Habari za Punde

SMZ Inalishukuru Shirika la Kimataifa la UNDP kwa Kuendelea Kuiunga Mkono Serikali Kwenye Masuala Mbalimbali ya Maendeleo.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Mwakilishi Mkaazi wa UNDP Nchini Tanzania Bi. Christine Musisi (kulia kwa Rais) akiwa na Ujumbe wake wa Maofisa wa UNDP, mazungumzo hayo yaliyofanyika leo 31-5-2023, katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inajitahidi kupambana maeneo tofauti ili ifanikishe miradi yake iliyoidhamiria kuifanikisha kwaajili ya kuendelea kuwaletea Maendeleo wananchi wake.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini Tanzania, Bi. Christine Musisi aliefika kumtembelea.

Dk. Mwinyi alisema daima Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inalishukuru Shirika la Kimataifa la UNDP kwa kuendelea kuiunga mkono Serikali kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo.

Alisema SMZ na UNDP wana ushirikiano mzuri na kulipongeza Shirika hilo kwa kuendelea kuiunga Mkono Tanzania ikiwemo Zanzibar hasa kwa kuiongezea nguvu za kifedha Taasisi ya Ufuatiliaji na Usimamizi utendaji kazi Serikalini, PDB, Zanzibar.

“Tunahitaji kuiwezesha zaidi PDB ili kuhakikisha inafanikisha ipasavyo majukumu yake” alieleza Rais Dk. Mwinyi.

Rais Dk. Mwinyi alimwelezea mgeni wake huyo ushirikiano anaoupata kwa PDB katika kutekeleza majukumu yake, hivyo aliipongeza UNDP kwa kuiunganga mkono.

Alisema Serikali imeweka nguvu zake huko bila ya kutegemea bajeti kutoka Serikali kuu pekee badala yake inahangaika kwa wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuiongezea bajeti.

Aidha Rais Dk. Mwinyi aliridhia ombi la UNDP la kukutana pamoja kwa baadhi ya Mabalozi ambao ni wadau wa maendeleo wa shirika hilo wakiwemo Canada, Uingereza na Norway.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mwakilishi huyo wa UNDP, Christine Mwasisi alimpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa uongozi wake wa kuendeleza amani na kuendelea kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Alimueleza Rais Dk. Mwinyi UNDP kwasasa inatekeleza miradi sita barani Afrika ikiwemo mitatu kwa Tanzania ambapo Zanzibar wanashirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza miradi ya kupambana na matukio ya Uhalifu Zanzibar, ambapo alieleza mradi huo wanashirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka chini ya ufadhili wa Serikali ya Uingereza na Umoja wa Ulaya (EU).

Alieleza mradi mwengine ni uwezeshaji kwenye masuala ya utawala wa kisheria ambapo alieleza mradi utaangalia haki na wajibu kwenye masuala ya jinsia ikiwemo masuala ya wanawake na watoto ambapo alieleza mradi huo unatarajiwa kushirikiana na Baraza wa Wawakilishi Zanzibar.

Pia Bi. Mwasisi alieleza mradi mwengine utahusisha masuala ya fedha ambao Mwakilishi huyo alisema tayari timu ya mradi huo imeshakutana na Waziri wa Fedha wa Zanzibar Dk. Saada Mkuya Salum na kujadiliana kwa hatua za awali na wadau wa wizara hiyo.

Aidha, mbali na mambo mengine pia mgeni huyo alimueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba UNDP ilivyojipanga kufanyakazi na Sekta ya Uchumi wa Buluu pamoja na sekta ya Mazingira endelevu.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.