Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma Bw. Mathew M. Kirama amewataka watumishi wa Tume hiyo kufanya kazi kwa uadilifu, kuzingatia Sheria na kulinda haki za watu ambao wanawahudumia ili uamuzi unaotolewa katika rufaa na malalamiko yanayowasilishwa Tume uwe ni uamuzi wa haki na haki tupu wakati wote.
Bw.
Kirama amesema hayo wakati anafungua mafunzo kuhusu usimamizi wa mfumo wa
vihatarishi katika Taasisi kwa ngazi ya Menejimenti ya Tume, Wakuu wa Sehemu na Wajumbe wa Kamati ya Ukaguzi ya
Tume ya Utumishi wa Umma, mafunzo yaliyofanyika jana katika Ukumbi wa Mikutano
wa Ofisi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi,
Jijini Dodoma.
“Watumishi
wa Tume mnayo dhamana ya kumsaidia Mheshimiwa Rais kutekeleza majukumu yake. Ni
dhamana kubwa, na kwa sababu hiyo ni lazima muilinde dhamana hiyo mliyopewa kwa
kuhakikisha wakati wote mnafanya kazi kwa bidii. Hakikisheni wakati wote
mnafanya kazi kwa uadilifu, mnazingatia maadili, Sheria na mnalinda haki za
watu ambao mnawahudumia ili uamuzi unaotolewa katika rufaa na malalamiko yao wanayowasilishwa
Tume uwe ni uamuzi wa haki na haki tupu”.
“Akitokea
mteja wetu mrufani amekata rufaa, akate rufaa kwa sababu anatumia haki yake ya
msingi na uamuzi ukitolewa, haki hiyo ionekane imetendeka mbele ya macho ya
Sheria. Hili ni jambo ambalo kila mmoja wetu anapaswa kuliona na kulisimamia
kwa nguvu zetu zote na ndio maana tupo hapa ” alisema Bw. Kirama.
Akizungumzia
kuhusu umuhimu wa mafunzo hayo alisema, Tume ni rekebu inatakiwa kuwa juu
katika viwango vya uzingatiaji wa Sheria, Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298
[marekebisho ya mwaka 2019] na Sheria nyingine zinazotuongoza katika
utekelezaji wa majukumu yetu. Aliishukuru Ofisi ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa
Serikali kwa kuipatia Tume mwezeshaji na alisema kuwa Tume inakusudia kuwa na
mfumo mzuri zaidi wa usimamizi wa vihatarishi katika mwaka ujao wa fedha wa 2022/2023.
“Tukiweza
kuainisha vizuri vihatarishi vilivyo katika Tume yetu maana yake malengo
tuliyojiwekea tutayafikia. Kushindwa kufanya hivyo tutabaki tunazungumza tu
katika daftari ambalo halina matokeo. Ni lazima kuwe na matokeo kwa sababu kuna
watu tunaowahudumia ndio watakaotupima ama tumefanikiwa au hatujafanikiwa. Ni
matarajio yangu kuwa baada ya mafunzo haya tutakwenda kutekeleza, ili wenzetu
wanaotupima waone usimamizi wa vitaharishi katika Ofisi ya Rais, Tume ya
Utumishi wa Umma unatekelezwa ipasavyo” alisisitiza Bw. Mathew M. Kirama.
Kwa
upande wake, muwezeshaji kutoka Ofisi ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Bw.
Onesmo Mbekenga, alisema ni muhimu kwa kila Taasisi ya Umma kuwa na mfumo wa
vihatarishi ambao unasimamiwa, unatekelezwa
na kufanyiwa tathmini vizuri ili kuisaidia Taasisi kuweza kufikia malengo yake.
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Tume ya Utumishi wa Umma
DODOMA
04 Juni 2022.
No comments:
Post a Comment