Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja kwa uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango  kuwa wabunifu katika kuhakikisha mafanikio zaidi yanapatikana ikiwa ni pamoja na kuongeza mapato.

Hayo aliyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi  kwa kipindi cha Julai hadi Disemba kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

Rais Dk. Shein alisema kuwa iwapo suala zima la ubunifu litapewa kipaumbele kwa Wizara hiyo mafanikio Zaidi yataendelea kupatikana hapa nchini hasa ikizingatiwa kuwa Wizara hiyo ndio tegemeo kubwa kwa Serikali na wananchi kutokana na kusimamia miradi muhimu ya maendeleo

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alieleza haja kwa Wizara hiyo kuendelea kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja kwani ni jambo lenye manufaa kwao pamoja na Taifa lao.

Aidha, Rais Dk. Shein aliutaka uongozi wa Wizara hiyo kuendeleza uadilifu, uaminifu,uzalendo pamoja sambamba na kusaidiana na kuendeleza udugu ili kuweza kupata manufaa zaidi katika kazi zao na Taifa kwa ujumla.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza viongozi na wafanyakazi wa Wizara hiyo na kutoa pongezi za pekee kwa Waziri wa Wizara hiyo, Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa kwa kutekeleza vyema majukumu yake kwa kushirikiana na wafanyakazi wa Wizara hiyo.

Dk. Shein alieleza imani yake kwa uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango na kusisitiza haja ya kuendelea kuvumiliana na kushirikiana sambamba na kupendana huku akisisitiza kuwa ataendelea kutumia hekima na busara katika uongozi wake.

Pia, aliipongeza Wizara hiyo kwa kazi nzuri ya uandaaji wa taarifa hiyo pamoja na uwasilishaji wake na kueleza jinsi anavyofarajika na uwasilishwaji mzuri unavyofanywa hivi sasa na Wizara mbali mbali ikilinganishwa na hapo siku za nyuma.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza haja ya usimamizi mzuri wa Maghala ya Serikali na kusisitiza umuhimu wa Wizara hiyo kuyafuatilia Maghala hayo ili kujulikana wasimamizi wake.

Alieleza haja kwa Wizara hiyo kuwatumia watafiti wazalendo kufanya tafiti mbali mbali badala ya kutumia watafiti kutoka nje ya nchi kwani tayari wapo watafiti wazalendo waliobobea katika shughuli hizo hapa hapa nchini hivi sasa.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuweka mikakati maalum ya kuyatangaza maeneo huru ya Vitega uchumi yaliopo hapa Zanzibar likiwemo eneo la Micheweni Pemba.

Akieleza kuhusu Shirika la Bima pamoja na Benki ya Watu wa Zanzibar, Rais Dk. Shein alisisitiza haja  ya kuendelea kushindana kibiashara kwa kupanua huduma zake ndani na nje ya nchi kwa azma ya kufikia lengo lililokusudiwa.

Dk. Shein, alisisitiza juu ya matumizi ya Takwimu pamoja na kuandaa taarifa ya mafanikio yanayotokana na maazimio ya Semina ya Takwimu na matumizi yake iliyofanyika Februari 2, mwaka 2017 iliyowashirikisha viongozi mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huku akieleza haja ya kuwepo mabadiliko katika suala zima la matumizi ya takwimu.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo na kupongeza kwa hatua za Wizara hiyo kwa kutoa mishahara kwa wakati hatua ambayo imekuwa ikitoa faraja kubwa kwa wafanyakazi wa sekta ya umma.

Mapema Waziri wa Wizara hiyo Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa alieleza kuwa  uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa Pato halisi la Taifa na kufikia thamani ya TZS Bilioni 2,684 mwaka 2017 sawa na kasi ya ukuaji wa wastani wa asilimia 7.1.

Alieleza kuwa kendelea kuwepo kwa Amani na utulivuna kuongezeka kwa vivutio vya watalii kumepelekea kuimarika idadi ya wataalii waliotembelea Zanzibar mwaka 2019 kufikia watalii 538,264 kutoka watalii 520,809 mwaka 2018 huku akieleza jinsi ukusanyaji wa mapato ulivyoimarika kwa kiasi kikubwa katika mwaka 2019.

Pamoja na hayo, Balozi Ramia alitumia fursa hiyo kutoa pongezi zinazotolewa na wazee wastaafu kutokana na hivi sasa wastaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wamekuwa wakilipwa Pencheni yao mapema ikilinganishwa na hapo siku za nyuma ambapo hivi sasa wanalipwa kuanzia tarehe 18 ya mwezi kabla ya wafanyakazi wa sekta ya umma.

Balozi Ramia pia, alitumia fursa hiyo kueleza utekelezaji wa miradi mbali mbali ya Wizara ya Fedha na Mipango inavyoendelea kwa kipindi cha Julai hadi Disemba mwaka 2019 ukiwemo mradi wa Uimarishaji Huduma za Jamii Mijini (ZUSP).

Mradi mwengine ni Uwekaji wa Taa za Barabarani Unguja na Pemba, Ujenzi wa Jaa la Kibele,ujenzi wa Ofisi za Serikali, ujenzi wa Mji Mpya wa Kwahani na miradi inayotekelezwa na Mfuko wa Jamii (ZSSF) ukiwemo Michenzani Mall, jengo la Sheikh Thabit Kombo Michenzani, Ofisi ya ZSSF Pemba na mradi wa ujenzi wa Hoteli ya Mkoani.

Mradi mwengine ni ujenzi wa jengo jipya la Ofisi ya Bodi ya Mapato (ZRB) Pemba pamoja na miradi inayotekelezwa na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) ukiwemo ujenzi wa Tawi la Wete, Huduma za Utawala, Huduma za Viza na mradi wa ujenzi wa Ofisi ya Shirika la Bima Pemba.

Nao viongozi wa Wizara hiyo walieleza juhudi zinazochukuliwa katika kufanikisha miradi pamoja na shughuli mbali mbali zinazofanywa na Wizara hiyo kupitia taasisi zake na akutumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa jinsi anavyowaongoza na kuwapa maelekezo.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Khamis Mussa Omar, alitumia fursa hiyo kueleza utekelezaji wa Malengo kwa robo mbili kuanzia mwezi wa Julai hadi Disemba katika mwaka wa fedha wa 2019/2020 kwa Wizara hiyo ambapo kwa upande wa Tume ya Mipango Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Mwita Mgeni Mwita nae alitoa taarifa ya Tume hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.