Habari za Punde

Kasi ya Ukuaji wa Uchumi Zanzibar Umeongezeka Kwa Asilimia 7.1 -Dk. Shein.


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa kasi ya ukuaji uchumi wa Zanzibar imeongezeka na kufikia wastani wa asilimia 7.1.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo wakati akifunga Semina ya siku moja ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa (NEC), huko katika ukumbi wa Taasisi ya Mafunzo wa Benki Kuu ya Tanzania (B.O.T) uliopo katika mtaa wa Nyamagana jijini Mwanza.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kwamba mafanikio hayo yamepatikana kutokana na kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kuziba mianya ya upotevu wa mapato hayo.
Alisema kuwa hali hiyo imeongeza mapato kutoka TZS bilioni 181.1 mwaka 2010 hadi kufikia TZS bilioni 748.9 mwaka 2018 ikiwa ni ongezeko la mara 4.1 au sawa na asilimia 314 na kuzipongeza taasisi za TRA na ZRB ambazo zinakusanya mapato.
Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba imeongeza bajeti yake kwa mara 3.2 kutoka TZS bilioni 444.6 mwaka 2010/2011 hadi TZS trilioni 1.4194 mwaka 2019/2020.
Aliongeza kuwa kutokana na ufanisi huo, hata bajeti za Wizara mbali mbali nazo zimeongezeka ikiwemo Wizara ya Elimu, Wizara ya Afya, Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji pamoja na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi.
Sambamba na hayo, Makamo huyo wa CCM Zanzibar alieleza kuwa huduma za jamii nazo zimimarika kutokana na mambo ya Kisera yaliopangwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mara tu baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 katika huduma za elimu na afya na kupelekea huduma hizo kutolewa bure.
Rais Dk. Shein alisema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imetoa umhimu mkubwa katika kuhakikisha Amani na utulivu vinakuwepo nchini wakati wote ambapo hali hiyo ndiyo iliyowezesha kupiga hatua kubwa za maendeleo katika nyanja ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Alieleza kuwa mafanikio hayo yote ya utekelezaji wa Ilani yametokana na kuwepo kwa amani na utulivu ambayo yametoa nafasi ya kuyaenzi Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 pamoja na Muungano uliopo.
“Ibara ya 127 ya Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2015-2020 inatuelekeza kuwa CCM itaendelea kuwa muumini wa kweli wa amani na utulivu na kuwaunganisha wananchi wa Zanzibar kuwa wamoja wenye mashirikiano na wanaopendana”, alisema Dk. Shein.
Aleleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanza kazi ya kuandaa Mwelekeo Mpya wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020-2050 baada ya kufanya tathmini ya utekelezaji wa Dira 2020.
Alisisitiza kuwa Dira hiyo mpya ya Maendeleo ya Zanzibar itakuwa na uhusiano wa moja kwa moja na Mwelekeo wa Sera za CCM katika miaka ya 2020-2030 na kuandaliwa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya 2020 kwa upande wa Zanzibar katika kuiletea maendeleo Zanzibar.
Alisema kuwa CCM imeimarika na inakubalika kwani imeweza kushinda katika chaguzi mbali mbali kwa sababu wananchi wanakikubali hivyo, aliwataka viongozi hao kuendelea kusimamia utekelezaji wa Ilani ya chama hicho huku akieleza kuwa kwa upande wa Zanzibar ushindi wa chama hicho katika uchaguzi ujao hauepukiki.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa, Katibu Mkuu wa CCM pamoja na viongozi wote wa chama hicho kwa upande wa Tanzania Bara kwa ushindi mkubwa wa asilimia 99.9 wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar aliwataka Wajumbe wote wa NEC kufanya kazi na wazee na kuziunga mkono jitihada wanazozifanya katika mabaraza yao katika maeneo wanayoishi sambamba na kuendelea kuwandaa vijana kuwa wazalendo.
Nae Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Samia Suluhu Hassan akitoa neno la shukurani alipongeza jitihada za Rais Dk. Shein katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambazo zimeipelekea Zanzibar kupata mafanikio makubwa.
Akifungua mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli alieleza mafanikio makubwa yaliopatikana katika miaka minne ya uongozi wa chama hicho ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM kwa kiasi kikubwa na kuwataka viongozi wa NEC kutumia nafasi waliyonayo katika kuleta mabadiliko ya Tanzania kiuchumi.
Alieleza juu ya mwelekeo mpya wa Sera za CCM katika miaka ya 2020-2030 katika kuhakikisha Tanzania inajitegemea kiuchumi kupitia sekta ya viwanda huku akisisitiza  kuwa Tanzania ni nchi tajiri kutokana na rasilimali nyingi zilizopo.
Sambamba na hayo, Mwenyekiti huyo wa CCM alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa ushirikiano mkubwa aliotoa katika kuhakikisha mafanikio hayo makubwa yanapatikana hapa nchini.
Alieleza mwelekeo mpya wa Sera za CCM katika miaka ya 2020 hadi 2030 na Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya 2020 katika kuimarisha sekta ya viwanda, elimu, maji, mawasiliano, kilimo, uvuvi na ufugaji, madini, utalii ambapo alieleza jinsi watalii walivyoongezeka kwa Tanzania Bara na Zanzibar kutokanana vivutio kadhaa vilivyopo.
Pamoja na hayo, Rais Magufuli aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa kununua meli mpya ambapo alieleza kuwa usafiri huo wa meli utawasaidia wananchi ikiwa ni pamoja na kusafiri ndani na nje ya nchi. 
Pia, Rais Magufuli alitumia fursa hiyo kutoa tangazo la kuachiwa kwa ndege ya Tanzania iliyokuwa inashikiliwa nchini Canada na kuwaeleza wananchi kuwa watatangaziwa siku ya kuwasili ili wakaipoke ambapo inatarajiwa kutua katika uwanja wa ndege wa Mwanza.
Mada mbali mbali zilitolewa katika semina hiyo ikiwemo Mafanikio ya Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa kipindi cha miaka mine kwa upande wa Tanzania Bara ambapo ilitolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa na kwa Zanzibar ilitolewa na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.