Habari za Punde

Mwenyekiti wa SADC Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Magufuli Ahutubia Mkutano wa 39 wa SADC Ukumbi wa Juluis Nyerere Jijini Dar es Salaam leo.YA mUUNGANO WA tANZANIA mHE. dK. jOHN mAGUFULI aHUTUBIA mKUTANO WA


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli leo amekabidhiwa rasmi Uwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) baada ya aliekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Dk. Hage Geingob Rais wa Namibia kumaliza muda wake.

Tukio hilo limefanyika leo katika Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi hizo za (SADC) uliofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar-es-Salaam ulihudhuriwa na viongozi mbali mbali kutoka nchi za (SADC) wakiwemo Marais 11 kutoka nchi hizo pamoja na viongozi wote wakuu wa Tanzania akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Mara baada ya kukabidhiwa wadhifa huo, Rais John Pombe Magufuli akisoma hotuba yake alitoa shukurani kwa viongozi wote wakuu wa Jumuiya huo kwa kuonesha mashirikiano nae katika kuiongoza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa rais wao.

Rais Magufuli alisema kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko tayari na itaendelea kushirikiana na nchi zote za (SADC) huku akiwahakikishia viongozi hao kuwa katika uongozi wake atahakikisha Tanzania haitoyumba.

Alieleza kuwa atahakikisha anafuata nyayo za waasisi wote wa nchi za (SADC) akiwemo Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na kueleza kuutumia uzoefu wa mwenyekiti aliyepita Dk. Hage Geingob, Rais wa Namibia.

Rais Magufuli alimpongeza Mwenyekiti huyo mstaafu kwa juhudi kubwa alizozichukua katika kupigania ajira kwa vijana huku akimpongeza kwa kuhakikisha nchi sita za (SADC) zimefanya uchaguzi kwa salama na Amani huku akiwa pole wananchi wa nchi zilizokuwemo katika Jumuiya hiyo ambazo zilipata maafa kutokana na kimbunga.

Aidha, Rais Magufuli alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Antoine Tshisekedi kwa kufanya uchaguzi kwa amani na utulivu mkubwa hali ambayo imeonesha wazi kukuwa kwa demokrasia.

Alitumia fursa hiyo kuushukuru uongozi wa (SADC) akiwemo Katibu Mtendaji wa (SADC) Dk. Stergomena Lawrence Tax pamoja na Sektarieti ya Umoja huo kwa kazi kubwa ulioifanya na kusisitiza kuwa akina mama wakipewa uongozi wanaweza.

Alieleza kuwa hatua hiyo imeweza kuonekana na Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania na ndio maana mwaka 2015 ikamchagua Mama Samia Suluhu Hassan kuwa Makamo wa Rais wake na tokea kupewa wadhifa huo amekua akitekeleza kazi zake vizuri.

Rais Magufuli alieleza kuwa tangu kuanzishwa kwa Umoja huo mafanikio makubwa yameweza kupatikana ikiwa ni pamoja na kupambana na ukoloni sambamba na kupambana na ubaguzi wa rangi.

Alisisitiza kuwa tangu kuanzishwa kwa Jumuiya hiyo mnamo mwaka 2008 biashara imekuwa kutoka asilimia 16  mwaka huo hadi kufikia asilimia 22 mwaka 2017 hiyo ni kutokana na kuwepo wka utamaduni wa kidemokrasia.

Sambamba na hayo. Rais Magufuli alieleza kuwa licha ya mafanikio yalipptikana katika Jumuiya hiyo pia, kuna baadhi ya changamoto zikiwemo amani na usalama katika baadhi ya nchi, njaa na ukame.

Katika hilo, Rais Magufuli alieleza kuwa katika nchi hizo za (SADC) kuna haja ya kufanya kazi kwa pamoja sanjari na kuendeleza amani na usalama kwani vitu hivyo pia huimarisha uchumi.

Alieleza kuwa katika kuhakikisha nchi za Jumuiya hiyo zinapata mafanikio ni vyema zikahakikisha hazina migogoro huku akimnukuu Rais mstaafu wa Zimbwabe Robert Mugabe pale aliposema “kamwe tusije tukakata tamaa katika eneo lolote la Afrika”.

Pamoja na hayo, Rais Magufuli alieleza jinsi uchumi wa nchi za (SADC) zilivyodorora katika kuimarisha uchumi wake hadi kuweza kupelekea baadhi ya nchi za Jumuiya hiyo zikawa na upungufu wa chakula.

Alieleza kuwa kutokana na kutokuwepo kwa mawasiliano katika nchi za Jumuiya hiyo kumechangia kuagizia bidhaa nje ya nchi wakati bidhaa hizo zimejaa katika nchi za (SADC) hali ambayo pia, inazidisha kuongezeka kwa gharama za uagiziaji.

"Rais Dk. Shein alieleza haja ya kujiendeleza katika viwanda na kusisitiza kuwa sio jambo la busara kuuza malighafi na badala yake ni vyema zikauzwa bidhaa zinazotokana na mali ghafi hizo kwani zinapouzwa malighafi soko la ajira linaondoshwa".

Aliongeza kuwa katika uongozi wake atahakikisha suala la viwanda linapewa kipaumbele katika uongozi wake na kusisitiza kuwa nchi za (SADC) sio masikini ni tajiri sana kwani zina rasilimali za aina zote.

“Ni lazima tuhakikishe kuwa nchi zetu zinanufaika na rasilimali zilizopo ndani ya nchi zetu waasisi wetu walionesha umoja ni nguvu na tunaweza kufika pazuri na kuleta ushindi mkubwa katika kujenga nchi zetu” alisisitiza Magufuli.

Sambamba na hayo, Katika hotuba yake Rais Magufuli aliwaeleza viongozi wa Umoja huo kuwa vikwazo vilivyowekwa kwa nchi ya Zimbabwe si vyao peke yao bali ni vya nchi zote za (SADC) hivyo, kwa mashirikiano ya pamoja ya nchi hizo kuna haja ya kupambana katika kuviondoa.

Pia, alieleza kuwa ajira zenye staha zitapatikana kama nchi hizo zitafanya kazi kwa pamoja sambamba na kuimarisha amani na utulivu kwani hatua hiyo pia, itaondosha changamoto zote ziliozopo.

Nae Mwenyekiti wa (SADC) aliemaliza  muda wake Rais Hage Geingob alimkabidhi Uwenyekiti huo Rais Magufuli na kumuelezea kuwa anaimani na kiongozi huyo kuwa wadhifa huo utautendea haki kutokana na ujasiri na mchapa kazi katika utendaji wake wa kazi.

Rais Hage Geingob alitumia fursa hiyo kuitangaza lugha ya Kiswahili kuwa ni lugha rasmi katika Jumuiya hiyo ya (SADC).

Alitumia fursa hiyo kupongeza Amani na utulivu inavyoendelea kuoneshwa katika nchi za (SADC) na kuonesha kukua kwa demokrasia katika ukanda huo huku akisisitiza kuwa amani na utulivu ni msingi wa maendeleo.

Mapema baadhi ya viongozi wa (SADC) walitoa hotuba zao kwa ufupi na kueleza jinsi mashirikiano mazuri yaliopo katika Umoja huo wakiwemo Rais Azali Assoumani wa Comoro, Rais wa Madagascar Andry Nirina Rajoelina, Rais wa Congo Felix Tshisekedi na viongozi wengine.

Pia, katika mkutano huo zilitolewa tunzo na vyeti kwa washindi wa insha pamoja Makala na vipindi vya redio na televisheni kwa waandishi wa habari wa nchi za (SADC).
   
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.