Habari za Punde

RC Kusini Pemba apongeza juhudi za TAMWA ZNZ kutetea haki za Wanawake kwenye uongozi.

 

Mkuu wa Mkoa kusini Pemba  Mattar Zahor Massoud  akimsikiliza Mratibu wa TAMWA Zanzibar, Fat-hiya Mussa Said (kushoto) wakati wa kikao tendaji na wanaume mawakala wa mabadiliko ambao wamewezeshwa na TAMWA ZNZ chenye lengo la kujadili na kuwakumbusha viongozi wa mikoa juu ya umuhimu wa kuzingatia usawa wa kijinsia katika uteuzi wa nafasi mbalimbali hasa kuanzia ngazi ya Shehia na Wilaya.  
 Wanaume mawakala wa mabadiliko, maafisa wa TAMWA Zanzibar wakiwa katika kikao na Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba  Mattar Zahor Massoud ofisini kwake mapema February 03 2021
Mkuu wa Mkoa kusini Pemba  Mattar Zahor Massoud akiwa katika kikao na Ujumbe wa TAMWA -Zanzibar walipofika Ofisini kwake kwa mazungumzo.


Na.Mwandishi Wetu TAMWA ZNZ.

MKUU wa Mkoa wa Kusini Pemba Mattar Zahor Massoud amepongeza juhudi zinazochukuliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibr (TAMWA ZNZ) katika kutetea na kupambania haki za wanawake kushiriki katika nafasi mbalimbali za uongozi nchini.

Mkuu huyo wa mkoa ametoa Pongezi hizo ofisini kwake wakati wa kikao tendaji na wanaume mawakala wa mabadiliko ambao wamewezeshwa na TAMWA ZNZ chenye lengo la kujadili na kuwakumbusha viongozi wa mikoa juu ya umuhimu wa kuzingatia usawa wa kijinsia katika uteuzi wa nafasi mbalimbali hasa kuanzia ngazi ya Shehia na Wilaya.

Amesema Serikali inatambua na kuthamini kwa kiasi kikubwa juhudi zinazochukuliwa na TAMWA Zanzibar katika kujenga jamii yenye kuzingatia haki na usawa katika ngazi za maamuzi na kuahidi kuendelea kutoa mashirikiano ili kuhakikisha malengo ya usawa wa kijinsia yanafanikiwa katika kila sekta.

“Serikali inatambua sana harakati na juhudi za TAMWA katika kutetea haki za wanawake, lakini bado tunayo kazi kubwa ya kuendelea kutoa elimu kwa jamii juu ya dhana ya wanawake na uongozi kwani suala hili ni suala la kihistoria hivyo linahitaji muda zaidi wa kuweza kufanikiwa,” alisema.

Aidha mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa licha ya juhudi hizo lakini pia bado kuna haja ya kujikita zaidi katika kuwaandaa wanawake kuwa viongozi ili kuwawezesha kutekeleza kwa ufanisi zaidi majukumu yao pale wanapopata fursa ya kuwa viongozi katika nafasi mbalimbali.

“Ni lazima tutambue kuwa bado kunahitajika nguvu zaidi kwanza za kuwaandaa wanawake kuwa viongozi ili waweze kuwa na ubora katika utendaji kwani mara nyingi nafasi za uongozi haziangalii tu suala la kijinsia bali uwezo, maadili na uwajibikaji wa mtu mwenyewe katika utendaji kwa lengo la kuleta ufanisi wa kazi,” alisema mkuu huyo wa Mkoa.

Hata hivyo amekishauri chama hicho kuendelea kuwatumia zaidi viongozi wa dini ili kusaidia kubadili mitazamo ya jamii juu ya ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi.

Alisema, “nawapongeza pia kwa mbinu mnazotumia kwa kuwashirikisha viongozi wa dini katika masuala haya, nikuombeni tuendelee kuwatumia sana viongozi hawa ili watusaidie kubadili mitazamo ya jamii yetu kwani inaonekana kwamba dini ni kikwazo kwa wanawake kugombea nafasi za uongozi.”

Katika hatua nyingine Mattar ameahidi kuweka kipaumbele kwa wanawake katika nafasi mbalimbali za uogozi kwenye Shehia kwa kuzingatia uwezo wa atakayeweza kusaidia katika utendaji.

“Tukipata fursa tutazingatia ushiriki wao kwa namba kwa kuangalia zaidi uwezo na nani ataweza kutusaidia kwa ufanisi,” alisema.

Mratibu wa TAMWA Zanzibar ofisi ya Pemba, Fat-hiya Mussa Said akizungumza mbele ya mkuu huyo wa Mkoa alisema Chama hicho kinatekeleza mradi wa kuwawezesha wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi wenye lengo la kujenga uwezo wa wanawake Zanzibar kushiriki kikamilifu katika nafasi za uongozi na siasa.

“Taasisi yetu inatekeleza mradi huu kwa lengo la kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi mbalimbali za uongozi na siasa kupitia kuhamasisha jamii kukubali kuwa mwanamke nae anaweza kuwa kiongozi,” alisema.

Nae mjumbe wa wanaume mawakala wa mabadiliko Dr. Amour Rashid Ali alisema mawakala hao wanafanya mikutano na makundi mbalimbali katika jamii kwa lengo kushawishi na kutetea haki za wanawake kwenye uongozi.

Alisema, “Wanaume mawakala wa mabadiliko tumejitolea kufanya mikutano na makundi mbalimbali kwenye jamii kwa lengo la kutoa elimu ili jamii itambue kuwa wanawake nao wanao uwezo wa kuwa viongozi.”

Kikao hicho cha Mkuu wa Mkoa na wanaume mawakala wa mabadiliko ambao wamewezeshwa na TAMWA Zanzibar ni mwendelezo wa juhudi za Chama hicho kutetea na kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi na Siasa.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.