Habari za Punde

Waandishi Wajengewa Uelewa Juu ya Maradhi ya Mripuko

Meneja wa Kitengo cha Elimu ya Afya Zanzibar  Bakari Hamad Magarawa akiwasilisha mada ya hali ya uchafu wa mazingira na uviko 19 Kwa Waandishi wahabari katika mafunzo ya kuwajengea uelewa juu ya Magonjwa ya mripuko( maleria ,macho na matumbo) huko kitengo cha elimu ya afya sogea Zanzibar.
Afisa wa Afya ya jamii wizara ya afya Mwinyi Khamis akiwasilisha mada ya hali ya maleria katika mafunzo ya Waandishi wa Habari juu Magonjwa ya mripuko( maleria ,macho na matumbo) huko Kitengo cha elimu ya afya sogea Zanzibar.
Baadhi ya Waandishi wa habari wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uelewa juu ya Magonjwa ya mripuko (maleria,macho na matumbo)huko Kitengo cha elimu ya afya sogea Zanzibar.
PICHA NA FAUZIA MUSSA-MAELEZO ZANZIBAR

Na Fauzia Mussa-Maelezo Zanzibar

Afisa wa afya ya jamii wizara ya afya Mwinyi Khamis amesema licha ya juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali za kupambana na ugonjwa wa malaria bado jamii haipo tayari kuunga mkono juhudi  hizo jambo ambalo linapelekea kuongezeka  kwa  ugonjwa huo visiwani Zanzibar.

 

Akizungumzia hali ya malaria nchini katika mafunzo ya kuwajengea uelewa waandishi wa habari  juu ya magonjwa ya mripuko yakiwemo malaria, macho na matumbo huko kitengo cha elimu ya afya Sogea amesema takwimu za wizara ya afya zinaonyesha kuwa ugonjwa huo umeongezeka takribani kwa wilaya zote za Zanzibar na kuwaathiri zaidi  wanaume wenye umri kati ya miaka  15 hadi 45.

“wanaoathirika zaidi  kwa ugonjwa huu ni wanaume ikiwemo  waendesha boda boda, wajenzi wa usiku, wanakwenda kumbi za starehe usiku pamoja na watazamaji mpira nyakati za usiku”, alifahamisha.

Alieleza kuwa kutokana na takwimu hizo  wilaya ya mjini inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa  ya wagonjwa  ikifuatiwa na wilaya ya magharibi B.

Amesema hali ya ongezeko la ugonjwa huo ni kutokana  na jamii kutokutumia njia za kujikinga ikiwemo kulala kwenye vyandarua ,kuchelewa kufika vituo vya afya kwa wenye dalili  za ugonjwa , kuwepo kwa mazalia ya mbu pamoja na mabadiliko ya tabia nchi.

 

Afisa huyo aliitaka jamii kudumisha usafi katika maeneo na kufika katika vituo vya afya ndani ya masaa 24 mara wanapopata dalili za homa ili kupata matibabu katika wakati sahihi.   

Aidha amesema  wizara kupitia kitengo cha elimu ya afya  inaendelea kudhibiti ugonjwa wa malaria  kwa  kutoa elimu ya afya kwa jamii, tiba kwa wale waliogundulika kuwa na vimelea vya malaria, upigaji wa dawa majumbani kwa maeneo yaliathiriwa zaidi, kutoa dawa na kuichunguza damu jamii iliyo karibu na  mgonjwa, pamoja na kutia viatilifu kwenye madimbwi ya maji.

 

Akizungumzia hali ya macho mekundu, Mratibu wa huduma za Afya ya Msingi na matibabu ya macho  Dkt Rajab Mohammed  Hilal amesema jumla ya watu 12860 wamepatiwa matibabu katika vituo mbalimbali vya afya Zanzibar na kwa  sasa hali ya ugonjwa huo imepungua.


Aidha alieleza kuwa jumla ya wagonjwa 5 walilazalwa katika  hospital ya rufaa ya  Mnazi mmoja baada ya kutumia dawa ambazo sio sahihi katika  kutibia ugonjwa huo akiwemo mtoto wa  miaka  11 ambapo walipoteza uoni wao.

 

Mratibu huyo aliisisitiza jamii kuacha utamaduni wa kutumia dawa za kienyeji na kufika katika vituo vya afya ili kupata matibabu sahihi.

 

“Baadhi ya takwimu kwa wagonjwa waliotibiwa  katika vituo vyetu  kwa Zanzibar ni pamoja na wagonjwa 1,459 katika kitengo cha matibabu ya macho Hospitali ya  Mnazi mmoja, 3,432 Kwamtipura, 2,316 Mpendae, 22 Chake chake,1,320 Kivunge, 993 Wete,25 Shungi, Kambini kichokochwe  65, 54 Wesha,  65Wingwi,   100 Pujini,  480 Micheweni  ,na 660 Mkoani .” alieleza mratibu huyo

 

Akiwasilisha mada ya mazingira Meneja wa Kitengo cha Elimu ya Afya Zanzibar  Bakari Hamad Magarawa amesema hali ya uchafu wa mazingira inachangia ongezeko la magonjwa ya mripuko ikiwemo malaria na kipindupindu na kuitaka jamii kudumisha usafi katika maeneo yao pamoja na kuzingatia maelezo ya kitaalamu ili kujiepusha na   magonjwa hayo.

 

Hata hivyo aliwasisitiza  waandishi waliopatiwa mafunzo hayo kuifikisha elimu  kwa jamii  ili kujua hali halisi juu ya Magonjwa hayo na kuweza  kujikinga.

Jumla ya watu 11 wamefariki kutokana na  ugonjwa  wa maleria kuanzia Januari 1 hadi januari 26 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.