TAARIFA KWA UMMA KUHUSU KAULI YA SERIKALI KWA WENYE
MADUKA YA KUBADILISHA FEDHA ZA KIGENI
Dodoma:
Tarehe 13. Sept. 2021: Kuna habari zinasambazwa kwenye mitandao ya
kijamii na kuandikwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari zikieleza kuwa Serikali
imewataka wafanyabiashara wote wa maduka ya kubadilishia fedha za kigeni
walionyang’anywa vifaa vyao na kikosi kazi kilichotumiwa na Serikali wakati wa
kuifunga biashara hiyo waende kuchukua vifaa vyao.
Habari hiyo
imepotosha kauli iliyotolewa na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Hamad
Yussuf Masauni (Mb) aliyoitoa bungeni wakati akijibu swali la nyongeza namba
118 la Mbunge wa Moshi Mjini Mhe. Priscus Tarimo aliyetaka kujua hatma ya
Maduka ya Kubadilishia Fedha za Kigeni, tarehe 10 Septemba, 2021.
Katika Majibu yake
Mhe. Masauni alitoa kauli ya Serikali kwamba baada ya hatua zilizochukuliwa,
wafanyabiashara waliitwa kufanya majadiliano na Mamlaka husika na baada ya
majadiliano hayo kumalizika walitakiwa wale waliopaswa kulipa walipe na wale
waliotakiwa kwenda kuchukua vifaa vyao waende wakavichukue baada ya kukamilisha
taratibu.
“Nitoe wito kama kuna
wafanyabiashara ambao hawajachukua vifaa vyao na wanastahili kwenda kuvichukua vifaa hivyo waende wakavichukue kwani
hakuna sababu ya Serikali kukaa na mali za mtu bila sababu ya msingi” Alisema
katika majibu yake
Taarifa inayosambazwa
inapotosha kwa kueleza kuwa wafanyabiashara wote wakachukue vifaa vyao wakati
kauli ya Serikali iliwataka wafanyabiashara wanaoona wanastahili kuchukua vifaa vyao wafanye hivyo baada ya
kutimiza vigezo na masharti na kama kuna mapungufu yoyote basi wapeleke taarifa
zao Wizara ya Fedha na Mipango ili yafanyiwe kazi.
Msimamo wa Serikali
ni kwamba wafanyabiashara wa Bereau de
Change waliokamilisha taratibu zinazotakiwa wakachukue vifaa na nyaraka
zao. Aidha, Wizara inatoa rai kwa vyombo vya habari kutumia weledi katika
kuhabarisha umma kikamilifu ili kuepusha taharuki isiyo na sababu za msingi
katika jamii.
Imetolewa na:
Benny Mwaipaja
Mkuu wa Kitengo cha
Mawasiliano Serikalini
WIZARA YA FEDHA NA
MIPANGO
No comments:
Post a Comment