Habari za Punde

SJMT na SMZ Zina Ushirikiano Katika Masuala ya Uchumi

 
Taasisi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zina ushirikiano wa kuridhisha katika shughuli za kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis wakati akijibu swali la Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi Mhe. Suleiman Haroub Suleiman aliyetaka kujua ni kwa kiasi gani Taasisi za Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinashirikiana katika shughuli za kiuchumi.

Mhe. Khamis amezitaja program hizo kuwa ni Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF II), Mradi wa Kuongeza Tija na Uzalishaji wa Zao la Mpunga (ERPP); Mradi wa Udhibiti Uvuvi na Maendeleo shirikishi Kusini Magharibi ya Bahari ya Hindi (SWIOFISH); Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR); Mkakati wa kudhibiti Sumu Kuvu Tanzania na Programu ya Maboresho ya Usimamizi wa Fedha.

Amesema kuwa SJMT kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais inasimamia na kutekeleza miradi mbalimbali ya kimazingira kwa upande wa Zanzibar katika maeneo tofauti ikiwa ni katika kuunga mkono Sera ya Uchumi wa Buluu.

“Mheshimwia Spika kuna miradi ya maabdiliko ya tabianchi inayotekelezwa Zanzibar kwa mfano hivi karibuni kama mtakumbuka tuliwahi kukabidhi boti za uvuvi Tumbatu na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar ambalo ni lengo la Serikali ya Muungano kuungano mkono uchumi buluu na suala zima la uhifahdi wa mazingira,” amesema.

Hata hivyo, amesema kuna miradi ambayo bado haijaanza kutekelezwa ikiwemo uchimbaji wa mabwawa ya maji Bumbwini Makoba ambao tayari Serikali imetoa malekezo uanze mara moja ndani ya mwezi huu ili wananchi waanze kunufaika nao.

Kwa upande mwingine akijibu swali la nyongeza la mbunge huyo kuhusu ushirikishwaji wa Zanzibar katika mikutano ya kimataifa, Naibu Waziri Khamis alisema SJMT inaipa ushirikiano mkubwa katika mikutano hiyo.

Ametolea mfano Mkutano wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi uliofanyika Novemba 2022 mjini Sharm El Sheikh nchini Misri ambapo viongozi wa SMZ walishiriki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.