Mkufunzi, Muhadhiri Muandamizi Kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, Dkt Gervas Kasiga akitoa mafunzo kwa wasanii wa filamu (hawapo pichani) kuhusu kufuata maadili katika Sanaa hizo huko katika ukumbi wa Sanaa Rahaleo .
.Naibu Katibu wa Chama cha Filamu Zanzibar Biubwa Kombo Haji akitaka ufafanuzi kwa Mkurugenzi wa Tamasha la Filamu Hatibu Madudu juu ya njia sahihi za kujiinua kisanaa kwa wasanii wa Zanzibar, katika Ukumbi wa Sanaa Rahaleo .
Baadhi ya Wasanii wa Filamu wakimsikiliza Mkufunzi, Muhadhiri Muandamizi Kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma Dkt Gervas Kasiga (hayupo pichani ) katika ukumbi wa Sanaa Rahaleo .
Baadhi ya Wasanii wa Filamu wakimsikiliza Mkufunzi, Muhadhiri Muandamizi Kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma Dkt Gervas Kasiga (hayupo pichani ) katika ukumbi wa Sanaa Rahaleo .
PICHA KUTOKA BSSFU.
Na Khadija Khamis – Maelezo .18/09 /2024.
Mkurugenzi wa Tamasha la Filamu Hatibu Madudu amewataka Wasanii kutumia fursa za Elimu wanazopewa kwa kukuza soko la Filamu Zanzibar ili kupata kutambulika Kimataifa.
Hayo ameyasema katika ukumbi wa Sanaa Rahaleo wakati wa ufungaji wa mafunzo ya Wasanii mbali mbali wa Filamu wenye lengo la kuwapatia elimu, mbinu, pamoja na njia sahihi ya kuzitangaza Sanaa zao.
Aidha amesema wasanii wanatakiwa kukimbilia fursa na sio kungojea mialiko ya warsha na kongamano jambo ambalo litasaidia kuzitangaza Sanaa zao.
Amefahamisha kuwa wasanii iwapo watatumia kuzitangaza Sanaa kupitia Televisheni na Mitandao mengine ya kijamii ambazo zitakuwa na ubora katika uigizaji wao zitasaidia kukuza Sanaa hizo.
Nae Katibu Mtendaji wa Baraza La Kiswahili Zanzibar Dkt Mwanahija Ali Juma amewataka vijana kutumia ubunifu ili kufikisha ujumbe sahihi katika jamii.
Kwa Upande wa Mkufunzi, Muhadhiri Muandamizi Kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma Dkt Gervas Kasiga ametoa wito Kwa Wasanii kuzingatia maadili Kwa kufuata utamaduni wa nchi yao .
Ameeleza kuwa Jamii hufuata kile ambacho huwasilishwa na wasanii hivyo iko haja ya wasanii wanapoigiza kubeba fikra na dhana nzima ya kuelimisha jamii.
Amefahamisha kuwa kubuni Sanaa ili Jamii iweze kuziamini kazi hizo, ni vyema kufuata Maadili mila silka na utamaduni katika kazi hizo pamoja na kutumia mbinu za kuwaingizia kipato chao .
Nao Washiriki hao wamezitaja changamoto mbali mbali zinazodumaza Sanaa ya Filamu Zanzibar ni pamoja na kukosa msukumo kwa Serikali Kampuni na Watu binafsi jambo ambalo linawachangia kushindwa kufikia malengo yao .
“Iwapo tutaungwa mkono kisanaa tunauwezo mkubwa wa kufikia malengo tuliyojiwekea kwani Sanaa ni kazi kama kazi nyengine .”walisema wasanii hao .
Wamesema kukosekana Kwa Sera ya filamu nchini kunachangia kudumaza maendeleo ya Sanaa hiyo pamoja na kukosekana Kwa soko la ndani.
Mafunzo hayo ya siku tatu kwa Wasanii mbali mbali yametayarishwa na Baraza la Sanaa, Sensa ya Filamu na Utamaduni ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra ya sherehe ya Tamasha la Utàmaduni wa Mzanzibar ambalo litaanza Septemba 19, 2024 katika viwanja vya Mahonda, Wilaya ya Kaskazini 'B' na kufungwa Tarehe 24 Pemba.
No comments:
Post a Comment