Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akiwasilisha mapitio ya utekelezaji wa mpango na bajeti kwa mwaka 2024/25 na mapendekezo ya mpango na bajeti ya Wizara ya Fedha kwa Mwaka wa Fedha 2025/26, bungeni jijini Dodoma.
Na Saidina Msangi, Dodoma
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha kwa kishindo bajeti ya Wizara ya Fedha kwa Mwaka wa Fedha 2025-2026 ya kiasi cha Sh. trilioni 20.19 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo kwa mafungu yake nane (8) ya kibajeti.
Awali Mhe. Dkt. Nchemba alitoa maombi ya kuidhinishiwa kiasi hicho wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Fedha bungeni Jijini Dodoma, ili iweze kutekeleza vipaumbele vyake vitano ilivyopanga kuvitekeleza katika Mwaka wa Fedha 2025/2026.
Alifafanua kuwa kati ya kiasi hicho, shilingi trilioni 19.43 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 757.79 kwa ajili ya matumizi ya maendeleo
Aidha, aliomba Bunge kuidhinishia Fungu 045 – Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi, jumla ya shilingi bilioni 122.52 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo ambapo kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 110.42 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 12.10 matumizi ya maendeleo.
‘‘Wizara ya Fedha imejipanga kutekeleza vipaumbele vitano ikiwemo kutafuta na kukusanya rasilimali fedha ya jumla ya shilingi trilioni 50.17 kwa ajili ya utekelezaji wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026’’, alisema Mhe. Dkt. Nchemba.
Alisema katika kiasi hicho Mamlaka ya Mapato Tanzania inatarajiwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 34.10, misaada shilingi trilioni 1.07, mikopo nafuu na ya kibiashara kutoka vyanzo vya ndani na nje shilingi trilioni 14.95 na maduhuli shilingi bilioni 53.54’’, alisema Mhe.Dkt. Nchemba.
Aidha, Fungu 045 – Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi inakadiriwa kukusanya shilingi milioni 843 ikiwa ni ukodishaji wa kumbi za mikutano na kodi ya pango kutokana na upangishaji wa majengo ya Ofisi yaliyopo katika mikoa mbalimbali nchini.
Mhe. Dkt. Nchemba alivitaja vipaumbele vingine vya Wizara kuwa ni kuhudumia kwa wakati deni la Serikali linalotarajiwa kuiva shilingi trilioni 14.22 pamoja na kuandaa Sera ya Usimamizi wa Mali za Umma.
‘‘Wizara ya Fedha itaendelea kuboresha, kuunganisha na kuimarisha usalama wa mifumo ya kielektroniki ya usimamizi wa fedha na mali za umma pamoja na kujenga mfumo wa pamoja wa kutoa Ankara za malipo ya Serikali ili kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato,’’alifafanua Mhe. Dkt. Nchemba.
Mafungu 8 ya Wizara ya Fedha ni pamoja na Fungu 01- Deni la Serikali, Fungu 06- Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Fungu 10- Tume ya Pamoja ya Fedha, Fungu 13- Kitengo cha Kudhibiti Fedha haramu, Fungu 21- Hazina, Fungu 22- Huduma za Mfuko Mkuu, Fungu 23- Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali na Fungu 50- Wizara ya Fedha, huku Fungu 045 – linalosimamiwa na Wizara ya Fedha linalohusisha Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi.
Mwisho.
No comments:
Post a Comment