Mkuu wa Mkoa wa Singida,
Mhe.Dkt.Rehema Nchimbi
(aliyeketi kati kati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo maalum kwa wazalishaji wa mafuta ya alizeti pamoja na wauzaji wa bidhaa za vyakula na vipodozi,
mara baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo yanayofanyika katika ukumbi wa VETA mkoani Singida,
wengine walioketi kulia ni Afisa Biashara wa mkoa wa Singida Bw.Daniel Munyi,
wa pili kutoka kulia ni Meneja wa Mafunzo na Utafiti kutoka TBS, Bw. Hamisi Sudi,
kushoto ni Meneja wa SIDO Singida, Bi Agnes
Yeseya na wa pili kutoka kushoto ni Kaimu Meneja wa kanda ya Kati - TBS Bw.
Sileja Lushibika.
Na
Mwandishi wetu -Singida,
Wazalishaji wa bidhaa mbalimbali mkoani Singida wametakiwa kutambua
kuwa suala la viwango ni la kisheria hivyo ni lazima kuthibitisha ubora wa
bidhaa ili kumlinda mlaji na kupata uhakika wa soko la bidhaa wanazozizalisha.
Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa
wiki na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Dkt
Rehema Nchimbi alipokuwa akifungua mafunzo ya wazalishaji wa bidhaa za vyakula yakiwemo
mafuta ya alizeti na wauzaji wa vipodozi na vyakula yaliyofanyika katika ukumbi
wa VETA mkoani Singida.
Dkt. Nchimbi alisema suala la ubora
wa bidhaa linapaswa kuzingatiwa katika mnyororo wote wa uzalishaji ili mlaji awe salama na kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza kutokana
na kutozingatia viwango.
“Shirika la Viwango Tanzania (TBS)
ndiyo hakikisho la wazalishaji na fursa zinazotengenezwa zitakuwa dhahiri iwapo
masuala ya viwango yatazingatiwa, vilevile TBS ni daraja kati ya mzalishaji na
soko, hivyo mzalishaji ni lazima kufuata utaratibu,” alisisitiza Dkt. Nchimbi.
Alisema maisha ya binadamu ni chakula hivyo ni muhimu kuzingatia
usalama wake, kwani bidhaa hafifu
zinagharimu afya ya walaji na kwamba
magonjwa mengi yanatokana na jinsi tunavyoandaa chakula na tunavyokula, hivyo
wazalishaji wanapaswa kuwa waaminifu katika kuzalisha bidhaa yoyote.
Dkt. Nchimbi alisema TBS siyo
adui wazalishaji hawapaswi kuichukia na wajenge
dhana kuwa TBS ni usama hivyo wazalishaji wa Singida wahakikishe kuwa
wanazalisha bidhaa bora wakati wote ili kudhidhirisha kauli kwamba Singida ni
njema wakati wote.
Akizungumzia kwa upande wa TBS, Dkt.
Nchimbi alisema Shirika linapaswa
kuangalia namna ya kuongea na wajasiriamali ili kuhakikisha kuwa yale
wanayowafundisha wanaelewa kikamilifu. Mafunzo haya yawe na kipimo ili kujua
kama yameeleweka vizuri na kwamba watakaopokea
mafunzo ndiyo watakaowapima.
Kwa upande wake Meneja wa Mafunzo na Utafiti kutoka TBS Bw. Hamisi Sudi
alisema Shirika litaendelea kutoa mafunzo kwa wajasiriamali ili kuhakikisha
kuwa wanazalisha bidhaa kwa kuzingatia viwango.
Alisema Shirika linatambua kuwa wajasiriamali wana mchango mkubwa katika
kukuza pato la taifa na kutengeneza ajira kwa wananchi walio wengi hivyo
Shirika lina mchakato endelevu wa kutoa elimu kwa jamii hasa wajasiriamali
kwakuwa ni mojawapo ya majukumu yake ya kila siku.
Shirika likiwa mkoani Singida
limetoa mafunzo kwa wajasiriamali 221 Katika wilaya za Iramba, Singida na
Manyoni, ambayo pia yamewashirikisha watendaji wa Halmashauri wakiwemo maafisa
Biashara, Maendeleo ya Jamii na Afya pamoja na Maafisa kutoka Shirika la
Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO).
Pia Shirika linatarajia kutoa
mafunzo katika wilaya za Kondoa, Kongwa na ikiwa ni muendelezo wa mafunzo
katika Kanda ya Kati.
No comments:
Post a Comment