Habari za Punde

Rais Dk Hussein Mwinyi akutana na Mabalozi walioteuliwa karibuni Ikulu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Mabalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,walipofika Ikulu Jijini Zanzibar leo 5-9-2023 kwa mazungumzo na kumuaga wakielekea katika vituo vyao vya Kazi waliopangiwa, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar,ujumbe huo ukiongozwa na Balozi wa Tanzania Nchini Canada Mhe.Balozi.Joseph Sokoine  (kulia kwa Rais) na (kushoto kwa Rais) Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said.
MABALOZI wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwa katika mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) walipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kumuaga, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 5-9-2023.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na Mabalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 5-9-2023, walipofika kwa ajili ya mazungumzo na kumuaga wakielekea katika vituo vyao vya Kazi waliopangiwa.(Picha na Ikulu)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amewataka mabalozi wanaoiwakilisha Tanzania kwenye maeneo yao ya kazi kuangalia zaidi fursa za Uchumi na Maendeleo kwa lengo la kuifanyia kazi kwa vitendo Sera ya mambo ya Nje ya Diplomasia ya uchumi.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na mabalozi waliofika kumuaga kuelekea kwenye vituo vyao vya kazi.

Dk. Mwinyi aliwaeleza mabalozi hao kuangalia zaidi fursa za uwekezaji kwani Tanzania ina maeneo mengi yanayohitaji wawekezaji hasa baada ya kukutana na wadau wa uwekezaji nchini na kujadiliana nao.

Akizungumzia masuala ya Fedha, Rais Dk. Mwinyi aliwataka mabalozi hao kuangalia fursa za mikopo nafuu.

Kuhusu Sekta ya Utalii, Rais Dk. Mwinyi alisema bado Utalii unanafasi pana kwa Uchumi wa taifa kwani unaingiza asilimia 30 ya pato la taifa, hivyo aliwataka mabalozi hao kuongeza jitihada zaidi za kuutangaza kwa wingi Utalii na fursa zilizomo nchini.

Alisema bado nchi inahitaji watalii wengi  zaidi ili kukuza Sekta hiyo.

Akizungumzia Sekta ya biashara Rais Dk. Mwinyi aliwaeleza mabalozi hao kuangalia fursa kuzitangaza bidhaa zinazozalishwa nchini kwa kuangalia uwezekano wa kuzipatia masoko likiwemo la karafuu na viungo vyengine.

Vilevile, Rais Dk. Mwinyi aliwaeleza mabalozi hao kuendelea kuitangaza Sera ya Uchumi wa Buluu kwani bado kuna maeneo mengi yanahitaji wawekezaji.

Akizungumza kwa niaba ya mabalozi wenziwe, Balozi Joseph Sokoine anakwenda kuiwakilisha Tanzania nchini, Canada alimuahidi Rais Dk. Mwinyi kuzifanyia kazi nasaha na miongozo yote aliyowapa kwa nia ya kuziendeleza Sera za Diplomasia ya uchumi na Uchumi wa buluu wa Maendeleo ya taifa.

Mabalozi waliofika hapo ni Balozi Fatma Rajab anaekwenda kuiwakislisha Tanzania nchini Oman, Balozi Naimi Azizi anaekwenda Austria, Balozi Ali Mwadini anakwenda Ufaransa na Balozi Ceasar Waitara anaekwenda kuiwakilisha Tanzania nchini Nabia                    

Mara baada ya mkutano huo na Mabalozi, Rais Dk.  Mwinyi aliodoka Zanzibar kuelekea Dar es Salaam kwa ziara ya kikazi.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.