Habari za Punde

WIZARA ZA ELIMU NA UTAMADUNI ZIWASAIDIE VIJANA KUMFAHAMU ZAIDI MWL. NYERERE - MAJALIWA

 

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza katika Kongamono la Kubukizi ya Miaka 101 ya kuzaliwa kwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lililofanyika kwenye ukumbi wa Chimwaga jijini Dodoma

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezitaka Wizara za Elimu, Sayansi na Teknolojia na ile ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ziandae utaratibu utakaosaidia vijana kujifunza na kumfahamu zaidi hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuanzia shule za msingi, hadi vyuo vikuu.

Ametoa wito huo leo (Jumamosi, Mei 6, 2023) alipomuwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye kongamano la kumbukizi ya miaka 101 ya hayati Mwalimu Nyerere lililofanyika katika ukumbi wa Chimwaga, Chuo Kikuu cha Dodoma.

 

Amesema kuwa kama lilivyo lengo la kongamano hilo ni muhimu kuwarithisha vijana wa Kitanzania fikra na falsafa za Baba wa Taifa. “Aidha, nyote mtakubaliana nami kwamba yapo mambo mengi ambayo tungetamani vijana wetu wayafahamu kuhusu urithi aliyotuachia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.”

 

Mheshimiwa Majaliwa amesema baadhi ya mambo ambayo vijana wanapaswa kurithishwa ni kuyafahamu maisha ya Mwalimu Nyerere hasa baada ya kustaafu uongozi wa nchi na siasa za majukwaani, kutambua juhudi zake katika harakati za kuleta amani na kufanikisha ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika na bara la Afrika.

 

Ameyataja masuala mengine kuwa ni kufahamu kipaji cha Mwalimu Nyerere katika harakati zake za kupigania uhuru na kuwaunganisha Watanzania na kuwa na uwezo wa kumfahamu na kumuelezea Mwalimu Nyerere alikuwa ni nani katika historia ya Tanzania.

 

“Miongoni mwa urithi huo ambao tungependa kizazi chetu kiufahamu ni pamoja na kuwa na uwezo wa kumfahamu na kumuelezea Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa ni nani katika historia ya Tanzania; kuzielewa na kuzitambua juhudi za zake katika kuimarisha ustawi wa Tanzania hususan kupitia falsafa yake ya kutokomeza maadui watatu yaani ujinga, umaskini na maradhi.”

 

Wakati huohuo, Mheshimiwa Majaliwa amesema kumekuwa na taarifa za malalamiko kuhusu kuongezeka kwa kelele na mitetemo katika sehemu mbalimbali nchini na maeneo yaliyoongoza kwa kulalamikiwa ni za nyumba za starehe, kumbi za burudani na nyumba za ibada.

 

Amesema katika kudhibiti kelele na mitetemo kutoka katika kumbi za starehe, Ofisi ya Makamu wa Rais ilitoa maelekezo mahususi yaliyolenga kudhibiti mitetemo iliyopitiliza katika kumbi za starehe hapa nchini. Pia, maelekezo hayo yaliainisha jinsi uratibu unavyopaswa kufanyika katika nyumba za ibada kwa kuwaomba viongozi wa dini kupitia Kamati za Amani kujadili suala la kelele na mitetemo iliyopitiliza kutoka kwa baadhi ya nyumba za ibada ili kupata namna bora ya kuendesha shughuli za ibada.

 

Hata hivyo, Mheshimiwa Majaliwa amesema, kumejitokeza taharuki kwa baadhi ya viongozi wa dini wakati Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashughulikia malalamiko kuhusu ongezeko la kelele na mitetemo.

 

“Serikali ingependa kutoa ufafanuzi kwamba shughuli za dini ziendelee kufanyika kama kawaida na suala la uratibu wa jambo hilo katika nyumba za ibada liendelee kuratibiwa na viongozi wa dini wenyewe kupitia Jumuiya ya Maridhiano na Amani.”

 

“Serikali itaendelea kushauriana na jumuiya ya maridhiano na amani katika kuona namna bora ya kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia mahitaji ya jamii na kulinda afya za Watanzania,” amesema.

 

Mapema, Mbunge wa Jimbo la Kilosa, Prof. Palamagamba Kabudi ametoa wito kwa Watanzania kuyaishi maono ya hayati Mwalimu Julius K. Nyerere na kuwa wazalendo kwa kuwa mwalimu Nyerere bado anaishi kutokana na falsafa zake alizoziacha kwa Taifa.

 

Naye, Naibu Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu amesema kazi za hayati Mwalimu Nyerere zitakumbukwa milele na milele kwani ni mtu muhimu kwa Taifa letu. “Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kupitia kongamano hili ndicho chombo kitakachoweza kuwasaidia vijana kufahamu nini Mwalimu Nyerere alifanya, tofauti na hapo historia itapotea.”

 

Naye, Mwenyekiti wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Mzee Paul Kimiti ameiomba Serikali itenge eneo kwa ajili ya makumbusho ya hayati Mwalimu Nyerere katika makao makuu ya Serikali hapa Dodoma ambayo yatahifadhi historia yake.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere na Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda amewasihi vijana wawe wazalendo kwa kuipenda Tanzania kwani uzalendo ni silaha muhimu sana katika kuliletea Taifa maendeleo.

 

Aidha, Mheshimiwa Pinda amempongeza Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kuwawezesha vijana ikiwemo kuanzisha mpango wa kesho iliyo bora (Building a Better Tomorrow) wenye lengo la kuwawezesha vijana kwenye sekta ya kilimo.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta na Waziri Mkuu Mstaafu na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius K. Nyerere, Mizengo Pinda katika Kongamano la Kubukizi ya Miaka 101 ya kuzaliwa kwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lililofanyika kwenye ukumbi wa Chimwaga jijini Dodoma,
Baadhi ya washiriki wa Kongamano la Kumbukizi ya Miaka 101 ya Kuzaliwa kwa Mwalimu Julius K. Nyerere wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  alipozungumza katika Kongamno hilo kwenye ukumbi wa Chimwaga jijini Dodoma
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikabidhi mche wa parachichi kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Sechelela ya jijini Dodoma ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa Klabu za Mazingira za Mwalimu Nyerere kuanzia shule za Msingi , Skindari,Vyuo vya Kati na Vyuo Vikuu,  baada ya kuhutubia   Kongamano la Kumbukizi  ya Miaka 101 ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa Mwalimu  Julius Nyerere Kwenye ukumbi wa Chimwaga Jijini Dodoma
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi Hati ya Huduma iliyotukuka Waziri Mkuu Mstaafu na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius K. Nyerere, Mizengo Pinda katika Kongamano la Kumbukizi  ya Miaka 101 ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa Mwalimu  Julius Nyerere lililofanyika kwenye ukumbi wa Chimwa ga Jijini Dodoma, Mei 6, 2023. Kushoto ni Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Paul Kimiti.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi cheti cha shukurani Meneja Mahusiano wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Zawadi  Kanyawana  baada ya benki hiyo kuwa mmoja wa wadhamini wa Kongamano la Kumbukizi ya  Miaka 101 ya Kuzaliwa Mwalimu Julius K. Nyerere lililohutubiwa na Waziri Mkuu kwenye ukumbi wa Chimwaga jijini Dodoma, Mei 6, 2023.  Wengine pichani kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius K. Nyerere, Paul Kimiti, Waziri Mkuu Mstaafu na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi hiyo, Mizengo Pinda, Naibu Spika wa Bunge, Azan Zungu na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.