Habari za Punde

Dk Saada Mkuya amewasisitiza wanajamii kuacha kuwadharau watu wenye ulemavu

Baadhi ya washiriki wa mbio za mita 100 zilizojumuisha watu wenye ulemavu wa Usikivu na Viungo wakikimbia katika mashindano hayo ya Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani yaliyofanyika Uwanja wa Amani.
Baadhi ya washiriki wa mbio za mita 100 zilizojumuisha watu wenye ulemavu wa Usikivu na Viungo wakikimbia katika mashindano hayo ya Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani yaliyofanyika Uwanja wa Amani.

Mwenyekiti wa Shirikisho la watu wenye Ulemavu Zanzibar  Mwandawa Khamis Mohamed akielezea umuhimu wa watu wenye Ulemavu katika  Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani lililowashirikisha watu hao huko Uwanja wa Amani Zanzibar. 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais Dk. Saada Mkuya Salum akizungumza na waandaaji na washiriki wa Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani lililowashirikisha watu wenye Ulemavu katika Uwanja wa Amani Mjini Unguja


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais Dkt. Saada Mkuya Salum akimvisha Medali  mshindi wa tatu katika mbio za mita 100 za ulemavu wa usikivu Murtala issa Daudi katika Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani hafla iliyofanyika Uwanja wa Amani .


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais Dkt. Saada Mkuya Salum akimvisha Medali mshindi wa kwanza katika mbio za mita 100 za Ulemavu wa Viungo Suleiman Hassan katika Bonanza la shamra shamra za kuelekea siku ya Vijana Duniani huko Uwanja wa Amani Zanzibar.

Picha Na Maryam Kidiko – Maelezo Zanzibar


Na Rahima Mohamed  Maelezo  12/8/2021.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Dk. Saada Mkuya Salum, amesema atahakikisha haki za watu wenye ulemavu zinashughulikiwa katika nyanja zote za maendeleo.

Akizungumza katika bonaza la shamra shamra za sherehe kuelekea siku ya Vijana Duniani, lililofanyika Uwanja wa Amani Mjini Unguja, amesema watu wenye ulemavu wanauwezo mkubwa wa kichumi na kiakili hivyo ipo haja ya kupewa kipaombele.

Alieleza kuwa, watu wenye ulemavu wanauwezo wa kufanya shughuli mbali mbali za kijamii ambazo zinaweza kuwainua kiuchumi ikiwemo michezo hivyo ni muhimu kupewa haki zao.

Aliwasisitiza  wanajamii kuacha kuwadharau watu hao kwani wana umuhimu mkubwa katika jamii na uwezo wa kufanya mambo tofauti hivyo ni lazima wathaminiwe.

Akizungumzia suala la kushirikishwa walemavu katika michezo, Dk.Saada amesema watu wenye ulemavu wanauwezo mkubwa wakushiriki michezo mbali mbali kama wanavyoshiriki watu wengine hivyo ni vyema yanapofanywa mabonaza washirikishwe ili waoneshe uwezo wao.

“Kwakweli sikuamini kuwaona watu wenye ulemavu kushiriki katika michezo mbali mbali nakuona vipaji walivyokuwa navyo, hivyo ipo haja ya kushirikishwa katika michezo mengine itakayofanyika”, alisema  Waziri huyo.

Aidha alitumia fursa hiyo kuvipongeza vyama vinavyoshughulikia watu wenye ulemavu,  kwa kuwashirikisha  katika michezo na kuwataka wadau mbali mbali kujitokeza ili kuwasaidia katika nyanja  tofauti za maendeleo.

 Nae Kaimu Mkurugenzi wa taasisi ya Madrasa Early Childhood Sharifa Suleiman Majid, amesema wameamua kwa makusudi kuzielekeza jitihada zao kwenye bonaza hilo, kwani wanaamini michezo ina manufaa makubwa kwa watu wote ikiwemo kukuza afya ya mwili ,akili, kijinsia na kijamii.

Mwenyekiti wa Shirikisho la watu wenye ulemavu Mwandawa Khamis Mohamed  amesema bonaza hilo limethibitisha  wazi kuwa  watu wenye ulemavu wanauwezo  wa kushiriki katika  michezo mbalimbali kama binadamu wa kawaida.

Bonaza hilo limeshirikisha michezo mbalimbali ikiwemo ,riaza,kuvuta kamba,kufukuza kuku,mpira na mchezo wa mpira kwa watu wasioona.

Kaulimbiu ya mwaka huu inasema michezo na lishe bora kwa afya ya vijana wenye ulemavu.

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.