Katibu wa Baraza la
Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee alisisitiza hayo
hivi karibuni katika vikao vya Utekelezaji wa Mpango Kazi Ofisi ya Makamo wa
Pili wa Rais wakati ilipowasilisha taarifa ya Julai 2018 hadi Machi 2019 huko
Ikulu ndogo Kibweni.
Katika maelezo yake Dk. Mzee alieleza kuwa ni
kawaida kwa wasafiri wakiwemo wageni wanaotoka nje ya nchi kununua bidhaa
katika maduka ndani ya viwanja vya ndege hasa vya Kimataifa ambapo kwa kawadia
mifuko wanayotumia kutiliwa bidhaa hizo huwa ni ya plastiki.
Aliongeza kuwa wasafisri hao wanapoingia nchini
katika viwanja vya ndege huingia na mifuko hiyo na kupita nayo bila ya kuweko
kwa uangalifu ama utaratibu maalum uliowekwa kwa ajili ya kuizuia na hatimae
kuwaelekeza juu ya athari na marufuku iliyowekwa hapa nchini.
Alisisitiza kuwa ni vyema zikawepo taratibu maalum
za kuwafahamisha wasafiri wakiwemo wageni kutoingia na mifuko ya plastiki ili
iwe njia moja wapo ya kuendeleza mikakati ya kuzuia uingizwaji na matumizi ya
mifuko ya plastiki hapa Zanzibar.
Dk. Mzee alitumia fursa hiyo, kuipongeza Ofisi
hiyo kwa juhudi kubwa inayochukua katika kuzuia ungizaji wa mifuko ya plastiki
hapa nchini na kusisitiza haja ya taasisi husika kukaza kamba kwani bado wapo
baadhi ya wafanyabiashara wakiwemo wadogo wadogo wanaitumia mifuko hiyo
masokoni.
“Mimi kwa kawaida nikisafiri nikipita “duty free” huwa
na mkoba wangu maalum kwa ajili ya kutilia vitu vyangu ninavyonunua
…………..hivyo, mikakati maalum inahitajika katika kuzuia mifuko ya plastiki
kuingia nchini”, alisisitiza Dk. Abdulhamid Mzee.
Alieleza kuwa iwapo juhudi za makusudi zitaendelea
kuchukuliwa Zanzibar inaweza kufikia malengo yake iliyojiwekea katika kuzuia
matumizi ya mifuko ya plastiki kutokana na athari zake kubwa za kimazingira.
Kwa mujibu wa maelezo ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa
Rais, Ofisi hiyo imeendelea kuchukua juhudi za kupambana na uharibifu na
uchafuzi wa mazingira kwa kutoa elimu kwa jamii juu ya uhifadhi wa mazingira.
Ofisi hiyo ilieleza kuwa tayari imeshafanya
operesheni 90 za kusimamia upigaji marufuku mifuko ya plastiki ambapo kilo 621
za mifuko ya plastiki zilikamatwa na watu 149 wamekamatwa na kuchukuliwa hatua
za kisheria.
Zanzibar tayari imeshetangaza rasmi utekelezaji wa
sheria namba 49 iliyopitishwa mwaka 2011 ambayo inapiga marufuku uingizwaji na
utumiaji wa mifuko ya plastiki hapa nchini.
Ingawa Zanzibar haijafanikiwa kwa asilimia 100
kudhibiti matumizi ya mifuko ya plastiki lakini tayari imepata mafanikio na
kupiga hatua kubwa katika kufanikisha suala hilo ambapo hivi sasa mifuko hiyo
imeweza kupungua kwa kiasi kikubwa.
Kabla ya kupitishwa kwa sheria hiyo mwaka 2011,
mifuko ya plastiki ilikuwa ni tishio kwa mazingira hali ambayo iliondosha haiba
ya kisiwa cha Zanzibar ambacho kilikuwa kinasifika kwa rangi ya kijani kutokana
na uwepo wa miti na mimea mbali mbali.
Kwa upande wa Tanzania bara mnamo Aprili 10, 2019
Bungeni Jijini Dodoma Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alitangaza marufuku ya mifuko
ya plaskiti kwa kusema Mei 31, 2019 itakuwa siku ya mwisho kuruhusu utengenezaji,
uuzaji, uingizaji na utumiaji mifuko ya plastiki kwa ajili ya kubebea bidhaa za
aina yoyote.
Uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka za
plastiki huathiri na kuharibu mazingira ya miji, ardhi, mito, maziwa, mashambani
na hata baharini na hata hivyo, kutokana na kuenea kwa taka hizo, viumbe kadhaa
wa baharini huathiriwa na kemikali zitokanazo na taka za plastiki au kwa kula
mabaki ya plastiki.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment