Habari za Punde

Mhe.Ulega Amewataka Wafugaji Owani Kuvuna Mifugo Yao.

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (kulia) akimsikiliza Mwenyekiti wa Kijiji cha Chumbi C, Muhidin Mtopa (katikati) alipokuwa akimuonesha moja ya eneo lililotengwa na Serikali kwa ajili ya Wafugaji Kijijini  hapo lakini baadhi ya Wafugaji wamebadirisha eneo hilo kuwa makazi na mashamba ya mpunga. Kwa  mujibu wa Mwenyekiti huyo, kitendo hicho kimesababisha migogoro ya wakulima na wafugaji kuendelea kushamiri katika Kijiji hicho. Naibu Waziri Ulega alitembelea Kijiji hicho Kilichopo Wilayani Rufiji Mkoani Pwani. 

  1. Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega akiongea na Wafugaji na Wakulima wa Wilaya ya Rufiji(hawapo pichani) alipofanya ziara Wilayani humo Septemba 19, 2021 kwa lengo la kusikiliza kero zao na kuzitatua. Naibu Waziri Ulega pamoja na mambo mengine aliwataka wafugaji wa Mkoa wa Pwani kwa ujumla kuvuna Mifugo yao ili kujiongezea kipato na kupunguza migogoro ya mara kwa mara kati yao na watumiaji wengine wa ardhi. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowelle.

Na Mbaraka Kambona, Rufiji.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amewataka Wafugaji wa Mkoa wa Pwani kuanza kuvuna Mifugo yao na kuiuza kwani kwa kufanya hivyo kutawasaidia kuwaongezea kipato na kupunguza migogoro kati yao na watumiaji wengine wa ardhi.

Ulega aliyasema hayo Septemba 19, 2021 wakati akiongea na Wafugaji na Wakulima wa Wilaya ya Rufiji alipofanya ziara  Wilayani humo ya kusikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi.

Alisema ni muhimu viongozi wa Wilaya za Rufiji, Mkuranga na Kibiti kukaa na wadau wa mifugo kutengeneza mkakati wa kuhamasisha uvunaji wa mifugo yao kwakuwa  soko la kuuza lipo mkoani humo na bado hawajalitumia ipasavyo.

"Hapa Mkoa wa Pwani tuna Kiwanda cha Nyama cha TanChoice lakini pamoja na kiwanda hicho kuwepo hakuna mifugo inayopelekwa  pale kutoka ukanda wetu huu wa Pwani," alisema Ulega.

Aliongeza kwa kusema kuwa ili faida ya uwepo wa kiwanda hicho ionekane ni vyema wadau wote wa mifugo mkoani humo waanze uvunaji mkubwa na kupeleka kuiuza kiwandani hapo.

"Tunatamani kuona mifugo inatoka katika ukanda huu wa Pwani na kwenda kuuzwa jijini Dar es Salaam ambapo ndipo kwenye biashara kubwa ya nyama, msione fahari kukaa na makundi makubwa ya mifugo ambayo mwisho wa siku yakaonekana kuwa ni kero na hayana faida," aliongeza Ulega

Kuhusu kuboresha huduma za Mifugo, Waziri Ulega alisema kuwa katika Bajeti ya Mwaka huu 2021/ 2022 Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Samia Suluhu Hassan imepanga kununua Pikipiki 300 na itazigawa kwa Maafisa Ugani nchi nzima ili waweze kutoa huduma ya mifugo kwa ufanisi.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowelle alisema kuwa kufuatia migogoro mingi iliyoibuka katika Wilaya yake ameanzisha zoezi la sensa ya Mifugo na Wafugaji ili waweze kujua idadi yao halisi na kupanga mipango ya matumizi bora ya ardhi kulingana na mahitaji.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.