Habari za Punde

Gallos Mnyimbo Asema CCM ni Kinara wa Demokrasia.

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Ndg. Casian Gallos Nyimbo, akipiga kura katika uchaguzi wa kuwachagua viongozi wa Shina namba 03, tawi la CCM Chuini Jimbo la Mfenesini Unguja.

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Ndg. Casian Gallos Nyimbo, amesema CCM itaendelea kuwa kinara wa Demokrasia nchini kwa kuhakikisha Wanachama wake wanapata haki ya kuchagua na kuchaguliwa kwa nafasi mbalimbali za uongozi  kupitia uchaguzi huru na haki wa ndani ya Chama.

 

Rai hiyo ameitoa wakati akishiriki  zoezi la kupiga kura za kuwachagua viongozi wa ngazi ya shina namba tatu(3),tawi la CCM Chuini Wilaya ya Mfenesini Unguja.

 

Alisema zoezi hilo la uchaguzi wa ngazi ya shina ni hatua muhimu ya kuwapata viongozi imara kutoka katika jamii wanayoishi na  wapo karibu zaidi na wapiga kura na wananchi kwa ujumla, watakaosaidia kuendeleza mafanikio ya kiuongozi na utendaji kupitia Sera,Ilani,Itikadi na miongozo mbalimbali ya Chama Cha Mapinduzi.

 

Katika maelezo yake Gallos, amewasisitiza Wanachama  hao kuwachagua viongozi bora watakaofanikisha ushindi wa CCM katika uchaguzi wa Dola mwaka 2025.

 

"Zoezi hili la kuwachagua viongozi wa mashina ni muhimu sana katika ustawi wa Chama kwani tunawapata Mabalozi wa mashina ambao ni viongozi wa ngazi ya shina.

 

Jambo la msingi katika uchaguzi huu ni kuwapata viongozi bora,imara na wenye uwezo na uzalendo wa kweli wa kulinda na kusimamia maslahi na Itikadi za CCM Kwa vitendo.",alieleza Gallos.

 

Katika uchaguzi huo wamechaguliwa viongozi mbalimbali ambapo nafasi ya Mwenyekiti  amepatikana Ndg.Fatma Baro Makame kura 63,Katibu Rukaiya Rashid Hussein kura 57 pamoja na Wajumbe watatu wa baraza la shina hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.