Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga
(katikati) akijibu baadhi ya hoja zilizoibuka katika kikao cha majadiliano kilichowakutanisha ujumbe wa THBUB na Viongozi
wa LHRC kwenye ofisi za kituo hicho jijini Dodoma leo (Februari 27, 2020).
Kulia ni Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu. Kushoto ni Mkurugenzi
wa Ujenzi wa Uwezo na Ufuatiliaji kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu,
Felista Mauya.
Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew
Mwaimu akiongea katika kikao cha majadiliano
kilichowakutanisha ujumbe wa THBUB na
Viongozi wa LHRC kwenye ofisi za kituo hicho jijini Dodoma leo (Februari 27,
2020). Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC),
Anna Henga.
Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew
Mwaimu (kushoto) akimsikiliza Mkurugenzi wa Ujenzi wa Uwezo na Ufuatiliaji
kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Felista Mauya muda mfupi
baada kumaliza kikao cha majadiliano kilichowakutanisha ujumbe wa THBUB na Viongozi
wa LHRC kwenye ofisi za kituo hicho jijini Dodoma leo (Februari 27, 2020).
Na Mbaraka Kambona,
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
(THBUB) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) wamekubaliana kuandaa mpango wa pamoja wa
kutoa elimu katika mashuleni ili
kuhamasisha na kukuza haki za binadamu nchini.
Makubaliano hayo yalifikiwa na pande
zote mbili baada ya majadiliano yaliyofanyika katika kikao kilichowakutanisha
ujumbe wa THBUB na Viongozi wa LHRC kwenye ofisi za kituo hicho jijini Dodoma
leo.
Akiongea katika kikao hicho, Mkurugenzi
wa Elimu kwa Umma, Mafunzo, Utafiti na Nyaraka wa THBUB, Alexander Hassan alisema
kuwa ili ushirikiano wa THBUB na LHRC uwe na tija ni vyema kuunganisha nguvu katika
maeneo wanayofanya kazi zinazofanana.
Alexander alisema kwakuwa taasisi zote
mbili zimeanzisha Klabu za haki za
binadamu mashuleni ni vyema kuunganisha
nguvu katika maeneo hayo ili kupata matokeo makubwa zaidi.
Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga akichangia
hoja hiyo alisema kuwa suala hilo la kuunganisha nguvu ni zuri na ni muhimu
likafanyiwa kazi kwa haraka na kama uongozi wa THBUB utaridhia basi maafisa wa
pande zote mbili wakutane mapema iwezekanavyo ili kuandaa mpango huo.
Henga alisema kuwa LHRC kwa muda mrefu imekuwa ikitoa elimu
kwa umma kuhusu masuala ya haki za binadamu kwa njia mbalimbali ikiwemo
matumizi ya vyombo vya habari, vipeperushi na mikutano ya hadhara na hivyo
kuwafikia watu wengi lakini ni muhimu kwa sasa kuunganisha nguvu na THBUB ili
kuepuka kutawanya nguvu na rasilimali
kwa mambo ambayo wanaweza kufanya kwa pamoja.
Henga alisema kuwa wamefurahishwa na
kuteuliwa kwa Makamishna wa THBUB kwani kutasaidia wananchi kupata haki zao na
ushirikiano wa wadau utaimarika zaidi.
Alisema kwa kuanza mpango huo itakuwa
vyema kama watashirikiana kwa pamoja kuimarisha elimu ya haki za binadamu
katika klabu za mashuleni kwani wakifanikiwa kuelimisha watoto shuleni wataweza
kusimama na kutetea haki zao wenyewe.
Mwenyekiti wa THBUB, Jaji Mstaafu Mathew
Mwaimu alisema katika kikao hicho kuwa
THBUB inatambua mchango mkubwa wa LHRC
katika kukuza na kutetea haki za binadamu na alimuhakikishia Mkurugenzi wa
kituo hicho kuwa tume itaendelea kushirikiana kwa karibu na kituo hicho kwa
kuwa wote lengo lao ni kusaidia wananchi kupata haki zao.
Aidha, alisisitiza kuwa katika
kutekeleza majukumu yao ni vyema
kujikita kusaidia jamii na serikali kwa ujumla kutekeleza majukumu yake, pale
ambapo serikali inafanya vizuri ni vyema kupongeza na pale inapoonekana
imekosea basi ni vyema kutafuta namna nzuri ya kukosoa.
No comments:
Post a Comment