Habari za Punde

Benki ya NMB yaendelea kukua ikipata matokeo mazuri katika robo ya kwanza mwaka 2021

 
Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Bi Ruth Zaipuna.

Benki inayoongoza nchini Tanzania, NMB imeendeleza ufanisi wake kiutendaji katika robo ya kwanza ya mwaka 2021. Faida ya benki kabla ya kodi imeongezeka kwa asilimia 34 na kufikia shilingi Bilioni 93 wakati faida baada ya kodi imeongezeka kwa asilimia thelathini na tatu (33%) na kufika Shilingi bilioni 65 katika robo iliyoishia Machi 31 mwaka 2021.

 

Ufanisi huu umetokana na ongezeko la mapato, udhibiti wa gharama za uendeshaji, na umakini katika utoaji wa mikopo.

 

Mapato yaliongezeka kwa ailimia kumi na sita ( 16% ) na kufika shilingi bilioni 224 ikilinganishwa na  shilingi bilioni 193  za robo ya kwanza mwaka 2020. Mapato hayo yalichangiwa na ongezeko la pato halisi la riba lililotokana na faida ya mikopo na ile ya kwenye amana za Serikali.

 

Vilevile, mapato yasiyotokana na riba yaliongezeka kwa 10% kutokana na ongezeko uimarishaji wa utoaji suluhishi za kibenki kwa njia  ya kidijitali.

 

Benki bado ina ufanisi wa kutosha. Utekelezaji wa mikakati ya kupunguza gharama za uendeshaji unaendelea kutoa matokeo chanya kwani uwiano wetu wa gharama na mapato umeimarika mpaka 48% katika robo ya kwanza mwaka 2021 kutoka 52% katika robo ya kwanza mwaka 2020, chini ya kiwango kilichowekwa na msimamiszi wa mabenki yaani Benki Kuu ya Tanzania cha asilimia hamsini tano (55%). 

 

Benki itaendelea kutekeleza mikakati ya kupunguza gharama na kuongeza ufanisi kwa mujibu wa malengo makuu ya kimkakati ya Benki huku tukiendelea kuwahudumia vyema wateja wetu.

 

Ubora wa mali zetu umeimarika kutokana na utoaji bora wa mikopo, kutathmini uwekezaji tunaofanya na juhudi za kukusanya madeni. Hii imesaidia kupunguza madeni sugu na tengo la mikopo isiyolipika kuongezeka kwa 5% na kushusha kiwango cha mikopo chechefu mpaka 5% hivyo kuwa ndani ya ukomo wa kikanuni kutoka 6.9% iliyokuwapo mwaka uliopita.

 

Mizania ya Benki imeendelea kuwa mizuri na imara na juhudi zetu za kuwafikia wananchi wengi zaidi. Mikopo ya benki iliongezeka kwa 11%.

 

Ubunifu wa huduma na bidhaa zinazokidhi matarajio ya wateja umechangia kuongeza amana za wateja kwa 9% na kufika TZS 5.3 trilioni katika robo ya kwanza mwaka 2021 kutoka TZS 4.8 trilioni katika robo ya kwanza mwaka 2020.  Tunaendelea kuweka msisitizo katika ukopeshaji makini na endelevu tunapoianza robo ya pili mwaka 2021.

 

Katika kipindi hicho, tuliimarish amtaji wetu na kuufanya uwiano wa mtaji msingi kufika   19.61% kutoka 17.8% katika robo ya kwanza mwaka 2020, na uwiano wa mtaji wa ziada kufika 20.4% kutoka 18.5% wa robo ya kwanza mwaka 2020, hivyo yote miwili kuwa juu ya mahitaji ya kikanuni.

 

Akizungumzia ufanisi na uimara wa Benki, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Bi Ruth Zaipuna alisema “Tumeanza vizuri. Tunahakikisha ongezeko la thamani kwa wanahisa wetu na nchi kwa ujumla. Matokeo haya ya Q1 yanaakisi uwezo wa kuendelea vyema huko mbele katika utekelezaji wa mikakati yetu kwa kutumia wafanyakazi wetu wanaojitoa kuhudumia wateja wetu kwa ufanisi mkubwa”.

 

Ruth Zaipuna aliongeza, “Mtaji wetu bado ni mkubwa na unatupatia nafasi ya kuendelea kukua kama benki na kuongeza thamani kwa wanahisa  na wateja wetu. Kutokana na msiingi imara tuliyo nayo, na kuimarika kwa matarajio ya uchumi wa dunia, tunaamini tutaendelea kukua katika robo ya pili ya mwaka.Tunawashukuru wateja wetu, wanahisa na wafanyakazi kutokana na matokeo haya mazuri ya robo mwaka. Tutaendelea kuzitumia fursa zilizo mbele yetu ipasavyo ili kuendelea kuwa Benki yenye ufanisi zaidi nchini.”


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.