Habari za Punde

Burundi Yaipongeza Tanzania kwa Kuongeza Fursa Kwenye Sekta ya Madini.

Na Lilian Shembilu-MAELEZO

Serikali ya Burundi imeipongeza Tanzania kwa kuendelea kuongeza fursa kwenye sekta ya madini ambayo imeonesha mafanikio makubwa katika kukuza uchumi wa nchi na kuinua vipato vya wananchi kwa ujumla.

Hayo yamebainishwa na mwakilishi kutoka nchini Burundi, Niongao John Bosco katika Mkutano wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Aidha, ameishukuru Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Madini kwa mualiko wa mkutano huo kwa kuwa ni fursa kubwa kwao kwa sababu wamejifunza mambo mengi kupitia mada zilizowasilishwa na ameiomba Tanzania kudumisha uhusiano mzuri wa nchi hizo mbili kupitia sekta ya madini.

“Nimejifunza mambo mengi kuhusu uandaaji wa shughuli za madini na mkutano huu umekuwa wenye manufaa makubwa katika kukuza sekta ya madini nchini kwetu Burundi” alisisitiza Bosco.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila amewashukuru watoa mada na washiriki wote kwa kuchangia hoja nyingi zenye mashiko ambazo zitaleta tija kwenye sekta ya madini nchini.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima ameipongeza Wizara ya Madini kwa mabadiliko makubwa yanayoendelea kwenye sekta hiyo ambayo yamepanua wigo katika biashara ya madini ikilinganishwa na miaka 6 iliyopita.

“Katika kikao hiki yamezungumzwa mambo makubwa sana hivyo Wizara inatakiwa kuyazingatia na kuyafanyia kazi. Naomba Wizara iteue kamati ya watu 10 ili iweze kusimamia hoja zilizojadiliwa kwenye mkutano huu” alisema Malima.

Pia Malima amewataka wachimbaji wadogo kujikusanya kama wafanyabiashara ili waweze kusaidiwa hasa katika mikopo na kuacha migogoro pamoja na kulalamika katika maeneo yao.

Sambamba na hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya  Nishati na Madini Mhe. Danstan Kitandula ameipongeza Wizara ya Madini na kubainisha kuwa yote hayo ni matokeo ya uongozi uliotukuka wa Rais John Pombe Magufuli, usimamizi mzuri wa Waziri wa Madini Dotto Biteko pamoja na timu yote ya madini.

“Ni vyema changamoto zote kuhusu sekta ya madini zipatiwe ufumbuzi ili wajumbe wa mkutano huu wasione wanapoteza muda. Maarifa yatumike ili changamoto za kikodi ziweze kutatuliwa kwani zimekuwepo kwa muda mrefu sasa” alisisitiza Kitandula.

Akifunga mkutano huo wa siku tatu Waziri Biteko aliwashukuru wadau wote waliohudhuria na walioshiriki kwa njia ya mtandao, ambapo mada tisa na hoja 17 ziliwasilishwa. Pia amewahakikishia kuwa sekretarieti itazifanyia kazi.

“Kongamano hili ni maono ya Mheshimiwa Rais na ukweli ni kwamba manufaa yake yanazidi kuonekana na mara zote maelekezo yake yanakazia Watanzania wafaidike na madini” aliongeza Biteko.

Mkutano wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini ulilenga kuwakutanisha wadau wa sekta ya madini wa ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kujadili na kupeleka mbele sekta hiyo katika kukuza uchumi na kuvutia wawekezaji.

Pamoja na hayo mkutano huo ulilenga kubainisha fursa za uwekezaji zilizopo nchini, kuhamasisha matumizi ya teknolojia kwa wachimbaji wadogo, kuzikutanisha taasisi za kifedha na wadau wa madini ili taasisi hizo ziweze kujifungamanisha na sekta ya madini na sekta nyingine za kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.