Habari za Punde

Utekelezaji wa Uchumi wa Buluu Tayari Hatua Kubwa Zinachukuliwa Kuhakikisha Lengo Hilo Linafikiwa -Dk.Shein.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akimsikiliza Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Ndg. Mussa Aboud Jumbe, akitowa maelezo ya michoro ya majengo ya Soko la Samaki na Bandari inayojengwa katika eneo la Malindi Wilaya ya Mjini Unguja.ikiwa ni shamrashamra za kusherehekea Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar, hafla hiyo imefanyika katika eneo la ujenzi huo. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesema kuwa Zanzibar imo katika mchakato wa kutekeleza uchumi wa buluu na tayari hatua kubwa zinachukuliwa kuhakikisha lengo hilo linafikiwa.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa  soko la samaki na bandari ya uvuvi linalojengwa huko Malindi, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja ikiwa ni shamrashamra za sherehe za miaka 56 ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964.

Alisema kuwa uchumi wa buluu ni chochote kiliopo baharini na katika ufukweni wa bahari ambapo tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imenza kushughulikia uchumi huo na haiko tayari kuachwa nyuma.

Alisema kuwa Zanzibar inajiandaa na uchumi wa bahari na tayari imeanzisha Kampuni ya uvuvi ya Zanzibar (ZAFICO), ikiwa ni tayari imeshazindua boti mpya ya uvuvi na nyengine iko njiani inakuja na boti nyengine nne za uvuvi zimeshatengewa fedha zake huku akisisitiza kuwa Kampuni hiyo imejiandaa vizuri sana.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali inajenga bandari pamoja na soko huko Malindi ambalo idadi ya wastani ya watu 6000 watafanya kazi katika eneo hilo la soko jambo ambalo litaleta tija sana katika sekta ya uvuvi.

Alisema kuwa watu wa Zanzibar wamezungukwa na bahari lakini bahari hiyo haijatumiwa vizuri na badala yake wamekwua wakija watu kutoka nje ya nchi na kuwaiba samaki wa Zanzibar wakiwemo samaki wa jodari.

Alisema kuwa samaki wakubwa na wazuri wako bahari kuu ambako kufikia huko kunahitajika uwezo wa vifaa vya kuvulia.

Alisema kuwa haiwezekani Zanzibar kuwa imezungukwa na bahari lakini haivui samaki ipasavyo sambamba na kutokuwa na kiwanda hata kimoja cha kusindika samaki.

Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa haiwezekani kuwepo bahari lakini hakuvuliwi hivyo, ni lazima kuimarishwe uvuvi ikiwa ni pamoja na kujenga viwanda vya kusarifu samaki Unguja na Pemba.

Alisema kuwa historia ya Zanzibar inaonesha kwamba watu wa Zanzibar walianza kuvua kwanza kuliko kulima, hivyo uvuvi una historia kubwa hapa Zanzibar na kueleza kuwa histira ya Zanzibar ni uvuvi.

Alisisitiza kuwa lazima kuvuliwe kisasa ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa bandari, soko pamoja na vifaa vyengine vya kisasa vya kuvulia samaki.

Uvuvi wa samaki ni sehemu moja tu katika uchumi wa buluu lakini pia, katika uchumi huo ni vyema kukawpo maandalizi ya usafiri wa uhakikia wa baharini, boti za kisasa sambamba na kuwawezesha wavuvi wa hapa nchini.

Uchumi wa bahari pia, unapaswa katika kuimarisha utalii hali ambayo imekuwa ikishuhudiwa hapa Zanzibar ambapo watalii wamekuwa wakiingia nchini kwa njia ya anga na baharini.

Aidha, alisisitiza haja ya kuendeleza bandari za kisasa kama Serikali ilivyoamua kujenga bandari mpya ya Mpigaduri pamoja na kujenga bandari ya gesi na mafuta huko Mangapwani na kuyaondosha matangi yote ya mafuta yaliopo Mtoni.

Aliongeza kuwa Serikali itakapojenga bandari mpya ajira na biashara vyote vitaongezeka kwa kiasi kikubwa hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar ina historia ya biashara.

Rais Dk. Shein aliendelea kuwataka wananchi kuendelea kufanya subira katika kusubiri matokeo ya utafiti wa mafuta na gesi hapa Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa ni lazima uvuvi hapa Zanzibar ufanyike kisasa na taratibu zote zifanyike kisasa ili na wageni pia, wakija kutembea wafurahi na wasiudhike pale watakapotembelea masoko ya samaki.

Alisisitiza haja ya kufuga samaki na kueleza hatua za Serikali katika kuimarisha mradi huo ili kila mwananchi aweze kufuga samaki.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Serikali ya Japan kwa msaada huo mkubwa ulioutoa kwa Zanzibar na kuwaahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itafanya na itaweza.

“Zanzibar tunapendwa sana na rafiki zetu na wanatusaidia kutokanana kodi za wananchi wao na wanatuletea sisi, hivyo lazima tuwashukuru sana”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein kwa niaba ya wananchi wa Zanzibar aliwaahidi Serikali ya Japan pamoja na Shirika la (JICA) kuwa mradi huo wa soko pamoja na ujenzi wa bandari utatunzwa na kuenziwa vizuri ili ulete tija kwa wananchi wa Zanzibar.

Mapema Rais Dk. Shein alifika katika eneo linalotarajiwa kujengwa soko hilo pamoja na bandari huko katika eneo la Malindi na kupata maelezo juu ya ujenzi huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Mussa Aboud Jumbe.

Nae Waziri wa Kilimo , Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mmanga Mjengo Mjawiri alisema kuwa   Wizara hiyoimeweka utaratibu maaluma wa kufaiutaia miradi yao ilikuhakikisha inamaliza kwa wakati na inakuwa bora.

Alisema kuwa kila mwisho wa mwezi wamekuwa wakitembelea miradi hiyo kwa lengo la kufahamu matatizo yaliopo kwa pande zote na kuahidi kuwa miradi yote inayotekelezwa na Wizara hiyo itamaliza kwa wakati

Alisema kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wavuvi ili waweze kuvua uvuvi wenye faida na kipato ili waondokane na uvuvi wa mazoea.

Alisema kuwa tayari wameshaanza kutoa elimu pamoja na kukutana na Kamati za wavuvi kwa lengo la kutoa elimu huku akisisitiza kuwa soko la samaki linakuwepo iwapo kutakuwa na wavuvi na wavuvi wanaweza kuvua iwapo kutakuwa na bahari kwani bahari ndio makaazi ya samaki.

Hivyo, alisisitiza haja ya kuyahifadhi na kuyatunza mazingira ya samaki hasa matumbawe na kuachana kabisa na uvuvi unaochafua bahari na kusisitiza kuwa iwapo wataachana na kadhia hiyo mafanikio makubwa zaidi yatapatikana.

Alisema kuwa wananchi wameshaanza kuelewa juu ya uvuvi haramu na tayari wamekuwa wakitoa taarifa kwa watendaji wa Wizara wakiwemo viongozi na baada ya hapo hatua madhubutizimekwua zikichukuliwa katikamkupambana na kadhia hiyo ambapo hiyo ni dalili njema ya kufahamu kuwa wananchi wanaanza kufahamu.

Alisema kuwa Serikali itaendelea kuweka Sera na taratibu nzuri kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi hali ambayo itapelekea kuongezeka kwa samaki hapa nchini na kutosheleza soko la utalii huku akieleza azma ya Wizara hiyo kujenga viwanda vya kusarifu samaki.

Alitumia fursa hiyo kumpongea Rais kwa kuanzisha taasisi ya utafiti wa uvuvi na kueleza kuwa ujenziwa taasisihiyo unatarajiwa kumalizika mwezi Juni mwaka huu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mariam  Juma Abdalla Saadalla katika risala yake ya kitaalamu alieleza kwamba uwekaji wa jiwe la Msingi la ujenzi wa soko hilo la kisasa na bandari ya wavuvi ni matokeo ya jitihada za muda mrefu za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Alieleza kuwa jitihada hizo ni katika kuhakikisha sekta ya uvuvi inaimarika kwa madhumuni ya kukuza uchumi wa buluu pamoja na kuepuka kuuza samaki katika maeneo yenye mazingira yasiyostahiki ya kuhifadhi samaki.

Alisema kuwa hali hiyo iliwapelekea wavuvi kupata kipato kidogo kulingana na jitihada na kazi wanazozifanya sambamba na kutishia afya ya jamii.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi baada ya kuona hali hiyo iliendelea na jitihada za muda mrefu za kuwasiliana na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), kupitia Serikali ya Japan kuangalia uwezekano wa kusaidia ujenzi wa soko la kisasa la samaki lililopo Malindi ambalo itawanufaisha wavuvi wanaotumia bandari hiyo ya Malindi.

Aidha, Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa jengo hilo la soko la kisasa na bandari ya uvuvi linajengwa na Kampuni ya Rinkai Nissan Construction Co. Ltd kutoka nchini Japan ikisaidiana na Kampuni ya SCI Co. Ltd ya Dar es Salaam na Coastal Dredging Co. Ltd ya Zanzibar.

Alisema kuwa ujenzi huo utagharimu TZS  bilioni 26.491 ambapo kati ya fedha hizo bilioni 22.776 ni msaada kutoka Serikali ya Japan kupitia (JICA) na TZS bilioni 3.715 ni kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapo Mkataba wa ujenzi ulifungwa rasmi Machi 26,2019 na ujenzi kuanza mnamo mwezi Juni, 2019.

Alisema kuwa soko hilo linajumuisha sehemu sita za kuendeshea mnada, meza 141 za wauzaji wadogo wadogo kati ya hizo 76 vitakuwa ni vibaraza vya kudumu na 65 ni meza za kuhamisha na sehemu 13 za kuchakatia samaki, mtambo wa barafu chenga wenye uwezo wa kuzalisha tani tatu za barafu kwa masaa 24.

Vile vile, alieleza kuwa soko hilo litakuwa na uwezo wa kuegesha  vyombo vya uvuvi wa kienyeji vipatavyo 24 kwa wakati mmoja ambapo pia, litakuwa na uwezo wa kuchukua wafanyakazi 1,400 kwa siku watakaohusika katika ushushaji na upakiaji samaki.

Pia, Katibu Mariam alisema kuwa soko hilo litakuwa na uwezo wa kutoa huduma kwa wafanyabiashara 6,500 watakaotumia eneo salama ndani ya soko hatua ambayo itakuwa chachu ya kuongeza kipato kwa wavuvi kwa kuwapa fursa ya kuanza kuuza samaki wao kwa wakati muwafaka kutokana na hali halisi ya miundombinu ya soko hilo.

Alieleza kuwa madhumuni ya soko hilo ni kuwawezesha watumiaji wa diko la Malindi kuuza na kununua samaki wao wakiwa katika hali ya ubora na salama kwa afya ya mlaji pamoja na kuwepo mazingira mazuri ya kuweka vyombo vya uvuvi na biashara kwa wavuvi, wachuuzi, madalali, wauzaji wadogo wadogo pamoja na wanunuzi.

Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa soko hilo linatarajiwa kukamilika mnamo mwezi  Oktoba mwaka huu ambapo kutakuwa na kazi ndogo ndogo za kumalizia ambazo zitaufikisha ujenzi huo mwezi wa Januari mwakani.;p

Nae Afisa Mdhamini wa Masuala ya Uchumi na Maendeleo katika Ofisi ya Ubalozi wa Japan nchini Tanzania Bwana Katsutoshi Dakeda ambaye alimuwakilisha Balozi wa Japan nchini Tanzania alisema kuwa  Serikali ya Japan imekuwa mshirika mkuu wa kuisaidia Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Alisema kuwa Serikali ya Japan imekuwa ikisaidia miradi mbali mbali ya maendeleo  ambayo imeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi.

Alisema kuwa mradi wa ujenzi wa soko pamoja na bandari ya Malindi utasaidia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi wa Zanzibar sambamba na kukuza kipato cha wavuvi wa Zanzibar huku akieleza kuwa zaidi ya miaka 50 Japan imekuwa na mashirikiano mazuri na Jamhuri ya Muunganowa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Nae Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) Bwana Matsuyama SATORU alisema kuwa fedha ambazo zimetolewa na Serikali ya Japan kupitia Shirika la (JICA) ni kielezo cha kutosha cha mahusiano na mashirikiano ya muda mrefu yalipo kati ya Japan na Serikali ya Jamhuriya Muungano wa Tanzania.

Alisema kuwa mradi huo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta ya uvuvi hapa Zanzibar hatua ambayo itaimarisha uchumi wa Zanzibar huku akieleza matumaini yake makubwa kuwa mradi huo utaleta tija kubwa kwa wananchi wa Zanzibar. 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.