Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli akiongoza Kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, kilichofanyika Mkoani Dodoma leo,19,Agosti 2020, ( kulia kwa Mwenyekiti) Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na Mjumbe wa Kamati Kuu na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi.
KIKAO cha Kamati Kuu ya
Chama Cha Mapinduzi kilichokaa leo chini ya Mwenyekiti wake Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli kimezipongeza Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mafanikio makubwa
yaliopatikana.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed
Shein naye alihudhuria katika kikao hicho ambacho kimefanyika leo mjini Dodoma.
Katika taarifa ya Umma kuhusu kikao cha Kamati Kuu
Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyotolewa na
Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi Humphrey Polepole ilieleza kuwa miongoni mwa
mafanikio hayo ni utekelezaji mzuri wa Dira ya Taifa ya mwaka 2020/2025,
Mwelekeo wa Sera za CCM kwa miaka ya 2010-2020, Ilani ya CCM ya 2015-2020
pamoja na usimamizi madhubuti wa Sera za kiuchumi nchini.
Kufuatia mafanikio hayo kwa kauli moja Kamati Kuu
imeipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mafanikio hayo
makubwa yaliopatikana.
Aidha, taarifa hiyo ilieleza kuwa kikao cha Kamati
Kuu ya CCM kilikaa leo kikiwa na lengo la kuandaa agenda ya Kikao cha
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM.
Kwa maelezo ya Polepole Halmashauri Kuu ya Taifa
ya CCM itakutana kesho tarehe 20 Agosti 2020 katika Makao Makuu ya CCM Mjini
Dodoma.
Sambamba na hayo, taarifa hiyo ilieleza kwamba
pamoja na kujali na kupitisha agenda za Kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa
Kikao hicho cha Kamati Kuu kinakuwa cha kwanza baada ya Tanzania kuvuka na
kuingia katika kundi la nchi zenye uchumi wa Kati.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment