Habari za Punde

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Wakuu wa Taasisi za SMZ, baada ya kumalizika kwa kuwasilishwa kwa Mada mbalimbali na baadhi ya Makatibu Wakuu, wakati wa mafunzo ya Upangaji wa Vipaumbele, yalioandaliwa na Taasisi ya Tony Blair pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP)  mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Utalii Maruhubi Jijini Zanzibar

BAADHI ya Wawakilishi wa Taasisi ya Tony Blair na Makatibu Wakuu,Manaibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Watendaji Wakuu wa Serikali.wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi.(hayupo pichani) akizungumza baada ya kusikiliza Mada zilizowakilishwa na baadhi ya Makatibu Wakuu, katika mafunzo ya Upangaji wa Vipaumbele yalioandaliwa na Taasisi ya Tony Blair pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) yaliofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Utalii Maruhubi Zanzibar.

BAADHI ya Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Watendaji wa Serikali  wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi.(hayupo pichani) akizungumza baada ya kuisikiliza kwa Mada zilizowasilishwa na baadhi ya Makatibu Wakuu, wakati wa Mafunzo ya Upangaji wa Vipaumbele, yalioandaliwa na Taasisi ya Tony Blair pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP)  mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Utalii Maruhubi Jijini Zanzibar



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesisitiza haja kwa watendaji Serikalini kubadilika na kutofanya kazi kwa mazoea ili mipango iliyopangwa na Serikali iweze kutekelezeka.

 

Rais Dk. Mwinyi amesema hayo mara baada ya kusikiliza mada zilizowasilishwa na Makatibu Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika Mafunzo ya Upangaji wa Vipaumbele, yalioandaliwa kwa ushirikiano kati ya Taasisi ya ‘Tony Blair’ pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), yaliyofanyika  katika ukumbi wa Chuo cha Utalii Maruhubi, nje kidogo ya Jiji la Zanzibar.

 

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa kazi iliyobaki mbele hivi sasa ni utekelezaji kwani hakuwa na shaka na utekelezaji kwani mipango ipo bali lengo ni kuimarisha Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano, kilichobaki ni utekelezaji.

 

Katika maelezo yake alirejea kauli yake aliyoitoa siku aliyoyafungua mafunzo hayo kwa kusema kwamba hajaridhika na utendaji Serikalini, na kueleza kwamba hakusema hilo kwa kwa kumnyooshea kidole mtu bali alisema kutokana na hali halisi ilivyo kwani bado watendaji Serikalini hawajawa wepesi katika kufanya mipango ya serikali itekelezeke.

 

Alisisitiza mabadiliko kubadilika na kueleza kwamba kila mmoja ni vyema ajione kwamba ana wajibu wa Ofisi yake kutekeleza mipango iliyopangwa na haitokuwa vyema kiongozi kumaliza kipindi chake cha uongozi bila ya kuonesha mradi hata mmoja aliotekeleza.

 

Alieleza kwamba hivyo, hawezi kusema amefanikiwa, bali atakuwa amefanikiwa kwa kwenda kazini tu lakini hakufanikiwa kuonesha ama kuacha alama katika Ofisi yake na kusisitiza kwamba kila mmoja anapaswa kuonesha alichokifanya pale atakapomaliza muda wake wa kazi.

 

Rais Dk. Miwnyi alisema kwamba hatokuwa tayari kusikia wawekezaji wanaokuja kuekeza wanazungushwa.

 

Alisema kwamba masuala ya uwekezaji yanataka fedha hivyo, si jambo la busara wawekezaji wakazungushwa kwani wenye fedha ni lazima wakapokewa vizuri na kuwapokea na kuwakarisha ili waweze kufanya kazi.

 

Rais Dk. Mwinyi alisisitiza kwamba bado kuna watu wanadhani kwamba urasimu ndio njia ya kufanyakazi na kusisitiza kwamba wakati umefika watu wabadilike.

 

“ .....bado kuna hali ya kutojali na hivyo ndipo niliposema kwamba siridhiki na utendaji wa Serikali.....nyinyi mliokuwepo hapa ndio wakuu wa taasisi zetu ...inawezekanaje upo katika kipindi chako cha uongozi kwa miaka mitano hata mtu mmoja hajakemewa....ina maana katika ofisi zetu hamna anayefanya kosa, hayo ndio yanayotufanya tushindwe kufanikiwa, ningependa kusikia kila mtu anachukua hatua ili kufanya ofisi zetu zifanye kazi vizuri zaidi”, alisisitiza Dk. Mwinyi.

 

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alisema kwamba ana amini semina hiyo itawasaidia watendaji kubadilika na wameshajua mipango na majukumu ya Serikali na lilobaki ni kwenda kupanda jinsi ya kuwezesha kifedha ili mipango hiyo iweze kutekelezeka.

 

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi alitoa pongezi kwa wadhamini wa mafunzo hayo pamoja na kuwapongeza viongozi wote waliopata mafunzo hayo ambayo alisema yana umuhimu mkubwa na yatasaidia kwa kiasi kikubwa katika kufikia malengo ya Serikali.

 

Nae Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said alitoa pongezi kwa Rais Dk. Mwinyi kwa kuhudhuria katika uwasilishwaji huo wa mada mbali mbali zilozotolewa na Makatibu Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kueleza kwamba mafunzo hayo yamewapa mwanga mkubwa wa kutekeleza mipango na upangaji wa vipaumbele vyake sambamba na kuyafanyia kazi maoni yake aliyoyatoa.

 

Mapema Makatibu Wakuu walipata fursa ya kuwasilisha mada zao na kueleza mipango kabambe waliyoipanga katika mafunzo hayo ikiwemo mipango ya kuimarisha sekta ya uchumi wa Buluu, sekta ya utalii, sekta ya miundombinu, pamoja na masuala ya kijamii.

 

Imetayarishwa na Kitengo cha Habari

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.