Habari za Punde

Mfumo wa Anwani za Makazi na Postikodi uwe agenda ya kudumu-Lukwere

Mkurugenzi wa Mawasiliano kutoka Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mha. Clarence Inchwekeleza (hayupo pichani) akizungumza wakati wa  mafunzo ya mfumo wa anwani za makazi kwa watendaji wa halmashauri 23 na mikoa 13 nchini unaofanyika katika ukumbi wa CCT mkoani Morogoro

Na Daudi Manongi WHMTH,Morogoro

Naibu Meya wa Manispaa ya Mkoa wa Morogoro Bw.Mohamed Lukwere amesema ni vyema suala la anwani za makazi iwe ajenda ya kudumu katika vikao vya ngazi zote ili kuchochea utekelezaji na matumizi ya mfumo huo nchini.

Bw.Lukwere ameyasema hayo leo Mkoani Morogoro wakati akifungua mafunzo ya mfumo wa anwani za makazi kwa watendaji wa halmashauri 23 na mikoa 13 nchini unaifanyika ukumbi wa CCT mjini hapa.

“Watendaji wa vijiji/mitaa watumike katika kukusanya taarifa za anwani za makazi na kutoa na kutoa anwani husika kwa wananchi kwa kutumia programu tumizi”amesema

Akieleza umuhimu wa mfumo huo amesema kuwa Utekelezaji wa Mfumo wa Anwani za makazi na Postikodi unalenga kuharakisha na kurahisisha upatikanaji, utoaji na upelekaj wa huduma ama bidhaa hadi mahali stahiki.

Amesisitiza kuwa Ili kurahisisha utekelezaji wa Mfumo huo ni vyema kila Halmashauri ikaweka msukumo katika kujenga uwezo kwa watendaji na wataalamu wa kata na mitaa ikiwa ni pamoja na kujenga uwezo katika matumizi ya programu tumizi ya mfumo.

Aidha ameipongeza Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari  kwa kujenga uelewa wa viongozi kuanzia Wakuu wa Mikoa,Makatibu tawala,Wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini pamoja na mameya/wenyeviti.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mawasiliano Wizara ya Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mha.Clarence Inchwekeleza amesema kuwa wameamua kufanya  mafunzo hayo kwa watendaji  wa Halmshauri  ili nao wakaendeleze mafunzo haya kwenye maeneo yao katika ngazi za kata na mitaa.

Amesema kuwa Serikali iko katika kutekeleza Sera zake na katika kuhakikisha kwamba kila mtu anafikiwa na huduma za mawasiliano na kuwa sehemu ya matumizi ya kidigitali.

“Utekelezaji wa mfumo huu wa anwani za makazi ni Utekelezaji wa Sera
 ya mwaka 2003 ya Posta”ameongeza

Ameeleza kuwa  Mafunzo hayo yameshirikisha mikoa 13 na maafisa kutoka Halmshauri 23.

Kwa upande wao wawakilishi kutoka TAMISEMI na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wamesema mfumo huo utasaidia sana Serikali katika kupanga shughuli za maendeleo  na kuraisisha shughuli za wananchi

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.