Habari za Punde

Uzinduzi wa Skuli ya Kisasa ya Msingi na Maandalizi Fuoni Pangawe Wilaya ya Magharibi"B" Unguja leo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa hafla ya ufunguzi wa Skuli ya Msingi na Maandalizi Fuoni Pangawe Wilaya ya Magharibi "B"Unguja, kulia Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mhe. Riziki Pembe Juma na Mwakilishi wa Balozi Mdogo wa Jamuhuri ya Watu wa China Zanzibar Bi. Shen Qi,

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amewataka walimu kote nchini kuwa wabunifu na kujiendeleza kitaaluma ili waweze kukidhi mahitaji ya kielimu na kwenda sambamba na wakati.

Dk. Shein amesema hayo katika ufunguzi wa  Skuli ya msingi ya Fuoni /Pangawe, iliyopo Wilaya ya Magharibi B Unguja.

Ujenzi wa skuli hiyo uliogharimu zaidi ya silingi Bilioni tano ni wa tatu kufanyika, ikiwa ni muendelezo wa misaada ya Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China kwa Zanzibar, ikitanguliwa na  ujenzi wa skuli za Kijichi na Urafiki iliyoko Mwanakwerekwe.

Dk. Shein amesema elimu ni fani inayokuwa na kuendelea siku hadi siku, hivyo ni vyema kwa walimu kwenda sambamba na mabadiliko hayo ili kukidhi haja ya zama hizi, akibainisha umuhimu wa  kuwa na mbinu mpya za ufundishaji.

Alizitaka mamlaka zinazosimamia uendeshaji wa skuli hiyo kushirikiana na kuweka walimu wenye uwezo wa kitaaluma, wanaopenda kujituma na wenye kuweka mbele uzalendo ili ufanisi unaotarajiwa uweze kupatikana.

“Ni busara tukaiwacha ile tabia ya kuwafundisha watoto wetu yale tuliosoma sisi miaka iliyopita, tuelewe kuwa elimu si sawa na maji ya vidimbwi yanayotuama, bali ni fani inayokuwa na kuendelea siku hadi siku”, alisema.

Alisema ufunguzi wa skuli hiyo ni uthibitisho wa dhamira njema ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miundombinu inayochochea maendeleo, ikiwemo ya elimu.

Aidha  alisema ujenzi huo umetokana na mipango ya serikali, iliozingatia ripoti ya sensa ya watu na mkaazi ya mwaka 2012 pamoja an ripoti ya Utafiti ya watoto walio nje ya skuli.

Dk. Shein alibainisha kuwa ripoti hizo zimeonyesha ongezeko kubwa la idadi ya watu, jambo lililopasa kwenda sambamba na mahitaji ya kijamii, zikiwemo skuli na kusema kuwa Wilaya hiyo ina jumla ya watoto 36,666 wenye umri wa kati ya miaka sita na 11, ambao ni wajibu kwao kupata elimu ya msingi.

“Ripoti hizo zimebainisha kuwepo msongamano  mkubwa wa wanafunzi unaofikia wastani wa wanafunzi 90 kwa darasa moja katika skuli za Wilaya hiyo, ikibainishwa ndio zinazoongoza katika changamoto ya aina hiyo”, alisema.

Rais Dk. Shein alisema uwepo wa skuli hiyo utasaidia sana upatikanaji wa nafasi za masomo kwa watoto wa maeneo hayo na hivyo kupunguza msongamano katika skuli za Kinuni, kijitoupelea, Chunga na Fuoni ambazo hivi sasa zina wanafunzi 17,054 ikiwa wastani wa wanafunzi 131 kwa darasa moja.

Alisema ujenzi wa skuli Fuoni /Pangawe utasogeza karibu sana mahitaji ya kielimu watoto wanaoishi maeneo hayo, akibainisha muendelezo wa juhudi za Serikali katika kupanua wigo wa miundombinu ya elimu Wilayani humo.

“Juhudi za serikali katika sekta ya elimu haziishi hapa, kuna ujenzi unaotarajiwa kukamilika ndani ya mwaka hu, utazihusisha skuli mpya za msingi Kwarara na ile ya Ghorofa ya Fuoni na Kinuni”alibainisha.

Alisema kukamilika kwa ujenzi wa skuli hizo za sekondari kutaongeza idadi ya skuli za msingi na Sekondari Wilayani humo, kutoka skuli za Sekondari 15  mwaka 2018 hadi kufikia 17, wakati skuli za Msingi nazo zikiongezeka kutoka 24 mwaka uliopita hadi kufikia 26.

Aliwataka wananchi kote nchini kudumisha amani pamoja na kuchangamkia fursa za kuendeleza elimu kwa kuwaandikisha watoto wote waliofikia umri wa kuanza masomo sambamba na kuwashajiisha kushughulikia masomo yao kwa maslahi yao na Taifa kwa ujumla.

Alisema mafanikio ya kielimu yaliofikiwa nchini yanatokana na juhudi na misingi bora uliyowekwa na mwasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar, Hayati Abeid Amani Karume, alielenga kuhakikisha vijana wote wanapata elimu bila ubaguzi.

Alisema katika kipindi cha miaka 55 sasa, Zanzibar imeshuhudiwa kupiga hatua kubwa ya maendeleo ya kijamii, ikiwemo uimarishaji wa sekta ya elimu

Dk. Shein aliipongeza Serikali ya watu wa China pamoja na  Kampuni ya China Qindao Construction (CNQC) kwa kusaidia ujen zi wa jingo hilo  zuri la kisasa na lenye viwango vinavyokubalika.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein aliagiza uongozi wa Wizara kwa kushirikiana na Kamati ya Skuli kuhakikisha skuli hiyo pamoja na samani zilizomo zinatunzwa vyema ili ziwe endelevu, na kubainisha haja ya wanafunzi kufunzwa uzalendo wa kuthamini mali za Taifa.

Aidha, alizitaka mamlaka hizo kuhakikisha michoro na mifumo yote ya umeme na maji taka iko vizuri, ili pale wakandarasi watakapoondoka kusiwepo na hitilafu zitakazojitokeza. 

Nae, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pemba Juma, alisema ujenzi wa skuli hiyo ni moja lati ya skuli tatu zilizotanguliwa kujengwa, ukiwa umevuka malengo ya Ilani ya CCM 2015 – 2020.

Alisema kupitia Ugatuzi Wizara hiyo itashirikiana an Wizara ya Nchi, (OR), Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ katika usimamizi wa suala zima la ufundishaji.

Mapema, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Dk. Idrisa Muslih Hijja alisema ujenzi wa skuli hiyo uliogharimu zaiidi ya shilingi Bilioni tano umetokana an msaada wa Serikali ya China, huku Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na mambo mengine imechangia msamaha wa ushuru wa vifaa vya ujenzi, umeme pamoja na maji.

Alisema hatua ya ujenzi huo ni kuunga mkono juhudi za serikali katika uimarishaji wa sekta ya elimu nchini, hivyo akawataka wazazi, walimu na jamii inayozunguka kuitunza skuli hiyo ili iweze kuwa endelevu.

Aidha, Mwakilishi wa Ubalozi mdogo wa China nchini, Bi.Shen Qi aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano mkubwa iliotowa hadi kufanikisha ujenzi huo.

Alisema kukamilika kwa ujenzi wa skuli hiyo kutasaidia kuwaweka wanafunzi katika mazingira  bora zaidi ya kupata elimu na hivyo kuinua viwango vyao.

Bi.Qi alielezea dhamira ya Serikali ya Watu wa China kuendelea kushirikiana na Zanzibar, ili kukuza maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kubainisha ushirikiano wa Kihistoria uliopo kati ya mataifa hayo.  

 Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
E-mail: abdya062@gmail.com


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.