Na Kijakazi Abdalla - Maelezo Zanzibar.
Mbio za Mwenge wa Uhuru zinatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 17 Mei 2021 katika Mkoa wa Kusini Unguja ,Wilaya ya Kusini katika Uwanja wa Mwehe Makunduchi.
Hayo ameyasema Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadidi Rashid huko Tunguu wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na Uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru.
Amesema Mwenge wa Uhuru umekuwa kichocheo kikubwa katika kuhamasisha maendeleo ,uzalendo,umoja,mshikamano na kudumisha amani ndani na nje ya taifa.
Aidha alisema uzinduzi huo unatarajiwa kufungua miradi mbalimbali ya kimaendeleo pamoja na kuweka mawe ya msingi katika majengo ya Mkoa wa Kusini Unguja .
Aidha amesema mwaka huu 2021 utakuwa ni mwaka wa 28 tangu mbio za Mwenge wa Uhuru zirejeshe chini ya utaratibu wa uzimamizi wa Serikali kutokana na mabadiliko ya kimfumo wa vyama vingi vya kisiasa katika mwaka 1992.
Amesema kuwa mabadiliko hayo ambayo yamelenga kuwathibitishia watanzania kuwa Mwenge wa Uhuru hauna itikadi ya kisiasa ,dini wala kimila bali ni mali ya Watanzania wote bila ya kujali tofauti zao .
Mkuu wa Mkoa huyo alieleza kutokana na tukio hilo kubwa la kitaifa Mkoa wa Kusini Unguja kupitia kamati ya usalama wa Mkoa na Wilaya zimejipanga kuhakikisha ulinzi na usalama kwa wananchi utaimarika katika siku zote za ukimbizaji Mwenge wa Uhuru
Amesema Ujumbe wa Mwaka huu ni TEHAMA ni msingi wa Taifa endelevu: itumie kwa usahihi na Uwajibikaji.”pamoja na mbio za Mwenge wa uhuru wa 2021 unaendelea na ujumbe wa kudumu ambao ni Mapambano Dhidi ya Ukimwi, Rushwa,Dawa za Kulevya Malaria na Lishe Bora.
No comments:
Post a Comment