HOTUBA YA WAZIRI
MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA KASSIM M. MAJALIWA (MB.),
KUHUSU MAPITIO NA MWELEKEO WA KAZI ZA SERIKALI NA MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA FEDHA ZA OFISI YA WAZIRI MKUU NA OFISI YA BUNGE
KWA MWAKA 2020/2021
UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba kutokana na taarifa
zilizowasilishwa leo katika Bunge lako Tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu
ya Bunge ya Bajeti, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria
na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI zilizochambua
Bajeti ya Mfuko wa Bunge na Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge lako sasa lipokee na
kujadili Taarifa ya Mapitio ya Utekelezaji wa Kazi za Serikali kwa Mwaka
2019/2020 na Mwelekeo wa Kazi za
Serikali kwa Mwaka 2020/2021. Aidha, naomba Bunge lako Tukufu likubali
kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na
Taasisi zilizopo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa Mwaka 2020/2021.
2. Mheshimiwa Spika, wakati tunapojadili Taarifa ya Mapitio ya
Utekelezaji wa Kazi za Serikali kwa Mwaka 2019/2020 na Mwelekeo wa Kazi za
Serikali kwa Mwaka 2020/2021 hatunabudi kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa
rehema kwa kuendelea kutujaalia afya na uzima.
3. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, Bunge lako Tukufu lilimpoteza aliyekuwa Mbunge
wa Jimbo la Newala Vijijini, Mheshimiwa Rashid Ajali Akbar. Pia naungana na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Watanzania wenzangu kutoa
salam za pole kwa familia ya Marehemu na wanachama wa CUF kufuatia kifo cha
aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Taifa Alhaji Khalifa Suleiman
Khalifa. Pia kwa masikitiko makubwa niungane na wananchi wote, familia na
wanahabari wote nchini kwa kifo cha Mwandishi wa Habari Mwandamizi wa Shirika
la Habari Tanzania (TBC) ndugu yetu Marin Hassan Marin kilichotokea leo
alfajiri, Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi – Amina.
Vilevile, Taifa letu lilikumbwa na majanga mbalimbali ikiwa ni pamoja na
mafuriko nchini kote na ajali za barabarani ambazo zilisababisha vifo, majeruhi
na uharibifu wa mali.
4.
Mheshimiwa Spika, sambamba na kutoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki kwa misiba
iliyotokea, tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu awajaalie afya njema waliopata
majeraha na azipumzishe roho za marehemu mahali pema peponi. Amina! Vilevile, nawashukuru kwa dhati
wale wote waliojitolea kwa hali na mali katika kuwasaidia majeruhi na wahanga
wa matukio hayo.
5.
Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu, mwaka huu Serikali ya Awamu ya Tano inahitimisha
kipindi cha kwanza cha miaka mitano kilichoanza Mwaka 2015. Kwa msingi huo,
hotuba yangu itaeleza kwa muhtasari baadhi ya mafanikio makubwa ambayo Serikali
imeyapata katika kipindi cha takriban miaka mitano ya utekelezaji wa Ilani ya
Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
6.
Mheshimiwa Spika, hotuba hii inaainisha baadhi ya kazi zilizotekelezwa na Serikali kwa
kuzingatia mipango na mikakati mbalimbali hususan Mpango wa Pili wa Maendeleo
wa Miaka Mitano wa Mwaka 2016/2017 hadi 2020/2021 ambao ni sehemu ya
utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2025. Mikakati na Mipango
hiyo, inatekelezwa sambamba na mipango mingine ya kikanda na kimataifa kama
vile Agenda ya Mwaka 2063 ya Umoja wa Afrika na Malengo Endelevu ya Umoja wa
Mataifa ya Mwaka 2030.
7.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano, tumeshuhudia
mafanikio makubwa katika kuimarisha miundombinu, huduma za
kiuchumi na kijamii, utawala bora, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi pamoja
na kuhamasisha uwekezaji. Ningependa kutumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wake mahiri wa Serikali ya
Awamu ya Tano katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya
Mwaka 2015 hadi 2020. Nawapongeza pia, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein,
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Mheshimiwa Balozi Seif Ally Idd, Makamu wa Pili wa Rais wa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kusimamia vyema utekelezaji wa Ilani
ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi.
8.
Mheshimiwa Spika, kipekee nakushukuru wewe binafsi, pia Mheshimiwa
Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa kuliongoza vyema Bunge lako Tukufu na
Wabunge wote katika kuisimamia Serikali kuhakikisha kuwa inatekeleza wajibu
wake ipasavyo wa kuhudumia wananchi. Vilevile, natoa shukrani zangu za dhati
kwa Kamati za Kudumu za Bunge kwa kazi kubwa ya kupitia Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara, Mikoa, Wakala, Idara zinazojitegemea na Mamlaka za Serikali
za Mitaa. Kipekee, nawashukuru sana Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Katiba na Sheria chini ya uenyekiti wa Mhe. Mohammed Omary Mchengerwa, Mbunge
wa Jimbo la Rufiji; Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI chini ya
uenyekiti wa Mhe. Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo
Magharibi na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti chini ya uenyekiti wa Mhe.
Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Jimbo la Maswa Magharibi. Maoni na ushauri
wa Kamati hizo umesaidia sana kuboresha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya
Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Mfuko wa Bunge kwa Mwaka 2020/2021.
9.
Mheshimiwa Spika, nawashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu
Mawaziri, Katibu Mkuu Kiongozi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Makatibu Wakuu na
Naibu Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Wakuu wa Idara, Mashirika,
Wakala na Taasisi zote za Serikali kwa ushirikiano mlionipatia
katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Aidha, nawashukuru
wafanyakazi wote wa Serikali na Taasisi zake kwa kutekeleza majukumu yao kwa
weledi mkubwa na hivyo, kuwezesha Serikali kutekeleza kazi zake kwa tija na
ufanisi. Vilevile, nawashukuru kwa michango yenu iliyowezesha kukamilisha
Mpango na Bajeti ya Serikali ya Mwaka 2020/2021.
10.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa, namshukuru Mhe. Jenista
Joakim Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Peramiho na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu); Mhe. Angellah Jasmine
Kairuki, Mbunge wa Viti Maalum na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu
(Uwekezaji); Mhe. Anthony Peter Mavunde, Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini na
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira); Mhe. Stella
Alex Ikupa, Mbunge wa Viti Maalum na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu
(Watu Wenye Ulemavu); Makatibu Wakuu Bw. Andrew Wilson Massawe (Kazi, Vijana,
Ajira na Wenye Ulemavu), Bibi Dorothy Aidan Mwaluko (Sera, Uratibu na
Uwekezaji) na Bw. Tixon Tuyangine Nzunda (Waziri Mkuu na Bunge) na Wakurugenzi,
Wakuu wa Taasisi zilizopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi Binafsi ya Waziri Mkuu na Wafanyakazi wote kwa
ushirikiano mkubwa wanaonipatia katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Waziri
Mkuu.
11.
Mheshimiwa Spika, napenda pia kuwashukuru washirika wa maendeleo
zikiwemo nchi rafiki, taasisi na mashirika ya kimataifa, madhehebu ya dini na
mashirika yasiyo ya kiserikali, kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali
katika kujenga uchumi wa viwanda na kuiletea nchi yetu maendeleo. Mchango wao
umekuwa muhimu kuwezesha nchi yetu kupiga hatua kubwa kimaendeleo kulingana na
mipango tuliyojiwekea.
12.
Mheshimiwa Spika, ninawashukuru wananchi wote kwa kuendelea kuiunga
mkono Serikali ya Awamu ya Tano katika kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Aidha, nawashukuru wananchi wa Jimbo la Ruangwa kwa kuendelea kushirikiana nami
na kwa kuniunga mkono. Niwapongeze na kuwashukuru kwa kutekeleza shughuli za
maendeleo jimboni kwa ufanisi. Kipekee, namshukuru sana mke wangu mpendwa,
Mary; watoto wangu na familia yangu kwa ujumla kwa upendo wao, uvumilivu na
maombi yao wakati wote ninapotekeleza majukumu yangu ya kitaifa. Nawashukuru sana.
Homa Kali ya
Mapafu
13.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa nchi yetu na dunia kwa
ujumla inapitia katika kipindi kigumu. Itakumbukwa kwamba, tarehe 11 Machi 2020, Shirika la Afya Duniani
(WHO) lilitangaza mlipuko
wa Homa Kali ya Mapafu ijulikanayo kama
COVID-19 inayosababishwa na virusi
vya CORONA kuwa ni janga la Kimataifa. Aidha, tarehe 16 Machi, 2020
Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ilitangaza kuwepo kwa mgonjwa wa
kwanza nchini.
14.
Mheshimiwa Spika, tangu kugundulika kwa ugonjwa huo, Serikali inaendelea kuchukua hatua
mbalimbali katika kukabiliana na ugonjwa huu ikiwa ni pamoja na kuimarisha ukaguzi, upimaji na ufuatiliaji wa
wasafiri wanaoingia nchini ili kubaini wasafiri wanaoonesha dalili za ugonjwa
au wenye viashiria hatari hata hivyo mashirika mengi yamesitisha ndege zao kwa
kukosa abiria. Abiria waingiao wote hupelekwa nyumba ya kujitenga kwa gharama
zao, tumetenga na hostel ili kuwapunguzia gharama. Kadhalika, katika
kukabiliana na virusi vya CORONA,
Serikali ilitoa maelekezo yafuatayo:
Moja: Kusitisha Mbio za Mwenge wa Uhuru na kwamba fedha
zilizotengwa kwa ajili ya jukumu hilo zitumike kusaidia hatua za kukabiliana na
janga la virusi vya Corona;
Mbili: Kusitisha michezo yote inayokusanya makundi ya
watu ikiwemo ligi kuu ya Tanzania Bara, ligi daraja la kwanza, ligi daraja la
pili na aina nyingine za michezo;
Tatu: Kusitisha shughuli zote za elimu kuanzia elimu ya
awali, msingi, Sekondari, vyuo vya kati hadi vyuo vikuu;
Nne: Kusitisha Semina, Warsha, Makongamano na Mikutano
yote ya ndani na ya hadhara yenye kuhusisha mjumuiko wa watu wengi;
Tano: Kuwatenga abiria waingiao nchini kwenye maeneo
maalum kwa siku 14 ili kufuatilia hali zao mpaka tutakapojiridhisha kuwa hana
ugonjwa;
Sita: Kuwasisitiza
watanzania kufuata kanuni za kudhibiti maambukizi ikiwemo kunawa maji kwa
sabuni, kukinga unapokohoa na kupiga chafya, kutopeana mikono bila sababu,
kukaa au kusimama kwa umbali na jirani yako n.k; na
Saba: Kuwaasa Watanzania wenye safari zisizo za
lazima kwenye nchi zenye maambukizi ya virusi vya Corona, kusitisha safari
hizo, na hatua zingine zitafuata.
15.
Mheshimiwa Spika, serikali inaendelea na usimamizi wa karibu sambamba na kufanya tathmini na
kuchukua hatua kadhaa. Tumeunda Kamati za kitaifa tatu (3) zinazosimamia
ugonjwa huu, niendelee kusisitiza kuwa sote tuzingatie maelekezo yaliyotolewa
na Serikali toka tulipoanza kampeni ya kupambana na ugonjwa huu. Aidha,
niwatake Watanzania kuzingatia masharti ya afya kwa kufuata ushauri unaotolewa
na wataalam. Mgonjwa akithibitika, atapelekwa eneo maalum bila kujali cheo
chake, atalala palipoandaliwa. Watanzania wenzangu tuendelee kupuuza taarifa za
uzushi zinazosambazwa katika mitandao ya kijamii.
MAFANIKIO YA
SERIKALI YA AWAMU YA TANO
16.
Mheshimiwa Spika, tarehe 20 Novemba 2015 wakati
akifungua rasmi Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania jijini Dodoma, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwaahidi wananchi wote kuwa Serikali ya Awamu ya Tano
itawatumikia na kuwajali.
17.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma hiyo, ndani ya kipindi cha
takriban miaka mitano mafanikio makubwa yamepatikana na yamesaidia kuimarisha
hali ya kiuchumi na kijamii kwenye Taifa letu. Ujenzi wa miundombinu muhimu ya
kiuchumi hususan ya usafiri na usafirishaji sambamba na uimarishaji wa huduma
muhimu za kijamii ni miongoni mwa masuala yaliyopewa kipaumbele na Serikali ya
Awamu ya Tano.
18.
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha kimataifa (Standard Gauge Railway), ufufuaji wa
Shirika la Ndege la Tanzania, ufufuaji wa ushirika na mali za ushirika mfano,
NCU, SHIRECU, WETCU na Mamlaka ya Mkonge Tanzania, ujenzi wa Bwawa la Kufua
Umeme la Julius Nyerere, ulinzi wa maliasili na rasilimali zetu pamoja na
ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya Elimu, Afya na Maji ni kati ya hatua za
msingi zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kufikia uchumi wa
kati unaoongozwa na viwanda ifikapo Mwaka 2025.
19.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki cha miaka mitano, tumeshuhudia
miradi hiyo muhimu ikiwa katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Kwa mfano,
ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha Kimataifa ambao hadi Machi 2020 umetumia
Shilingi trilioni 2.96 na kukamilika kwa asilimia 75 kwa kipande cha Dar es
Salaam hadi Morogoro na asilimia 28 kwa kipande cha Morogoro hadi Makutupora.
20.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatumia gharama kubwa katika kujenga miundombinu hiyo wezeshi ya
kiuchumi kwa lengo la kulifanya Taifa letu kuwa na uchumi imara wa kujitegemea
na wenye kuhimili ushindani. Fedha hizo pia zimekuwa chanzo cha ajira na zabuni
kwa Watanzania zinazowasaidia kuongeza kipato.
21.
Mheshimiwa Spika, mradi huu
utakapokamilika utaongeza ufanisi wa huduma za usafiri na usafirishaji wa
bidhaa na abiria pamoja na kupunguza gharama za uchukuzi. Kadhalika, utachochea
ukuaji wa miji na sekta nyingine kama vile kilimo, viwanda, utalii na biashara.
Vilevile, mradi huu utakuwa chanzo cha ongezeko la mapato ya Serikali
yatakayosaidia katika kuboresha maslahi ya watumishi na huduma za kijamii kama
vile afya, elimu na maji.
22.
Mheshimiwa Spika, vilevile, ujenzi wa Mradi wa Bwawa la Kufua Umeme
wa Maji wa Julius Nyerere ambalo litakapokamilika litazalisha umeme wa Megawati
2,115. Hadi Machi 2020 mradi huo umegharimu Shilingi trilioni 1.28 na
umekamilika kwa asilimia 10.74. Kukamilika kwa bwawa hilo kutalihakikishia
Taifa letu umeme wa uhakika na wa nafuu zaidi. Aidha, ongezeko hilo la
uzalishaji wa umeme litawezesha shughuli za uzalishaji viwandani kuwa za
uhakika, tija, ufanisi na gharama nafuu. Vilevile, mradi huu utachangia kwa
kiasi kikubwa katika juhudi za kuhifadhi mazingira kutokana na kuongezeka kwa
matumizi ya nishati ya umeme kwa watu wengi.
23.
Mheshimiwa Spika, Serikali imefanikiwa kutekeleza Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini
(REA) ambapo vijiji vilivyounganishiwa umeme nchini vimeongezeka kutoka vijiji
2,118 Mwaka 2015 hadi vijiji 9,001 mwezi Machi 2020. Mradi huo pia
umezinufaisha Taasisi 11,128 zikiwemo za elimu, afya, dini, mashine za kusukuma
maji na huduma za biashara.
24.
Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha huduma za usafiri wa anga,
Serikali inaendelea kuliimarisha Shirika la Ndege la Tanzania. Hadi kufikia
Machi, 2020 tayari ndege 8 mpya zenye thamani ya Shilingi trilioni 1.27
zimepokelewa na kuanza kazi. Kadhalika, malipo ya awali ya Shilingi bilioni
85.7 kwa ajili ya ununuzi wa ndege nyingine 3 mpya yamefanyika. Ununuzi wa
ndege hizi, umeongeza ufanisi katika usafiri wa anga, kuongezeka kwa mapato ya
Serikali, kuimarika kwa utalii na kuongezeka kwa fursa za ajira katika sekta ya
huduma.
25.
Mheshimiwa Spika, bajeti ya dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi
imeongezeka kutoka Shilingi bilioni 31 kwa Mwaka 2015 hadi Shilingi bilioni 269
kwa Mwaka 2019. Serikali pia imegharamia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya
afya kwa kujenga zahanati 1,198, ukarabati wa vituo vya afya 487, hospitali za
Halmashauri za Wilaya 69 na hospitali za rufaa za mikoa 10 za Njombe, Simiyu,
Mara, Geita, Songwe, Katavi, Sekou Toure, Mwananyamala, Mawenzi, Manyara,
hospitali za rufaa za kanda 3 za Mtwara, Mbeya na Burigi-Chato na Hospitali
Maalum ya Kibong’oto na Uhuru - Chamwino. Katika kipindi cha Julai 2015 hadi
Januari 2020 jumla ya Shilingi trilioni 3.01 zimetumika kugharamia huduma za
afya.
Kuongezeka kwa bajeti ya dawa na uboreshaji wa miundombinu ya afya,
kumeleta mapinduzi makubwa katika sekta ya afya kwa kuimarisha afya za
Watanzania.
26.
Mheshimiwa Spika, nyote mtakubaliana nami kuwa ujenzi na uboreshaji
wa miundombinu ya afya, ununuzi wa dawa na vifaa vya kisasa vya tiba ni
utekelezaji wa dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuhakikisha
kila Mtanzania anapatiwa haki yake ya kupata matibabu tena katika eneo alipo.
27.
Mheshimiwa Spika, katika eneo la elimu, Serikali imeongeza mikopo kwa
ajili ya elimu ya juu kutoka Shilingi bilioni 365 Mwaka 2015 hadi Shilingi
bilioni 450 Mwaka 2019. Elimumsingi bila Ada nayo imetekelezwa kwa mafanikio
makubwa na kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanaandikishwa na
kupatiwa elimu.
28.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji mzuri wa Mpango wa Elimumsingi bila Ada, uliwezesha
kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi walioandikishwa darasa la kwanza. Kwa mfano,
kabla ya kuanza kwa Mpango huo Mwaka 2015 ni wanafunzi 1,568,378
walioandikishwa. Aidha, baada ya kuanza utekelezaji wa Mpango Elimumsingi Bila
Ada wanafunzi 2,120,667 waliandikishwa Mwaka 2016. Katika kipindi cha mwaka 2015
hadi Februari 2020 jumla ya Shilingi trilioni 1.2 zimetumika kugharamia
Elimumsingi Bila Ada.
29.
Mheshimiwa Spika, maboresho yanayofanyika kwa upande wa elimumsingi yanazingatia uhitaji
wa miundombinu ya kujifunzia na kufundishia. Kuanzia Mwaka 2015 hadi Februari, 2020 vyumba vya madarasa 166,627,
maabara 5,801, nyumba za walimu 57,541, matundu ya vyoo 231,612 yamejengwa na
madawati 2,886,459 yamenunuliwa. Aidha, idadi ya
shule za msingi zenye madarasa ya elimu ya awali imeongezeka kutoka madarasa
16,889 Mwaka 2015 hadi kufikia madarasa 17,771 Mwaka 2020. Kadhalika, idadi ya
shule za sekondari imeongezeka kutoka shule 4,708 Mwaka 2015 hadi shule 5,330
Mwaka 2020.
30.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango wa Elimumsingi Bila Ada
unawahakikishia watoto wote wa kitanzania hususan wale wa hali ya chini kupata
haki yao ya msingi ya kupata elimu. Aidha, Mpango huo umewapunguzia wazazi
mzigo wa ada na michango isiyokuwa ya lazima na hivyo kujielekeza zaidi katika
kutafuta na kuwapatia mahitaji ya msingi vijana wetu kama vile sare za shule na
madaftari.
31.
Mheshimiwa Spika, kama utakavyokumbuka, katika vikao vingi vya Bunge
lako Tukufu vilivyotangulia, changamoto ya maji ni suala lililoongoza
kuchangiwa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge. Katika kipindi cha takribani miaka
mitano, Serikali yetu sikivu ya Awamu ya Tano imetekeleza ujenzi na ukarabati
wa miradi ya maji 1,423. Kati ya miradi hiyo, 792 imekamilika ikihusisha miradi
710 vijijini na miradi 82 mijini. Vilevile, Serikali ilipokea ombi la
Waheshimiwa Wabunge na kuanzisha Mfuko wa Taifa wa Maji na Wakala wa Usambazaji
Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA). Lengo la Serikali ni kuhakikisha
vyombo hivi vinakuwa chanzo cha uhakika cha upatikanaji wa fedha za kugharamia
miradi ya maji na kusimamia utoaji wa huduma ya maji na usafi wa mazingira.
Juhudi hizi kwa pamoja zitasaidia kusogeza huduma ya maji kwa kasi zaidi karibu
na wananchi katika maeneo ya mijini na vijijini.
32.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha takriban miaka
mitano, Serikali imefanikiwa kulinda na kuendeleza rasilimali na maliasili za
Taifa hususan madini na kuhakikisha zinatumika kwa maslahi mapana ya Taifa na
watu wake. Mafanikio hayo, yametokana na Serikali kutekeleza kwa ufanisi mkubwa
Mkakati wa Utekelezaji wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusu Umiliki wa Utajiri
na Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017 na Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu
Masharti Hasi katika Mikataba ya Utajiri na Maliasili za Nchi ya Mwaka 2017.
33.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mkakati na sheria hiyo umechangia
kuongezeka kwa maduhuli ya Serikali yatokanayo na sekta ya madini mwaka hadi
mwaka. Maduhuli ya Serikali yameongezeka kutoka Shilingi bilioni 205.2 Mwaka 2015/2016,
hadi Shilingi bilioni 346.6 Mwaka 2018/2019. Aidha, katika Mwaka 2019/2020
Serikali inatarajia kukusanya Shilingi bilioni 471.
34.
Mheshimiwa Spika, ukusanyaji wa mapato nao
umeongezeka kutoka wastani wa Shilingi bilioni 850 kwa mwezi Mwaka 2015 hadi
kufikia wastani wa Shilingi trilioni 1.3 Mwaka 2019. Ongezeko hili limechangiwa
na hatua za makusudi zilizochukuliwa na Serikali hususan kuimarisha matumizi ya
mifumo ya ukusanyaji mapato kwa njia za kielektroniki, kuongeza idadi ya walipa
kodi na kuibua vyanzo vipya vya mapato. Aidha, ongezeko hilo limekuwa chachu
katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo imesaidia kuimarisha utoaji wa
huduma pamoja na kusogeza huduma hizo karibu na wananchi.
35.
Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kuwashukuru wananchi na walipa
kodi wote kwa kuendelea kuitikia wito wa Serikali wa kulipa kodi kwani hatua
hiyo ni muhimu katika kulifanya Taifa letu kujitegemea. Serikali itaendelea
kusimamia matumizi kwa lengo la kuongeza ufanisi na tija kwa mustakabali wa
maendeleo ya Taifa.
36.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imefanikiwa kudhibiti matumizi ya hovyo ya fedha za Umma kwa kuziba mianya ya ukwepaji
kodi sambamba na kuhakikisha kwamba wale wote wanaotakiwa kulipa kodi wanafanya
hivyo. Kwa mfano, katika kipindi cha miaka mitano (2015 – 2019), Serikali
imeweza kuokoa Shilingi bilioni 19.83
ya mishahara kwa kuwaondoa kwenye mfumo wa malipo watumishi hewa 19,708 na
wenye vyeti vya kughushi 15,411. Msingi huu tunaojenga ni muhimu katika kujenga
uchumi imara na usio tegemezi.
37.
Mheshimiwa Spika, katika siku ya
Mashujaa iliyofanyika kitaifa katika viwanja vya Mashujaa Jijini Dodoma tarehe
25 Julai 2016, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania alitangaza na kusisitiza azma ya Serikali kuhamia Dodoma
ambapo alisema, nanukuu:
“.......ninazungumza kutoka kwenye dhamira yangu kabla
sijamaliza kipindi changu cha miaka mitano Serikali yote itakuwa hapa
Dodoma.....”
38.
Mheshimiwa Spika, ninapenda kuliarifu
Bunge lako Tukufu na watanzania kuwa tayari Serikali imehamia Dodoma. Hadi
Machi 2020, jumla ya watumishi 15,361 wa Wizara na Taasisi za Serikali
wamehamia Makao Makuu ya Serikali Dodoma, ujenzi wa awali wa ofisi za Serikali
katika Mji wa Serikali Mtumba umekamilika, maandalizi ya ujenzi wa majengo ya ofisi
za Serikali awamu ya pili na ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika mji
huo unaendelea. Vilevile, Serikali imekamilisha mapitio ya Mpango Kabambe wa
Jiji la Dodoma ambao niliuzindua tarehe 13 Februari 2020 kwa ajili ya kusimamia
shughuli za upangaji wa Jiji la Dodoma. Naielekeza Halmashauri ya Jiji la
Dodoma kusimamia ipasavyo utekelezaji wa mpango huo ili kuhakikisha Jiji la
Dodoma linaendelezwa kwa kuzingatia Mpango huo.
39.
Mheshimiwa Spika, nyote mtakubaliana nami kuwa
Serikali ya Awamu ya Tano imefanikiwa katika usimamizi madhubuti wa sheria,
kanuni na taratibu za uwajibikaji wa viongozi na watumishi wa umma. Usimamizi
huo, umewezesha viongozi na watendaji wa umma kuwajibika ipasavyo kwa wananchi
ambao ndiyo waajiri wao. Sambamba na hilo, nidhamu Serikalini imeongezeka
kutokana na Serikali kuwachukulia hatua za
kinidhamu watumishi wazembe, wadanganyifu na wasio waadilifu.
40.
Mheshimiwa Spika, tunapotaja mafanikio haya tuna kila sababu ya
kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kwani uongozi wake mahiri na wenye uthubutu ndiyo msingi
mkuu wa mafanikio yaliyopatikana. Dhana na falsafa aliyojenga ya Hapa Kazi Tu imesaidia kubadili mtazamo
wa Watanzania wengi ambapo sasa tunashuhudia uwajibikaji wa kiwango cha juu wa
mtu mmoja mmoja, katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na uzalishaji iwe
shambani, ofisini, kiwandani, sokoni na kwingineko badala ya tabia ya awali ya
baadhi ya wananchi wachache kupoteza muda mwingi katika shughuli zisizokuwa na
tija kwa Taifa.
41.
Mheshimiwa Spika, mafanikio haya
katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na uboreshaji wa huduma za jamii
yameenda sambamba na uzalishaji wa ajira zipatazo milioni 12.6 zikiwemo ajira za moja kwa moja milioni 11.7 kwenye
sekta mbalimbali nchini. Kwa mfano:
·
Sekta za Afya, Elimu na Utawala zimetoa ajira za kudumu kwa kuajiri
watumishi 28,403 katika mamlaka za Serikali za Mitaa,
·
Mradi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa umewezesha kuzalishwa ajira
zipatazo 13,177 za kitaalam na
zisizo za kitalaam. Kati ya hizo, ajira za kitaalam kwa wazawa ni asilimia
46.5. Pia kupitia mradi huu kumekuwa na utoaji wa zabuni zenye thamani ya
Shilingi bilioni 664.7 kwa wazabuni na wakandarasi wa ndani 640,
·
Mradi wa umeme wa mwalimu
Nyerere kupitia maporomoko ya mto Rufiji umezalisha jumla ya ajira 3,897 ikiwemo ajira za wazawa
3,422,
·
Ufufuaji wa shirika la ndege
la Tanzania (ATCL) pamoja na kuboresha viwanja vya ndege jumla ya ajira 2,970,
·
Ujenzi wa Viwanda nchini jumla
ya ajira zilizozalishwa ni 41,900.
·
Ujenzi na uboreshaji wa
miundombinu mbalimbali ikiwemo Hospitali za Wilaya, vituo vya afya, Zahanati,
Madarasa, Nyumba na majengo maeneo mapya ya utawala, Miradi ya barabara chini
ya TARURA kwa kutumia force Account jumla
ya mafundi 845,348 walipata ajira za mikataba na muda.
42.
Mheshimiwa Spika, baada ya kueleza mafanikio hayo, nyote ni mashuhuda kwamba Chama Cha Mapinduzi kiliahidi na
kimetekeleza kwa vitendo na ndiyo maana kinaendelea kuwa Chama cha mfano na cha
kuigwa siyo tu Nchini, bali hata katika Bara la Afrika. Hata hivyo,
mafanikio mengine yataelezwa kwa kina wakati Mawaziri watakapokuwa
wanawasilisha hotuba za bajeti za Wizara zao.
43.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa taarifa kuhusu utekelezaji wa
Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2019/2020 na shughuli zitakazotekelezwa na
Serikali katika Mwaka 2020/2021.
MPANGO
WA MAENDELEO NA BAJETI YA MWAKA 2020/2021
44.
Mheshimiwa Spika, Mapendekezo ya Bajeti ya Serikali ya Mwaka 2020/2021 yamezingatia Sera na Miongozo ikiwa
ni pamoja na Mpango wa Maendeleo
wa Taifa wa Mwaka 2020/2021. Mpango huu ni wa mwisho katika mfululizo wa
mipango ya kila mwaka wa kutekeleza Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano (2016/2017
– 2020/2021) wenye dhima ya Kujenga Uchumi wa Viwanda ili Kuchochea Mageuzi ya
Uchumi na Maendeleo ya Watu.
45.
Mheshimiwa Spika, Mpango wa Maendeleo na
Bajeti wa Mwaka 2020/2021 umezingatia yafuatayo: Dira ya Taifa ya Maendeleo ya
Mwaka 2025 yenye lengo la kuiwezesha Tanzania kuwa Nchi ya hadhi ya uchumi wa
kipato cha kati inayoongozwa na viwanda ifikapo Mwaka 2025; Mpango wa Pili wa
Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, 2016/2017 – 2020/2021; Sera na Mikakati
mbalimbali; Malengo ya Maendeleo Endelevu na Makubaliano ya Kikanda na
Kimataifa ambayo Serikali imeyaridhia. Aidha, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha
Mapinduzi ya Mwaka 2015 - 2020 imezingatiwa pamoja na Maelekezo ya Serikali
yaliyoainishwa na Mheshimiwa Rais wakati wa uzinduzi rasmi wa Bunge la 11 mwezi
Novemba 2015. Vilevile, Mpango umezingatia hali halisi ya utekelezaji wa Mpango
wa Maendeleo wa Mwaka 2019/2020; changamoto zilizojitokeza; hali ya uchumi
kitaifa, kikanda na kidunia kwa Mwaka 2019 na maoteo ya ukuaji wa uchumi kwa
Mwaka 2020.
46.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kueleza kwa kifupi vipaumbele vya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2020/2021 ambavyo
vimejikita katika masuala makuu manne yafuatayo: Ujenzi wa Msingi wa Uchumi wa
Viwanda; Kufungamanisha ukuaji
wa uchumi na maendeleo ya watu; Uboreshaji wa mazingira wezeshi kwa uendeshaji
wa biashara na uwekezaji na Kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa Mpango wa
Maendeleo. Katika kufikia malengo ya Mpango, Serikali itaendelea kutoa
kipaumbele cha pekee katika kutekeleza miradi ya kielelezo ya kimkakati ikiwa
ni pamoja na: Ujenzi wa Reli ya Kati ya Kiwango cha Kimataifa; Mradi wa kufua
umeme wa Maji wa Julius Nyerere – MW 2,115; Kuboresha Shirika la Ndege la
Tanzania (ATCL); Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi kutoka Hoima (Uganda)
hadi Tanga (Tanzania); Uanzishwaji wa kanda maalum za Kiuchumi na Kusomesha
wataalam wengi zaidi katika fani za Ujuzi Adimu na Maalum. Hatua hizo,
zitasaidia kufungamanisha ujenzi wa miundombinu wezeshi na sekta nyingine za
kiuchumi ili kuongeza kasi ya maendeleo, ajira na kipato na hatimaye
kuliwezesha Taifa kupiga hatua kubwa za kimaendeleo.
47.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kutoa rai kwa
Wafanyabiashara, Wawekezaji, Wajasiriamali, Wabunge, Viongozi na Watendaji wa
Serikali, Taasisi za Dini, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, na Wananchi
wote kwa ujumla, kushirikiana na Serikali bega kwa bega katika kutekeleza
Mpango huu ili azma ya kufikia uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda ifikapo
Mwaka 2025 iweze kutimia.
HALI YA UCHUMI
48.
Mheshimiwa Spika, uchumi wa Taifa
umeendelea kuimarika ambapo katika kipindi cha Januari hadi Septemba 2019,
ukuaji halisi wa Pato la Taifa ulifikia asilimia 6.9. Baadhi ya shughuli
zilizochangia ukuaji huo kwa viwango vikubwa ni pamoja na ujenzi asilimia 14.8;
uchimbaji wa madini na mawe asilimia 12.6; habari na mawasiliano asilimia 11.0;
uchukuzi na uhifadhi wa mizigo asilimia 8.8 na huduma za usambazaji maji
asilimia 8.5.
49.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia Julai
hadi Januari 2020, mfumuko wa bei ulikuwa wastani wa asilimia 3.7. Kiwango hiki
ni chini ya lengo la Taifa la kipindi cha muda wa kati la asilimia 5.0, na
chini ya malengo ya asilimia 7.0 kwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa
Afrika (SADC) na asilimia 8.0 kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hali
hii inatokana na utekelezaji madhubuti wa sera za fedha na za bajeti,
uhakika wa upatikanaji wa chakula na utulivu wa thamani ya Shilingi ya Tanzania
dhidi ya sarafu nyingine duniani.
50.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha sekta za uzalishaji na utoaji huduma ili
kuongeza kasi ya ukuaji wa Pato Halisi la Taifa. Vilevile, Serikali itaendelea
kutekeleza mikakati na sera za uchumi jumla ili kudhibiti kasi ya mfumuko wa
bei na kuwa na mwenendo tulivu wa uchumi. Serikali pia, itaendelea kuimarisha Mfumo wa Serikali wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato (GePG) kwa
kuharakisha ufungaji wa mfumo huo katika wizara na taasisi za Serikali.
HALI YA SIASA
51.
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imeendelea kusimamia utekelezaji wa
sheria na maadili ya vyama vya siasa ili kuhakikisha demokrasia ya vyama vingi
inaimarika pamoja na kudumisha amani, utulivu na mshikamano uliopo katika nchi
yetu.
52.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa itaendelea kusimamia
utekelezaji na utoaji elimu kuhusu Sheria ya Vyama vya Siasa, Kanuni za Maadili
ya Vyama vya Siasa, pamoja na Sheria ya Gharama za Uchaguzi katika Uchaguzi Mkuu wa
Mwaka 2020. Vilevile, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa itaendelea kufuatilia
uhai wa Vyama vya Siasa vyenye usajili wa kudumu kwa lengo la kuwawezesha
wananchi kushiriki na kutoa michango yao ya mawazo na fikra kupitia vyama hivyo
ili kuimarisha demokrasia na maendeleo nchini.
Uchaguzi wa
Serikali za Mitaa
53.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeratibu na kusimamia
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika tarehe 24 Novemba 2019. Uchaguzi huo
ulihusisha Mitaa 4,263, Vijiji 12,319 na Vitongoji 64,384. Katika uchaguzi huo,
Chama Cha Mapinduzi kilipata ushindi wa kishindo wa asilimia 99.9 kwa nafasi
zote zilizogombewa. Matokeo hayo yameendelea kudhihirisha imani kubwa
waliyonayo wananchi kwa Chama Cha Mapinduzi. Hivyo, basi natoa rai kwa wananchi
kuendelea kushirikiana na viongozi waliochaguliwa ili kutimiza azma ya
kuwaletea maendeleo.
Maandalizi ya
Uchaguzi Mkuu
54.
Mheshimiwa Spika, Tume ya Taifa ya Uchaguzi
imeanza maandalizi ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba 2020. Pamoja na
mambo mengine, maandalizi hayo yanahusisha Zoezi la Kuboresha Daftari la Kudumu
la Wapiga Kura lililofanyika nchi nzima. Awamu ya kwanza ilizinduliwa
tarehe 18 Julai, 2019 Mkoani Kilimanjaro na kukamilika tarehe 23 Februari, 2020
katika Mkoa wa Dar es Salaam.
55.
Mheshimiwa Spika, uboreshaji wa
daftari hili ulihusisha: Uandikishaji wa Wapiga Kura wapya ambao wametimiza
umri wa miaka 18 au watatimiza umri huo ifikapo siku ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka
2020; urekebishaji wa taarifa za Wapiga Kura walioandikishwa katika Uchaguzi
Mkuu wa Mwaka 2015 pamoja na ufutaji wa taarifa za Wapiga Kura waliopoteza sifa
za kuwemo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
56.
Mheshimiwa Spika, katika zoezi hilo,
jumla ya Wapiga Kura 10,285,732 wameandikishwa na kati yao, Wapiga
Kura wapya ni 7,043,247, Wapiga Kura walioboreshewa taarifa zao ni 3,225,778 na
Wapiga Kura waliofutwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kutokana na
kupoteza sifa ni 16,707. Zoezi
la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Awamu ya Pili
linatarajiwa kuanza tarehe 5 Aprili 2020 na kukamilika tarehe 26 Juni 2020.
Zoezi hili litaenda sambamba na uhakiki wa taarifa za wapiga kura katika
daftari hilo. Natoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na
kuboresha taarifa zao katika daftari hilo, ili waweze kutumia haki yao ya
Kikatiba ya kuchagua viongozi wanaowataka.
57.
Mheshimiwa Spika, niwasihi Watanzania kushiriki kikamilifu kwenye Uchaguzi Mkuu ujao kwa
kufuata sheria, kanuni na taratibu za Nchi. Viongozi wa Vyama vya Siasa waoneshe
mfano wa kuendesha siasa za kistaarabu zenye lengo la kuwaunganisha watanzania
na siyo kuwatenganisha. Hakuna kiongozi aliyewahi kupata sifa nzuri kwa kuwa
chanzo cha mifarakano. Hivyo basi, tudumishe utulivu, amani, mshikamano pamoja
na ustaarabu wetu wa kitanzania katika kipindi chote cha kampeni na Uchaguzi
Mkuu ili kulifanya Taifa letu kuendelea kuwa kisiwa cha amani na mfano wa
kuigwa barani Afrika na duniani kwa ujumla.
BUNGE
58.
Mheshimiwa Spika, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania limeendelea kutimiza wajibu wake wa kikatiba na kikanuni kwa kufanya
mikutano mitatu na huu ukiwa ni wa nne kwa mwaka 2019/2020. Ofisi ya Bunge kwa sasa inatekeleza shughuli za Bunge
kwa kutumia TEHAMA kupitia mfumo wa Bunge Mtandao (e-Parliament) uliotengenezwa na kusimamiwa na wataalam wa ndani wa
Ofisi ya Bunge. Hivi sasa Wizara, Idara na Taasisi za Serikali zinawasilisha
taarifa na nyaraka mbalimbali Bungeni kwa kutumia nakala tete badala ya nakala
ngumu. Hatua hii imeweza kupunguza
gharama za uendeshaji hivyo kuokoa kiasi kikubwa cha fedha cha takribani
Shilingi bilioni 2 kilichokuwa
kinatumika kila mwaka katika uandaaji na uhifadhi wa nyaraka mbalimbali
zinazoandaliwa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Bunge. Pia,
Ofisi ya Bunge imeweza kuzindua
‘Bunge Mobile Application’ ambayo
imewezesha Waheshimiwa Wabunge pamoja na wadau mbalimbali kupata kwa urahisi
taarifa mbalimbali kama vile orodha ya shughuli za Bunge (Order Paper), Hansard pamoja na sheria na miswada. Ni matumaini
yangu kwamba Bunge lako Tukufu litaendelea kuisimamia Serikali ili itekeleze
majukumu yake ipasavyo.
MAHAKAMA
59.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa gharama
nafuu, Mahakama imeendelea kuimarisha huduma kwa kuweka mifumo na taratibu
mbalimbali za kuwafikia wananchi katika maeneo yote nchini ili kupunguza
mlundikano wa mashauri. Mojawapo ya utaratibu unaotumika ni kuwatumia Mahakimu wenye Mamlaka ya Ziada (Extended Jurisdiction) kusikiliza mashauri ya Mahakama Kuu ambapo
Mahakimu 195 walipewa Mamlaka hiyo ya ziada. Katika kipindi cha Mwaka 2019 mashauri 1,132 yalisikilizwa na kumalizwa kwa
utaratibu huo.
60.
Mheshimiwa Spika, Mahakama imeendelea kuboresha miundombinu katika
ngazi mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa majengo.
Katika kutekeleza hilo, ujenzi wa majengo ya Mahakama Kuu katika Mikoa ya
Kigoma na Mara, Mahakama ya Hakimu Mkazi katika Mikoa ya Simiyu, Manyara,
Geita, Njombe, Mahakama za Wilaya 14, pamoja na Mahakama za Mwanzo za Mlowo, Magoma, Uyole, Mtowisa, Msanzi
na Mkunya umekamilika.
61.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kulinda,
kuheshimu na kuzingatia haki za binadamu na kuimarisha mifumo ya usimamizi wa
sheria na utoaji Haki kwa kutumia TEHAMA. Vilevile, Serikali itaendelea kufanya
maboresho katika mfumo wa Haki Jinai ili kuwezesha shughuli za uchunguzi,
upelelezi, uendeshaji wa mashauri na usikilizaji wa mashauri kufanyika kwa
ufanisi.
UWEKEZAJI
62.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuratibu na kusimamia shughuli za kuhamasisha na kufanikisha
wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuvutia mitaji, teknolojia na
ujuzi ambao ni chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali. Serikali imeendelea
kuhakikisha mazingira ya uwekezaji na biashara
yanakuwa rafiki.
63.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutumia vyema
uwepo wa fursa nyingi za uwekezaji na kuwepo kwenye eneo la
kimkakati la kijiografia kwa kuhudumia nchi zipatazo 6 ambazo hazipo kwenye
mwambao wa bahari. Hali hii inaifanya nchi yetu kuwa lango la biashara ya
kimataifa hususani katika ukanda wa nchi za Afrika Mashariki na Kati pamoja na
Kusini mwa Afrika. Aidha, Serikali inaendelea kuboresha mazingiza ya uwekezaji
na biashara ikiwemo kufanya tathmini ya utekelezaji wa Sera ya Taifa ya
Uwekezaji ya Mwaka 1996 ili kubaini changamoto za kisera, kisheria na
kiutendaji zitakazopelekea kuhuisha Sera ya Uwekezaji ya Mwaka 1996 na Sheria
ya Uwekezaji ya Mwaka 1997.
64.
Mheshimiwa Spika, vilevile, Serikali imeendelea kuratibu utekelezaji wa Kuboresha Mfumo wa Udhibiti wa Biashara (Blueprint) ambapo kupitia Mpango huo Serikali imefuta tozo mbalimbali 54 katika Mwaka wa Fedha
2019/2020 pamoja na kuondoa mwingiliano wa majukumu kati ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS)
na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ili kurahisisha shughuli za uwekezaji
na biashara.
65.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2019/2020 Serikali pia imeratibu mikutano ya mashauriano kati yake na wawekezaji na
wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kusikiliza na kutatua
changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo. Katika mikutano hiyo hoja nyingi na
changamoto zilipatiwa ufumbuzi na nyingine kutolewa ufafanuzi ambapo pia
wafanyabiashara na wawekezaji walikumbushwa wajibu wao katika uendeshaji
biashara na uwekezaji wao.
66.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) kwa kushirikiana na
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iliendesha mikutano
kati ya Serikali na wawekezaji kutoka China, Uingereza na Marekani waliowekeza
hapa nchini. Kwa nia ya kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili na
kupata maoni na ushauri zaidi.
67.
Mheshimiwa Spika, katika kuongeza
njia za kushughulikia malalamiko ya wawekezaji, Serikali kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta
Binafsi Tanzania (TPSF) imeandaa mfumo wa kielektroniki wa kupokea malalamiko
na kupata mrejesho wa wawekezaji (Online
Complaints and Feedback Platform) ambao utaanza kutumika katika Mwaka
2020/2021. Mfumo huo utapokea maoni na ushauri kwa njia ya haraka na kuleta
ufanisi katika kuwahudumia.
68.
Mheshimiwa Spika, Mazingira ya uwekezaji na
ufanyaji biashara nchini yameendelea kuimarika. Taarifa ya Benki ya Dunia ya
Wepesi wa Kufanya Biashara (Ease of Doing
Business Report) ya Mwaka 2020 iliyotolewa Oktoba 2019 inaonesha kuwa
Tanzania imepanda kwa nafasi tatu (3) kutoka nafasi ya 144 hadi kufikia nafasi
ya 141. Lengo letu ni kufikia nafasi ya juu kufikia Mwaka 2025. Naziagiza
Wizara na Taasisi zote za Serikali zinazohusika na utekelezaji wa maboresho na
kuweka mazingira mazuri na rafiki ya kuratibu kwa ukaribu ili kufungua fursa
zaidi.
69.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa kukuza uwekezaji,
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuhamasisha Mikoa yote nchini kuandaa Makongamano ya Uwekezaji sambamba na kuzindua
Miongozo ya Uwekezaji ya Mikoa inayobainisha fursa za uwekezaji za Mikoa pamoja
na maeneo ya uwekezaji yaliyotengwa ili kuhamasisha na kuvutia uwekezaji zaidi
katika Mikoa hiyo. Hadi sasa, Mikoa 14 ya Ruvuma, Songwe, Pwani, Lindi, Kagera,
Mtwara, Geita, Kilimanjaro, Simiyu, Manyara, Dodoma, Mwanza, Kigoma na Morogoro
imezindua miongozo hiyo. Mikoa yote ambayo haijakamilisha kuandaa miongozo hiyo
ifanye hivyo kabla ya Septemba 2020.
70.
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuratibu makongamano ya uwekezaji
yaliyofanyika hapa nchini kama vile Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya
Tanzania na Uganda, Tanzania na Afrika
Kusini; Afrika Mashariki na Sweden na Makongamano mengine yaliyofanyika nje ya
Nchi kama vile Tanzania na Burundi; “Investment for Africa” lililofanyika
nchini Misri; Kongamano lililoandaliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)
lililofanyika Afrika Kusini; na Kongamano kati ya Pakistani na Afrika
lililofanyika nchini Kenya. Tumeendelea kupokea wawekezaji wanaofika nchini kwa
ajili ya kutafuta fursa za uwekezaji kutoka Nchi mbalimbali.
71.
Mheshimiwa Spika, Serikali inahakikisha maeneo ya uwekezaji yanatengwa na kuendelezwa kwa
kuwekewa miundombinu ya msingi ya maji, umeme, mawasiliano na barabara. Hadi
Februari 2020, jumla ya hekta 854,821.61 zimetengwa kwa ajili ya uwekezaji
katika Halmashauri zote nchini.
72.
Mheshimiwa Spika, kupitia kitengo cha Huduma za Mahala Pamoja (One Stop Facilitation Centre) kilichopo Kituo cha Uwekezaji
Tanzania (TIC) chenye watendaji kutoka Taasisi 10 wameendelea kutoa huduma za
muda mfupi kwa wawekezaji wetu kupitia Kituo hicho hadi kufikia Februari 2020,
jumla ya miradi 146 yenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 1,514.57
inayotegemewa kutoa ajira za moja kwa moja zipatazo 26,384 ilisajiliwa ambapo
miradi 52 sawa na asilimia 36 inamilikiwa na wageni, miradi 50 sawa na asilimia
34 inamilikiwa na Watanzania na miradi 44 sawa na asilimia 30 inamilikiwa kwa
ubia kati ya wageni na Watanzania. Katika miradi iliyosajiliwa katika Mwaka huu
wa Fedha miradi 95 sawa na asilimia 65 ya miradi yote inahusisha sekta ya
uzalishaji viwandani.
SEKTA
ZA UZALISHAJI
Viwanda
73.
Mheshimiwa Spika, kwa
kutambua umuhimu wa viwanda Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti ili kuwezesha sekta hii
kukua kwa haraka na kutoa mchango mkubwa zaidi katika Pato la Taifa pamoja na
kupunguza umaskini. Katika kutekeleza dhana hii kwa vitendo katika mwaka
2019/2020, Serikali iliimarisha kiwanda cha Ngozi na Bidhaa za Ngozi cha
Karanga (Moshi) na kuimarisha Shirika la Nyumbu (Pwani) ili kuongeza uzalishaji
ikiwemo wa magari ya zimamoto. Vilevile, ada na tozo 54 zilifutwa ili kuondoa
kero na urasimu kwa wafanyabiashara na wawekezaji katika sekta hii. Aidha,
uzalishaji katika baadhi ya viwanda ulianza ikiwa ni pamoja na Pipe Industries
Co. Limited (Dar es Salaam), Kiwanda cha Chai cha Kabambe (Njombe), kiwanda cha
Yalin Cashewnut Co. Limited (Mtwara), kiwanda cha 21st Century Food
and Packaging (Dar es Salaam), kiwanda cha kusaga mahindi (MeTL, Dar es
Salaam), kiwanda cha bidhaa za plastiki cha Plasco Pipelines Co. Ltd (Dar es
Salaam), kiwanda cha kupakia na kuhifadhi parachichi, Rungwe Avocado na kiwanda
cha kuchakata parachichi kwa ajili ya kutengeneza mafuta (KUZA Afrika).
74.
Mheshimiwa Spika, kutokana na jitihada kubwa zinazoendelea kufanywa na Serikali za
kujenga uchumi wa viwanda, jumla ya viwanda vipya zaidi ya 4,000 vimejengwa
katika mikoa mbalimbali. Viwanda vilivyojengwa vinazalisha bidhaa za ujenzi;
pamoja na viwanda vya kusindika mazao ya kilimo ikiwemo nafaka, matunda, mafuta
ya kupikia na bidhaa za ngozi. Ujenzi wa viwanda vipya nchini, katika kipindi
cha Serikali ya awamu ya tano, umechangia kupatikana kwa ajira mpya 482,601
nchi nzima.
75.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuondoa kero
zinazokwamisha ufanisi na ukuaji wa sekta ya viwanda. Aidha, Serikali
itaimarisha ushindani katika soko kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani
sawa hususan wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi kama vile nondo, mabomba ya
plastiki, nguo na mavazi, bidhaa za ngozi na marumaru. Lengo ni kuimarisha
msingi wa ukuaji wa sekta ya viwanda nchini pamoja na kuvutia sekta binafsi
kuwekeza au kushirikiana na Serikali kuwekeza kwenye viwanda.
Kilimo
76.
Mheshimiwa Spika, sekta ya kilimo ni muhimu katika kuhakikisha usalama wa chakula,
kupambana na umaskini, kuongeza ajira pamoja na kuleta maendeleo ya Nchi kwa
ujumla. Kwa kulitambua hilo, Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kutoa
kipaumbele kikubwa kwenye sekta hiyo kwa lengo la kuwawezesha wakulima kupata
pembejeo na zana za kisasa ili kuongeza tija katika kilimo na hivyo kuleta
mageuzi ya kiuchumi.
Hali ya Upatikanaji wa Chakula
77.
Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mengine
hususan kuimarika kwa hali ya hewa, mageuzi yanayofanywa katika sekta ya
kilimo, yamechangia kuimarika kwa hali ya upatikanaji wa chakula nchini na
upatikanaji wa malighafi za viwanda, sambamba na kuongeza tija kwa wakulima.
Katika msimu wa kilimo wa Mwaka 2018/2019, uzalishaji wa mazao ya chakula
kitaifa ulikuwa tani milioni 16.3 ikilinganishwa na
mahitaji halisi ya tani milioni 13.6. Uzalishaji huo umeihakikishia Nchi utoshelevu wa
chakula kwa asilimia 118 kwa msimu wa kilimo wa Mwaka
2019/2020.
Upatikanaji wa Pembejeo
za Kilimo
78.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea
kuhamasisha matumizi ya pembejeo na mbinu bora za kilimo na teknolojia kwa
lengo la kukifanya kilimo chetu kuwa cha kisasa zaidi na chenye tija. Hadi
kufikia Februari 2020, upatikanaji wa mbegu bora za mazao umefikia tani 71,207
ikilinganishwa na tani 57,023 za msimu wa Mwaka 2018/2019. Kati ya mbegu hizo,
tani 66,031 zimezalishwa nchini ambayo ni sawa na asilimia 93 na tani 5,175
sawa na asilimia 7 zimeingizwa kutoka nje ya nchi.
79.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea
kuimarisha upatikanaji wa mbolea nchini kwa kutumia Mfumo wa Ununuzi wa Mbolea
kwa Pamoja ambao umesaidia kupunguza bei ya mbolea kwa wakulima. Kutokana na
mfumo huo, upatikanaji wa mbolea hadi Februari 2020 umefikia tani 516,813 sawa
na asilimia 89 ya lengo la tani 586,604. Kwa kuwa mbolea hizo hutumika
kulingana na hatua mbalimbali za ukuaji wa mazao, Serikali inaendelea
kuhakikisha asilimia 11 iliyobaki inapatikana na kusambazwa kwa wakulima kwa
wakati. Aidha, Serikali imeendelea kuratibu upatikanaji wa viuatilifu ambapo
hadi Januari 2020, jumla ya tani 8,719 za viuatilifu zimeingizwa nchini ili
kudhibiti visumbufu vya mimea na mazao.
Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB)
80.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai
2019 hadi Februari 2020, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), imetoa
mikopo ya Shilingi bilioni 34 kwa miradi ya kilimo 38 na kufanya jumla ya
mikopo iliyotolewa kufikia Shilingi bilioni 160.6 toka Benki ilipoanza utoaji
wa mikopo. Mikopo iliyotolewa imewanufaisha wakulima wadogo, wa kati na wakubwa
wapatao milioni 2.1 wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi pamoja na viwanda
vidogo vya uchakataji wa mazao.
81.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho TADB
imetoa mikopo ya ziada ya Shilingi bilioni 31.77 kupitia Mfuko wa Dhamana kwa
Wakulima Wadogo. Mikopo hiyo imewanufaisha wakulima wapatao 5,080, biashara
ndogo na za kati za kilimo zipatazo 30, Vyama vya Msingi (AMCOS) 20 katika
mikoa mbalimbali nchini pamoja na kufanikisha ununuzi wa matrekta 19 katika
mikoa hiyo.
Uzalishaji wa Zao la Chikichi
82.
Mheshimiwa Spika, Serikali imedhamiria kumaliza tatizo la upatikanaji wa mafuta ya kula
nchini kwa kuendeleza zao la chikichi sambamba na mazao mengine yanayozalisha
mafuta. Uendelezaji wa zao la chikichi unahusisha kupanda kwa wingi miche mipya
yenye uzalishaji wenye tija. Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo
nchini (TARI) imeanza uzalishaji wa mbegu bora za
chikichi aina ya TENERA inayotoa mafuta mengi. Lengo ni kuzalisha mbegu bora na
za kutosha zitakazowezesha wakulima kuongeza uzalishaji na hivyo kujiongezea
kipato na kupunguza matumizi ya fedha za kigeni kuagiza mafuta ya kula kutoka
nje ya nchi.
83.
Mheshimiwa Spika, hadi tarehe 15 Februari 2020, mbegu 1,525,017 zimezalishwa ambazo
zitatosha kupanda eneo la ekari 30,500. Tayari mbegu 1,026,111 zimesambazwa kwa
ajili ya kuziotesha ili miche bora iweze kusambazwa kwa wakulima. Usambazaji
kwa ajili ya uoteshaji umefanyika katika halmashauri za mkoa wa Kigoma na
taasisi nyingine ikiwemo Magereza ya Kwitanga na Ilagala na JKT Bulombora.
84.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha huduma za ugani,
kilimo cha umwagiliaji, ushirika na upatikanaji wa pembejeo ikiwa ni pamoja na
mbegu bora za mazao. Aidha, itajenga na kukarabati miundombinu ya kuhifadhi
mazao ya kilimo na masoko.
Zao la Mkonge
85.
Mheshimiwa Spika, sote ni mashahidi kuwa zao la Mkonge lilikatiwa tamaa na wakulima na
wakulima wengi waliacha kulima zao hili. Serikali imeanza kuchukua hatua za
kufufua kilimo cha Mkonge na masoko yake. Tunafufua mamlaka ya Mkonge ili
itambue mashamba yake na mali zingine ili ianze kuhamasisha wakulima wadogo na
wakubwa na kukaribisha uwekezaji wa sekta ya Mkonge. Tunaimarisha Taasisi ya
Utafiti ya Mlingano ili izalishe miche zaidi na kuisambaza kwa wakulima. Natoa
wito kwa Wizara, Wakuu wa Mikoa inakolima Mkonge kutambua wakulima wa Mkonge na
wapate msaada wa kitaalam.
Mifugo
86.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuimarisha sekta ya mifugo nchini ili iweze kutoa
mchango mkubwa zaidi katika Pato la Taifa na kutoa fursa za ajira. Ili kufikia lengo hili, Serikali imehamasisha wafugaji kuendelea
kuimarisha ufugaji wa kisasa, kuchakata bidhaa za mifugo kwa ajili ya mahitaji
ya ndani, ikiwemo lishe bora na kuuza nje pamoja na kuhamasisha uwekezaji wa
sekta binafsi. Aidha, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imekarabati majosho 292, inaendelea na ukarabati wa majosho
207 na kuendelea na ujenzi wa
majosho mapya 84 katika halmashauri mbalimbali nchini. Hatua hii imewezesha kuongezeka kwa majosho yanayofanya kazi kutoka 1,486 Mwaka 2018/2019 hadi majosho 1,738 Mwaka 2019/2020. Aidha, Serikali imenunua
lita 12,549 za dawa za kuogesha mifugo.
87.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021 Serikali
itaendelea kuhimiza ufugaji wa kisasa pamoja na kuimarisha afya ya mifugo kwa
kuwezesha upatikanaji wa huduma za chanjo na tiba kwa kuimarisha vituo vya
utengenezaji wa chanjo za mifugo. Aidha, Serikali itaendelea kuhakikisha
upatikanaji wa malisho kwa kutambua, kutenga, kumilikisha, kusimamia na
kuendeleza maeneo ya malisho. Vilevile, huduma za ugani zitaboreshwa na mafunzo
kwa wafugaji na maafisa ugani yatatolewa ili kuwapatia maarifa na teknolojia
mbalimbali kwa lengo la kuongeza tija.
Uvuvi
88.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha Sekta ndogo ya Uvuvi ili iweze kuchangia
kikamilifu katika Pato la Taifa na ajira kwa ujumla. Hatua zilizochukuliwa ni
pamoja na kuondolewa kwa kodi katika zana na malighafi za uvuvi, kupambana na
uvuvi haramu, kuboreshwa kwa mialo ya kupokelea samaki na kuwa ya kisasa,
kuhamasisha uwekezaji katika ukuzaji wa viumbe maji pamoja na kuhamasisha sekta
binafsi kuwekeza katika viwanda vya kuchakata samaki.
89.
Mheshimwia Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaimarisha sekta ya uvuvi ili
kuongeza mchango wa sekta hiyo katika pato la Taifa na kuwaongezea wavuvi
kipato. Hatua zitakazochukuliwa zitahusisha, utekelezaji wa Mkakati wa kujenga
na kuboresha miundombinu ya uvuvi, mkakati wa kufufua Shirika la Uvuvi
Tanzania, kuweka mazingira bora katika uvuvi wa bahari kuu kwa kuweka vivutio
kwa wawekezaji, kuendelea kupambana na wavuvi haramu na kuhamasisha matumizi
endelevu ya rasilimali za uvuvi, uhifadhi na uchakataji wa samaki ili
kuimarisha mnyororo wa thamani.
Utalii
90.
Mheshimiwa Spika, sekta ya utalii nchini
imeendelea kuimarika ikichagizwa pamoja na mambo mengine na uwekezaji mkubwa
uliofanyika katika miundombinu ya usafiri na usafirishaji na utoaji huduma. Katika Mwaka 2019, idadi ya watalii walioingia
nchini ilifikia 1,510,151 ikilinganishwa na 1,505,702 Mwaka 2018. Ongezeko la idadi ya watalii nchini limeongeza mapato ya Serikali
yatokanayo na utalii kutoka Dola za Marekani bilioni 2.4 Mwaka 2018 hadi Dola
za Marekani bilioni 2.6 Mwaka 2019.
91.
Mheshimiwa Spika, katika hatua nyingine ya kuimarisha shughuli za utalii nchini, Serikali imepandisha hadhi Mapori ya Akiba 6 ambayo ni Burigi (Chato),
Ibanda (Kyerwa), Rumanyika (Karagwe), Nyerere, Mto Ugalla na Kigosi kuwa Hifadhi za Taifa. Lengo ni kuimarisha Sekta ya Utalii kwa kuwa na
maeneo mengi ya hifadhi na vivutio vya watalii yatakayosaidia kuongeza wigo wa
utalii na mapato yatokanayo na sekta hiyo.
92.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2020/2021, Serikali itaendelea kuvitangaza vituo vya utalii
ndani na nje ya nchi hususan kwenye masoko ya kimkakati, kuimarisha hifadhi
mpya 6 za Taifa, kukuza wigo wa mazao ya utalii na kuweka mazingira wezeshi ili sekta
binafsi ishiriki kikamilifu katika uwekezaji kwenye utalii. Kadhalika, maeneo
mengine yatakayopewa kipaumbele ni utalii wa meli, mikutano, fukwe, utamaduni,
malikale, ikolojia na jiolojia.
Madini
93.
Mheshimiwa Spika, usimamizi mzuri wa mikakati na
sheria za ulinzi wa rasilimali na maliasili zetu umekuwa chachu ya kukua na
kuimarika kwa sekta ya Madini nchini. Usimamizi huo umeifanya sekta hiyo kutoa
mchango mkubwa katika ukuaji wa Pato la Taifa. Mathalan, katika kipindi cha
nusu ya kwanza ya Mwaka 2019/2020 mchango wa Sekta ya madini ulikuwa asilimia
13.7. Katika kipindi hicho, sekta ya madini ilishika nafasi ya pili katika
kuchangia Pato la Taifa baada ya sekta ya ujenzi iliyochangia asilimia 16.5.
94.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Januari 2020, maduhuli
ya Serikali yaliyokusanywa kupitia Sekta ya Madini ni Shilingi bilioni 284.4.
Kiwango hicho ni sawa na asilimia 60.4 ya lengo la mwaka la kukusanya Shilingi
bilioni 470.89. Mafanikio hayo, ni ishara tosha ya kuendelea kuimarika kwa
sekta hii kufuatia usimamizi thabiti unaowekwa na Serikali.
95.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeanzisha masoko ya madini nchini kwa lengo la kupata takwimu
sahihi za mauzo ya madini, kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata soko la uhakika,
kupata bei stahiki kwa bidhaa za madini na kuondoa tatizo la utoroshaji na
biashara haramu ya madini. Hatua hiyo imewezesha kuongezeka kwa mapato ya
Serikali kupitia tozo za mrabaha na ada ya ukaguzi wa mauzo ya madini kwenye
masoko.
96.
Mheshimiwa Spika, hadi Januari 2020, jumla ya masoko ya madini 28 na vituo vidogo vya ununuzi
wa madini 28 vimeanzishwa nchini. Kupitia masoko na vituo hivyo, katika kipindi
cha Machi 2019 hadi Januari 2020, jumla ya kilogramu 9,237.34 za dhahabu;
karati 12,973.14 za madini ya almasi; kilogramu 20,099.17 za madini ya bati na
kilogramu 514,683.28 za madini ya vito mbalimbali ziliuzwa na kuipatia Serikali
mapato ya Shilingi bilioni 66.57 ambazo zimetokana na mrabaha, ada ya ukaguzi
na ushuru wa Halmashauri.
97.
Mheshimiwa Spika, masoko ya madini yamekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji
wa takwimu sahihi za madini tofauti na ilivyokuwa awali kabla ya kuanzishwa
kwake. Masoko hayo, yana ulinzi na usalama wa kutosha na sifa zote za kimataifa
zinazohitajika katika kuendesha biashara ya madini. Hivyo, natoa rai kwa wadau
wa ndani na nje ya nchi kutumia masoko na vituo hivyo ambavyo vinaendeshwa kwa
misingi ya kisheria kwa kuzingatia ushindani na uwazi wa kibiashara.
98.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha uchimbaji mdogo na wa kati wa madini nchini; ukusanyaji wa mapato
yatokanayo na madini; kuhamasisha uwekezaji katika Sekta ya Madini; kuimarisha
shughuli za ugani na utafiti, uongezaji thamani madini na masoko.
Nishati
99.
Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa umeme
nchini imeendelea kuimarika na kuchangia katika ukuaji wa uchumi na ustawi wa
Taifa kwa ujumla. Uwezo wa mitambo ya kufua umeme nchini ni Megawati 1,602.32
ambapo kati ya hizo Megawati 1,565.72 zipo katika Mfumo wa Gridi ya Taifa na
Megawati 36.6 zipo nje ya Mfumo wa Gridi ya Taifa. Aidha,
hali ya maji katika mabwawa ya Mtera, Kidatu, Kihansi, Nyumba ya Mungu na New Pangani Falls imeendelea kuwa nzuri
na hivyo kutuhakikishia kuwa na umeme wa uhakika.
100.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuelezea juu ya mafanikio tuliyoyapata katika utekelezaji wa Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere hapo awali, Serikali
vilevile inatekeleza Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Rusumo utakaozalisha Megawati
80. Kukamilika kwa miradi hii na mingine itaimarisha upatikanaji wa umeme nafuu
na wa uhakika na hivyo kuchangia katika maendeleo ya ukuaji wa viwanda na
uchumi.
101.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali
itaendelea kutekeleza miradi mikubwa na
ya kielelezo ya uzalishaji wa umeme hususan Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa
Julius Nyerere (MW 2,115), upanuzi wa Mradi wa Kinyerezi I (MW 185) pamoja na
kuimarisha mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini. Aidha,
Serikali itaendelea kutekeleza Awamu ya Tatu ya Mradi wa Kupeleka Umeme
Vijijini ili kuhakikisha vijiji vilivyobaki vinapatiwa umeme.
HUDUMA ZA
KIUCHUMI
Ardhi
102.
Mheshimiwa Spika, ardhi ni
rasilimali namba moja katika kuifikia ndoto ya Serikali ya kujenga uchumi wa
viwanda. Kwa msingi huo, Serikali imeendelea kusimamia upimaji wa ardhi,
mipango ya matumizi ya ardhi kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa na umilikishaji
ardhi kwa wananchi. Sambamba na kuimarisha utoaji huduma kwa njia ya
kielektroniki, Serikali inatekeleza mpango wa kusogeza huduma za ardhi karibu
na wananchi. Hadi sasa ofisi za ardhi za mikoa 26 zimeanzishwa pamoja na
kuendelea kuziimarisha ofisi zote za ardhi za Halmashauri kwa kuwapatia mafunzo
wataalam wa sekta ya ardhi na kununua vifaa.
103.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2019/2020, Serikali imekamilisha awamu ya kwanza ya usimikaji wa Mfumo
Unganishi wa Kuhifadhi Kumbukumbu za Ardhi katika Ofisi za Ardhi Kanda ya Dar
es Salaam na Halmashauri za Manispaa ya Kinondoni na Ubungo. Lengo ni
kuharakisha upimaji na utoaji hatimiliki za ardhi ili kuwawezesha wananchi
wengi zaidi kumiliki ardhi kisheria na kutumia hati hizo kupata mikopo katika
taasisi za fedha itakayowezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za
ujasiriamali.
Mipango ya Matumizi ya Ardhi
104.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia upangaji na utekelezaji
wa mipango ya matumizi ya ardhi katika ngazi ya Kanda, Wilaya na Vijiji. Lengo
la Serikali ni kuharakisha upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya makazi na shughuli
mbalimbali ikiwemo kilimo, ufugaji, biashara na uwekezaji. Katika kipindi cha
Julai 2019 hadi Februari 2020, mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji 132
imeandaliwa katika Wilaya 27.
105.
Mheshimiwa Spika, sambamba na
uandaaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Serikali imeendelea kutatua migogoro ya
matumizi ya ardhi katika maeneo mbalimbali. Katika Mwaka 2019/2020 Mheshimiwa
Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ametoa kibali kwa vijiji 920
kati ya vijiji 975 vilivyokuwemo ndani ya hifadhi na mapori ya akiba
kuhalalishwa rasmi kwa ajili ya shughuli za kiuchumi na kijamii. Hatua hiyo
itapunguza migogoro iliyokuwa ikiendelea katika maeneo mbalimbali nchini na
hivyo kuwawezesha wananchi kutumia muda mwingi katika shughuli za uzalishaji.
Miundombinu ya
Usafiri na Usafirishaji
106.
Mheshimiwa Spika, sekta ya miundombinu hususan ya
usafiri na usafirishaji ndio kiunganishi cha sekta za uchumi wa nchi ili
kuwezesha shughuli za uzalishaji mali na utoaji huduma katika jamii. Kuimarika
kwa sekta hii, ni kichocheo muhimu katika kukua kwa uchumi na maendeleo ya
wananchi kwa ujumla.
107.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa sekta hii Serikali ya
Awamu ya Tano ilichukua hatua za makusudi kuanza ujenzi mkubwa wa barabara,
madaraja, vivuko, ufufuaji na ujenzi wa reli mpya, uimarishaji wa usafiri wa majini, na uboreshaji wa
usafiri wa anga ili kuchochea ukuaji wa uchumi kwa kurahisisha huduma za
uchukuzi na usafirishaji wa watu na bidhaa.
Barabara na Madaraja
108.
Mheshimiwa
Spika, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imepata mafanikio
makubwa katika kujenga mtandao wa barabara za kiwango cha lami nchini. Serikali
imeendelea kuhakikisha mikoa yote inaunganishwa na mtandao wa barabara za lami
ili kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa.
109.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi hicho jumla
ya kilomita 399.07 za barabara kuu na barabara za mikoa zilijengwa kwa kiwango
cha lami. Aidha, kilomita 56 za barabara kuu zilifanyiwa ukarabati kwa kiwango
cha lami na kilomita 84 za barabara za mikoa zilifanyiwa ukarabati kwa kiwango
cha changarawe. Hadi kufikia Februari 2020, jumla ya kilomita 6,960 zimefanyiwa
matengenezo ya kawaida, kilomita 1,444 zimefanyiwa matengenezo maalum na
madaraja 416 yamefanyiwa matengenezo.
110.
Mheshimiwa
Spika, katika kuondoa msongamano
wa magari Jijini Dar es Salaam, Serikali inaendelea na ujenzi wa barabara ya
njia 8 kutoka Kimara hadi Kibaha yenye urefu wa Kilomita 19 ambapo ujenzi
umefikia asilimia 63. Mradi mwingine ni ujenzi wa Ubungo Interchange ambao umefikia asilimia 65.
111.
Mheshimiwa
Spika, miradi mingine
inayotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa Daraja la Tanzanite (Salender) lenye
urefu wa Kilomita 6.2 uliofikia asilimia 25 na kuanza maandalizi ya ujenzi wa
daraja la Kigongo - Busisi lenye urefu wa kilomita 3.2 na upana wa mita 28.45.
Aidha, kati ya Julai 2019 hadi Januari 2020 Serikali imetoa Shilingi bilioni
703.6 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya barabara na madaraja nchini.
112.
Mheshimiwa
Spika, katika Mwaka 2020/2021,
Serikali itaendelea na utekelezaji wa miradi mikubwa niliyoitaja pamoja na
mingine inayoendelea. Vilevile, Serikali itaanza ujenzi wa barabara na madaraja
mapya ili kuwahakikishia wananchi, wawekezaji na wafanyabiashara huduma bora na
za uhakika za usafirishaji katika kipindi chote cha mwaka.
Reli
113.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza
hapo awali, moja ya mafanikio makubwa tuliyoyapata katika eneo la reli ni
kuendelea na ujenzi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa. Nikiri pia kuwa,
katika kipindi hiki, Serikali inajivunia kurejesha huduma ya reli kati ya Dar es Salaam na Moshi
ambayo ilisimama kwa zaidi ya miaka 20 na kufufuliwa kwa huduma ya reli kati ya
Tanga na Moshi iliyosimama kwa takribani miaka 12 ambapo hadi Machi 2020 jumla
ya abiria 33,459 na mizigo tani 5,080 imesafirishwa kupitia reli hizo. Aidha, ukarabati wa reli
ya kati kutoka Dar es Salaam hadi Isaka nao unaendelea kwa kuondoa reli zote
nyepesi na kuweka reli mpya nzito. Ukarabati huo umewezesha kurejea kwa huduma
za usafiri wa abiria na mizigo na hivyo kurahisisha usafirishaji, kupunguza
kero ya usafiri na ajali za barabarani.
114.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali
itakamilisha ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa kwa kipande cha
Dar es Salaam – Morogoro na kuendelea na ujenzi wa kipande cha Morogoro –
Makutupora sambamba na kukarabati miundombinu mingine ya reli.
Bandari
115.
Mheshimiwa Spika, katika eneo la bandari, Serikali
imeendelea kuboresha na kuimarisha miundombinu ya bandari zilizopo katika
mwambao wa pwani na maziwa kwa lengo la kuendeleza huduma ya usafiri wa majini
ndani ya nchi na nchi jirani. Katika Mwaka 2019/2020, Serikali imekamilisha
ujenzi wa gati namba 1, 2, 3 na gati la kupakia na kupakua magari (RoRo Berth) katika Bandari ya Dar es
Salaam. Kazi ya ukarabati wa gati namba 5 hadi 7 inaendelea.
116.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa
Bandari ya Mtwara, ujenzi wa Gati lenye urefu wa mita 300 umefikia asilimia 60
wakati ukarabati wa Gati namba 2 na uongezaji wa kina cha Bandari ya Tanga
unaendelea na umefikia asilimia 60. Ujenzi na ukarabati wa bandari zetu
utaifanya nchi yetu kuendelea kuwa lango muhimu la uagizaji na uingizaji bidhaa
kuelekea nchi jirani.
Ujenzi wa Meli
117.
Mheshimiwa Spika, Serikali inafanyia kazi changamoto
ya utoaji wa huduma za usafiri katika Maziwa Makuu ya Victoria, Tanganyika na
Nyasa. Kwa upande wa ziwa Nyasa, tayari ujenzi wa Meli ya MV Mbeya yenye uwezo
wa kubeba abiria 200 na tani 200 za mizigo umekamilika. Vilevile, tarehe 8
Desemba 2019, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliweka jiwe la
msingi la ujenzi wa chelezo, meli mpya ya MV Mwanza na ukarabati wa Meli za MV
Victoria na MV Butiama.
118.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia
Februari 2020, ujenzi wa meli ya MV
Mwanza itakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo
ulikuwa umefikia asilimia 52. Aidha, ujenzi wa chelezo umefikia asilimia 80,
ukarabati wa meli za MV Victoria asilimia 75 na MV Butiama asilimia 70. Katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea
kuboresha huduma za usafiri kwa njia ya maji ikiwa ni pamoja na kukamilisha
miradi inayoendelea, kukarabati vyombo vilivyopo na kununua vyombo vipya.
Usafiri wa Anga na Viwanja vya Ndege
119.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na
mafanikio niliyoyaeleza hapo awali kuhusu kufufua Shirika la Ndege Tanzania,
katika Mwaka 2019/2020 Serikali imeendelea kuhakikisha kuwa anga la
Tanzania ni salama ili kuimarisha utoaji wa huduma za usafiri wa anga. Aidha,
Serikali inakamilisha usimikaji wa mfumo wa rada 4 za kuongozea ndege za kiraia
katika viwanja vya ndege vya Julius Nyerere, Kilimanjaro, Mwanza na Songwe.
120.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha viwanja vya ndege mbalimbali vilivyopo
nchini. Hadi kufikia Februari, 2020 Serikali imekamilisha ujenzi wa jengo la
tatu la abiria katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere.
Kukamilika kwa jengo hilo kunawezesha kuwahudumia abiria milioni 6 kwa mwaka na
hivyo kuongeza mapato. Serikali pia, imekamilisha upanuzi wa Kiwanja cha Ndege
cha Mwanza na inaendelea na ujenzi wa jengo la abiria katika uwanja huo. Jengo
hilo ambalo litagharimu Shilingi bilioni 13.26 litahudumia abiria 400,000 kwa
mwaka. Vilevile, Serikali inaendelea na ujenzi na ukarabati wa viwanja vya
ndege vya Mtwara, Songea, Geita, Nachingwea, Iringa na Musoma.
121.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021,
Serikali itaendelea kuboresha usafiri wa anga nchini ili kuhakikisha kuwa
Tanzania inakuwa kitovu cha usafiri wa anga kwa nchi za Afrika Mashariki na
Kati. Katika kufanikisha azma hiyo, Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa
usalama na miundombinu ya viwanja vya ndege inaboreshwa.
Mawasiliano
122.
Mheshimiwa Spika, katika eneo la
mawasiliano Serikali
imeendelea na zoezi la usajili wa laini za simu kwa njia ya biometria Nchi
nzima. Hadi mwisho wa mwezi Februari, 2020 jumla ya laini milioni 31.4 kati ya
laini milioni 43.9 zilikuwa zimesajiliwa. Idadi hii ni sawa na asilimia 71 ya
zoezi zima la usajili. Nitoe wito kwa wananchi waliopata namba za vitambulisho
vya Taifa kukamilisha usajili wa laini zao kwa njia ya biometria ili waendelee
kupata huduma za mawasiliano. Zoezi hili lina umuhimu kwa Taifa kwani
linasaidia kuimarisha usalama wa watumiaji wa huduma za mawasiliano nchini na
Taifa kwa ujumla.
123.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia, imeendelea kusimamia mtambo
wa Telecommunications Traffic Monitoring
System (TTMS) ili kuhakikisha kuwa tunapata mapato stahiki kutokana na
huduma za mawasiliano. Mfumo huu umeongeza ufanisi katika kusimamia huduma ya
mawasiliano ya simu nchini. Katika kipindi cha Julai, 2019 hadi Februari, 2020
jumla ya miamala bilioni 2 yenye thamani ya Shilingi trilioni 12.2 imefanyika
ambapo Serikali imepata mapato ya Shilingi bilioni 7.3.
124.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali
itaendelea kushirikiana na makampuni ya simu kuboresha huduma za mawasiliano
hususan maeneo ya pembezoni ili kuongeza kasi ya mawasiliano ya kimtandao kwa
wananchi wa maeneo hayo. Aidha, Serikali itaendelea na ujenzi wa Mkongo wa
Taifa wa Mawasiliano ili kufikisha huduma katika Makao Makuu ya Wilaya zote
nchini pamoja na kuanza ujenzi wa Kituo cha Data Dodoma.
HUDUMA ZA JAMII
Elimu
125.
Mheshimiwa Spika, elimu ya kisasa na hasa yenye mwelekeo wa sayansi na teknolojia ina
nafasi ya pekee katika kufanikisha ujenzi wa msingi wa uchumi wa kisasa wa
Taifa linalojitegemea. Kwa kutambua umuhimu huo na kama nilivyoeleza awali
Serikali ilianzisha na kutekeleza Mpango wa Elimumsingi Bila Ada ili
kuhakikisha kila mtoto mwenye umri wa kwenda shule anaandikishwa.
126.
Mheshimiwa Spika, katika hatua nyingine ya kuboresha elimu ya sekondari ninayo furaha
kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa tarehe 31 Machi, 2020 Benki ya Dunia imeridhia
kuipatia Tanzania mkopo wa Dola za Marekani Milioni 500 sawa na takriban
shilingi trilioni 1.14 kwa ajili ya kutekeleza mpango wa maboresho ya elimu ya
sekondari nchini.
127.
Mheshimiwa Spika, Benki ya Dunia imeridhia kuipatia Tanzani mkopo huo baada ya
kuridhishwa na utekelezaji wa sera ya Elimumsingi Bila Ada. Hivyo, mpango huu
utaimarisha usalama wa watoto shuleni, kuongeza uandikishaji katika shule za
sekondari na elimu mbadala, kuimarisha mafunzo kwa walimu na matumizi ya TEHAMA
katika kufundisha hususan masomo ya sayansi.
128.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mpango huo utaongeza wigo wa elimu ya sekondari hususan
kwa watoto wa kike na kuwawezesha wavulana na wasichana kukamilisha elimu hiyo.
Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa sera ya Elimumsingi Bila Ada kwa
lengo la kuwawezesha watoto wetu wa kike kupata elimu ya sekondari na stadi za
kazi, kuondoa vikwazo kwa watoto wa kike kupata elimu ya sekondari, kuimarisha
matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji pamoja na uratibu,
usimamizi na tathmini ya ubora wa elimu ya sekondari.
129.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa elimu ya juu, Serikali imeongeza wigo wa upatikanaji wa
mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu na kutoa kipaumbele kwa watu wenye
mahitaji maalum. Katika Mwaka 2019/2020, Serikali imeongeza fursa za
upatikanaji wa elimu ya juu kwa kutoa mikopo kwa wanafunzi 130,883 ikilinganishwa
na wanafunzi 122,754 kwa Mwaka 2018/2019.
Aidha, Shilingi bilioni 450 zilitumika katika kipindi hicho
ikilinganishwa na Shilingi bilioni 424.8 kwa Mwaka 2018/2019.
130.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa Mpango
wa Elimumsingi Bila Ada, kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu na kuhimiza
uwekezaji kwa kushirikiana na sekta binafsi hususan katika kuboresha
miundombinu, vifaa vya kufundishia na kujifunzia na kuendeleza rasilimali watu
ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu.
Maji
Upatikanaji wa Maji Vijijini
131.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imeendelea kutekeleza
Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa
huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wote hususan wale wanaoishi maeneo
ya vijijini. Katika Mwaka 2019/2020, jumla ya miradi 94 ya maji yenye vituo vya kuchotea maji 2,495 katika
maeneo mbalimbali vijijini imekamilika. Aidha, miradi 558 ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
132.
Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi kubwa za Serikali katika
utekelezaji wa miradi hiyo, hadi Desemba 2019, upatikanaji wa huduma ya maji
katika maeneo ya vijijini umefikia asilimia 64.8. Vilevile, ili kuboresha utoaji wa huduma ya maji vijijini, Serikali imeanzisha Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa
Mazingira Vijijini (RUWASA) wenye
jukumu la kutekeleza miradi na kusimamia utoaji wa huduma za maji na usafi wa
mazingira vijijini.
Upatikanaji wa Maji Mijini
133.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa maji mijini, Serikali
imetekeleza miradi mipya ya maji katika Jiji la Dodoma na Dar es Salaam pamoja
na maeneo ya Kibaha, Bagamoyo na Kisarawe. Aidha, Serikali
pia imeboresha miundombinu ya upatikanaji wa huduma ya maji katika miji mikuu
ya mikoa, wilaya, miji midogo na maeneo yanayohudumiwa na miradi ya maji ya
kitaifa ya Chalinze, Mugango – Kiabakari, Maswa, Wanging’ombe, Masasi -
Nachingwea na Kahama – Shinyanga. Utekelezaji wa
miradi hiyo umewezesha upatikanaji wa maji katika miji ya mikoa kufikia
asilimia 85.
134.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021,
Serikali itaifanyia mapitio Sera ya Taifa ya Maji ya Mwaka 2002 ili kuzingatia
masuala mapya ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, kutilia mkazo suala
la usafi wa mazingira na matumizi ya vyanzo vya maji chini ya ardhi. Serikali
pia, itakamilisha miradi inayoendelea, kuanza miradi mipya ya maji na kuanza
upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria
kupeleka Singida hadi Dodoma.
Afya
Ujenzi na Ukarabati wa Hospitali
135.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na miradi ya ujenzi wa hospitali za Rufaa za Mikoa,
ikiwemo ujenzi wa hospitali za Mikoa mipya ya Geita, Simiyu, Songwe, Katavi,
Njombe (Mgondechi). Vilevile, Serikali inaendelea na ujenzi wa hospitali za
Mikoa ya Mara, Singida na Shinyanga pamoja na ujenzi wa hospitali za Wilaya
katika Halmashauri 70 nchini. Vilevile, Serikali inajenga Hospitali ya Uhuru
wilayani Chamwino, Dodoma na hospitali za rufaa za kanda za Mtwara, Mbeya na
Burigi - Chato.
Huduma za Afya
za Kibingwa
136.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuimarisha huduma za
kibingwa bobezi (super specialist)
katika Hospitali za Rufaa za Kanda, Hospitali Maalum na Hospitali ya Taifa.
Utoaji wa huduma hizo umewezesha wananchi wengi kupata huduma ambazo awali
zilikuwa zinapatikana nje ya Nchi. Katika kipindi cha Julai hadi Machi 2020, Hospitali ya Taifa Muhimbili,
Hospitali ya Rufaa ya Benjamini Mkapa, MOI na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete
zimetoa huduma mbalimbali za kibingwa kwa wagonjwa wa ndani na nje ya Nchi.
137.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2019 hadi Machi 2020,
idadi ya wagonjwa waliopata huduma za kibingwa bobezi katika hospitali hizo ni
1,970. Kati yao, wagonjwa 18 walipata huduma za kupandikiza figo, 330 walipata
huduma ya upasuaji wa uti wa mgongo, 730 upasuaji wa ubongo, 507 upasuaji wa
moyo kwa kufungua kifua, 610 upasuaji wa moyo kupitia tundu dogo, 101 upasuaji wa mishipa ya damu na watoto 284 walifanyiwa upasuaji wa
vichwa vikubwa na mgongo wazi.
138.
Mheshimiwa Spika, Taasisi ya Saratani ya Ocean
Road imetoa tiba mionzi kwa wagonjwa 110,979 ikilinganishwa na wagonjwa
52,890 Mwaka 2018. Kati ya wagonjwa hao, 5,788 walipatiwa tiba ya mionzi.
Ongezeko la tiba mionzi kwa wagonjwa limetokana na uwepo wa mitambo mipya
miwili kwa ajili ya tiba ya saratani (LINAC) ambayo imesaidia kupunguza muda wa
wagonjwa kusubiri tiba mionzi kutoka wiki nne Mwaka 2018 hadi wiki mbili Mwaka
2020.
139.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya
afya ikiwemo ukarabati na ujenzi wa hospitali, vituo vya afya na zahanati.
Vilevile, itaendelea kuimarisha upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba pamoja
na kuboresha huduma za kibingwa za afya na ubobezi katika Hospitali ya Taifa,
Hospitali Maalum na Hospitali za Rufaa za Kanda ili kuziwezesha kutoa huduma
bora zaidi za kibingwa nchini.
Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu
140.
Mheshimiwa Spika, watu wenye ulemavu wanayo haki kwa mujibu wa Katiba ya kutambuliwa utu
wao, kuendelezwa, kuheshimiwa na kulindwa dhidi ya vitendo vinavyoshusha utu
wao ikiwemo ubaguzi, uonevu, ukatili na mila potofu. Katika Mwaka 2019/2020,
Serikali imeendelea kusimamia
utekelezaji wa miongozo na mipango mbalimbali inayolenga kuongeza
upatikanaji wa haki na ustawi wa Watu Wenye
Ulemavu na kuhakikisha huduma zinazotolewa katika ngazi zote kwa ajili
ya Watu Wenye
Ulemavu
na wenye mahitaji maalum zinatolewa kwa haki na usawa.
141.
Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili
Watu Wenye Ulemavu hususan kiuchumi, Serikali imezielekeza Halmashauri kutenga
asilimia 2 ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya kutoa mikopo kwa Watu Wenye
Ulemavu. Kupitia mikopo hiyo jumla ya vikundi 160 vya Watu Wenye Ulemavu
vimeundwa na vilipatiwa mikopo yenye thamani ya Shilingi bilioni 3.87. Pamoja
na hatua tuliyofikia napenda kutoa rai kwa Halmashauri zote nchini kutoa fedha
hizi ili ziweze kutatua changamoto za kiuchumi zinazowakabili Watu Wenye
Ulemavu kama ilivyokusudiwa na Serikali.
142.
Mheshimiwa Spika, vilevile, Serikali imefanikiwa kuanzisha Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu na
kufungua akaunti kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi ikiwa ni pamoja na
kuwajengea uwezo wa kuanzisha miradi mbalimbali ya uzalishaji. Serikali
itatumia Mfuko huo kuratibu upatikanaji wa rasilimali fedha kutoka kwa wadau
ili kuhakikisha Mfuko huo unakidhi malengo ya uanzishwaji wake.
143.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia, iliwezesha uendeshaji wa Baraza la Ushauri la Taifa la
Watu Wenye Ulemavu ambalo limekuwa likitekeleza majukumu yake kwa mujibu wa
Sheria ya Watu wenye Ulemavu Na 9. ya Mwaka 2010. Aidha, wajumbe wa Baraza hilo
wamepatiwa mafunzo kuhusu Sera, Sheria, miongozo na mipango inayowahusu Watu
Wenye Ulemavu ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
144.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, wahitimu wa vyuo vikuu 167 wenye ulemavu,
walipatiwa mafunzo ya kukuza ujuzi kupitia Programu ya Miaka Mitano ya Kukuza
Ujuzi. Serikali itaendelea kuwahamasisha wahitimu wenye ulemavu kujiandikisha
kwenye daftari la wanaotafuta ajira ili kupata fursa ya kuajiriwa pale nafasi
zinapotangazwa. Aidha, Serikali imefanya jitihada na kufanikiwa kufufua vyuo
vitatu vya mafunzo ya ufundi kwa Watu Wenye Ulemavu. Vyuo hivyo ni Mirongo
(Mwanza), Ruwanzari (Tabora) na Masiwani (Tanga).
145.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuweka mazingira
wezeshi na rafiki kwa Watu Wenye Ulemavu ili kushiriki kikamilifu katika
maendeleo ya Taifa. Baadhi ya shughuli zitakazopewa kipaumbele ni pamoja na
kukamilisha maandalizi ya Mfuko wa Taifa wa Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu,
kuratibu maadhimisho ya Siku za Kitaifa na Kimataifa za Watu Wenye Ulemavu na
kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Baraza la Taifa la Ushauri kwa Watu Wenye
Ulemavu. Vilevile, Serikali itaendeleza vyuo vya mafunzo ya ufundi kwa Watu
Wenye Ulemavu.
ULINZI NA USALAMA
146.
Mheshimiwa Spika, hali ya amani na usalama ndani ya mipaka ya Tanzania ni shwari. Vyombo
vyetu vya ulinzi na usalama vinatekeleza majukumu yake ya kulinda mipaka ya
Nchi, kudumisha amani, usalama wa raia na mali zao pamoja na kufundisha
wananchi ulinzi wa umma. Serikali imeendelea kuliimarisha na kuliongezea uwezo
Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kulipatia vifaa na zana bora za kisasa pamoja
na kutoa mafunzo na mazoezi stahiki kwa wanajeshi ili kuliwezesha Jeshi
kutekeleza majukumu yake ya msingi ya ulinzi wa mipaka ya Nchi yetu.
147.
Mheshimiwa Spika, vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimekuwa na mchango mkubwa katika
kukabiliana na majanga na matukio yenye kuleta athari
kwa watu na mali zao na kutekeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi
hususan ujenzi, uendelezaji viwanda na shughuli za kilimo. Nitumie fursa hii kuvipongeza vyombo hivyo hususan Jeshi la
Wananchi wa Tanzania na Jeshi la Magereza kwa kushiriki ipasavyo katika ujenzi
wa Mji wa Serikali Mtumba, Dodoma.
148.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuimarisha usalama wa raia
na mali zao na kutokana na juhudi hizo, hali ya ulinzi na
usalama imeendelea kuimarika na uhalifu kupungua kwa asilimia 2.8 kwa makosa
makubwa ya jinai ikilinganishwa na Mwaka 2018/2019. Halikadhalika, ajali za
barabarani zimepungua kwa asilimia 25.7 ikilinganishwa na Mwaka 2018/2019.
149.
Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto ya uhamiaji haramu, Serikali ipo katika hatua
za mwisho za uwekaji wa mfumo wa kielektroniki wa usimamizi wa mipaka (e-Border Management System). Kukamilika kwa mfumo huo
kutawezesha utoaji wa huduma bora za uhamiaji,
kuimarisha ulinzi na usalama wa mipaka na kuongeza udhibiti katika ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.
150.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha wananchi wote kwamba msingi wa usalama
wa raia na mali zao ni jukumu letu sote. Hivyo, ni muhimu wananchi wote
tushirikiane na vyombo vya ulinzi na usalama kubaini wahalifu pamoja na vitendo
vinavyohatarisha usalama wetu kwa kutoa taarifa kwenye vyombo husika.
151.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kulinda mipaka ya nchi
yetu, kuimarisha usalama wa raia na mali zao ili kuhakikisha wananchi wanaishi
na kufanya shughuli za maendeleo kwa amani. Vilevile Serikali itaendelea
kuboresha mazingira ya kazi na zana za kisasa zinazoendana na teknolojia ya
kisasa pamoja na kuendelea kuhamasisha na kuelimisha wananchi juu ya masuala ya
ulinzi, uzalendo, usalama na umuhimu wa kushiriki katika ulinzi.
USIMAMIZI WA
KAZI NA WAFANYAKAZI
Kazi na Wafanyakazi
152.
Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali ni kuona wafanyakazi na wananchi kwa ujumla wanafanya
kazi za staha na katika mazingira yanayokubalika. Katika kutekeleza azma hiyo,
Serikali imeendelea kusimamia viwango vya kazi na wafanyakazi, afya na usalama
mahali pa kazi, na kusimamia Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri.
153.
Mheshimiwa Spika, katika kusimamia viwango vya kazi na wafanyakazi, Serikali imeendelea
kusimamia utekelezaji wa
Sheria za Kazi kwa kufanya kaguzi na kutoa elimu kwa wafanyakazi na waajiri.
Aidha, mpaka kufikia mwezi Februari, 2020 kaguzi 3,663 zilifanyika katika
maeneo mbalimbali ya kazi, ikiwa ni sawa na asilimia 76.3 ya lengo
lililopangwa. Kupitia kaguzi hizo, waajiri 36 na raia wa kigeni 82 walifikishwa
Mahakamani kwa kukiuka sheria za kazi ambapo, baada ya kupatikana na hatia
walitozwa faini ya jumla ya Shilingi milioni 872.
154.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Serikali imeendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya
Kuratibu Ajira za Wageni Nchini. Hadi kufikia mwezi Februari, 2020 jumla ya
vibali vya kazi 6,625 vilitolewa kwa wageni na maombi 984 ya vibali vya kazi yalikataliwa
kutokana na kutokidhi vigezo na masharti yaliyowekwa kwa mujibu wa Sheria.
Vilevile, katika jitihada za kuongeza ufanisi, Serikali imejenga Mfumo wa
Kielektroniki wa Vibali vya Kazi (On Line
Work Permit Application and Information System) pamoja na kuanza kutoa
mafunzo ya matumizi yake kabla ya kuzinduliwa na kuanza kutumika.
Afya na Usalama Mahali pa Kazi
155.
Mheshimiwa Spika, katika kusimamia na kudhibiti afya na usalama Mahali pa Kazi, Serikali
kupitia Wakala wa Afya na Usalama mahali pa Kazi imeendelea kufanya kaguzi
mbalimbali katika maeneo ya kazi. Aidha, kwa Mwaka 2019/2020, jumla ya sehemu
za kazi 2,270 zilisajiliwa, kaguzi 8,662 zilifanyika na wafanyakazi 93,575
walipimwa afya.
156.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kusajili vyama vya
wafanyakazi, sehemu mpya za kazi, kufanya kaguzi za kawaida, kaguzi maalum,
kupima afya za wafanyakazi na kutoa elimu ya Afya na Usalama kwa Wajasiriamali
wadogo na wa kati.
UTUMISHI WA UMMA
157.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha utendaji kazi
wenye tija kwa kuboresha vitendea kazi, kuongeza na kuwajengea uwezo watumishi.
Hadi kufikia mwezi Machi 2020, Serikali imetoa ajira mpya na mbadala 6,975 na
kuwapandisha vyeo Watumishi 290,625 wa Kada mbalimbali. Aidha, Serikali imelipa Shilingi bilioni 130.4 kwa Watumishi wa Umma 100,684
waliokuwa wanadai madeni mbalimbali na uhakiki wa Watumishi 36,981 wenye madeni
ya Shilingi bilioni 88.389 unaendelea. Uhakiki huo ukikamilika madeni hayo
yatalipwa.
158.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii
kuwashukuru wafanyakazi wote kwa mchango wao mkubwa katika kujenga Taifa letu.
Napenda kuwahakikishia watumishi wote kuwa, katika mwaka 2020/2021, Serikali
itaendelea kuweka mazingira bora ya kufanya kazi ili Watumishi wa Umma wafanye
kazi kwa weledi, juhudi, uadilifu na uwajibikaji.
UWEZESHAJI
WANANCHI KIUCHUMI
159.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia utekelezaji wa
Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya Mwaka 2004 kwa lengo la
kuwakwamua kiuchumi. Katika kutekeleza azma hiyo, Serikali imefanikiwa kuongeza
ushiriki wa Watanzania kwenye miradi ya kielelezo na kimkakati ikiwemo Mradi wa
Ujenzi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa na Mradi wa Kufua Umeme wa
Maji wa Julius Nyerere ambapo Watanzania 250,000 wameajiriwa katika nafasi
mbalimbali zenye ujuzi wa juu, kati na chini, ikilinganishwa na wageni 1,338.
Idadi hiyo ni sawa na asilimia 99 ya ajira zote kwenye miradi hiyo. Aidha,
Shilingi bilioni 170 zililipwa kwa kampuni za kitanzania ambazo zilipata kazi
katika miradi ya kielelezo na kimkakati inayotekelezwa nchini.
160.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuzitumia Taasisi zake za
ndani za masuala ya ujuzi na teknolojia zikiwemo Vyuo vya VETA, Chuo cha Ufundi
Dar es salaam (DIT), Chuo cha Ubaharia Dar es Salaam (DMI) na vyuo vya ufundi
vya Don Bosco katika kuandaa na kufundisha programu zitakazowezesha Watanzania
kushiriki katika miradi ya kimkakati,
kujiajiri na kuajiriwa katika maeneo mbalimbali.
161.
Mheshimiwa Spika, kufuatia utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kuwa kila Halmashauri itenge asilimia 10 ya makusanyo yake kwa Wanawake, Vijana na
Wenye Ulemavu, Halmashauri zilitenga jumla ya Shilingi bilioni 54.1 na kutoa
jumla ya Shilingi bilioni 25.4 kwa Wanawake, Vijana na Wenye Ulemavu. Kati ya
fedha hizo; Shilingi 12.9 bilioni zilitolewa kwa wanawake, Shilingi 9.5 bilioni
zilitolewa kwa vijana na Shilingi bilioni 2.9 zilitolewa kwa watu wenye
ulemavu. Napenda kusisitiza
Halmashauri zote nchini kuendelea kutenga na kutoa mikopo hiyo kwa walengwa ili
waweze kuinua hali zao kiuchumi na kuongeza mchango wao katika kujenga uchumi
wa Taifa.
162.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imeendelea kusimamia uanzishwaji wa vituo
maalum vya uwezeshaji katika mikoa mbalimbali nchini. Lengo ni kuwawezesha
wananchi kupata taarifa mbalimbali kuhusu fursa za uwezeshaji, usajili na
uendelezaji wa biashara, upatikanaji wa mitaji na mafunzo ya kuongeza thamani
ya mazao na bidhaa mbalimbali.
Mfuko wa
Taifa wa Maendeleo ya Vijana
163.
Mheshimiwa Spika, ili kutumia kundi
la vijana kama fursa muhimu kwa maendeleo ya Taifa, Serikali imeendelea na
uboreshaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Katika Mwaka 2019/2020,
Mfuko wa Taifa wa Maendeleo ya Vijana umetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi
bilioni 3.2 ambapo vikundi 586 vyenye jumla ya vijana 4,222 kutoka katika Halmashauri 155 walipata
mikopo hiyo.
Mfuko wa
Maendeleo ya Jamii (TASAF)
164.
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 17
Februari 2020, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania alizindua Kipindi cha Pili cha Mpango wa Kunusuru Kaya
Maskini katika Awamu ya Tatu ya TASAF utakaotekelezwa Tanzania Bara na
Zanzibar. Kuzinduliwa kwa kipindi hiki cha Pili cha Mpango huo, kunadhihirisha
nia ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kutetea
wanyonge na wasiojiweza.
165.
Mheshimiwa Spika, Mpango huu umewezesha kaya maskini kuongeza kipato, fursa na uwezo wa
kugharamia mahitaji muhimu pamoja na kujenga rasilimali watu. Mathalan, kipindi
cha Kwanza cha TASAF Awamu ya Tatu kilihudumia kaya milioni 1.1 zenye watu
milioni 5.2 katika Halmashauri 159 za Tanzania Bara na wilaya zote za Zanzibar.
166.
Mheshimiwa Spika, kupitia Mpango huu wa TASAF kaya maskini zimemudu kujiunga na Mfuko
wa Bima ya Afya ya Jamii pamoja na kujikwamua dhidi ya umaskini. Kwa mfano,
asilimia 32 ya kaya zilijiunga na Bima ya Afya ya Jamii ikilinganishwa na
asilimia 11 kabla ya mpango wa TASAF. Aidha,
katika kipindi cha Mwaka 2011/2012 hadi 2017/2018 umaskini wa
mahitaji ya msingi kwa Tanzania Bara, ulipungua kwa asilimia 1.8 na wa chakula
kwa asilimia 1.7. Aidha, takwimu zinaonesha pia kuwa, umaskini uliokithiri
umepungua kutoka asilimia 28.2 hadi asilimia 26.4. Kupungua huko kumechangiwa
na utekelezaji wa mpango wa TASAF wa kunusuru kaya maskini.
167.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itafanya utambuzi na uhakiki wa hali
za ustawi wa maisha ya walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika
Halmashauri 101. Lengo ni kubaini kaya ambazo si maskini tena sambamba na
kuandikisha kaya mpya 235,647 ambazo hazikufikiwa katika kipindi cha kwanza cha
Mpango. Natoa wito kwa wote waliopewa dhamana ya kutekeleza Mpango huu kufanya
kazi kwa uadilifu, weledi na uaminifu mkubwa ili kufikia malengo
yaliyokusudiwa.
Ukuzaji Ujuzi
168.
Mheshimiwa Spika, suala la ukuzaji ujuzi wa nguvukazi nchini
ni miongoni mwa ajenda muhimu ya kisera katika kuwezesha wananchi kujikwamua
kiuchumi. Serikali imeendelea kuwezesha wananchi wake kupitia Programu ya
Kukuza Ujuzi Nchini kwa lengo la kuwapatia ujuzi na stadi za kazi hasa kundi la
vijana, wanawake na Watu Wenye Ulemavu. Ujuzi huo, utawawezesha kumudu
ushindani katika soko la ajira na hivyo kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa
uchumi wa viwanda.
169.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, jumla ya vijana 30,099 wamewezeshwa kupata ujuzi
kupitia programu hiyo. Kati yao, vijana 5,875 wamepata mafunzo ya uanagenzi
katika fani za ufundi stadi katika maeneo mbalimbali. Mafunzo haya yamefanyika katika Mikoa 13
ya Tanzania Bara ambayo ni Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Lindi, Geita, Mara,
Kilimanjaro, Iringa, Morogoro, Kagera, Singida, Shinyanga na Ruvuma. Aidha,
jumla ya vijana 5,395 wamepewa mafunzo na kurasimishiwa ujuzi walioupata
kupitia mfumo usio rasmi wa mafunzo kupitia VETA katika fani za uashi,
useremala, ushonaji, ufundi bomba, uchomeleaji na
uungaji vyuma, ufundi magari, ufundi umeme, ukarabati wa bodi za magari, upishi na uhudumu katika hoteli.
170.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wahitimu wa elimu ya juu wanapata uzoefu wa kazi ili
kuwawezesha kupata ajira, jumla ya wahitimu 2,115 wamewezeshwa kupata mafunzo
ya uzoefu kazini kupitia viwanda na kampuni mbalimbali nchini. Kati yao,
wahitimu 100 wa fani ya kilimo wamewezeshwa kwenda nchini
Israeli kuhudhuria mafunzo ya uzoefu kazini katika kilimo cha kisasa kwa muda
wa mwaka mmoja. Aidha, vijana
wengine 3,200 wataanza mafunzo mwezi huu wa Aprili 2020. Nichukue fursa hii
kuzishukuru taasisi za umma na binafsi ambazo zinaendelea kutoa nafasi za
mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi na wahitimu wetu.
171.
Mheshimia Spika, kwa Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kutoa mafunzo ya ujuzi wa
kujiajiri na stadi za kazi kwa vijana katika fani mbalimbali. Aidha, Serikali
itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika nyanja mbalimbali ili kukuza
ujuzi wa rasilimali watu.
Ukuzaji wa Fursa za Ajira
172.
Mheshimiwa Spika, sambamba na ukuzaji ujuzi, Serikali pia imeendelea kuratibu juhudi za
ukuzaji wa fursa za ajira. Katika kipindi cha Julai hadi Februari 2020, jumla
ya ajira 1,577,622
zimezalishwa katika sekta
mbalimbali ambapo ajira 579,518 zimezalishwa na sekta rasmi na ajira 998,104 zimezalishwa na sekta isiyo rasmi. Serikali pia, imeendelea na utoaji wa huduma za
ajira ili kuwezesha watafutakazi kumudu ushindani wa soko la ajira. Hadi
kufikia tarehe 31 Januari 2020, jumla ya watafutakazi 6,756 wamesajiliwa na
Kitengo cha Huduma za Ajira ili kupatiwa huduma mbalimbali za ajira hususan,
ushauri nasihi (vocational guidance and
employment counselling) na mafunzo ya kumudu ushindani katika soko la
ajira. Watafutakazi waliopatiwa huduma ya ushauri nasihi pamoja na mafunzo hayo
walikuwa 5,266.
173.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kutekeleza mikakati
mbalimbali ya ukuzaji wa fursa za ajira. Mikakati hiyo ni pamoja na kuwawezesha
vijana wabunifu na makundi mbalimbali ya vijana na wanawake kuanzisha shughuli
za uzalishaji mali na ujasiriamali ili waweze kujiajiri na kuajiri wengine na
kuimarisha mifumo ya taarifa za soko la ajira na mitaji ili kuwezesha vijana kutumia fursa hizo.
HIFADHI YA JAMII
Usimamizi
na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii
174.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imeendelea kutekeleza programu ya
maboresho ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii kwa kuhakikisha kuwa Kinga ya Jamii
inawafikia wananchi walio wengi.
Maboresho yaliyofanyika yamelenga kuongeza ufanisi katika sekta ya hifadhi
ya jamii. Vilevile, Serikali imeanza kutekeleza kipindi cha Mpito cha miaka
mitano (2019 – 2023) cha kuendelea kuboresha Sekta ya Hifadhi ya Jamii hususan
suala la pensheni kwa wanachama wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.
Mifuko ya Pensheni
175.
Mheshimiwa Spika, Mifuko ya Pensheni ya NSSF na PSSSF imekuwa ikifanya kazi muhimu ya
kulipa pensheni pamoja na mafao mengine kwa wastaafu katika sekta za umma na
binafsi. Katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2019, Mifuko hiyo ililipa
pensheni, malipo ya mkupuo pamoja na mafao mengine yenye jumla ya Shilingi
trilioni 1.4 kwa wanachama 206,897 na wastani wa Shilingi bilioni 51.7
zimelipwa kila mwezi kwa wastaafu kama pensheni.
176.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali
itaboresha uchakataji wa mafao ili kulipa mafao stahiki na kwa wakati; na kuimarisha ukusanyaji wa
michango na mapato yatokanayo na uwekezaji na Mifumo ya
TEHAMA ili kurahisisha utendaji kazi.
MASUALA MTAMBUKA
Vita Dhidi ya Rushwa
177.
Mheshimiwa Spika, jitihada za kuinua uchumi na kuongeza huduma za jamii hazitaleta manufaa
kwa wananchi na kuondoa umasikini iwapo adui rushwa ataendelea kulitafuna Taifa
letu. Rushwa ni adui wa haki, maendeleo na ustawi wa wananchi, pia ni moja ya changamoto
kubwa inayoikabili Nchi yetu na dunia kwa ujumla.
178.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua hilo, Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza mikakati
mbalimbali ya kupambana na rushwa ambayo imeweza kupunguza vitendo vya rushwa
kwa kiasi kikubwa nchini. Mikakati hiyo ni pamoja na Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Tatu wa
Mwaka 2017 - 2022. Hii inadhihirishwa na matokeo ya tafiti zilizofanywa Mwaka
2019 na Taasisi za Kitaifa na Kimataifa na kuonesha kuwa Tanzania inafanya
vizuri katika kudhibiti vitendo vya rushwa na ufisadi. Aidha, kiashiria cha Corruption Perception
Index (CPI) cha taasisi ya Transparency
International kimeonesha Tanzania imefikia kiwango cha asilimia 37 na
kushika nafasi ya 96 kati ya nchi 180 ikilinganishwa na kiwango cha asilimia 30
katika nafasi ya 119 Mwaka 2015.
179.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imeokoa kiasi cha Shilingi bilioni 47.3 zikiwa ni thamani ya mali na fedha taslimu zilizotokana na
operesheni mbalimbali za kiuchunguzi
zilizofanyika nchini. Serikali pia, ilifanya ufuatiliaji katika miradi
244 ya maendeleo iliyohusisha sekta za Afya, Elimu, Maji, Ujenzi na Nishati
yenye thamani ya Shilingi trilioni 9.86 ili kuhakikisha inatekelezwa kulingana
na thamani halisi ya fedha.
180.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha mifumo mbalimbali
kwenye Sekta za Umma katika ngazi zote nchini ili kubaini na kupendekeza njia
madhubuti za kuziba mianya ya rushwa na kuboresha utoaji wa huduma kwa
wananchi. Aidha, Serikali itaendelea kufuatilia miradi ya maendeleo ili
kuhakikisha inatekelezwa kulingana na thamani ya fedha zilizotolewa kwa ajili
hiyo.
Mapambano Dhidi ya UKIMWI
181.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na
wadau inaendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa Nne wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI
wa Mwaka 2018/2019 - 2022/2023 ambao unalenga kutekeleza malengo ya dunia yenye
mwelekeo wa kupambana na UKIMWI ili kufikia TISINI TATU (90:90:90). Katika
kutekeleza malengo hayo, lengo la 90 ya kwanza ni kuhakikisha asilimia 90 ya
watu wanapima na kujua hali zao ambapo hadi Desemba 2019 wenye VVU na waliopima
na kujua hali zao ilikuwa asilimia 80.1 ikilinganishwa na asilimia 75 kwa Mwaka
2018. Lengo la 90 ya pili ni kuhakikisha asilimia 90 ya waliokutwa na VVU
wanaanzishiwa dawa za kufubaza VVU ambapo walioanza dawa za ARV na kubaki
katika dawa ni asilimia 98.8 ikilinganishwa na asilimia 98 kwa Mwaka 2018.
Lengo la 90 ya tatu ni kuhakikisha asilimia 90 ya wanaoanzishiwa dawa za ARV
kinga zao za mwili zinaimarika ambapo lengo hili limefikiwa kwa asilimia 92
ikilinganishwa na asilimia 88 kwa Mwaka 2018.
182.
Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi za dhati zilizofanywa na Serikali, hali ya maambukizi
ya UKIMWI inaonesha kuna Watanzania takribani milioni 1.6 wanaoishi na
VVU ambapo kiwango cha maambukizi kimeshuka kutoka asilimia 7 ya Mwaka 2014
hadi kufikia asilimia 4.7 kwa Mwaka 2020.
183.
Mheshimiwa Spika, mafanikio hayo yamechangiwa na
jitihada mbalimbali za Serikali ikiwa ni pamoja na kupitia
miongozo na Sheria mbalimbali ambapo umri wa vijana kupima VVU bila ya
kuambatana na wazazi au walezi wao umeshushwa kutoka miaka 18 hadi 15. Aidha, dawa mpya ya ARV yenye ufanisi (Dolutegravir) imeruhusiwa kuingizwa na
kutumika nchini ambapo hadi Desemba 2019 asilimia 53 ya watu wanaoishi na
virusi vya UKIMWI (WAVIU) wameanza kutumia dawa hiyo. Serikali pia
imeridhia mfumo wa watu kujipima wenyewe.
184.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali
itaendelea kufanya jitihada za kupunguza kasi ya maambukizi katika jamii kwa
kuhamasisha upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya mapambano dhidi ya
UKIMWI; kupunguza kiwango cha maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa
mtoto na kuimarisha huduma za elimu ya UKIMWI.
Mapambano Dhidi ya Dawa za Kulevya
185.
Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea
kuwa mfano wa kuigwa kimataifa katika kudhibiti na kupambana na dawa za
kulevya. Nchi yetu imefanikiwa kwa ufanisi mkubwa kudhibiti uzalishaji, uuzaji,
usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya. Mafanikio hayo, yamewezesha
waathirika wengi hasa vijana kubadilika na kujihusisha katika shughuli za
uzalishaji mali pamoja na kuipatia sifa Tanzania kutoka kwa Jumuiya ya
Kimataifa.
186.
Mheshimiwa Spika, katika
kikao cha 63 cha Kamisheni ya Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia
Dawa za Kulevya na Uhalifu kilichofanyika Machi 2020, Tanzania ilipongezwa kwa
kufanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kutekeleza miongozo ya Umoja wa Mataifa ya
kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya.
187.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi
cha Julai 2019 hadi Januari 2020 Serikali ilifanikiwa kukamata watuhumiwa wa
dawa za kulevya 6,350. Katika
kipindi hicho, kilogramu 34.986 za heroine na kilogramu 1.556 za cocaine
zilikamatwa. Kadhalika, tani 10.559 za bangi, tani 6.016 za mirungi na mashamba
ya bangi 9 yenye jumla ya ekari 4.25 yaliteketezwa.
188.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kukamata watuhumiwa na madawa ya
kulevya, Serikali imeendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu athari za matumizi ya
dawa za kulevya kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii. Elimu kuhusu dawa za kulevya na UKIMWI pia
imetolewa kwa wasanii 600 pamoja na makundi maalum ikiwemo Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na viongozi wa mbio za Mwenge.
Elimu hiyo, imesaidia kujenga uelewa wa pamoja juu ya athari na namna ya
kupambana na kudhibiti dawa za kulevya nchini.
189.
Mheshimiwa Spika, katika hatua nyingine, Serikali imefanya ukaguzi wa kampuni 58 zinazojihusisha na
biashara ya kemikali bashirifu na usafirishaji wa vifurushi. Kupitia ukaguzi
huo, imegundulika kuwa baadhi ya kampuni hizo hutumia majina bandia katika
kuingiza kemikali bashirifu na kusafirisha vifurushi vya dawa za kulevya. Katika
kukabiliana na tatizo hilo, Serikali imefanikiwa kukamata watuhumiwa 7 na zaidi
ya kilo 890 za dawa za kulevya aina ya mirungi katika Ofisi za Posta zilizokuwa
na majina bandia kama vile mlonge na majani ya chai zikisafirishwa kwenda nchi
za Ulaya, Marekani na Canada.
190.
Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na hali hiyo, Serikali imeimarisha ukaguzi katika
kampuni zinazosafirisha vifurushi kwenda nje ya nchi zikiwemo Ofisi za Posta.
Aidha, katika kuboresha shughuli za ukaguzi wa kemikali bashirifu na dawa tiba
zenye asili ya kulevya, Serikali imeandaa miongozo ya ukaguzi na uchukuaji
sampuli itakayosaidia kufanya ukaguzi wenye ufanisi kubaini usafirishaji dawa
za kulevya, kemikali bashirifu na dawa tiba zenye asili ya kulevya.
191.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa tiba dhidi
ya waathirika wa dawa za kulevya, Serikali inapanua
wigo wa utoaji huduma za tiba kwa kujenga na
kuanzisha vituo vya utoaji wa huduma ya methadone
katika Mikoa ya Tanga na Pwani. Hadi sasa, zaidi ya watumiaji 8,200
wanapata huduma za tiba ya methadone
kila siku katika vituo vilivyopo katika mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya,
Tanga na Pwani.
192.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kudhibiti uingizaji,
usafirishaji na matumizi ya dawa za kulevya kwa kutoa elimu kwa umma juu ya
madhara ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya na kuongeza huduma za tiba
kwa waathirika wa dawa za kulevya.
Uratibu wa Maafa
193.
Mheshimiwa Spika, katika
kipindi cha Mwaka 2019/2020, Nchi yetu imekumbwa na maafa mbalimbali ikiwemo
mafuriko, maporomoko ya ardhi na majanga ya moto. Wananchi wa Bonde la Mto
Rufiji wamepata athari ya mafuriko ambako serikali kupitia Mkoa na Wilaya, pia
Ofisi ya Waziri Mkuu inashirikiana na Viongozi wa Wilaya kutoa huduma kadiri
tathmini inavyoendelea. Maeneo mengi nchini yameendelea kupata mafuriko na
kuathiri shughuli za wananchi. Kufuatia hali hiyo, Serikali imechukua hatua
mbalimbali katika kukabili na kurejesha hali ikiwa ni pamoja na kujenga
miundombinu ya barabara, umeme, reli na majengo ya umma yaliyoathirika na kutoa
misaada ya kibinadamu kwa waathirika.
194.
Mheshimiwa
Spika, Serikali pia imeendelea kutoa elimu kwa umma pamoja na
kuzijengea uwezo Kamati za Usimamizi wa Maafa katika ngazi zote. Lengo ni
kuongeza uelewa na kuimarisha ustahimilivu dhidi ya
majanga kwa kupunguza vihatarishi na vyanzo vinavyoweza kusababisha maafa. Aidha,
kutokana na mvua nyingi zinazoendelea kunyesha nchini, naelekeza wakuu wote wa Mikoa na Wilaya
kuhakikisha wananchi walioweka makazi katika maeneo hatarishi ikiwemo
kandokando ya mito na mabonde wanahama mara moja katika maeneo hayo ili
kupunguza madhara yanayoendelea kujitokeza katika jamii.
195.
Mheshimiwa
Spika,
katika Mwaka 2020/2021, Serikali itaendelea kuimarisha
mifumo ya utoaji wa taarifa za tahadhari za awali na kuzingatia Wasifu wa Janga la Mafuriko na Ukame
nchini. Wasifu huo, unajumuisha taarifa za ramani ya maeneo
hatarishi, rasilimali, miundombinu
muhimu katika maeneo hayo, hatari ya kudhurika na makadirio ya hasara za
kiuchumi kutokana na madhara ya mafuriko na ukame.
Mazingira
196.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kukabiliana na uharibifu
wa mazingira ikiwemo kuhamasisha upandaji miti, usafi na utunzaji wa mazingira
sambamba na kuanza mradi wa usambazaji gesi majumbani na kupiga marufuku matumizi
ya mifuko ya plastiki.
197.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2019/2020, Serikali imeendelea kutekeleza mradi wa
usambazaji wa gesi majumbani, viwandani na katika magari. Hadi kufikia Desemba
2019, Serikali imekamilisha ujenzi wa miundombinu ya usambazaji gesi asilia na
kuunganisha nyumba 125 na Taasisi 4 mkoani Mtwara. Aidha, viwanda 48
vimeunganishwa na gesi asilia ikiwemo viwanda vya Coca Cola, Tanzania Breweries
Ltd, Kiwanda cha Cement cha Wazo Hill vilivyopo Dar es Salaam na kiwanda cha
Saruji cha Dangote kilichopo Mtwara. Halikadhalika, ujenzi wa miundombinu ya
kuunganisha nyumba 185 na Taasisi 4 jijini Dar es Salaam nao umekamilika.
198.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imefanikiwa
kusimamia utekelezaji wa katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki hapa nchini.
Katika Mwaka 2019/2020, tani 259.2 za mifuko ya plastiki zilikusanywa nchi
nzima. Kati ya hizo, tani 171.5 ziliteketezwa na tani 86.7 zilirejelezwa katika
viwanda mbalimbali hapa nchini. Aidha, Serikali imeendelea kusimamia ubora na
matumizi ya mifuko mbadala.
199.
Mheshimiwa Spika, katazo la mifuko ya plastiki limetoa fursa za kuzalisha mifuko mbadala
ambapo wadau wengi wamejitokeza kuwekeza katika sekta hiyo. Kwa mfano, hadi
sasa idadi ya viwanda vipya vinavyozalisha mifuko mbadala vimefikia 7. Kati ya
hivyo viwanda 6 vipo Dar es Salaam na kimoja kipo Arusha.
200.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuziagiza
Halmashauri zote nchini kuendelea kutunza mazingira ili kukabiliana na
uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu na
mabadiliko ya tabianchi.
201.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, pamoja na
mambo mengine, Serikali itaendelea na zoezi la kuunganisha viwanda na nyumba
nyingi zaidi kwenye mtandao wa matumizi ya gesi asilia katika Mikoa ya Dar es
Salaam na Mtwara. Vilevile, Serikali itaimarisha juhudi za kuhifadhi na kulinda
mazingira kwa kutekeleza miradi mbalimbali.
MUUNGANO
202.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kushirikiana
vyema na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuuendeleza na kuudumisha
Muungano wetu. Katika Mwaka 2019/2020, vikao mbalimbali vya Wataalam na
Makatibu Wakuu vilifanyika na kujadili masuala ya uvuvi kwenye ukanda wa bahari
kuu, na hoja za fedha na biashara baina ya Zanzibar na Tanzania Bara. Aidha,
maandalizi ya vikao vya pamoja vya Mawaziri wa SMT na SMZ yamefanyika ikiwemo
na kuundwa kwa kamati ya kitaifa inayoratibu ugonjwa wa Corona.
203.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Dkt. Ali
Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa
kuendelea kuenzi dhamira ya Waasisi wa Muungano.
204.
Mheshimiwa Spika, ndugu zetu Wachina wanao msemo maarufu usemao, “When we drink water from the well, we
should not forget those who dug it.” Msemo huu humaanisha kuwa,
tunapokunywa maji kutoka kwenye kisima basi tusisahau fadhila za waliochimba
kisima hicho. Hivyo basi, nasi hatuna budi kuendelea kuenzi na kuheshimu juhudi
za Waasisi wa Muungano wetu
Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Mzee Abeid
Amani Karume kwa kutuachia alama ya Muungano ambao umekuwa funzo kwa mataifa
mengine. Kwa msingi huo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea
kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza wajibu wake
wa kikatiba na kisheria wa kuuenzi na kuulinda Muungano wetu sambamba na
kudumisha amani na utulivu katika pande zote mbili za Muungano.
205.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kuwashukuru wananchi wote wa Unguja na Pemba
ambao sio tu walinipokea vizuri, lakini pia walinipatia ushirikiano mkubwa
wakati wa ziara yangu ya kikazi mwezi Januari 2020 kwa ajili ya kukagua
utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015 hadi 2020
kwa upande wa Zanzibar.
206.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuimarisha
ziara na ushiriki wa viongozi wakuu katika matukio muhimu ya kitaifa sambamba
na kufanya mikutano ya mashauriano ya viongozi na watendaji kwa lengo la
kuimarisha Muungano wetu.
UHUSIANO
WA KIMATAIFA
207.
Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea kuwa na ushawishi mkubwa katika kutekeleza
majukumu yake mbalimbali ya kidiplomasia kwa mujibu wa Katiba ya Nchi, Sheria,
Kanuni na Taratibu zilizopo. Aidha, mahusiano kati ya Tanzania na Jumuiya ya
Kimataifa yameendelea kuimarika.
208.
Mheshimiwa Spika, kuimarika kwa mahusiano na ushawishi wetu kwa Jumuiya ya Kimataifa
kumewezesha Tanzania kuanzisha Balozi mpya 2 katika nchi rafiki katika Mwaka
2019/2020. Balozi hizo ni Windhoek – Namibia na Havana – Cuba. Sanjari na hilo,
Tanzania imeendelea kuridhia na kutekeleza Itifaki na Mikataba mbalimbali ya
Kikanda na Kimataifa.
209.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2020/2021, Tanzania itaendelea kuridhia na kutekeleza mikataba mbalimbali ya
kimataifa na kikanda sambamba na kuheshimu misingi ya mahusiano na mataifa
mengine duniani. Aidha, kupitia ushirikiano mzuri uliopo na ushawishi wetu kwenye jumuiya za
kikanda na kimataifa, Tanzania italinda uhuru wa
kujiamulia mambo yake yenyewe, na kujenga umoja na mtangamano wa kikanda wa Bara la
Afrika. Halikadhalika, Tanzania itashiriki kikamilifu katika kuendeleza siasa
ya kutofungamana na upande wowote kama dira na msimamo wetu katika mahusiano
baina yetu na Nchi nyingine katika Jumuiya ya Kimataifa.
210.
Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine
Serikali itaendelea kuweka mkazo katika kukuza ushirikiano kwenye nyanja
za biashara, uwekezaji, masoko ya bidhaa zetu, utalii na lugha ya Kiswahili ili
kuchochea maendeleo ya Nchi.
HABARI,
UTAMADUNI NA MICHEZO
211.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2019/2020 Serikali imeendelea kutekeleza mikakati ya kuimarisha upatikanaji wa
habari, kurasimisha kazi za kitamaduni, sanaa na ubunifu na kuhakikisha
watendaji wa kazi hizo wanapata maslahi yanayoendana na kazi zao. Aidha,
Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba lugha ya Kiswahili inaendelezwa ndani na
nje ya Nchi na kutumika kama bidhaa ya soko na chanzo cha ajira kwa wataalam wa
lugha yetu ya Kiswahili.
212.
Mheshimiwa Spika, Mkutano wa
39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa
Afrika (SADC) uliofanyika Tanzania tarehe 17 na 18 Agosti, 2019 jijini Dar es
Salaam ulipitisha lugha adhimu ya Kiswahili kuwa moja ya lugha rasmi za Jumuiya
hiyo. Serikali imeandaa Miongozo ya Ufundishaji Kiswahili kwa Wageni na
kubainisha mahitaji ya uandaaji wa Mitaala ya kufundishia Kiswahili katika Nchi
za kigeni. Aidha, kupitia kanzidata ya usajili wa Wataalam wa Kiswahili iliyopo
Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA), jumla ya wataalam 1,159
wamesajiliwa hadi mwezi Machi, 2020.
213.
Mheshimiwa Spika, nitumie
fursa hii kulipongeza Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kufuatia maboresho
muhimu kwenye mfumo wa urushaji matangazo. Tarehe 30 Machi, 2020 TBC iliweka
jiwe la msingi wa ujenzi wa jengo la studio na kuzindua programu tumizi na
tovuti ya Safari Channel. Maboresho hayo yataimarisha mfumo mzima wa urushaji
matangazo hususan taarifa ya habari (Aridhio).
214.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2020/2021, Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Huduma za
Habari Na. 12 ya Mwaka 2016 na kuratibu na kusimamia maendeleo ya michezo
nchini ikiwemo ushiriki wa timu za Taifa katika mashindano mbalimbali ya
Kimataifa.
HITIMISHO
215.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kueleza, katika kipindi cha takriban miaka mitano
tangu Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iingie
madarakani tumeshuhudia mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii.
216.
Mheshimiwa Spika, mafanikio hayo
ni ishara tosha kwa Watanzania kwamba ahadi za Chama Cha Mapinduzi ndani ya
kipindi cha miaka mitano (2015 hadi 2020) zinatekelezwa vyema na kwa mafanikio
makubwa. Hivyo basi, katika Mwaka 2020/2021, Serikali pamoja na mambo mengine,
itaweka mkazo katika masuala yafuatayo:
Mosi: Kuimarisha na kudumisha amani, utulivu, mshikamano na umoja wa kitaifa
uliopo ili kuleta maendeleo endelevu hususan tunapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu
mwezi Oktoba 2020;
Pili: Kulinda
uhuru wa kujiamulia mambo yetu wenyewe bila kuingiliwa; mipaka ya Nchi; haki;
kuimarisha ujirani mwema na kuunga mkono Sera ya Kutofungamana na Upande wowote
kama dira na msimamo wetu katika mahusiano na Nchi nyingine katika Jumuiya ya
Kimataifa;
Tatu: Kudhibiti
upotevu wa mapato kwa kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki ya
ukusanyaji wa mapato na utoaji huduma hususan kwenye Mamlaka za Serikali za
Mitaa kwa lengo la kuondoa urasimu usio wa lazima pamoja na kuwahudumia
wananchi wote kwa tija tena bila ubaguzi wa aina yoyote;
Nne: Kuendelea kuboresha zaidi mazingira ya biashara na uwekezaji;
Tano: Kuhimiza
uwajibikaji wa watendaji wa Serikali katika ufuatiliaji wa miradi ya kielelezo
hususan ujenzi wa miundombinu muhimu ya usafiri na usafirishaji, ikiwemo reli,
bandari, ujenzi wa meli, vivuko, viwanja vya ndege, barabara na madaraja;
Sita: Kuwatumikia Watanzania wote kwa kuondoa kero mbalimbali zinazowakabili
katika maeneo yao sambamba na kuimarisha upatikanaji wa huduma za jamii kwa
kukamilisha na kuendelea na ujenzi wa miradi ya miundombinu ya maji, afya na
elimu;
Saba: Kuimarisha
uzalishaji na usambazaji wa nishati ya uhakika kwa kukamilisha Ujenzi wa Bwawa
la Kufua Umeme wa MW 2,115 la Julius Nyerere na kuhakikisha vijiji vilivyobaki
katika utekelezaji wa mradi wa REA III vinapatiwa umeme;
Nane: Kuongeza
kasi ya upimaji wa ardhi, mashamba na maeneo ya makazi, uwekezaji na ujenzi wa
viwanda ili kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kutengeneza ajira zaidi kwa
watanzania;
Tisa: Kusimamia kikamilifu matumizi sahihi na yenye tija ya rasilimali
zilizopo ili zitumike kwenye maeneo yanayochochea ukuaji uchumi na utoaji
huduma bora kwa wananchi; na
Kumi: Kuhimiza Watanzania kufuata maelekezo ya Serikali
kuhusu kujikinga, kudhibiti na kutosambaza virusi vya Corona ili kupunguza
athari za kijamii na kiuchumi zinazoweza kujitokeza kutokana na maambukizi
hayo. Serikali kwa upande wake inashirikiana kwa karibu na Jumuiya ya Kimataifa
katika kukabiliana na kutokomeza maambukizi ya virusi hivyo vya Corona.
217.
Mheshimiwa Spika, natoa wito kwa kila mwananchi kuendelea kuunga mkono jitihada kubwa
zinazofanywa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya uongozi mahiri na
thabiti wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, kwa kufanya kazi kwa bidii, weledi, uadilifu, tija na
ufanisi, uaminifu na kupiga vita rushwa.
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA
ZA OFISI YA WAZIRI MKUU NA OFISI YA BUNGE KWA MWAKA 2020/2021
218.
Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2020/2021, Ofisi ya
Waziri Mkuu na Taasisi zilizo chini yake inaliomba Bunge lako Tukufu
liidhinishe jumla ya Shilingi bilioni
mia tatu kumi na mbili, milioni mia nane na mbili na mia tano ishirini elfu
(312,802,520,000); kati ya fedha hizo, Shilingi
bilioni themanini na nane, milioni mia nne ishirini na tisa na mia moja hamsini
na sita elfu (88,429,156,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni mia mbili ishirini na nne,
milioni mia tatu sabini na tatu na mia tatu sitini na nne elfu
(224,373,364,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo.
219.
Mheshimiwa Spika, Vilevile naliomba Bunge lako Tukufu
liidhinishe jumla ya Shilingi bilioni
mia moja ishirini na moja, milioni mia saba themanini na sita na mia mbili
hamsini na saba elfu (121,786,257,000) kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya
fedha hizo, Shilingi bilioni mia moja
kumi na tatu, milioni mia tano sitini na saba na mia sita arobaini na saba elfu
(113,567,647,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni nane, milioni mia mbili
kumi na nane na mia sita na kumi elfu (8,218,610,000) ni kwa ajili ya
Matumizi ya Maendeleo.
220.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment