Na.Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar.
Chuo Kikuu cha AL-Sumait kimetakiwa kuzidisha mbinu za ufundishaji katika kozi mbali mbali ili kuweza kumsaidia mwanafunzi kujiajiri mwenyewe pindi amalizapo masomo yake katika kujikwamua kimaisha.
Hayo ameyasema Naibu Waziri wa Elimu Mhe.Simai Mohammed Said kwa Niaba ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali,Mhe. Riziki Pembe Juma huko katika Chuo Kikuu cha AL- Sumait wakati wa mahafali ya chuo hicho .
Alisema mbinu bora ya ufundishaji wanafunzi itamsaidia uwelewa mpana wa kujua namna ya kujiendesha kimaisha na kujipatia maendeleo .
Aidha aliwataka wanafunzi waliomaliza masomo yao wasitosheke na elimu walioipata wajiunge na vyuo vya nje na vya ndani ili kujaitumikia nchi yao.
Vilevile Naibu Waziri huyo aliwataka wanafunzi na walimu kuendeleza kufanya utafiti wa hali ya juu ili uendane na hadhi ya kimataifa pamoja na kuendeleza kushika hadhi ya kuwa na nafasi ya juu katika chuo hicho.
Akizungumzia kuhusu changamoto za uhaba wa eneo la Chuo Naibu Waziri huyo alisema tatizo hilo tayari limeshawasilishwa Wizarani husika ili kupatiwa ufumbuzi.
Nae Mkuu wa Chuo Kikuu Dkt Amani Abeid Karume amesema mahitaji ya elimu yanaongezeka siku hadi siku na chuo kinatarajia kutoa udhamini wa masomo ili kuvutia wanafunzi kuweza kuendeleza masomo katika chuo hicho na kutokana kuwa bodi ya mikopo ya Zanzibar na Tanzania bara ina kiwango maalumu cha kutoa huduma hiyo.
“Mpango wa kuanzisha msingi wa kuwasaidia wanafunzi wenye hali ngumu kimasomo unaandaliwa ili kuwapatia haki ya elimu wanafunzi hao ‘Alisema mkuu huyo.
Alisema kuwa Chuo cha AL- Sumait kimekuwa na hadhi kwa Afrika kimetimiza malengo kwa kutoa huduma katika nafasi tofauti za kielimu ikiwemo Ushauri nasaha, komputa, elimu ya sayansi, masomo ya arti na teknolojia habari na mawasiliano.
Kwa upande Balozi wa Kuwait Mubarak Alsehaijani alisema lengo lao la kukuza elimu katika chuo hicho kwa kuengeza vifaa kufundisha pamoja na kujenga kituo cha komputa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuendeleza kukuza uhusiano uliopo na kuunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Jumla ya wanafunzi 364 wamefanikiwa kumaliza masomo yao katika ngazi ya cheti, shahada na stashahada.
No comments:
Post a Comment