Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Ahutubia Wananchi Kisiwani Pemba Siku ya Sheria Zanzibar.Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar, zilizofanyika Kitaifa Kisiwani Pemba Wilaya ya Wete Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Pemba. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa umadhubuti wa nchi pamoja na utajiri wake unategemea kwa kiasi kikubwa jinsi gani nchi hiyo imejidhatiti katika kuendeleza na kudumisha utawala wa sheria (Utawala Bora).

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar yaliyofanyika huko katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi, Wete Pemba, Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa maadhimisho ya siku ya Sheria yana umuhimu mkubwa katika kutoa mwamko kwa wananchi katika kuzifahamu na kuzitii sheria za nchi zikiwa ndio msingi mkubwa wa kukuza utulivu, amani na maendeleo.
Aliongeza kuwa suala la kuzifahamu na kuzitii sheria hupelekea kuishi kwa nidhamu na misingi ya kuheshimiana katika maisha ya kila siku kwani sheria lazima zitambuliwe ili wananchi waweze kupambanua haki na wajibu.
Alisema kuwa ikiwa jamii itaishi bila ya kuzifata sheria basi utakosekana ustaarabu katika utekelezaji wa mambo kwani sheria ni suala nyeti linalogusa maisha katika nyanja mbali mbali.
Dk. Shein alisema kuwa kwa msingi huo Mamlaka tatu zilizopo katika mfumo wa mgawanyo wa madaraka yaani mamlaka ya Utendaji ambayo ni Serikali, Mamlaka ya Kutunga Sheria yaani Baraza la Wawakilishi pamoja na Mahkama ni lazima zihakikishe zinashikamana bila ya kuathiri uhuru wa sehemu moja.
Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein pia aliwahimiza wananchi wote kuendelea kutii sheria za nchi kama Katiba inavyoelekeza huku akiwahiziwa viongozi wa dini zote zinazofuatwa na wananchi wa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla kuendelea kuhubiri utii wa sheria za nchi.
Alieleza kufurahishwa na Kaulimbiu ya mwaka huu isemayo “ Uimarishaji wa Taasisi za Umma ni Ustawi Bora wa Upatikanaji wa Haki kwa Jamii” alisisitiza kuwa Kauli mbiu hiyo inakwenda sambamba na jitihada zinazofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha taasisi za umma kwa maendeleo ya jamii.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali katika vipindi mbali mbali na awamu zote saba tafauti imefanya jitihada kubwa kuimarisha taasisi za umma ili kuhakikisha kuwa ustawi wa upatikanaji wa haki kwa jamii unakuwa siku hadi siku.
Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba  imefanya jitihada kubwa za kuimarisha taasisi za umma zinazosimamia haki na sharia, Taasisi zinazoshughulikia huduma za jamii, elimu, afya, maji safi na salama, kilimo, miundombinu ya usafiri, utalii, michezo na mengineyo.
Akinukuu Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 Ibara ya 18 (2), Rais Dk. Shein ameendelea kuwasisitiza viogozi wenzake wahakikishe wanatekeleza amatakwa ya Kikatiba ya kutoa taarifa kwa wananchi kwa kujiwekea utaratibu maalum wa kutoa taarifa kwa wananchi kupitia vyombo  ya habari.
Rais Dk. Shein alieleza jitihada za kuziimarisha taasisi zinazosimamia haki na sharia zinazozingatia maendeleo ya Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020 ambayo katika Ibara ya 145 inafahamisha jinsi ya kuimarisha mfumo wa utoaji haki kwa  ufanya maboresho katika utendaji wa vyombo vya maamuzi ikiwemo Mahkama, Ofisi ya Mwendesha Mashataka na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza hatua zilizochukuwa na Serikali katika matengenezo ya majengo ya Mahkama huku akieleza kuwa Serikali imo mbioni kujenga jingo la Mahkama Kuu mpya pamoja na jingo la skuli ya sharia yaani “Law School,” huko Tunguu ambapo jumla ya TZS bilioni 5.0 zimetengwa kwa kazi hiyo.
Akieleza masikitiko yake Rais Dk. Shein alieleza kusikitishwa na Jeshi la Polisi inavyoingilia vyombo vya Sheria katika suala zima la kupambana na rushwa.
 Aliongeza kuwa hivi karaibuni kumetokea tokea ambalo halileti picha nzuri hali iliyopelekea jeshi hilo la Polisi kuanza kuwatisha wafanyakazi wa Taasisi ya Kupambana na rushwa ZAECA na kusisitiza kuwa taasisi hiyo iwachwe ifanye kazi yake kwa uhuru na sheria zilizowekwa.
Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika kuhakikisha tatizo la kupata ushahidi kwa kesi za makosa ya jinai yanayohitaji uchunguzi, Serikali imejenga Maabara mpya ya kisasa ya Mkemia Mkuu wa  Serikali ambapo imenunua vifaa vipya na nyenzo mbali mbali ikiwa ni pamoja na uwezo wa kuchunguza vinasaba vya urithi kwa kupima DNA na kutoa majibu ya uhakika.
Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuongeza kasi zaidikatika kuliondosha tatizo la ucheleweshaji wa kesi ili kuweza kupata ufanisi utakaooana na ajuhudi kubwa za Serikali za kuimarisha taasisi hizo.
Alieleza kuwa Majaji, Mahkama pamoja na Makadhi ni kioo cha jamii hivyo suala la kuzingatoa maadili ya kazi ni wajibu wa kila mfanyakazi lakini jamii hupata mshtuko Zaidi pindi inaposikia kuwa Jaji amam Hakimu Fulani ana tabia zinazokwenda kinyume na maadili ya kazi na jamii anayoishi.
“Kwa hivyo ni vyema kwa Majaji na Mahakimu mkaendelea kutekeleza wajibu wenu kwa kuzingatia maadili ya kazi zenu ndani ya jamii mnayoishi katika maisha yenu ya kila siku, sina shaka kwamba mtaendelea kujijengea sifa njema ili muendelee kwua mfano bora miongoni mwa watumishi wa umma”alisema Dk. Shein.
Pia, alipokea ombi la kutaka Mawakili kuandaliwa Sheria yao itakayowapelekea kufanya kazi zaokwa ufanisi mkubwa Zaidi na kuitaka Serikali kuandaa mswada wa sharia juu ya ombi hilo.
Alieleza kuwa mafanikio ni makubwa yaliopatikana katika masuala ya kisheria hapa Zanzibar kuliko changamoto zilizopo.
Nao viongozi mbali mbali kutoka Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora walieleza mafanikio yaliopatikana katika suala zima la sharia hapa Zanzibar na kueleza hatua zinazoendelea katika kuhakikisha mafanikio Zaidi yanapatikana.
Pia, walipongeza wazo la Rais Dk. Shein la kufanywa sherehe hizo kisiwani Pemba mwaka huu na kueleza jinsi sherehe hizo zilivyofana.
Dk. Shein pia, alizindua kitabu cha Sheria cha mwaka huu wa 2019 ambacho kila yanapofika maadhimisho ya siku ya sharia huzinduliwa kitabu.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.