Habari za Punde

Chama Cha Mapinduzi Kimetoa Pole kwa Wananchi Waliopata Maafa ya Upepo Mkoa wa Kaskazini Unguja

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, kimeeleza kupokea kwa masikitiko taarifa za maafa yaliyotokana na upepo katika shehia sita za Mkoa wa Kaskazini Unguja.  

Maaafa hayo yaliyotokea kati ya Aprili 1 na 7 mwaka huu, yalileta madhara kwa makaazi ya wananchi na majengo ya kijamii yameziacha baadhi ya kaya katika hali ngumu.

 

Hivyo Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, anatoa pole kwa familia zilizoathiriwa na maafa hayo na kuwaomba watu waliothiriwa kuwa watulivu wakati serikali na wadau wengine wakiendelea na jitihada za kuwarudisha katika hali zao za kawaida.

 

“Nazisihi familia zote zilizopata maafa hayo kuendelea kuwa wavumilivu, huku mamlaka zinazohusika kukabiliana na maafa ziendelee kuchukua hatua za haraka za kuhakikisha wananchi hawa wanapata huduma zote muhimu”, alielekeza Makamu Mwenyekiti ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

 

Aidha Dk. Mwinyi, anawashukru wadau mbali mbali waliojitokeza kutoa misaada ya vifaa vya ujenzi na mahitaji mengine ya kibinadamu ikiwemo kuwapatia chakula na hifadhi ya muda.

 

Aidha anawapongeza wananchi wa maeneo hayo kwa juhudi walizochukua kuzuia athari zaidi na kuwahifadhi waathirika wa maafa hayo katika makaazi yao kitendo kinachodhihirisha uwepo wa umoja, mshikamano, imani, utu na upendo ndani ya jamii ya wazanzibari.

 

Jumla ya nyumba 124 na Misikiti miwili (2) miti na vipando vimeathirika kutokana na upepo mkali uliotokea katika Shehia sita za Mkoa wa Kaskazini Unguja.

 

NDG. KHAMIS MBETO KHAMIS,

 

KATIBU WA KAMATI MAALUM YA NEC,

 

IDARA YA ITIKADI NA UENEZI CCM-ZANZIBAR,

 

11/04/2023

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.