Habari za Punde

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa Ametembelea na Kukagua Maeneo Yalioathirika kwa Mvua Lindi. Aipa Maagizo TANROADS Ukarabati wa Barabara na Madaraja

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa leo Aprili 16, 2025 amefika na kukagua  eneo la Matandu na Somanga Mtama barabara kuu ya Dar es Salaam - Lindi  yaliyokuwa yamekatika hivi karibuni kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha Wilayani Kilwa Mkoani Lindi.

Katika Ziara hiyo, Waziri Mkuu Mhe.Majaliwa ameambatana na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, Waziri wa Ulinzi,  Stergomena Tax, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Tellack pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, Francis Ndulane.




 

*Asema Rais Dkt. Samia ametoa shilingi bilioni 130 kwa ajili ya ukarabati madaraja mkoa wa Lindi.

 

*Awatoa hofu wakazi na watumiaji wa barabara ya Dar, Lindi.

 

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ametoa maagizo kwa Mameneja wa Wakala ya Barabara nchini (TANROADS) kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye madaraja na makalavati yote ya barabara kuu nchini ili kuepuka athari zinazoweza kusababishwa na maji ya mvua.

 

Ametoa agizo hilo leo Jumatano (Aprili 16, 2025) alipokagua maendeleo ya ukarabati wa madaraja katika maeneo ya Matandu na Somanga Mtama, Wilaya Kilwa Mkoani Lindi kwenye barabara kuu ya Dar es Salaam - Lindi yaliyokuwa yamekatika kufuatia mvua zinazonyesha nchini.

 

“Fedha ambayo tunatenga kwa ajili ya ukarabati itumike ipasavyo kila baada ya mvua kubwa kunyesha wakajiridhishe na kama kipenyo cha daraja na makavati yapo vilevile”

 

Pia amemuagiza Meneja wa Tanroads Mkoa wa Lindi kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha maeneo yote yaliyoathirika na maji ya mvua yanatengenezwa na kuyarudisha katika hali yake ya kawaida.

 

Amesema kuwa Serikali ina mpango wa muda mrefu wa kujenga upya barabara ya Dar es Salaam, Lindi na Mtwara kwa viwango, hivyo ujenzi wa madaraja ni hatua ya awali ya mpango mkakati huo. “Tumetenga fedha ya ujenzi wa kilomita 100, tumefanya hivi ili kuepuka kuweka viraka viraka badala yake tujenge upya eneo lote korofi.”

 

Kadhalika amewahakikishia watumiaji wa barabara hiyo kwamba hakuna shughuli itakayo simama wakati Serikali ipo na itaendelea kufuatilia mwenendo wa uimarishaji wa barabara hiyo. “Lengo ni kuhakikisha, Serikali ipo kazini, na imeshaleta wakandarasi hii ni kutokana na maelekezo ya Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan.”

 

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amewahakikishia wakazi wa mikoa ya  Lindi na Mtwara kuwa Rais Dkt. Samia ametoa fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vipande vilivyoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

 

Naye, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema kuwa mpaka sasa mkandarasi ameshaweka nguzo 23 kati ya 43 kwa ajili ya ujenzi wa daraja la kudumu kwenye eneo la Somanga. “

 

(mwisho)

 

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

S. L. P. 980,

41193 – DODOMA.

JUMATANO, APRILI 16, 2025.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.