Habari za Punde

Dk. Shein Ametuma Salamu za Rambirambi Kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe;Dkt John Pombe Magufuli Kufuatia Kifo Cha Rais Mstaaf wa Awamu ya Tatu Tanzania Benjamin Mkapa. li

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli kufuatia kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bejamin William Mkapa.

Katika salamu hizo za Rambirambi, Rais Dk. Shein alisema kuwa amepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa ya kifo cha mpendwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Benjamin William Mkapa, kilichotokea mapema usiku wa kuamkia leo Ijumaa, tarehe 24, Julai, 2020 Jijini Dar es Salaam.

Salamu hizo zilieleza kuwa Rais Dk. Shein yeye binafsi na kwa niaba ya wananchi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, anatoa salamu za rambirambi kwa Rais Dk. John Pombe Magufuli kwa msiba huo mzito.

“Tutamkumbuka Mheshimiwa Benjamin William Mkapa kwa uongozi wake wa busara, uzalendo, ukweli na uwazi, sifa ambazo zimeweza kuendeleza umoja na mshikamano wa Watanzania wote hasa katika ule wakati mgumu wa mabadiliko ya kisiasa, ambapo Taifa letu liliingia katika mfumo wa vyama vingi”, ilieleza sehemu ya salamu hizo za rambirambi alizotuma Rais Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein katika salamu hizo za rambirambi alieleza kwamba kwa hakika kifo hicho kinaacha pengo kubwa kwa Watanzania, na Afrika kwa jumla na wananchi wote wa Zanzibar wanaungana na Watanzania na Waafrika wote kuomboleza msiba huo.

‘Kupitia kwako Mheshimiwa Rais, tunatoa salamu zetu za pole kwa familia, ndugu, marafiki na jamaa wote wa marehemu”,ilieelza sehemu ya salamu hizo.

Sambamba na hayo, salamu hizo za rambirambi zilieleza kwamba kutokana na thamani kubwa aliyo nayo Rais mstaafu Benjamin Mkapa kwa Watanzania, wanamuomba MwenyeziMungu amuweke mahala pema na awape subira na ustahamilivu wafiwa na Watanzania wote katika kipindi hiki kigumu cha msiba.

Kifo cha Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Benjamin Willium Mkapa kimetokea usiku wa kuamkia leo ambapo kiongozi huyo amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 81.

Taarifa za kifo chake zilitangazwa kwa taifa usiku wa kuamkia leo kupitia televisheni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli kutoka Jijini Dodoma.

Kufuatia kifo hicho, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza siku saba za maombolezo ambapo bendera itapepea nusu mlingoti.  Rais mstaafu Mkapa ambaye alizaliwa tarehe 12 Novemba mwaka 1938 alishika nyadhifa hiyo kubwa zaidi Tanzania kuanzia mwaka 1995 hadi mwaka 2005 baada ya kumaliza awamu zake mbili za uongozi wake.

Rais Mstaafu Benjamin Willium Mkapa atakubukwa kwa uongozi wake mkubwa uliotukuka ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo kwa upande wa Umoja wa Mataifa (UN), hayati Mkapa atakumbukwa kwa mchango wake katika diplomasia ya kuleta amani, hususan baada ya kustaafu.
Tarehe 21 mwezi Septemba mwaka 2010, aliteuliwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati huo, Ban Ki-Moon kuongoza jopo la kusimamia kura ya maoni ya kujitenga kwa Sudan Kusini kutoka Sudan.
Mkapa akiongozana na wajumbe ambao ni Antonio Monteiro, Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje wa Ureno na Bhoiraj Pokharel, Mwenyekiti wa zamani wa Tume ya Uchaguzi nchini Nepal, walitembelea mara kadhaa Sudan kuhakikisha ufanikishaji wa kura hiyo ya maoni.
Kura ya maoni ya Sudan Kusini kujitenga kutoka Sudan ilifanyika kuanzia tarehe 9 hadi 15 Januari mwaka 2011 na matokeo ya kura hiyo yalidhihirisha nia ya Sudan Kusini kujitenga na hatimaye ikapata uhuru tarehe 9 Julai mwaka 2011.
Aidha, kutokana na uwezo wake wa diplomasia ya usuluhishi, Mkapa ambaye pia, aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania aliteuliwa na wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC, kuwa msuluhishi wa mgogoro wa Burundi ambapo ilikuwa inaelekea kwenye uchaguzi Mkuu mwaka 2020.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.