JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA VIWANDA NA
BIASHARA
HOTUBA FUPI (TALKING
NOTES)
YA
WAZIRI WA VIWANDA NA
BIASHARA
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA (MB.),
AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2020/2021
Dodoma
Mei 05, 2020
1. UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika; kutokana na taarifa
iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Viwanda, Biashara na Mazingira, ambayo ilichambua Bajeti ya Wizara ya Viwanda
na Biashara Fungu 44 (Viwanda) na Fungu 60 (Biashara) tarehe 24 na 25 Machi,
2020 Jijini Dodoma, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu sasa likubali kupokea
na kujadili taarifa ya utekelezaji wa Mipango na Bajeti kwa Mwaka 2019/2020.
Aidha, naliomba Bunge lako tukufu likubali kupitisha Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Fedha kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa Mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Spika, naomba
Hotuba yangu yote iliyowasilishwa kwa Waheshimiwa Wabunge iweze kuingia katika
kumbukumbu za Bunge (Hansard) kama ilivyo.
Mheshimiwa Spika; awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na baraka katika majukumu niliyokasimiwa. Kwa
namna ya pekee namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniteua kuwa Waziri na kunipa majukumu
yanayobeba ajenda kuu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya ujenzi wa uchumi wa
viwanda. Nampongeza kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya SADC na namna
anavyoshughulikia masuala ya biashara katika nchi za SADC na EAC ikiwa ni
pamoja na kuomba kufutiwa madeni kwa nchi za Afrika katika kipindi hiki cha
mlipuko wa ugonjwa wa COVID -19. Nampongeza pia kwa namna anavyotuongoza kwa
ujasiri na misingi imara, yenye kusheheni uzalendo na mapenzi kwa nchi yetu.
Napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi; na Mheshimiwa
Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania; kwa jinsi wanavyomsaidia Mhe. Rais kusimamia ipasavyo misingi ya
utaifa wetu kupunguza pengo la walionacho na wasiokuwa nacho, kujenga Tanzania
yenye kutoa fursa za uhakika za kujiletea maendeleo kwa mtu mmoja mmoja na
Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika; napenda kuchukua nafasi hii, kukupongeza wewe binafsi na
Naibu Spika kwa umakini wenu katika kuliongoza na kulisimamia Bunge letu. Pia,
naipongeza na kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na
Mazingira, chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Suleiman Ahmed Saddiq, Mbunge wa
Jimbo la Mvomero, Makamu wake Mheshimiwa Kanali Mstaafu Ali Khamis Masoud,
Mbunge wa Jimbo la Mfenesini na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati. Ushauri na
maelekezo yao yamekuwa chachu muhimu sana, katika mageuzi ya kifikra na
kiutendaji ya Wizara, na hivyo kuchochea kasi ya maendeleo ya viwanda na biashara
nchini.
Mheshimiwa Spika; kwa namna
ya pekee, niwashukuru watangulizi wangu Mheshimiwa Charles John Mwijage, Mbunge
wa Jimbo la Muleba Kaskazini na Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa
Jimbo la Sikonge, waliokuwa mawaziri wa Viwanda na Biashara. Nikiri kuwa
misingi waliyoweka imeendelea kuwa chachu muhimu katika kuendeleza Sekta ya
Viwanda na Biashara nchini. Aidha, nimshukuru Katibu Mkuu mstaafu Prof. Joseph
Buchweshaija kwa ushirikiano alionipa kipindi nilichofanya naye kazi na nimkaribishe
Prof. Riziki Shemdoe Katibu Mkuu wetu mpya. Nampongeza Prof. Shemdoe kwa nguvu
na kasi aliyokuja nayo kwenye Wizara.
Mheshimiwa Spika; niwapongeze pia Mhe. Mussa Zungu, Mbunge wa Ilala, Mhe. Geogre
Simbachawene, Mbunge wa Kibakwe na Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Mbunge wa Iramba
Magharibi kwa kuaminiwa na Mhe. Rais na kuteuliwa kuwa Mawaziri. Naahidi
kuendelea kuwapa ushirikiano wa kutosha katika kutimiza majukumu yao.
Mheshimiwa Spika; naungana pia na
Waheshimiwa Wabunge kutoa pole kwa familia zilizoondokewa na Wabunge wenzetu
ambao ni Mheshimiwa Rashid Akbar, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini;
Mheshimiwa Dkt. Getrude Rwakatare aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum; Mheshimiwa
Richard Mganga Ndassa aliyekuwa Mbunge wa Sumve; na Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustino
Mahiga aliyekuwa Mbunge wa Kuteuliwa na Waziri wa Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Spika; naomba kutumia
fursa hii pia kuwashukuru viongozi na watendaji wote wa sekta binafsi,
kwa michango yao katika kuendeleza Sekta za Viwanda na Biashara. Nawashukuru
TPSF, CTI, TCCIA, TNBC, CEO Roundtable, JWT na wengine wengi. Tunaendelea
kuwategemea kama nguzo na mihimili ya kushirikiana katika kuendeleza viwanda na
biashara na kuchochea uchumi wetu kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika; hotuba hii
ya Bajeti ninayoiwasilisha leo ni matokeo ya uratibu na ushirikiano mzuri wa
viongozi wenzangu katika Wizara, akiwemo Naibu Waziri Mheshimiwa Mhandisi
Stella Manyanya, Mbunge wa Jimbo la Nyasa; Katibu Mkuu, Prof. Riziki Shemdoe;
Naibu Katibu Mkuu, Ndugu Ludovick Nduhiye; Wakuu wa Idara, Vitengo, Taasisi na
Watumishi wote wa Wizara na Taasisi. Napenda kuwashukuru na kuwapongeza kwa
kujituma, na kuonesha daima utayari wa kuboresha mbinu na mikakati ya kisekta
kwa vitendo.
Mheshimiwa Spika; nawapongeza
na kuwashukuru wananchi
wa Jimbo langu la Karagwe kwa kuendelea
kunipa ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya kitaifa
na ya Jimbo. Nawapongeza
kwa namna wanavyojibidiisha katika
kujiletea maendeleo. Aidha, ninawaahidi kwamba
nitaendelea kutetea maslahi yenu hapa Bungeni na hata nje ya
Bunge ili kuhakikisha Karagwe inaendelea kushamiri na kuleta matokeo ya mtu
mmoja mmoja, Wilaya, Mkoa na hatimaye kuongeza mchango wake kwa Taifa letu.
Kipekee namshukuru sana mke wangu mpendwa Jennifer Bashungwa, watoto na familia
yangu kwa upendo wao, uvumilivu na maombi yao wakati wote ninapotekeleza
majukumu yangu ya kitaifa.
Mheshimiwa Spika; naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuomba ushiriki wa dhati
wa kila Mtanzania katika kupambana na virusi vya KORONA ili kulinda nguvukazi
ya Taifa. Nawaomba sana Watanzania wote kuwa kila mmoja, kila familia na
jumuiya zote nchini, kutambua kuwa usalama wetu hutegemea jitihada ya kila
mmoja kujilinda na kumlinda mwenzake.
Mheshimiwa
Spika; katika
kukabiliana na janga la ugonjwa wa KORONA, Kampuni ya Kilombero Sugar ilichangia jumla ya lita 30,000 za Ethanol kwa ajili ya kutengeneza
vitakasa mikono ambapo Wizara ya Afya ilipewa lita 20,000 na kiasi kilichobaki cha
kita 10,000 zilipewa Taasisi za SIDO na TIRDO.
Mheshimiwa
Spika; hadi
sasa tayari Viwanda na Makampuni 65 yanazalisha vitakasa mikono vyenye ubora
unaokubalika na TMDA. Kwa Wastani Viwanda hivyo vinatumia kiasi cha Ethanol kwa mwezi kisichopungua lita 2,548,951. Umoja wa wenye Viwanda Vya
Dawa na Vifaa Tiba (TMPA) kwa ujumla wao (viwanda vikubwa 4) vinazalisha
vitakasa mikono kwa mwezi lita zipatazo 900,000
na viwanda vya kati na vidogo vipatavyo 61, vinazalisha lita zipatazo 2,745,000 za vitasa mikono kwa mwezi,
na kufanya jumla ya uzalishaji vitakasa mikono kuwa lita 3,645,000 kila mwezi. Kati ya hizo TIRDO huzalisha lita 90,000 kwa mwezi na SIDO huzalisha lita
18,000.
Mheshimiwa
Spika; kwa
sasa tuna viwanda viwili vya kutengeneza barakoa aina ya Surgical Masks ambavyo ni Pristine
na Five Star. Viwanda hivyo vina
uwezo uliosimikwa wa kutengeneza barakoa 150,000
kwa siku na uwezo wa uzalishaji kwa sasa ni barakoa 30,000 kwa kiwanda cha Pristine na barakoa 40,000 kwa kiwanda cha Five
Star kwa siku. Aidha, barakoa za vitambaa (cloth masks) kwa ajili ya kujikinga, tayari jumla ya viwanda 123
vimeitikia wito wa kutengeneza barakoa hizo ambapo kati yao viwanda vikubwa ni
13 na vidogo 110. Wizara inaendelea kuhamasiha viwanda vya ndani vya nguo
kutengeneza barakoa kwa wingi kuwasaidia watanzania na mapambano ya KORONA.
Natoa wito kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya zetu kuhamasisha na mafundi vyerehani
kwenye kila kijiji kushona barakoa za nguo kuwasaidia wananchi vijijini. TMDA
na TBS toeni mafunzo kupitia vyombo vya habari na wapeni ushirikiano Wakuu wa
Mikoa na Wilaya katika majukumu haya.
Mheshimiwa
Spika; katika kipindi cha kwanza cha
utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali iliweka nguvu kubwa katika
kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi 2015 – 2020.
Umakini wa utekelezaji Ilani ya CCM umehamasisha na kuchochea ujenzi wa uchumi
wa viwanda ili kufikia malengo ya maendeleo yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa
2025.
2.1
Kukidhi Mahitaji ya Ndani ya Bidhaa za
Viwandani
Mheshimiwa Spika; Nchi yetu imejitosheleza katika baadhi ya bidhaa muhimu zinazozalishwa
nchini. Saruji (uzalishaji halisi ni tani Milioni 7.4 na mahitaji halisi tani Milioni
4.8); marumaru (uzalishaji halisi ni mita za mraba Milioni 32.4 na mahitaji
halisi ni wastani wa mita za mraba Milioni 30).
2.2
Ujenzi wa Viwanda Vipya
Mheshimiwa Spika; Serikali inaendelea kuhamasisha
uendelezaji na ujenzi wa viwanda nchini. Kutokana na uhamasishaji huo, jumla ya
viwanda vipya 8,477 vimeanzishwa kati ya mwaka 2015 hadi 2019. Viwanda hivyo
vinajumuisha, viwanda 201 vikubwa, 460 vya kati, 3,406 vidogo; na 4,410 vidogo
sana.
Mheshimiwa Spika; Sekta ya Viwanda Vidogo
na Biashara Ndogo imetoa ajira kwa wingi kwa Watanzania ambapo kwa sasa
inaajiri zaidi ya Watanzania 8,000,000. Ajira hizo zimewezesha wananchi
kujiongezea vipato na kutatua changamoto zao za kijamii na kiuchumi. Hii
imetokea kutokana na Serikali ya Awamu ya Tano kuweka mazingira wezeshi ikiwemo
kupunguza mamlaka za udhibiti na kufanya watanzania wengi kujiajiri na kutekeleza
azma ya ujenzi wa viwanda nchini ambapo takribani asilimia 99 ya viwanda vyote
nchini vipo chini ya sekta hiyo.
2.3
Uzalishaji wa Dawa na Vifaa Tiba
Mheshimiwa Spika; Sekta
ya Viwanda vya Dawa na Vifaa Tiba kwa sasa ina jumla ya viwanda 15 ambapo
viwanda 12 vinatengeneza dawa za binadamu, viwanda 2 ni vya dawa za mifugo na
kiwanda 1 kinatengeneza vifaa tiba. Kwa sasa viwanda vya dawa vinazalisha chini
ya asilimia 12 ya uwezo wake uliosimikwa na Serikali imekuwa ikiwawekea
wawekezaji mazingira wezeshi ili kufikia asilimia 60 ya uwezo uliosimikwa. Hatua
zilizochukuliwa ni pamoja na kuweka vivutio vya uwekezaji kwa lengo la
kuhamasisha wawekezaji wa ndani na Nje ya Nchi kwa kuondoa VAT kwa vifungashio
vya dawa zinazozalishwa nje na ndani ya nchi; kushusha kodi ya mapato kutoka asilimia
30 hadi 20 kwa mwekezaji mpya ndani ya miaka mitatu ya mwanzo; na kuweka
upendeleo maalum kwa ununuzi wa dawa zinazozalishwa na viwanda vya ndani
kupitia MSD.
2.4
Uzalishaji wa Sukari
Mheshimiwa
Spika; makadirio
ya uzalishaji wa sukari kwa msimu wa mwaka 2019/2020 yalikuwa tani 345,296 kwa
viwanda vya ndani sawa na asilimia 73.46 ya kiasi cha sukari inayokadiriwa kwa
matumizi ya kawaida. Aidha, hadi kufikia mwezi Aprili, 2020 uzalishaji wa sukari
nchini ulikuwa jumla ya tani 298,949, wakati mahitaji ya sukari kwa mwaka ni
wastani wa tani 635,000. Kati ya mahitaji hayo, tani 470,000 ni kwa ajili ya
matumizi ya kawaida na tani 165,000 kwa matumizi ya viwandani. Makadirio hayo
yametokana na ukweli kwamba mahitaji ya sukari ya matumizi ya kawaida kwa mwezi
ni wastani wa tani 38,000. Sababu zilipelekea kushuka kwa bei ni pamoja na mvua
nyingi kipindi cha vuli na kupunguza kiwango cha sukari kwenye miwa na taratibu
za usafirishaji ambazo zimesababishwa na ugonjwa wa KORONA ulioenea duniani.
Mheshimiwa
Spika; kwa
sasa Serikali imetoa tamko kuhusu uuzaji wa sukari. Matamko hayo ni pamoja na
sukari iuzwe kwa kuzingatia bei elekezi na endapo wafanyabiashara
hawatazingatia maelekezo hayo, hatua kali zitachukuliwa dhidi yao. Napenda
kuwapongeza Wakuu wa Mikoa na Wilaya ambao tumeshuhudia jitihada zao katika
kusimamia tamko la bei elekezi kwa lengo la kuwalinda walaji. Aiidha, niwaombe
Wakuu wa Mikoa na Wilaya zote nchini kwa kutumia kamati za ulinzi na usalama
kuendelea kusimamia bei za ukomo zilizotangazwa na Serikali ili wananchi waweze
kupata bidhaa hii muhimu kwa bei nafuu.
2.5
Uendelezaji
Maeneo Maalum ya Uwekezaji na Mapato Kutokana na Uwekezaji Chini ya EPZA/SEZ
Mheshimiwa
Spika; Wizara kupitia EPZA, imefanya tafiti tatu kutathmini
tija inayopatikana kutokana na kampuni zilizowekeza chini ya EPZA na tafiti
hizo zimeonesha uwepo wa tija katika uwekezaji wa maeneo hayo. Hadi kufikia
Desemba 2019, chini ya BWM-SEZ, mauzo ya Nje ya Nchi yameingizia nchi Tsh.
Bilioni 293.56 (USD 127.64); matumizi mengine ya kuendeshea biashara yameingiza
Tsh. Bilioni 146.58 (USD
63.73); kodi na tozo mbalimbali zilizolipwa kupitia TRA zimeingiza Tsh. Bilioni 17.24 (USD 7.50);
na zimepatikana ajira za moja kwa moja viwandani zipatazo 3,000.
Kutokana na manufaa hayo,
Wizara
kupitia EPZA, imekuwa ikihamasisha ushiriki wa Serikali za Mikoa katika
uendelezaji wa Maeneo ya SEZ ili kuiwezesha Mikoa husika kutumia Maeneo ya SEZ
kama chanzo cha mapato na mbinu mojawapo ya kuchochea shughuli za kiuchumi
katika mikoa husika. Hadi sasa, mikoa ya Arusha, Geita, Mwanza, Kigoma na
Songwe imetenga maeneo yatakayoendelezwa kama Maeneo Maalum ya Kiuchumi. Kupitia uhamasishaji huo,
katika
kipindi cha mwaka 2019/2020 EPZA imesajili kampuni sita (06) na hivyo kufanya
viwanda vilivyo chini ya EPZA kuongezeka kutoka viwanda 163 hadi viwanda 169
vikichangia ongezeko la mtaji unaokadiriwa kutoka Tsh. Tilioni 5.41 (USD
Bilioni 2.35) hadi Tsh. Tilioni 5.47 (USD Bilioni 2.38). Mauzo ya nje
yanakadiriwa kuongezeka kutoka Tsh. Trilioni 5.17 (USD Bilioni 2.25) hadi
takriban Tsh. Trilioni 5.21 (USD Bilioni 2.27) na fursa za ajira za moja kwa
moja kutoka 56,442 hadi 57,342.
Mheshimiwa Spika; utekelezaji wa mradi
wa Kurasini ni kuliendeleza eneo hilo kama Kituo cha Biashara na Ugavi -“Trade
and Logistic Centre”. Serikali kupitia Mamlaka ya EPZ imedhamiria kuliendeleza
eneo la kituo cha Biashara cha kurasini kama Soko la Mazao Mchanganyiko kwa
kuanzia na zao la chai, kahawa na mazao ya bustani.
Umuhimu
wa kutekeleza wazo la kujenga kituo cha Biashara na Ugavi -Kurasini kwa ajili
ya mazao ya kilimo ni kuwezesha Sekta ya kilimo kuchangia vizuri zaidi katika
pato la Taifa kwa kuwezesha uongezaji wa thamani ya mazao na biashara ya mauzo
ya nje kufanyika. Baada ya kilimo shughuli zinazofuata ni uchakataji (viwanda)
na hatimae mauzo (biashara).
Mheshimiwa Spika; Wizara kupitia NDC imekamilisha upimaji wa eneo la TAMCO ambapo jumla ya ekari 201.63 zimetengwa kwa ajili
ya ujenzi wa viwanda na miundombinu. Hadi sasa viwanda viwili (02) vinavyofanya
kazi vimeajiri watumishi 200 na ujenzi wa viwanda vipya eneo la TAMCO kibaha vinakadiriwa vitaajiri watumishi
21,220 ajira za kudumu. Madhumuni ya
Serikali ni kuwa na Industrial Park nyingi nchini ama kupitia EPZA ama NDC ama
Halmashauri zetu ili wafanyabishara na wawekezaji wenye mtaji na business plan
wakute tayari eneo lina maji, umeme na huduma nyingine muhimu.
2.6
Mikopo kwa Wajasiriamali
Mheshimiwa
Spika; Wizara
kupitia SIDO imefanikiwa kuchochea uanzishwaji wa shughuli za kiuchumi kwa
kutumia mikopo inayotolewa na Skimu ya Ukopeshaji kwa Wajasirimali (SME Credit
Guarantee Scheme-CGS) na Mfuko wa Wafanyabiashara Wananchi (NEDF). Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi Machi 2020, mtaji wa Mfuko wa NEDF umeongezeka kutoka Shilingi Bilioni
6.429 Machi 2016 hadi Bilioni 8.65 Machi, 2020 ikiwa ni ongezeko la Shilingi Bilioni 2.22. Ongezeko hilo limetokana na riba inayopatikana kutokana na fedha
inayojizungusha (Revolving Fund) kupitia mikopo hiyo. Aidha, jumla ya wajasiriamali 17,696
wakiwemo wanawake 8,933 na wanaume 8,721 walipatiwa mikopo iliyowezesha kupatikana jumla ya ajira 47,180. Kupitia mifuko hiyo, jumla ya viwanda vipya
437 vilianzishwa na kutoa ajira 1,481. Jitihada hizo ni kichocheo na
chachu kubwa kwa huduma na taasisi za fedha ambazo nazo hutoa huduma ya mikopo.
Mheshimiwa
Spika; mwezi Februari 2020, yalisainiwa makubaliano kati ya SIDO,
VETA, AZANIA BANK, NSSF na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) ya
kuanzisha programu ya kutoa mikopo kwa wajasiriamali waliohudumiwa na SIDO na
wahitimu wa VETA kupitia Benki ya AZANIA. Makubaliano hayo yalifanyika chini ya
uratibu wa NEEC yanatoa nafasi kwa SIDO na VETA kuwapeleka wajasiriamali na
wahitimu Benki ya AZANIA kuomba mikopo ya viwanda ya kuanzia Tshs milioni 8 hadi
milioni 500. Fedha zitakazokopeshwa kiasi cha TSh. Bilioni tano (5) zimetolewa
na NSSF kwa mkopeshaji ambaye ni Benki ya AZANIA.
Mwongozo wa utekelezaji wa programu
unaandaliwa ndipo utekelezaji wa programu hiyo uanze. Wizara inakusudia kuweka
msukumo mkubwa wa program hiyo ili iwafikie wajasiriamali wengi nchini na wapate
kunufaika. Tunawashukuru NSSF na AZANIA Bank na natoa wito kwa mabenki yote
nchini na mifuko ya jamii kuiga mfano huu ili kuinua wajasiriamali nchini.
2.7
Majengo
na Maeneo kwa Shughuli za Wajasiriamali
Mheshimiwa Spika; Serikali imefanikiwa kutenga maeneo
maalum kwa ajili ya wajasiriamali kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi. Jitihada
hizo zimewezesha ujenzi wa majengo viwanda (Industrial Shades) 12 katika mitaa ya viwanda ya SIDO
iliyopo mikoa ya Dodoma (3), Manyara (3), Kagera (1), Mtwara (1) na Geita (4). Jumla
ya viwanda 29 vimeweza kusimikwa katika majengo hayo na hivyo kuzalisha ajira
648. Kutokana na umuhimu huo, Wizara inaendelea na ujenzi wa majengo ya viwanda
katika mikoa mingine kwa kuanzia mikoa ya Kigoma, Mtwara na Ruvuma ambapo SIDO imekamilisha
upembuzi yakinifu wa majengo matatu pamoja na michoro ya usanifu (architectural
drawings) katika mikoa ya Mtwara (2) na Kigoma (1) na ujenzi umeanza.
Mheshimiwa Spika; ukamilishaji
wa majengo viwanda (industrial sheds)
unategemewa kuwezesha uanzishwaji wa viwanda vipya saba vitakavyotengeneza
ajira 76. Vilevile, Serikali imefanikisha
kusogeza karibu
huduma za kusaidia na kuhamasisha wananchi kushiriki katika ujenzi wa uchumi wa
viwanda kwa kujenga ofisi nne (4) za SIDO katika
mikoa mipya ya Simiyu, Katavi na Geita.
Mheshimiwa Spika; katika kutumia fursa za masoko ya
kikanda, Wizara imefanikisha kuongezeka kwa mauzo ya bidhaa na huduma kwenye masoko hayo
yanayotoa fursa za upendeleo maalum (preferential market access). Tanzania
imekuwa na urari chanya wa mauzo ya bidhaa kwenda kwenye masoko ya nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa
Afrika (SADC). Mfano, kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka mwaka
2015 hadi mwaka 2018 Tanzania imekuwa na
urari chanya wa mauzo ya bidhaa kwa wastani wa USD Milioni 288.04.
2.9
Uboreshaji Mazingira ya Biashara Nchini
Mheshimiwa Spika; katika kuboresha mazingira ya biashara nchini, Wizara
imefanikiwa kuandaa na kutekeleza Mpango wa Kuboresha Mfumo wa Udhibiti wa
Biashara Nchini – BLUEPRINT. Mpango huo umewezesha maboresho ya tozo 173 ambapo tozo 163
zimefutwa na tozo kero 10 zimepunguzwa kiwango. Kati ya tozo zilizofutwa, 114
ni za Sekta ya Kilimo na Mifugo, 5 za OSHA, 44 za TBS, Mamlaka za Mkemia Mkuu
wa Serikali (GCLA), Utalii, Maji, Uvuvi na iliyokuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa
- TFDA. Aidha, tozo zilizopunguzwa ni za GCLA. Mpango huo umewezesha kuhamisha
jukumu la usimamizi wa masuala ya chakula kutoka iliyokuwa TFDA kwenda TBS, ili
kuondoa muingiliano wa majukumu. Maboresho hayo yamesaidia kuondoa urasimu na
kupunguza gharama za kufanya biashara.
2.10
Utoaji Huduma za Kieletroniki kwa Wafanyabiashara na
Wajasiriamali Nchini
Mheshimiwa Spika; kutokana na kufutwa kwa tozo hizo, usajili wa usalama mahali
pa kazi (workplace) umeongezeka kutoka 16,457 mwaka 2019 ikilinganishwa na mahala
pa kazi 11,963 mwaka 2018. Aidha, BLUEPRINT imeandaliwa Mpango Kazi (Blueprint
Action Plan-BAP) ili kuongoza utekelezaji wake. Sambamba na hilo, Serikali inaendelea na
maandalizi ya kutunga Sheria ya
Uwezeshaji Biashara ya mwaka 2020 (Business Facilitation Act, 2020), ili kuipa
nguvu ya kisheria misingi ya maboresho iliyobainishwa katika Blueprint. Rasimu ya Waraka wa Sheria hiyo imekwishawasilishwa
kwenye ngazi za maamuzi Serikalini.
Mheshimiwa Spika; Wizara inafanya kila
linalowezekana kuboresha utendaji wa
BRELA na mifumo yake ya Usajili wa Majina ya Biashara, Makampuni, Alama za
Biashara na Huduma, Hataza, Leseni za Viwanda na Leseni za Biashara kwa njia ya
Mtandao. Hadi kufikia Machi, 2020, Wakala imesajili Makampuni
7,549, Majina ya Biashara 12,627, Alama za Biashara na Huduma 1,970, Hataza 55,
Leseni za Viwanda 200 na Leseni za Biashara 9,927.
Mheshimiwa Spika; Wizara kupitia BRELA imekusanya taarifa za bidhaa mbalimbali kutoka
Taasisi za Serikali zaidi ya ishirini (20) za kutoka Tanzania Bara na Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar. Tayari taarifa za bidhaa zaidi ya 18 zinazosafirishwa
nje ya nchi (Export) na zaidi ya bidhaa 8 zinazoingizwa nchini (Import) zimekwishakusanywa
na kuingizwa kwenye Mfumo.
2.11 Kuwaunganisha
Wazalishaji, Wasindikaji na Wafanyabiashara na Masoko ya Ndani na Nje ya Nchi
Mheshimiwa Spika; Wizara kwa
kushirikiana na Wizara ya Kilimo, Taasisi za Soko la Bidhaa Tanzania (TMX),
Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TanTrade) na AGRA inaandaa mkakati wa namna
bora ya kufungamanisha Sekta za Kilimo na masoko kwa mazao ya kimkakati
yatakayozalishwa nchini. Mkakati huo unalenga: Kuunganisha wazalishaji ikiwemo
wakulima na wasindikaji wa ndani na nje ya nchi; Kujenga na kuhamasisha uelewa
wa pamoja kuhusu dhana ya uwezeshaji badala ya kudhibiti biashara kwa Taasisi
na Mamlaka za Serikali zinazohusika na utoaji wa vibali na leseni za biashara;
na Kuweka vivutio kwa sekta binafsi kuwekeza katika uzalishaji wa mazao ya
kilimo.
Mheshimiwa Spika; Wizara kupitia TanTrade imeratibu
tafiti za kutambua fursa za masoko ili kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika
masoko ya nje. Kipaumbele ni katika masoko ya: China (Madini, Vito, Nyama,
Tumbaku, Korosho na Muhogo); India (Mikunde, Korosho, Ngozi na Nafaka); Ulaya
(Matunda, Mbogamboga, Asali, Kahawa na Korosho); na Nchi za EAC (nafaka, bidhaa
za ujenzi, bidhaa za ngozi, bidhaa za viwandani na vyakula vya mifugo); na Nchi
za SADC (Madini, nafaka, bidhaa za viwandani, bidhaa za ujenzi). Aidha,
mikutano na misafara ya kibiashara iliyoratibiwa ilizingatia na kutumia matokeo
ya tafiti hizo na hivyo kufanikisha kutumia fursa hizo za biashara.
2.12
Kuimarika kwa Biashara za Mipakani
Mheshimiwa Spika; Serikali imewezesha kuanzishwa kwa Vituo
kumi vya Mipakani. Aidha, kati ya hivyo Vituo sita vinafanya kazi kwa mujibu wa
utaratibu wa OSBPs, Vituo viwili (Hororo/Lungalunga; na Sirari/Isebania) ujenzi
wake umeshakamilika vinasubiri kuzinduliwa rasmi. Vituo viwili vilivyobaki
(Kasumulo/Songwe; na Mugina/Manyovu) viko kwenye hatua za awali za ujenzi. Vilevile, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na
masoko ya kimkakati kwa ajili ya kukuza biashara na mauzo nje ya nchi kwa
maendeleo ya wananchi wake na Taifa kwa ujumla. Kutokana na umuhimu huo,
Serikali imekuwa ikichukua hatua za kuanzisha, kuboresha na kuendeleza masoko
ya kimkakati ya mipakani ya Nkwenda na Murongo (Kyerwa), Kabanga (Ngara),
Kahama (Kahama), Remagwa (Tarime) na Bweranyange (Karagwe) ili kurasimisha
ufanyaji biashara. Kwa sasa Wizara inaratibu Mradi wa Ujenzi na Uboreshaji wa
Masoko ya Mipakani ili kuhakikisha wananchi waishio mipakani wananufaika
ipasavyo. Jitihada
hizo zimekwenda sambamba na mpango wa Wizara wa ujenzi wa masoko ya kimkakati
mipakani.
2.13
Kuhuisha Soko la Biashara ya Zao la Tumbaku
Mheshimiwa
Spika; kipekee
naomba nimpongeze Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali anayoingoza kwa namna alivyosimama imara na kuweka msimamo thabiti
dhidi ya mifumo ya kumyonya mkulima katika mazao mbalimbali na hususan korosho,
pamba, kahawa na mazao mengine. Wizara itahakikisha kupitia taasisi zake
ikiwemo FCC inasimamia na maeneo mengine kuharibu mifumo ya aina hiyo
iliyowekwa na wafanyabishara wasio waaminifu kwa lengo la kumnyonya mkulima.
Mheshimiwa Rais ni mfano wa kuigwa katika utendaji wetu hasa katika kuhakikisha
haki za wakulima na wananchi wanyonge zinalindwa. Na hii inadhihirisha utayari
wake katika kuhamasisha wananchi kufanya kazi kwa kujituma na hivyo kuakisi
kauli yake ya “HAPA KAZI TU”.
Mheshimiwa Spika; Wizara imefanikiwa
kuhuisha soko la zao la Sekta ya Tumbaku baada ya Serikali kufikia muafaka na
wanunuzi wakuu wa zao hilo kuhusiana na madai ya ukiukwaji wa taratibu za
ushindani. Mahauri dhidi ya allince one, Alliance one international na ATTT
yameshamalizika kwa suluhu na kufungwa ili wadau hao waendelee na shughuli zao
katika kuendeleza sekta ya tumbaku. Aidha, mashuri yaliyokuwa yanaikabili TLTC,
TTPL, ULT na ATTT nayo pia yamemalizwa kwa suluhu.
Hadi sasa mchakato wa kumaliza kwa suluhu mashauri
yanayowakabili kampuni ya JTI Leaf Services Limited na JT International
uko hatua za mwisho. Kutokana na mwenendo huu wa suluhu kampuni ya JTI Leaf
Services Limited katika mpango wake wa ununuzi imethibitisha kununua
tumbaku yenye thamani ya USD Milioni 12.6 kwa mwaka 2019/2020, USD Milioni 14.1
kwa mwaka 2020/2021, USD Milioni 15 kwa mwaka 2021/2022 na USD Milioni 15.5 kwa
mwaka 2022/2023.
2.14 Miradi ya NDC
Mheshimiwa
Spika;
Serikali kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) inatekeleza miradi mikubwa
mitatu ambayo ni; mradi wa kuunganisha na kuuza matrekta aina ya URSUS (Ubia wa
NDC na kampuni ya URSUS ya Poland); mradi wa ujenzi na uendeshaji wa kiwanda
cha viuadudu (Ubia wa NDC na kampuni ya LABIOFAM ya Cuba); na mradi wa makaa ya
mawe (Ubia wa NDC na kampuni ya Intra
Energy Tanzania Ltd na kuendesha kampuni ya TANCOAL Energy Ltd).
Mheshimiwa
Spika;
utekelezaji wa miradi hiyo umekabiliwa na changamoto mbalimbali kiasi cha
kuathiri matokeo chanya yaliyotarajiwa na Serikali. Aidha, jitihada mbalimbali
zimekuwa zikifanywa na Serikali ili kupata ufumbuzi wa changamoto hizo. Mwezi
Machi,2019 Wizara kwa kushirikiana na Taasisi mbalimbali za Serikali tumeanza kufanya
mapitio, tathmini na uchunguzi wa miradi hiyo, ikiwemo kuunda timu za Serikali
zijadiliane na timu ya Serikali ya Poland kwa mradi wa matrekta ya URSUS; Serikali
ya Cuba kwa mradi wa viuadudu uliopo Kibaha; na timu ya kampuni ya Intraenergy Tanzania kwa ajili ya mradi
wa makaa ya mawe ya ngaka (TANCOAL).
Mheshimiwa
Spika;
timu hizo zimeshaundwa na zinatarajia kuanza vikao vyake hivi karibuni. Kutokana
na changamoto za CORONA tunatarajia vikao hivyo vitafanyika kwa njia ya Video Conference. Wizara inaamini kuwa
makubaliano katika majadilino hayo yataleta matokeo chanya katika utekelezaji
wa miradi hiyo na inakuwa na manufaa zaidi kiuchumi na kijamii kwa Taifa,
hususani katika ujenzi na uendelezaji wa sekta ya viwanda nchini.
Mheshimiwa Spika; Wizara iliandaa na kuwasilisha Waraka wa Itifaki ya
Marekebisho ya Mkataba wa Marrakesh
ulionzisha Shirika la Biashara la Dunia ili kufanya Mkataba wa Uwezeshaji
Biashara (Trade Facilitation Agreement) kuwa sehemu rasmi ya mikataba ya WTO. Tayari
waraka huo umekwisharidhiwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Hati
ya Kuridhia (Instrument of Ratification) ya Itifaki hiyo imekwishasainiwa na kuwasilishwa
WTO. Vilevile, Itifaki ya Marrakesh inayolenga
kuwezesha upatikanaji wa kazi zilizochapishwa kwa watu wasioona, wenye uoni
hafifu, ulemavu unaofanya mtu kushindwa kusoma wa mwaka 2013 iliridhiwa
na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tayari, Hati ya
Itifaki hiyo imesainiwa na kuwasilishwa WIPO. Tunashukuru Waheshimiwa Wabunge
na Mheshimiwa Rais kwa kuridhia na kufanikisha Mikataba na Itifaki hizo.
3.
MWELEKEO
NA VIPAUMBELE VYA SEKTA YA VIWANDA NA BIASHARA
3.1
Mwelekeo wa
Sekta ya Viwanda na Biashara
Mheshimiwa Spika; mtazamo na mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Chama
cha Mapinduzi kuhusu maendeleo ya viwanda na biashara nchini, unalenga kujenga
uchumi wa viwanda utakaowawezesha Watanzania kufikia na kunufaika na uchumi wa
kati ifikapo 2025. Hatua hiyo itawezesha Watanzania kutumia fursa za kiuchumi na
kijamii katika mifumo iliyoboreshwa na inayozingatia haki na utawala bora. Ni
dhamira ya nchi yetu kumfanya kila Mtanzania kuwa na maisha bora na kunufaika
na rasilimali na fursa zilizopo na zinazojitokeza.
i.
Kuhamasisha Uendelezaji na Matumizi ya
Bidhaa za Ndani
Mheshimiwa Spika; kuthamini rasilimali na bidhaa za ndani ni
ukombozi muhimu wa kiuchumi kwa Taifa lolote. Mifano hai ni nchi ya Japan na
China ambazo wananchi wake wamejijengea utamaduni wa kuthamini bidhaa
zinazozalishwa katika uchumi wao. Hivyo, Wizara itaendelea kuhamasisha uimarishaji
wa ubora na matumizi ya bidhaa za ndani, nguvukazi na malighafi za ndani ili
kuleta ufungamanisho wa sekta katika kujenga uchumi na kuleta maendeleo kwa
wananchi wake. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na TanTrade inaendelea
kuhamasisha wananchi kutumia bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya ndani kupitia
kauli mbiu ya Nunua Bidhaa za Tanzania, Jenga Tanzania (Buy Tanzania, Build
Tanzania). Mbinu hiyo ni muhimu sana katika kipindi hiki cha ujenzi wa uchumi
wa viwanda ili kuimarisha viwanda vya ndani na kutumia Kiswahili katika bidhaa.
ii.
Kuimarisha
SIDO
Mheshimiwa Spika; kwa kutambua umuhimu na mchango wa Sekta ya
Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo katika uchumi na hususan ujenzi wa viwanda,
Serikali itachukua hatua za makusudi kuimarisha ujasiriamali nchini. Kipaumbele
kitakuwa katika kuimarisha taasisi ya SIDO kwa kupitia upya muundo wake na
kuijengea uwezo ili iweze kubeba ipasavyo dhamana ya uendelezaji wa viwanda
vidogo na biashara ndogo inayowabeba Watanzania walio wengi. Jitihada hizo
zitaenda sambamba na kuendelea ujenzi wa shades katika mikoa yote nchini
ili manufaa yalioyoonekana ya ajira na uongezaji thamani wa mazao, na kuongeza
ushindani katika soko yasambae nchi nzima.
Mweshimiwa Spika; Wizara pia itaweka mkazo na umuhimu katika
upatikanaji wa teknolojia, kuongeza miundombinu ya uzalishaji (Industrial
shades) ili kuwawezesha wajasiriamali kupata mahali pa kufanyia uzalishaji, na
kuweza kuhudumiwa kirahisi na taasisi mbalimbali zikiwemo za udhibiti wa ubora
wa bidhaa, taasisi za fedha na mafunzo muafaka. Juhudi za kuimarisha
jasiriamali nchini zitaenda sambamba na kuimarisha SIDO ili imudu kutoa huduma
bora na zenye kuleta tija katika uzalishaji wa bidhaa, huduma na ufanyaji
biashara.
iii.
Kuvilinda Viwanda na Biashara za Nchini
Mheshimiwa Spika; uchumi himilivu unaotabirika na shindani
unatokana na jitihada za kuujenga, kuuendeleza na kuulinda. Kujilinda
isitafsiriwe kuwa ndiyo kujitenga kiuchumi na nchi nyingine, na wala siyo
dhambi, kwani hata nchi zilizoendelea kiuchumi duniani mbinu mbalimbali zinaendelea
kutumika kwa njia tofauti. Hivyo, sera, sheria na mikakati ya kisekta
itaendelea kuhakikisha kuwa kunakuwepo ushindani wa haki ili kulinda viwanda na
biashara nchini. Aidha, tutaendelea kulinda haki za msingi za walaji kwa kuweka
utaratibu wa kisheria utakaotaka wawekezaji, wenye viwanda na wafanyabiashara
katika mazao, bidhaa na huduma kutotumia nguvu ya soko isivyotakiwa na
kusababisha kuwakandamiza wanyonge.
Mheshimiwa Spika; ili kuongeza nguvu za utafutaji wa fursa za
masoko ya nje, Wizara inafanya uchambuzi wa kina wa kuona umuhimu wa kuhuisha
na kurejesha Waambata wa Biashara (Trade Attachee) katika ofisi za Balozi zetu
zilizo nje ya nchi, ili kuweka mfumo wa kufanya tathmini na utafiti wa mahitaji
ya soko la bidhaa zinazozalishwa nchini. Tathmini na tafiti hizo zitatoa picha
ya mahitaji ya soko la nje na kuwezesha wazalishaji wa bidhaa za ndani
kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko la nje.
Mheshimiwa Spika; utoaji huduma bora kwa
wananchi kwa kiwango kinachoridhisha ni lengo kuu la mabadiliko ya kiutendaji
ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inayapa kipaumbele. Hivyo, mwelekeo wetu ni
kuhakikisha kuwa taasisi za kisekta zinajielekeza katika kutoa huduma kwa
kiwango kinachokidhi matarajio ya wananchi. Wizara yangu na taasisi zake
zitaongeza ubunifu katika utendaji kazi kwa tija na kutoa huduma kwa weledi ili
kuchochea ufanisi katika Sekta ya Viwanda na Biashara na hatimaye kuongeza Pato
la Taifa.
iv.
Uimarishaji wa Taasisi za Udhibiti na
Maendeleo ya Teknolojia na Uwekezaji Nchini
Mheshimiwa Spika; katika kuendeleza uchumi wa viwanda, Serikali
inaimarisha taasisi zake ili ziweze kukidhi na kuhimili mahitaji ya maendeleo
na ujenzi wa viwanda nchini. Wizara inajizatiti kuimarisha Taasisi za Utafiti
na Maendeleo ya Teknolojia yaani TIRDO, TEMDO na CAMARTEC kwa kufanya tathmnini
ya kitaalam, kupitia upya na kwa kina majukumu na miundo ya kisheria ya taasisi
hizo. Lengo ni kuzifanyia maboresho mahsusi yatakayozingatia ushauri wa
kitaalam na itakapoonekana inafaa, zitafanyiwa maamuzi ya kimuundo ikiwemo
kuziunganisha ili ziweze kuwa na tija na ufanisi katika kuleta mwendelezo wa
mafanikio ya taasisi hizo na pia kuongeza nguvu katika kuendeleza viwanda
nchini.
Mheshimiwa Spika; Serikali pia kwa kuzingatia tathmini ya
kitaalam, itajielekeza katika kuimarisha taasisi za uwekezaji nchini hususan
EPZA na NDC ili ziwe mihimili na nguzo za uwekezaji katika viwanda ambavyo ni
muhimu katika kujenga uchumi wa Taifa lakini wakati mwingine sekta binafsi
haiko tayari kuwekeza. Msukumo ukiwa ni kuunda taasisi / mamlaka mpya
itakayobeba jukumu la kujenga viwanda mama, viwanda vya kimkakati.
v.
Kutunga Sheria (Business Facilitation Act)
kutekeleza Mpango Kazi - BLUEPRINT
Mheshimiwa Spika; ujenzi wa mazingira bora na endelevu ya
biashara ni kichocheo kikubwa na muhimu katika kuvutia uwekezaji wa ndani na
nje. Hivyo, Serikali kupitia Wizara yangu imejipanga kuhakikisha kuwa
inaendelea kuboresha mazingira ya biashara nchini. Maboresho hayo yatavutia
wawekezaji wa ndani na nje katika viwanda na biashara na hivyo kuwezesha kutumia
fursa mbalimbali za ndani na nje ya nchi kadri zinavyojitokeza. Misingi ya
maboresho ya mazingira ya kibiashara yanategemewa kuwekewa nguvu ya kisheria na
utaratibu wenye ushirikishaji mpana zaidi wa wadau.
vi.
Muunganisho
wa Kiutendaji Kati ya Wizara na Mamlaka za Serikali za Mitaa
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa utendaji kazi
wenye tija katika ngazi za Makatibu Tawala Mkoa (RAS) na Mamlaka za Serikali za
Mitaa (LGAs), Kada za Maafisa Biashara zitapewa msukumo wa kipekee, ili
kuhakikisha inahuishwa na kufanya kazi zake kitaaluma. Aidha, Wizara imeanza
mazungumzo na Ofisi ya Rais TAMISEMI ili kuandaa Mkataba wa Makubaliano
(Memorandum of Undestanding) wa kuweka mifumo na mazingira bora ya kufanya kazi
pamoja na kwa kushirikiana.
vii. Utungaji wa Sheria ya Kujilinda Dhidi ya Athari za Biashara (Trade Remedies Act, 2020)
Mheshimiwa Spika;
Wizara inaendelea na taratibu za kutunga Sheria ya Kujilinda Dhidi ya Athari za
Kibiashara ya mwaka 2020 (Trade Remedies Act, 2020) ambayo inalenga kulinda
biashara na viwanda vya ndani. Ulinzi huo unalenga kuzuia uingizwaji wa bidhaa
kwa wingi (import surge); bidhaa kuuzwa kwa bei ya chini ikilinganishwa na bei
ya bidhaa kama hizo kwenye nchi zinakotoka (dumping); na bidhaa nyingine kupewa
ruzuku (subsidies) na nchi zao au taasisi nyingine na hivyo kuathiri bidhaa
ambazo zinazalishwa ndani ya nchi bila kupata ruzuku. Mapendekezo ya kutunga
Sheria hiyo yamekwishawasilishwa Serikalini kwa ajili ya maamuzi.
viii.
Utekelezaji wa Mikakati Mbalimbali ya
Uendelezaji Viwanda Nchini
Mheshimiwa Spika; Mkakati wa Kuendeleza Sekta ya Ngozi wa mwaka 2016-2020 umejikita katika
kuendeleza mnyororo wa thamani wa Zao la Ngozi. Katika kutekeleza mkakati huo,
Serikali imetoa msamaha wa ushuru wa forodha kwenye malighafi na vifaa vinavyotumika
kutengenezea viatu na bidhaa za ngozi vinavyoingizwa kutoka nje ya nchi. Lengo
likiwa ni kupunguza gharama za uzalishaji kwa viwanda vya ngozi na kuvutia
uwekezaji. Fursa hiyo imetumiwa na Kiwanda cha Karanga Leather Industries ambacho hivi karibuni kimeingiza mashine
na vifuasi (accessories). Vilevile, Kiwanda cha ACE leather Morogoro kimetumia fursa hiyo kuingiza mashine na
vifuasi ili kusindika ngozi hadi hatua ya mwisho. Mkakati huo pia
umehamasisha taasisi za umma na shule kununua bidhaa za ngozi hususan viatu
kutoka viwanda vya ndani kulingana na upatikanaji. Kwa sasa maandalizi
ya kuhuisha Mkakati huo yanaendelea.
ix.
Kuimarisha Sekta Binafsi
Mheshimiwa Spika; mtazamo wa Sera za Taifa zinatambua nafasi ya
sekta binafsi kama injini ya maendeleo ya kiuchumi. Kujenga sekta binafsi hasa
wajasiriamali wadogo kwa kuwawekea mazingira wezeshi na rafiki kupitia
upatikanaji wa mitaji, teknolojia rahisi na rafiki, masoko ya uhakika na huduma
muhimu zinazolenga kuongeza tija na ufanisi katika uzalishaji ni suala lisilohitaji
mjadala. Hivyo, katika kuendeleza Sekta ya Viwanda na Biashara, mtazamo wa kisera
utalenga kukuza na kutengeneza uwekezaji kuanzia ngazi ya ujasiriamali mdogo
hadi kuwa matajiri wazalendo wa baadaye. Msukumo utawekwa katika kuweka sera zinazotabirika,
kujenga mazingira yanayotabirika na kutoa fursa ya masoko.
x.
Nguvukazi Kukidhi Mahitaji ya Viwanda
Mheshimiwa Spika; suala la kuwa na rasilimali watu ya kutosha
yenye sifa, uwezo na inayotumika vizuri ni muhimu katika kujenga uchumi
endelevu wa viwanda. Wizara imejipanga kuendeleza kimkakati rasilimaliwatu iliyonayo
kwa kuwa na mpango mpana wa kuwaendeleza na kuwajengea uwezo watumishi wa Wizara
ili kuongeza ujuzi na weledi katika kutekeleza majukumu yao. Hii itawezesha
kuboresha huduma zitolewazo na kukidhi matarajio ya wadau na umma wa ujumla. Tutajielekeza
zaidi katika maeneo ya kuboresha huduma (service delivery) kwa njia mbalimbali,
kuimarisha usimamizi na uratibu wa shughuli za kisekta (Regulatory role) na kuishirikisha
sekta binafsi na wadau wengine kuchangia kikamilifu katika kukuza uchumi. Ili
kuwa na rasilimaliwatu yenye afya, Wizara itahakikisha kuwa watumishi wanapata
elimu ya afya na huduma za kinga dhidi ya magonjwa yanayoambukiza na
yasiyoambukiza.
xi.
Kuendeleza Maeneo Maalum ya Uwekezaji
Mheshimiwa Spika; kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya
msingi na wezeshi kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na ufanyaji biashara ni suala
la msingi. Uendelezaji wa miundombinu hiyo kwa kushirikiana na sekta binafsi
utapewa msukumo zaidi ili kuleta tija na mvuto kwa wawekezaji wa ndani na nje
ya nchi. Wizara itashirikiana na Balozi za Tanzania pamoja na Ofisi ya Waziri
Mkuu-Uwekezaji kuja na mkakati wa kuvutia wawekezji kutumia sehemu ambazo
zimefidiwa chini ya EPZA. Pia, imezindua miradi ya ujenzi wa miundombinu hiyo
katika mikoa yote nchini ambapo kwa Mkoa wa Dodoma tumeanza na ujenzi wa
Kongano la Viwanda Kizota (Kizota Industrial Cluster).
xii.
Uendelezaji wa Miradi ya Kimkakati na ya Kielelezo
Mheshimiwa Spika; katika
kuendeleza Miradi ya Kimakati, Wizara, TIRDO, Wakala wa Jiolojia Tanzania
(GST), na African Minerals and
Geosciences Centre (AMGC) ilifanya
uhakiki wa awali wa wingi na aina za madini yaliyopo kwenye miamba ya Liganga.
Matokeo ya awali yalibainisha kuwa kuna tofauti ya wingi na aina za madini
ikilinganishwa na ilivyobainishwa katika taarifa ya mwekezaji. Utafiti wa kina
unaendelea kufanyika kwa nia ya kubainisha hali halisi ya rasilimali zilizopo.
Aidha, NDC kwa kushirikisha na uongozi wa Wilaya ya Ludewa na Wizara ya Ardhi,
Nyumba na Maendeleo ya Makazi imekamilisha kazi ya uthaminishaji mali ndani ya
eneo la mradi ili kufidia wananchi watakaopisha Mradi unganishi wa Mchuchuma na
Liganga.
Mheshimiwa
Spika; TIRDO inaendelea kufanya “Techno Economic
Study” katika Mradi wa Magadi Soda Engaruka.
Lengo la utafiti huo ni kubainisha
kiasi cha mahitaji ya magadi nchini, thamani ya uwekezaji utakaofanyika na
faida za mradi huo kwa ujumla. Makadirio ya awali ya rasilimali magadi (brine)
yameonesha uwepo wa kiasi cha mita za ujazo Bilioni 4.68. Aidha, ilibanika kuwa
rasilimali hiyo inajiongeza kwa kiasi cha mita za ujazo wa Milioni 1.9 kwa
mwaka. Uhakiki wa rasilimali hiyo unaendelea sambamba na
ukamilishaji wa upembuzi yakinifu wa mradi na athari ya mradi katika mazingira
na jamii. Utafiti huo unategemewa kukamilika mwisho mwa mwezi Aprili, 2020.
3.2 Vipaumbele kwa Bajeti ya
Mwaka 2020/2021
Mheshimiwa Spika; vipaumbele vya bajeti na malengo ya sekta ya viwanda
na biashara ya mwaka 2020/2021 vimeelezewa kwa kina ukurasa 138 hadi 181 ya
hotuba ya bajeti.
4. MAKADIRIO
YA MAKUSANYO NA MAOMBI YA FEDHA KWA MWAKA 2020/2021
4.1
Makusanyo
ya Serikali
4.2
Maombi
ya Fedha
5. SHUKRANI
Mheshimiwa Spika; Naomba
nihitimishe kwa kuwashukuru tena Watanzania kwa kuendelea kuunga mkono jitihada
za Serikali katika ujenzi wa uchumi wa viwanda na hivyo kuwa kichocheo cha
kukua kwa sekta nyingine za uchumi. Ni dhahiri kuwa Taifa kwa kipindi hiki kinahitaji
kuendeleza ari hiyo katika kupambana na majanga mbalimbali ikiwemo ugonjwa wa
mafua makali wa KORONA. Kwa pamoja tuungane kujikinga na kulindana ili Taifa
libaki salama na likiwa na nguvukazi ya kutegemewa.
6. HITIMISHO
7. MAOMBI RASMI YA FEDHA
8.
MWISHO
Mheshimiwa Spika; Naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment