Habari za Punde

Kutoka Baraza la Wawakilishi Zanzibar Maoni ya Kamati Mbili .

HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA SHERIA, UTAWALA BORA NA IDARA MAALUM KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA OFISI YA RAIS, UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA
KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021
                                                                                                                                 

Mheshimiwa Spika, kila sifa njema anastahiki Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa Rehma, kwa kutujaalia Uzima na Afya njema ambavyo vimetuwezesha kukutana tena katika Baraza hili kwa lengo la kujadili na kuidhinisha Mapato na Matumizi ya Fedha za Serikali yetu Tukufu. Vile vile, nachukua fursa hii kukushukuru wewe Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Baraza kwa kuliongoza Baraza hili kwa umahiri mkubwa na ninaamini kwamba mtaendelea kuliongoza Baraza hili kwa uadilifu wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, aidha, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru na kumpongeza kwa dhati kabisa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuiongoza nchi yetu kwa uadilifu, hali inayopelekea kupatikana kwa maendeleo pamoja na kuendelea kudumu kwa amani na utulivu katika nchi yetu.


Mheshimiwa Spika, pia, sina budi kumshukuru Waziri wa Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mheshimiwa Mwalimu Haroun Ali Suleiman kwa umahiri wake uliomfanya aweze kuteuliwa tena kuwa Waziri katika Wizara hii mpya pamoja na kuwapongeza watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na bila ya kuwasahau watendaji wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa mashirikiano waliyotupatia wakati wa kupitia makadirio ya Bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, vile vile, nachukua fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati yetu kwa umoja wao na kazi nzuri waliyoifanya kiasi cha kunirahisishia kazi yangu ya kuongoza kikao kuwa nyepesi zaidi, kwa hakika ni Wajumbe mahiri, wameweza kuijadili ipasavyo na kuhoji mambo mbali mbali kwa lengo la kuhakikisha kwamba fedha wanazoidhinisha kwa Wizara hii zinatumiwa kwa matumizi yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa heshima ya hali ya juu kabisa napenda kuwatambua Wajumbe hao kwa majina kama ifuatavyo:
1.     
Mhe. Machano Othman Said
Mwenyekiti
2.     
Mhe. Zulfa Mmaka Omara
Makamu Mwenyekiti
3.     
Mhe. Ali Khamis Bakar
Mjumbe
4.     
Mhe. Salma Mussa Bilal
Mjumbe
5.     
Mhe. Dkt. Khalid Salum Mohamed
Mjumbe
6.     
Mhe. Suleiman Makame Ali
Mjumbe
7.     
Mhe. Maryam Thani Juma
Mjumbe
8.     
Ndg. Ali Alawy Ali
Katibu
9.     
Ndg. Haji Jecha Salim
Katibu
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora katika kusimamia na kutekeleza Bajeti yake,inatekeleza jumla ya Mafungu matano (5) ambayo ni Fungu E 06 – Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Fungu E 02 – Kamisheni ya Utumishi wa Umma, Fungu E 03 – Tume ya Utumishi wa Umma, Fungu E 04 – Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali na Fungu E 05 – Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ina jumla ya Programu kuu nne (4) ambazo ni:

(i)      Usimamizi na Uendelezaji wa Utumishi wa Umma;
(ii)    Huduma za Serikali Mtandao;
(iii)  Usimamizi wa Utawala Bora; na
(iv)   Uendeshaji na Uratibu wa Ofisi ya Rais Uumishi wa Umma na Utawala Bora.

Hata hivyo, Kamati yetu haikujadili fungu nambari4 la Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa vile fungu hilo lilipitiwa na Kamati ya PAC.

FUNGU E 06:       OFISI YA RAIS – UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA                                         BORA

Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza na kusimamia dhana ya Utawala Bora nchini, Kamati yetu imeridhishwa sana na utekelezaji wa programu mbali mbali ambazo zimepangwa kwa lengo la kuendeleza Utawala Bora baada ya kuona taasisi zinazohusika na usimamizi wa masuala haya zimepiga hatua kubwa za kuitetea Nchi yetu na kusimamia Haki katika jamii.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa elimu bora ndio msingi wa maendeleo na utendaji bora ambayo pia hujengwa kwa misingi imara ya elimu. Kamati yetu imeridhishwa kwa kiasi kikubwa na utekelezaji wa programu za masomo na maendeleo ya Chuo cha Utumishi wa Umma (IPA) kwa jinsi walivyojipanga katika kuhakikisha kuwa maendeleo endelevu yanafikiwa kwa kutumia dira na malengo ya elimu wanayotoa. Aidha, Kamati inazishauri Taasisi zote za Serikali na zile zisizo za Serikali kukitumia Chuo hiki kwa kuwapatia watendaji wao mafunzo ya muda mfupi kwa mwaka huu ambao nchi nyingi duniani zimezuia kutoa mafunzo ya aina hii kutokana na athari za corona.

Mheshimiwa Spika, kwa kutumia makadirio ya Bajeti ya mwaka2020/2021, Kamati inaishauri Serikali kukiwezeshana kukijengea uwezo wa kufanya tafiti Chuo hiki ili kiweze kufanya tafiti mbali mbali za kitaalamu ambazo ni dhahiri zina mchango mkubwa kwa Serikali na maendeleo ya nchi yetu. Aidha, Kamati inaishauri Serikali kukipatia Chuo hiki walimu wenye uzoefu katika kada mbali mbali ambao watakiwezesha Chuo hiki kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.

FUNGU E 02:       KAMISHENI YA UTUMISHI WA UMMA

Mheshimiwa Spika, Kamisheni ya Utumishi wa Umma, miongoni mwa programu zake ni Usimamizi wa Utumishi wa Umma na Usimamizi wa Nidhamu na Maadili ya Utumishi wa Umma. Kamati imebaini kuwepo kwa changamoto kubwa kwa baadhi ya watumishi wa Umma kushindwa kuzifahamu kikamilifu Sheria ya utumishi wa Umma na Kanuni zake ambapo kupelekea kutoweka kwa nidhamu za kiutumishi katika maeneo yao ya kazi, hali ambayo inaathiri kwa kiasi kikubwa uwajibikaji wao kazini.

Aidha, Kamati  inashauri utaratibu maalum uandaliwe wa kutolewa mafunzo kwa watumishi licha ya mafunzo ya awali yanayotolewa kwa waajiriwa wapya lakini ipo haja kwa watumishi wakongwe ambao wana uzoefu wa kutosha katika utekelezaji wa majukumu yao, kupatiwa elimu juu ya sheria na miongozo ya kazi. Mafunzo haya yatapunguzakwa kiasi kikubwa tabia mbaya kwa waajiriwa.

FUNGU E 03:       TUME YA UTUMISHI SERIKALINI

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Tume ya Utumishi Serikalini ina wajibu na jukumu la kusimamia watumishi wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na tume nyenginezo za kiutumishi, Kamati inashauri kuzidi kusimamia watumishi wa Serikali katika kuhakikisha wanapata haki zao zote za msingi sambamba na kuimarika kwa maslahi yao ya msingi.

Vile vile, Kamati inashauri Tume hii kusimamia kikamilifu na kuona kwamba watumishi wa Serikali wanapatiwa fursa zaidi za kujiendeleza kielimu kwa misingi kwamba elimu bora ndio msingi wa maendeleo katika Taasisi yoyote katika Nchi yetu. Aidha, Kamati inaishauri Tume kufuatilia kwa karibu hali za watumishi wa Umma na kuona namna wanavyojikinga na maambukizi ya virusi vya corona na kupelekea kupotea kwa rasilimali watu katika nchi.

FUNGU E 05:       MAMLAKA YA KUZUIA RUSHWA NA UHUJUMU WA UCHUMI

Mheshimiwa Spika, wajibu wa Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi ni Taasisi yenye jukumu la kuhakikisha makosa yanayohusiana na rushwa na uhujumu wa uchumi yanapungua nchini. Mamlaka hii inatarajia kuhakikisha kwamba Mfumo wa Utawala Bora na Muundo wa Serikali unakuwa wa wazi na wenye uwajibikaji wa kupingana na vitendo vya rushwa.

Mheshimiwa Spika, Kamati imeridhishwa na kipaumbele cha Ofisi hii katika ujenzi wa jengo la kudumu la Ofisi ya ZAECA huko Tunguu na hivyo, Kamati inaiomba Serikali pia,kuliingiza katika vipaumbele vyake suala hili ili ujenzi huu ufanyike kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Spika, Kamati imebaini kuwepo kwa baadhi ya changamoto ambazo zinarudisha nyuma juhudi za watumishi wa Ofisi hii Unguja na Pemba. Katika kutekeleza majukumu hayo, Kamati imebaini wapo baadhi ya watendaji wa Ofisi za Serikali na zile za binafsi kutotekeleza majukumu yao ipasavyo jambo ambalo linawanyima haki raia wasiokuwa na uwezo kiuchumi na kusimamia haki zao kisheria. Licha ya hayo, kwa kuwa maadili ya viongozi ni jambo lenye nafasi kubwa katika uimarishaji wa utawala Bora nchini, taasisi hii kwa kushirikiana na Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma inashauriwa kuwachukulia hatua viongozi wote wenye kuvunja maadili na desturi za uongozi ambao wanaonesha taswira mbaya katika ujenzi wa utawala bora.

HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, mwisho, napenda kuchukuwa fursa hii kukushukuru tena kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha maoni machache sana ya Kamati yangu, kwa niaba ya Kamati pamoja na kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako kwa kunisikiliza kwa umakini mkubwa wakati wote wa uwasilishaji wa maoni yetu.

Kamati pia, inatoa shukrani zake za dhati kwa Katibu wa Baraza la Wawakilishi ndugu Raya Issa Mselem, Mratibu wa Shughuli za Kamati ndugu, Khamis Hamad Haji pamoja na watendaji wote kwa ujumla wa Afisi ya Baraza la Wawakilishi ambao wameisaidia sana Kamati hii kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, nachukuwa nafasi hii ya pekee kuwashukuru kwa dhati kabisa Makatibu wetu wa Kamati kwa namna walivyoweza kutekeleza vyema majukumu yao katika kipindi chote cha uhai wa Kamati hii na wakati wa kujadili makadirio ya Bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, Kamati inawaomba Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako waichangie Bajeti hii na hatimae waiidhinishie Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, makadirio ya fedha zilizopangwa kutumiwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 ili wapate kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
                                                      
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kamati yangu Naomba Kuunga Mkono Hoja.

Ahsante,
(Mhe. Salma Mussa Bilal)                                                             
Mjumbe,
Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.