Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Azungumza na Wenyeviti wa CCM wa Mikoa Ikulu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  ambae pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar.Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na wageni wake  Ujumbe wa Wenyeviti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar, ukiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tabora Ndg.Hassan Wakasuvi, walipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kumsalimia , mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar leo 30-8-2023
 

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amekiahidi chama hicho kufanya mkutano mkuu wake Taifa ndani ya visiwa vya Zanzibar.

Makamu Mwenyekiti huyo aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Wenyeviti wa Chama hicho wa mikoa yote ya Tanzania waliofika kumsalimia.

Alisema CCM Zanzibar, itahakikisha inalifanikisha hilo kwa kuwezesha ufanisi wa rasilimali zote ikiwemo eneo muafaka la kuhudumia wajumbe wote wa mkutano mkuu taifa pamoja na mikutano mengine ya Halmashauri kuu taifa kwa kujenga ukumbi mkubwa wa mikutano ambao chama utajivunia nchi nzima ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya chama hicho.

Rais Dk. Mwinyi, alimpongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa ambae pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan kwa hatua ya kuwaalika viongozi hao wa chama kuhudhuria Tamasha la Kizimkazi.

Aidha, alisifu ujio wa viongozi hao kuwa ni njia moja ya ushirikiano na kudumisha umoja na mshikamo wao ndani ya chama, hivyo aliwaomba viongozi hao kutembelea maeneo mengine na kujionea miradi ya maendeleo ya chama hicho kwa kubadilishana uzoefu.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mjini Kichama Ndg.Talib Ali Talib alimueleza Makamu Mwenyekiti huyo jinsi walivyoupokea ugeni huo na kuutembeza maeneo mbalimbali ya historia ya Zanzibar ikiwemo, Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar na kuangalia maeneo mengine ya Utalii.

Naye, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Tabora, Hassan Wakasuvi kwaniaba ya wenyeviti wa chama hicho kwa ngazi za mikoa yote nchini, walimpongeza Makamo Mwenyekiti Rais Dk. Mwinyi kwa hatua kubwa ya maendeleo aliyoifanikisha ndani ya kipindi kifupi cha uongozi wake.

Pia, Wenyeviti hao walimshukuru Mwenyekiti wa CCM taifa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan kwa mwaliko aliowapa kuhudhuria Tamasha la Kizimkazi na kujionea mandhari halisi ya Zanzibar kwa waliokuwa hawajawahi kufika.

Walisifu hatua hiyo, njia ya kukuza utalii wa ndani na kudumisha ushirikiano kwa viongozi wa chama hicho wa mikoa yote nchini.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU - ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.