Na Khadija Khamis Maelezo Zanzibar 12/10/2021.
Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora Mathew P.M.Mwaimu amewataka Masheha kulitafutia ufumbuzi tatizo la ukatili na udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto kwa njia ya kutoa elimu katika jamii .
Hayo ameyasema leo katika Ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe wakati akitoa mafunzo ya haki za binaadamu na utawala bora kwa Masheha wa Shehia mbali mbali za Wilaya ya Magharibi “A” na “B”.
Alisema suala zima la utoaji wa elimu kwa jamii iwe ndio agenda ya kudumu na kuhakikisha athari za ukiukwaji wa misingi ya utawala bora zinaondoshwa .
Aidha amesema Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora inatambua na kupongeza juhudi mbali mbali zinazofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wadau mbali mbali za kulinda na kukuza haki za wanawake na watoto pamoja na kulitafutia ufumbuzi tatizo la ukatili na udhalilishaji wa kijinsia.
Ameeleza kuwa pamoja na hatua hizo na mikakati mbali mbali ya kukabiliana na ukatili huo, bado suala la rushwa limepungua kwa kiwango kidogo sana hivyo mikakati madhubuti zaidi inahitajika kukabiliana na tatizo hilo.
Alifahamisha kuwa kazi ya Tume hiyo ni kutoa ushauri kwa Serikali katika changamoto mbali mbali ili ziweze kupatiwa ufumbuzi unaostahiki kwa mujibu wa sheria .
Nae Mkurugenzi Msaidizi wa Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora, Fides Shao akitoa mada ya Ukatili alisema ni kitendo chochote kinachofanywa kwa mtu na kusababisha madhara ya kimwili na kiakili au mateso kwa wanajamii ikiwa kwa kutishiwa maisha pamoja na kunjimwa uhuru wa hadharani au kificho .
“kitendo hicho kinachangia kukosesha ushirikiano katika jamii hasa wakati wa kutoa ushahidi katika kesi za ukatili na udhalilishaji, “alisema Mkurugenzi huyo .
Nao Masheha hao walisema wanasikitishwa na baadhi ya kesi zinazowafikia ambazo zinaushahidi wa kutosha na kukanushwa kukosa ushahidi katika hatua za mwisho.
Sheha wa Shehia ya Chuini Mohammed Sheha Kheir akichangia mada katika mafunzo ya Haki za Binaadamu na Utawala bora yaliyofanyika Ukumbi wa Maleria Mwanakwerekwe Zanzibar.
Walisema kuwa suala la rushwa na muhali bado ni tatizo katika jamii jambo ambalo linazorotesha mfumo sahihi wa kutoa taarifa na kudai haki .
No comments:
Post a Comment