Habari za Punde

NHIF Yatajwa Kuchangia Mageuzi Sekta ya Afya Miaka Minne ya JPM

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bw. Bernard Konga akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dodoma kuhusu mafanikio ya mfuko huo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano (4), Kushoto ni Afisa Habari Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Catherine Sungura na Kulia ni Meneja Uhusiano wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bi. Angela Mziray
Waandishi wa Habari wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bw. Bernard Konga wakati akiongelea kuhusu mafanikio ya mfuko huo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano.
Picha na Maelezo Dar es Salaam.
Na Mwandishi wetu- Dodoma.                                                                                                                                             
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umetajwa kuwezesha mageuzi yenye tija katika sekta ya afya katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano  .
Akizungumza waandishi wa habari leo, Desemba 12, 2019 Jijini Dodoma kuhusu mafanikio ya mfuko huo, Mkurugenzi Mkuu wa mfuko huo Bw. Bernard Konga amesema kuwa baadhi ya Hospitali zilizonufaika  ni Hospitali ya Taifa Muhimbili, Bugando, KCMC, MOI,  Ocean Road,na Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa kuwezeshwa kupata vifaa kama MRI, CT SCAN, uanzishwaji  wa viwanda vidogo vya kuzalisha maji ya dripu, gesi  na ujenzi wa majengo.
‘’ NHIF imetoa fedha kuwezesha uwekezaji wa awamu  ya pili katika Hospitali ya Benjamin Mkapa na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa kuwezesha huduma za kibingwa kama upandikizaji figo,   ambapo  shilingi Bilioni 32.10 zimetolewa kwa ajili ya ujenzi na Bilioni 43.12 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa  katika Hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma ’’ Alisisitiza Konga
Akifafanua amesema kuwa uwekezaji wa majengo pacha ya MOI  umesaidia  kuongeza uwezo wa kulaza wagonjwa na kuboresha huduma za Kibingwa katika Taasisi hiyo, majengo mengine yamejengwa  kwa uwekezaji wa NHIF katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Hospitali ya Rufaa Dodoma, Hospitali ya Rufaa Bugando  na KCMC. 
‘’Wanachama wa NHIF wanapata huduma katika vituo 7,606 nchi nzima vikiwemo vya Serikali na Binafsi kwa ngazi zote ikilinganishwa na vituo  6,185 vya mwaka 2014/2015 ,Ongezeko hili ni sawa na vituo 1,421 kwa kipindi cha miaka minne’’. Alisistiza Konga
Katika kipindi cha miaka minne, NHIF imelipa jumla ya shilingi trilioni 1,283,109,701,067 kwa vituo  vyote vinavyohudumia wanachama wake nchini wakati mwaka 2018/2019 Mfuko umelipa kiasi cha Shilingi Bilioni 444.1 ambayo ni ongezeko la asilimia 64 ikilinganishwa na malipo yaliyofanyika mwaka 2014/2015 ya shilingi bilioni  157.9
Akizungumzia utekelezaji wa mradi wa Tumaini la Mama ulilenga kuwapatia wanawake wajawazito Bw. Konga amesema kuwa mradi huo umetekeelzwa kupitia NHIF na umewanufaisha jumla ya akina mama milioni 1,044,000.
Katika kipindi cha miaka minne mradi huu umewanufaisha akina mama 796,404 sawa na ongezeko la la asilimia 76 kutoka wanufaika 247,596 wa mwaka 2014/2015 mradi huo  umesaidia kupunguza vifo vya uzazi na umewezesha wakinamama kujifungulia Hospitali. 
Serikali kupitia Wizara ya Fedha na NHIF imesaini mkataba wa awamu ya tatu na KfW wenye thamani ya  EURO milioni 13 sawa na Shilingi Bilioni 32.7 kuwezesha utekelezaji wa mradi huo utakamilika mwaka 2020.
NHIF  imethibitishwa  kwa utoaji wa huduma bora kwa viwango vya kimataifa  na kukabidhiwa cheti cha ubora  (ISO 9001:2015) mwaka 2018, ndani ya kipindi  cha miaka minne ya Awamu ya Tano, mfuko umeimarisha mawasiliano na wanachama  na wadau wake kwa kuanzisha Kituo cha Huduma kwa Wateja. 
Mfuko unahudumia wanachama 966,792 sawa na wanufaika 4,025,693 ikilinganishwa na idadi ya wanufaika 3,237,434k kwa mwaka 2014/15 sawa na ongezeko la asilimia 20.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.