
Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Qabi akijiandaa kumkaribisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kuifungua Ijitimai ya Kimataifa hapo Kidoti.
Na.Othman Khamis OMPR.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al – Hajj Ali Mohamed Shein alisema katika kuimarisha mapenzi baina ya Waumini wa Dini ya Kiislamu na kuleta Ustawi wa jamii ni vyema zikatumika fursa za mikusanyiko ya kupeana nasaha juu ya athari ya mambo yanayoweza kuiharibu jamii.
Alisema migogoro na mivutano inayojichomoza miongoni mwa Waumini akitolea mfano baadhi ya Misikiti haitoi taswira nzuri na hatma yake amani hutoweka ambayo ni muhimu kwa ustawi wa Jamii na kupelekea  kuwakosesha Waumini kufanya Ibada kwa utulivu.
Al – Hajj Dr. Ali Mohamed Shein alitoa katuli hiyo katika Hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akiifungua Rasmi Ijitimai  ya Kimataifa inayofanyika katika Kijiji cha Kidoti Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Alisema kuhitilafiana mitazamo ni jambo ambalo lilikuwepo tokea zama za Kiongozi wa Waumini wa Dini ya Kiislamu Mtume Muhammad {SAW}, lakini Waumini wenyewe walikuwa wakikaa pamoja {Shura} katika kutafuta muwafaka wa hitilafu inayojitokeza na baadae waliendelea na Ibada zao kama kawaida.
Rais wa Zanzibar alisema Ijitimai ni miongoni mwa Vielelezo vinavyoonyesha mshikamano na Umoja wa Waumini wa Kiislamu ambao Mola Mtukufu huongeza Baraka na kuleta neema zake kwa Waja hao walioamua kushikamana katika kufanya mambo ya kheir.
Alieleza kwamba utaratibu wa kupeana mawaidha lazima uendelee kwa namna mbali mbali kupitia Ijitimai kama hizi na hata Misikiti  kwa vile maisha ya Wanaadamu wakiwemo Waumini yanakabiliwa na changamoto mbali mbali ambazo zinaweza kupelekea Watu kutoka kwenye njia sahihi ya Mwenyezi Mungu.
“ Utaratibu huu wa Waumini kupeana mawadisha ni ishara ya kauli ya Mwenyezi Mungu katika Maandiko yake matukufu alipousifia Umma wa Nabii Muhammad {SAW} kwamba ni umma bora kutokana na kujamrishana mema na kukatazama yaliyo maovu na kumuamini Mwenyezi Mungu”. Al – Hajj  Dr. Shein alikuwa akiikariri aya ya 110 ya Suratul Al – Imran.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliwanasihi Waislamu kutoitumia vibaya kinyume na makusudio  neema waliyoipata ya mkusanyiko wao unaosaidia kuimarisha imani zao kupitia mihadhara inayotolewa na Masheikh na Walimu mbali mbali.
Akizungumzia vitendo viovu vya udhalilishaji vilavyolitia aibu Taifa,  Al – Hajj Dr. Ali Mohamed Shein alitahadharisha wazi kwamba Ustawi wa Jamii hauwezi kupatikana iwapo Akina Mama na Watoto wanaishi kwa hofu kutokana na kufanyiwa vitendo hivyo.
Alisema Jamii imekumbwa na Mtihani mkubwa wa kuibuka kila kukicha kwa kesi zinazotokana na vitendo vya udhalilishaji vinavyoleta maudhi vikitendeka kinyume na Mafundisho ya Dini yenyewe ambapo vile vile ni kinyume na Haki za Binaadamu.
“ Mwenyezi Mungu ametuonya kuacha kufanyiana vitendo vya maudhi miongoni mwetu kwa kutuambia – na wale wanaowaudhi wanaume Waislamu na Wanawake Waislamu pasipo na kufanya kosa lolote, bila shaka wamebeba dhulma kubwa na dhambi zilizo dhahiri”. Dr. Shein alikariri Quran Tukjufu aya ya 58 ya Suratul Ahzab.
Rais wa Zanzibar aliwanasihi Waumini na Wananchi wote kuungana pamoja na Serikali katika mapambano dhidi ya vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa Wanawake na Watoto bila ya kuwaonea muhali wale watakaobainika kuhusika na vitendo hivyo viovu.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi sasa inatekeleza  Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji na kumuomba kila Mwana Jamii atimize wajibu wake katika mapambano hayo ili kupatikana Ustawi bora wa Jamii nzima.
Al – Hajj Dr. Ali Mohamed Shein aliishukuru na kuipongeza Jumuiya ya Fiysabilillahi Tablih Markaz kwa mafanikio yake katika kutekeleza malengo ya kuanzishwa kwa Taasisi hiyo tokea iliposajiliwa rasmi Mnamo Mwaka 1999.
Alisema mafanikio mengi yamepatikana yakiwemo kumudu kuendeleza mikusanyiko ya Ijitihai kila Mwaka, kuanzishwa Ujenzi wa Majengo ya Skuli mbali mbali pamoja na Ujenzi wa Msikiti uliopo Kidoti ambao tayari umeshafikia hatua kubwa.
Hata hivyo aliunasihi Uongozi huo kwamba changamoto zinazojichomoza zisiwakatishe tamaa bali ziwe chachu ya kuungana na kubuni mikakati ya kupata nyenzo ya kufikia malengo ya Miradi waliyojipangia.
“ Nina matumaini makubwa  kwa Uongozi wa Taasisi hii mna uwezo wa kutuvusha kutoka hapa tulipo, ili kwenda mbele zaidi, iwapo  mtaendelea kutuhamasisha tuchangie mambo haya ya kheir”. Alisema  Al – Hajj Dr. Ali Mohamed Shein.
Alisisitiza kwamba mafanikio huenda pole pole ingawa huhitaji uhamasishaji, kuhimizana na kuendelea kuelimashana juu ya umuhimu wa kuchangia katika masuala hayo yakiwa miongoni mwa Sadakatul Jaariya.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alielezea matumaini yake kwamba Waumini watakaopata chakula cha roho katika kipindi hicho cha Siku Tatu kwenye mjumuiko huo wataondoka na hazina kubwa ya maarifa , imani na ucha Mungu kwa kuanza maisha mapya yanayoendana na mafundisho watakayoyapata.
“ Tuondoke hapa tukiwa Mabalozi wema na wale wanaotoka nje ya Zanzibar warudi wakitusifu kwa sifa njema, ukarimu na hali ya amani wanayoishuhudia wakati wote wanapokuwa Nchini”. Alisema Dr. Shein.
Alifahamisha kwamba haitakuwa vyema kwamba wanaijitihmai hao waondoke katika mkusanyiko huo wa kheir wakiwa kama walivyokwenda, na yale mazuri waliyojifunza kuyaacha huko kidoti.
Akitoa Taarifa ya Ijitimai hiyo Mwenyekiti wa Jumuiya ya Fiysabililah Tablih Markaz Amir Ali Khamis Mwinyi alisema hiyo ni Ijitimai ya 23 tokea kuanzishwa kwake ambao kwa Kidoi imefikia ya Tatu.
Amir Ali alisema Mada Nne zitakazowasilishwa na Wataalamu mahiri zimepangwa katika Ijitimai hiyo akizitaja kuwa ni pamoja na Umuhimu wa Umoja, Amani, Maendeleo pamoja na Familia inayojitambua.
Alisema lengo la kuanzishwa kwa Ijitimai hiyo ni muendelezo wa utekelezaji wa amri ya Mwenyezi Muungu ya kuandaliwa kwa mikusanyiko ya kuamrishana mema na kukatazana mabaya.
Amir Ali alifahamisha kwamba kazi hiyo ya Allah inakwenda sambamba na Jumuiya hiyo kuendelea kuwalea Watoto wanaoishi katika mazingira magumu ambao kwa sasa wamefikia 1011 ambapo Kijiji cha kidoti pekee kina Watoto 56.
Alifahamisha kwamba katika kufikia malengo hayo Jumuiya hiyo imekusudia kuendelea na Miundombinu ya kukamilisha majengo yake yaliyopo katika eneo hilo la Majengo liliopo Kidoti.
Alieleza kuwa hatua zinachukuliwa katika kuyakamilisha Majengo Saba kwa ajili ya Waumini wa Kike, Jengo la Ghorofa kwa ajili ya Wageni pamoja na kukamilisha Msikiti Mkuu unaotarajiwa kuchukuwa Waumini Elfu 5,5000 kwa sala moja.
Akitoa salamu ya Mufti Mkuu wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir Mwakilishi wake Sheikh Jongo amesisitiza suala la kuimarishwa Amani mingoni mwa Waumini na Wenanchi wote.
Sheikh Ahmed Jongo alisema kitendo cha kudumisha amani ndio silaha pekee itakayowasaidia Waumini kuendelea kufanya Ibada zao kwa uhakika na utulivu zaidi.
Akimkaribisha mgeni rasmi kuwawaaidhi waumini waliohudhuria Ijitimai hiyo Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Oman Kabi alisema suala la kumuabudu Mwenyezi Mungu ni kitu cha msingi katika maisha ya kila Siku ya Muumini aliyeshiba Taqwa.
Alisema Malaika uwa Mwenhyezi muungu mara zote hutanda kila pembe ya Dunia kufuatilia ibada zinazotekelezwa na Waja walioamini kumsujudia Mwenyekiti Muungu Mmoja asiya na mshirika.
Zaidi ya Waumini Elfu Tano  Wake na Waume kutoka Nchi za Zambia, Uganda, Kenya, Rwanda, Malawi, Mikoa ya Tanzania Bara na Wenyeji Mikoa Kumi ya Visiwa vya Unguja na Pemba wamehuduria Ijitimai hiyo ya 23.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.