RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali
Mohamed Shein, amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Makampuni ya S.S.
Bakhresa, Sheikh Said Salim Bakhressa kufuatia vifo vya wafanyakazi watano wa
Azam Media Limited kutokana na ajali ya barabarani.
Ajali hiyuo
imetokea juzi (Jumatatu) Julai 8, 2019 katika eneo la katikati ya Igunga
(Tabora) na Shelui (Singida). Wafanyakazi hao ni kati ya watu saba waliofariki
dunia katika ajali hio baada ya basi aina ya Coaster waliokuwa wakisafiria
kugongana uso kwa uso na gari la mizigo wakati wakielekea Wilayani Chato kwa
ajili ya uzinduzi wa Hifadhi hiyo ya Taifa ya Chato-Burigi.
Katika salamu
hizo za rambirambi Rais Dk. Shein alieleza kuwa amepokea kwa mshtuko na huzuni
kubwa taarifa ya ajali hio na kwamba yeye binafsi pamoja na wananchi wote wa
Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla wamejawa na simanzi nzito kufuatia vifo
vya wafanyakazi hao.
“Kutokana na
msiba huu, natoa salamu za rambirambi kwako Sheikh Said Salim Bakhressa, ndugu,
wanafamilia wa marehemu, marafiki, wafanyakazi wote wa Makampuni ya S.S.
Bakhressa pamoja na watazamaji, wasikilizaji na wafuatiliaji wa vipindi na
habari mbali mbali zinazotolewa na Azam Media Limited, ndani na nje ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania”, ilieleza sehemu ya salamu za rambirambi alizozituma
Dk. Shein.
Kadhalika,
Rais Dk. Shein katika salamu hizo za rambirambi amemuomba Mwenyezi Mungu ampe
moyo wa subira Sheikh Said Bakhressa katika kipindi hiki kigumu pamoja na wale
wote walioguswa na msiba huo wakiwemo wafanyakazi wote wa nyanja ya habari.
Sambamba na
hayo, Rais Dk. Shein amemuomba Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu hao
pahala pema peponi na awape afuweni na afya njema wale wote waliojeruhiwa
katika ajali hio, ili waweze kuendelea na majukumu yao mbali mbali.
Uongozi wa Azam Media Limited
umethibitisha wafanyakazi waliofariki kuwa ni Salim Mhando, Said Haji, Florence
Ndibalema, Sylvanus Kasongo, Charles Wandwi pamoja na dereva na utingo wa gari
hilo ambapo waliojeruhiwa na kulazwa ni Mohamed Mwinshehe, Mohamed Mainde na
Artus Masawe.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment