Habari za Punde

Zanzibar kufanya utafiti wa viashiria vya magonjwa yasiyoambukiza

Naibu Waziri Wa Afya Zanzibar Hassan Khamis Hafidh akizungumza wakati akitoa taarifa kwa umma juu ya  utafiti wa kitaifa wa viashiria vya magonjwa  yasioambukiza (NCDs steps survey) unaotarajiwa kuanza Septemba 09 katika kaya 540 za Unguja na Pemba,hafla iliyofanyika Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Unguja 

Meneja wa kitengo cha magonjwa yasioambukiza Omar Mohammed Suleiman akijibu baadhi ya maswali ya Waandishi wa Habari kuhusiana na ugonjwa huo wakati wa utoaji wa taarifa ya utafiti wa kitaifa wa viashiria vya magonjwa  yasioambukiza (NCDs steps survey) unaotarajiwa kuanza Septemba 09 katika kaya 540 za Unguja na Pemba ,hafla iliyofanyika  Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Unguja.

PICHA NA FAUZIA MUSSA MAELEZO ZANZIBAR


Na Rahma Khamisi Maelezo   8/9/2023

 

Wizara ya Afya Zanzibar inatarajia kufanya Utafiti wa kitaifa wa viashiria vya magonjwa  yasiyoambukiza(NCDs step servey ) kuanzia  kesho  Septemba 9 mwaka huu.

 

Akitoa Taarifa kwa waandishi wa habari  kuhusiana na utafiti huo huko Ofisini kwake Mnazimmoja Naibu Waziri wa Afya Hassan Khamis Hafidhi amesema utafiti huo utafanyika Tanzania Nzima ambapo kwa upande wa Zanzibar utaanza Rasmi Siku ya Jumamosi katika Shehia zilizochaguliwa kitaalamu.

 

Naibu Waziri alifahamisha kuwa kwa mujibu wa miongozo ya Kitaalamu ya kiutafiti jumla ya kaya 540 zitahojiwa Unguja na Pemba na kuwataka wananchi wa kaya hizo kutoa ushirikiano  na kuwapatia tarifa sahihi wataalamu ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

 

Ameongeza kwa kusema kuwa  miongoni mwao taarifa zotakazokusanywa katika utafiti huo ni pamoja na  vichecheo vinavyopelekea maradhi hayo ikiwemo matumizi ya pombe,tumbaku, uzito wa mwili, kiwango cha kuushughulisha mwili na ulaji wa matunda na mbogamboga,hivyo aliwataka wanakaya husika kuwa wawazi ili kupatikana kwa taarifa na takwimu sahihi.

 

Amesema lengo la utafiti huo ni kutathmini hali ya afya juu ya  viashiria hatarishi na mwenendo wa magonjwa yasiyoambukiza nchini kufuatia kuongezeka kwa magonjwa hayo mwaka hadi  mwaka.

 

“Maradhi haya yamekuwa tishio duniani kote ambapo kwa Zanzibar yanaongezeka  mwaka hadi mwaka jambo ambalo linatia hofu tushirikiane katika mapambano dhidi ya maradhi haya “.alisisitiza Naibu huyo

 

Utafiti kama huo ulifanyika  Zanzibar mwaka 2011 na Tanzania Bara  ulifanyika 2012 ambapo Zanzibar ilikua Nchi ya kwanza kufanya utafiti  huo katika Ukanda wa Afrika Mashariki.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.