Habari za Punde

Matukio 504 ya Udhalilishaji Yaliripotiwa Zanzibar

MWENYEKITI wa Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation,Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi akiwahutubia Wananchi katika viwanja vya mpira vya Nungwi Wilaya ya Kaskazini “A” Unguja, baada ya kumaliza kwa Matembezi ya Kupiga Vita Vitendo vya Udhalilishaji kwa Watoto yalioazia katika eneo la Kendwa na kumalizia kwa mazoezi ya pamoja ya viungo na kuadhimisha  Mwaka Mmoja wa Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation
Na Mwashamba Juma

JUMLA ya matukio 504 ya udhalilishaji yaliripotiwa Zanzibar nzima kwa kipindi cha miezi mitatu, kutoka Novemnba 2022 hadi mwezi Januari, 2023 ambayo yalihusisha vitendo vya ubakaji, kulawiti, vipigo kwa watoto na udhalilishaji wa kijinsia.

Miongoni mwa matukio hayo 41 pekee yaliripotiwa Mkoa wa Kaskazini Unguja kwa kipindi hicho.

Mwenyekiti wa taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation na Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi alitoa takwimu hizo alipozungumza na watoto, wazazi, walezi, walimu na viongozi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja alikojumuika nao kwenye matembezi ya kupinga vita dhidi ya udhalilidhaji.

Aliposhiriki matembezi ya kupinga vita dhidi ya udhalilishaji

Mama Mariam Mwinyi alisema matukio hayo ni mengi na yanazidi kila uchao hivyo, alivitaka vyombo vya sheria kutekeleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutowaachia huru watuhumiwa wa makosa ya udhalilishaji nchini.

“Tunawaomba sana Jeshi la polisi wasiwatoe hawa watu wanaotuhumiwa kwa makosa ya udhalilishaji” Kwa hisia alisisitiza Mama Mariam.

Mwenyekiti huyo wa Zanzibar Maishabora Foundation, aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuanzisha mahakama maalumu ya kushughulikia mashauri ya udhalilishaji, kuonhgeza mahakimu 10, majaji watatu ambao wameongeza idadi ya majaji kwa Majakama kuu kufikia 12 pamoja na kuajiri makaadhi wanne wanaoshughulikia mashauri ya familia.

Aidha, alipongeza hatua ya Serikali kwa kuzuia dhamana kwa watuhumiwa wote wa makosa ya udhalilidhaji.

Akizungumzia masuala ya vipigo kwa watoto, aliwasihi wazazi/walezi na walimu wa skuli na madrsa kutowaadhibu watoto kwa kipigo chenye kupitiliza na kuwataka watumie busara ya kuwapa adhabu zenye huruma badala ya kuwazuru kwa vipigo vikali.

“Hatupingi watoto kuchapwa wanapokosea, sababu ni sehemu ya ulezi na makuuzi yao lakini isiwe vipigo vyenye kupitiliza” alionya Mama Mariam Mwinyi.

Pia aliwasihi walimu na wazazi/walezi hao kuweka tabia ya kuwasikiliza watoto/wanafunzi kwani kunawengine hupitia ukatili mkubwa lakini kutokana na hofu kwa wanayoyapitia kwenye jamii  zao huogopa kusema wanapokua majumbani ana skuli kwa walimu wao.

Mama Mariam Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwaeleza watoto kuvunja ukimya badala yake wawe jasiri kuzungumza kwa yanayowatokezea, ikiwemo vitisho, vipigo, kunyanyaswa kwa namna yoyote iwe na watu wazima au watoto wenzao wawe tayari kuzungumza badala ya kuweka usiri ili jamii iwasaidie.

Pia aliwataka kuwa makini na watu wakaribu na familia zao, wakiwemo walezi, jirani na jamii wanayoishi nayo hata kwenye mazingira wanayosomea kwa kutotoa fursa ya mtu yeyote kushika miili yao kwa namna yoyote.

Alisema matukio mengi ya udhalilishaji nayoripotiwa kwenye vyombo vya sheria yanahusisha watu wa karibu na familia na jamii ya watoto inayowazunguruka.

“Msiruhusu watu washike miili yenu, msiruhusu kukoshwa na mtu asiekua mama yako au kuvaa nguo mbele za watu, mujitahidi kuheshimu miili yenu, hata wakati wa kuvaa nguo jitahidi uwe peke yako kuutunza mwili wako.” alisihi Mama Mariam.

Pia Mama Mariam alikemea tabia ya baadhi ya wazazi/walezi kuwabusu watoto midomoni nakueleza kwamba tabia hiyo inachochea viashiria vya udhalilishaji nakuongeza ni chanzo cha maambukizi kwa baadhi ya maradhi.

Katika hatua nyengine Mama Mariam Mwinyi aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada ya kuimarisha sekta ya elimu nchini kwa kuongeza skuli mpya  nchi nzima na kukarabati za zamani hali iliyopunguza msongamano wa wanafunzi mashuleni.

Naye, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, jinsia Wanawake na Watoto, Riziki Pembe Juma aliwataka wanaume kwa nafasi na dhamana zao kuungana na jamii kuendelea kuwalinda na kuwastahi watoto, kukemea na kuwa msatari wambele kupinga udhalilishaji wa kijinsia.

Alieleza matukio mengi ya udhalilishaji wa kijinsia yakiwemo ubakaji, kulawiti, kutelekeza na kutorosha wasichana wanaume ndio wahusika wakubwa wa vitendo hivyo.

Hata hivyo, aliipongeza Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation kwa kuungamkono juhudi za Serikali kwa kuendelea kuwa bega kwa bega kupinga vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia katika harakati zake.

Akizungumza kwenye hafla hiyo Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Ayoub Mahmoud alisema, Mkoa huo wanaendelea kupambana na ongezeko la vitendo hivyo, kwa kuchukua hatua mbalimbali za kupunguza na kutokomeza udhalilishaji, ikiwemo ya kuongeza uelewa kwa jamii yakiwemo makundi ya wavuvi ambao wanalalamikiwa sana kwa kutelekeza familia wanapokua dagoni, elimu kwa wakulima na vyombo vya ulinzi na usalama, madrasa na mashuleni.

Alieleza mkoa pia umewafikia watu wenye ulemavu kuwa nao karibu  kuwalinda na kuwathamini na kutoa uelewa kwa jamii juu ya kushirikiana nao kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo.

Alisema licha ya juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya mkoa huo  kupinga udhalilishaji bado suala la muhali mkoani humo ni changamoto sugu, nakueleza kwamba wanawake na watoto wanaathiriwa zaidi na masuala ya ubakaji, kulawiti, kutorosha, shambulio la aibu, kukashifu, mvutano wa malezi, shabulio la kuumiza mwili,  dawa za kulenya pamoja na mashambulio ya hatari

Aidha, alieleza ndoa za umri mdogo huongeza talaka nyingi mkoani humo, hali inayochangia kushindwa kuhimili familia na watoto, pia alieleza serikali ya mkoa imejitahidi kuzibiti maundi maovu na kufanya ziara za kustukiza maeneo yenye vichocheo vya mporomoko wa maadili.

Matembezi ya kupinga vita dhidi ya udhalilidhaji yaliandaliwa na Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation yakiwa na kaulimbiu “Mimi ni shujaa, nitaulinda mwili wangu na kuutunza” yalikwenda sambamba na maadhimisho ya mwaka mmoja tokea kuzinduliwa kwa taasisi hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.