HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI,
MHESHIMIWA DK. AMANI ABEID KARUME, WAKATI WA KUAGANA NA WAHESHIMIWA WAJUMBE WA BARAZA LA WAWAKILISHI LA SABA, KATIKA UKUMBI WA BARAZA LA WAWAKILISHI, ZANZIBAR
TAREHE 11 AGOSTI, 2010
Mheshimiwa Spika,
Mheshimiwa Waziri Kiongozi,
Mheshimiwa Jaji Mkuu,
Mheshimiwa Naibu Waziri Kiongozi,
Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Mabalozi wadogo walioko Zanzibar,
Viongozi wa vyama vya siasa,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana,
ASSALAAMU ALAYKUM,
Naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma na Mwenye Uwezo wa kila Jambo, kwa kutupa afya na uzima tukaweza kujumuika hapa leo kwa ajili ya shughuli hii adhimu. Namshukuru pia kutujaalia amani na utulivu ndani ya nchi yetu vinavyotuwezesha kuendesha mambo yetu kwa mafanikio makubwa.
Nakushukuru Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi hii ya kutumia uwezo wangu wa kikatiba kuhutubia Baraza la Wawakilishi la Saba na kutoa tathmini ya utekelezaji wa baadhi ya shughuli za Awamu ya Sita ya Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar, chini ya Uongozi wangu, kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza na wananchi wote kwa jumla. Hii ndio nafasi yangu ya mwisho kulihutubia Baraza hili nikiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Nashukuru sana kupata fursa hii ambayo, pia, nitaitumia kutangaza rasmi kuvunjwa kwa Baraza hili.
Mheshimiwa Spika,
Nchi yetu inaendelea na utaratibu tuliojiwekea wa utekelezaji wa demokrasia ya kupokezana uongozi wa nchi kwa njia ya uchaguzi. Awamu ya Sita ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliingia madarakani Novemba, mwaka 2000 kufuatia Uchaguzi Mkuu nchini kwetu. Muda wa kikatiba na kisheria wa Awamu hiyo unamalizika baada ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 31, mwaka huu.
Mheshimiwa Spika,
Ni vyema kujikumbusha tunakotoka, tokea mwaka 2000 mpaka hapa tulipo 2010. Kwanza, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa viongozi walionitangulia wa Awamu zilizopita kwa jitihada zao za kuweka misingi ya maendeleo ya nchi yetu.
Awamu ya Sita iliingia katika wakati ambao nchi yetu ilikuwa imekabiliwa na matatizo ya kisiasa ambayo yalichangia kuleta hali ya mgawanyiko wa wananchi, kuathiri maendeleo ya miundombinu, kuwepo uchumi dhaifu na uhusiano usioridhisha na baadhi ya nchi marafiki.
Takwimu zinaonesha kwamba Pato la Taifa kwa mwaka 2000 lilikuwa T.Shs. 190.5 bilioni na pato la wastani la kila mtu lilikuwa T.Shs. 207,987 sawa na US$ 260 kwa mwaka. Ukusanyaji wa mapato ya ndani ya serikali kwa mwaka 2000/2001 ulifikia T.Shs. 38,674 milioni. Huduma za jamii zikiwemo elimu, afya, maji safi na salama haikuwa ya kuridhisha kutokana na kudhoofika kwa uchumi wetu. Hali ya miundombinu, zikiwemo bandari, barabara na mawasiliamo, pia ilikuwa si ya kuridhisha. Mwaka huo kulikuwepo skuli za msingi na kati 181, sekondari 28, vyuo 3 na vyuo vikuu 2.
Kwa upande wa afya, vituo vya afya vilikuwa 106 kwa Unguja na Pemba na wananchi wetu wengi waliathirika na ugonjwa wa malaria.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Mapinduzi Awamu ya Sita haikuridhika na hali hiyo na ikaamua kufuatilia kiini cha matatizo hayo, yaliyochangiwa kwa kiasi kikubwa na hali mbaya ya siasa, na kuyatafutia ufumbuzi.
Kwa jitihada za pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chama tawala cha CCM na chama cha upinzani CUF, tulifanya mazungumzo ya pamoja na tukafanikiwa kufikia mwafaka wa mwaka 2001. Hatua hiyo ilisaidia kupunguza hali ngumu ya siasa na kuwafanya wawakilishi wa CUF kuingia Baraza la Wawakilishi na Washirika wetu wa Maendeleo kurejesha uhusiano mzuri na sisi.
Hali hiyo ilisaidia kufungua sura mpya katika kuendeleza uchumi wa nchi yetu, miundombinu na huduma za jamii.
Kwa mfano, katika mwaka 2004, pato la taifa lilipanda na kufikia T.Shs. 344.3 bilioni wakati pato la wastani la mtu lilikuwa T.Shs. 330,764 sawa na US$ 303. Makusanyo ya kodi yaliimarika na kufikia T.Shs. 59,479 milioni. Serikali kwa makusudi ilifanya mageuzi ya uchumi ambayo yaliwezesha ukuaji wa ukusanyaji kodi, kustawi kwa biashara na vianzio vya uchumi kama utalii, mawasiliano, huduma za fedha nakadhalika. Jumla ya watalii 125,522 walitembelea Zanzibar mwaka 2004 ikilinganishwa na 97,165 mwaka 2000. Idadi ya benki iliongezeka kutoka benki 5 mwaka 2000 kufikia 6 mwaka 2004, na maduka ya biashara ya fedha za kigeni kuongezeka kutoka 14 mwaka 2000 hadi kufikia 24 mwaka 2004.
Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2000-2005 ulitupa mafanikio katika sekta zote. Huduma za jamii zilipata msukumo mkubwa wa maendeleo. Kwa upande wa elimu, mwaka 2004 tulikuwa na skuli za msingi na kati 229, sekondari 49, vyuo 3 na vyuo vikuu 3, kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar - SUZA tulichokifungua mwaka 2001. Idadi ya wanafunzi katika skuli za msingi ilifikia 199,938 mwaka 2004 kutoka 163,113 mwaka 2000; na wanafunzi wa sekondari 61,002 mwaka 2004, kutoka 42,542 mwaka 2000.
Huduma za afya ziliimarika na vituo vya afya viliongezeka kufikia 122 mwaka 2004. Watoto 37,581 walipatiwa chanjo za magonjwa mbali mbali ya watoto.
Upatikanaji wa maji safi na salama uliimarika kutoka asilimia 35 kwa maeneo ya vijijini na asilimia 70 katika maeneo ya mijini Unguja na Pemba mnamo mwaka 2000 hadi asilimia 51 kwa maeneo ya vijijini na asilimia 75 kwa maeneo ya mijini Unguja na Pemba mwaka 2004.
Mheshimiwa Spika,
Mipango ya uimarishaji miundombinu iliendelea kutekelezwa na ilipofikia mwaka 2004 barabara kadhaa kuu zilijengwa au kufanyiwa matengenezo.
Kuanzia mwaka 2005 hadi 2010 utekelezaji wa mipango yetu ya kazi za maendeleo ulikwenda sambamba na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2005-2010 na katika kipindi cha uhai wa Baraza hili, serikali iliendelea kuchukua hatua mbalimbali zilizolenga kuimarisha maendeleo ya wananchi. Kuhusiana na siha, Sera ya Chakula na Lishe iliandaliwa na kuanza kutekelezwa. Lazima tukiri kuwa upatikanaji wa uhakika wa chakula na lishe bora bado ni changamoto kwa sehemu fulani ya jamii yetu. Kwa vile upatikanaji wa maji safi na salama, pia, ni nyenzo muhimu kwa kuhakikisha jamii ina siha njema miaka mitano iliyopita serikali iliendeleza juhudi za kuwafikishia huduma hiyo muhimu wananchi wengi zaidi, mijini na vijijini, Pemba na Unguja.
Mafanikio ya Kiuchumi:
Mheshimiwa Spika, Kama nilivyotangulia kusema, sambamba na juhudi za kumuendeleza Mzanzibari kiafya na kielimu, katika miaka mitano inayomalizika mkazo uliwekwa katika maendeleo ya uchumi. Wataalamu wanasema kuwa hakuna maendeleo pasipo ukuaji wa uchumi. Dira yetu ya Maendeleo ya 2020 imeweka msisitizo maalumu katika mabadiliko ya kiuchumi (economic transformation) kutoka uchumi duni unaotegemea kilimo cha asili na kuelekea kwenye uchumi wa kisasa. Dira pia ilisisitiza maeneo matatu makubwa ya kiuchumi. Mosi, Utalii endelevu; pili, Uzalishaji viwandani; na tatu, Kilimo cha kisasa. Ili kutekeleza mahitaji hayo ya Dira ya Maendeleo, na kwa kutambua hali duni ya miundombinu ya kiuchumi, serikali katika kipindi cha 2005 – 2010 iliweka mkazo katika ujenzi wa mazingira mazuri na misingi imara ya kiuchumi. Mafanikio makubwa yamepatikana katika kukuza uchumi ingawa bado kuna baadhi ya changamoto kuelekea mageuzi makubwa ya uchumi kama yanavyotarajiwa chini ya Dira yetu.
Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana ni kukua kwa thamani ya Pato la Taifa kutoka T.Shs. 394.9 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 878.4 bilioni mwaka 2009 kwa kutumia bei za kudumu za mwaka 2001. Kutokana na ukuaji huo, Wastani wa pato la mtu binafsi uliongezeka kutoka T.Shs. 368,000 mwaka 2005 sawa na dola za Marekani 327.0 hadi T.Shs. 728,000 sawa dola za Marekani 557.0 Ongezeko hilo ni la kujivunia ingawa wastani wake umeendelea kuathiriwa na kasi kubwa ya ongezeko la idadi ya watu nchini petu. Juhudi maalum zinahitajika kudhibiti kasi hii ili kuendana na ukuaji wa uchumi na kuzuia athari kubwa kwa mazingira. Kasi ya wastani wa ukuaji wa uchumi imekua kutoka asilimia 4.9 mwaka 2005 kufikia asilimia 6.7 mwaka 2009. Kasi hiyo ya ukuaji ingekuwa kubwa zaidi lakini imeathiriwa na misukosuko ya kiuchumi na fedha iliyojitokeza duniani kote.
Mchango wa Kisekta:
Mheshimiwa Spika, Kufuatia mageuzi yaliyotarajiwa katika Dira ya Maendeleo ya 2020, mafanikio ya kuridhisha yamepatikana. Sekta ya huduma ndio iliyoongoza katika mchango wa Pato la Taifa na ukuaji wa uchumi kwa kuchangia wastani wa asilimia 45 ya Pato la Taifa katika kipindi hicho. Lengo katika Dira 2020 ni kuwa, sekta hii ichukue jukumu kubwa zaidi la uchumi.
Mafanikio makubwa yamepatikana katika kuimarisha Utalii nchini, ikiwa ni mojawapo ya shughuli za kiuchumi iliyopo chini ya sekta hii. Thamani ya huduma za mahoteli na mikahawa imeongezeka maradufu kutoka T.Shs. 30.6 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 63.1 bilioni mwaka 2009. Aidha, idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu nayo imekua kutoka watalii 125,522 hadi 134,954 katika kipindi hicho. Kwa jumla, mwenendo umekuwa wa kuridhisha katika maendeleo ya shughuli za utalii nchini yanaendana na Dira yetu ya Maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Sekta ya Viwanda nayo ilitarajiwa kuchukua nafasi kubwa katika kukuza uchumi. Hata hivyo, imejitokeza kuwa hili ni eneo ambalo linahitaji msukumo wa hatua zaidi katika nusu ya pili ya Dira yetu ya Maendeleo. Sekta binafsi katika uwekezaji na uzalishaji viwandani inahitaji kuhamasishwa na kushiriki vizuri zaidi. Katika miaka mitano iliyopita, mchango wa sekta hii kwa Pato la Taifa kwa wastani ulikuwa asilimia 14.1 tu. Kwa hivyo juhudi maalum zinahitajika katika awamu ya pili ya utekelezaji wa Dira ya 2020.
Uwekezaji wa Rasilimali:
Mheshimiwa Spika, Moja ya kichocheo kikubwa cha ukuzaji uchumi ni uwekezaji wa rasilimali. Nchi yetu imeshuhudia kasi kubwa ya kuongezeka kwa thamani ya raslimali iliyowekezwa kati ya mwaka 2005 na 2010 kutoka T.Shs. 76.2 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 178.9 bilioni mwaka 2009. Maeneo yote makuu ya uwekezaji yalirikodi mafanikio makubwa yanayofanana. Uwekezaji kwenye ujenzi wa nyumba uliongezeka kwa asilimia 155 kutoka T.Shs. 20.8 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 52.8 bilioni mwaka 2009. Ujenzi wa nyumba za biashara ndio ulioongoza ndani ya kundi hili ambapo uwekezaji wake umepanda kutoka T.Shs. 13 bilioni hadi T.Shs. 32.2 bilioni. Ujenzi wa nyumba za makaazi umeongezeka kutoka T.Shs. 4.1 bilioni hadi T.Shs. 10.9 bilioni katika kipindi hicho. Ongezeko hilo ni ishara ya kutosha kuwa wananchi wetu wanaendelea kupata makaazi bora. Jambo la kufurahisha zaidi ni kuwa ujenzi wa nyumba vijijini umeongezeka kutoka T.Shs. 3.6 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 9.6 bilioni mwaka 2009. Nawapongeza wananchi wote wa Zanzibar kwa muamko wao wa kujijengea makaazi bora.
Mheshimiwa Spika, Uwekezaji mwengine muhimu kwa uchumi na maendeleo yetu ni katika ununuzi wa mashine na mitambo kwa ajili ya uzalishaji. Baina ya mwaka 2005 na 2009 uwekezaji huo uliongezeka maradufu (kwa asilimia 101) kutoka thamani ya T.Shs. 30.5 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 61.4 bilioni mwaka 2009. Aidha, thamani ya uwekezaji kwenye ardhi, ujenzi wa barabara na madaraja iliongezeka kwa asilimia 155 kutoka T.Shs. 23.1 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 58.9 bilioni mwaka 2009. Kwa jumla tunapaswa kwa pamoja kujivunia ukubwa wa ongezeko la thamani ya uwekezaji katika maeneo hayo matatu na kwa uwiano uliopatikana.
Biashara ya Kimataifa:
Mheshimiwa Spika, Uhusiano wa kibiashara na nchi za nje nao una umuhimu mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi ikiwemo uwazi wa biashara (Trade Openness) unaopimwa kwa jumla ya thamani ya uingizaji na usafirishaji. Jumla ya thamani ya biashara na nchi za nje ilifikia T.Shs. 150.6 bilioni mwaka 2009 kutoka T.Shs. 133.4 bilioni mwaka 2005. Hii ni ishara kuwa nchi yetu imeshiriki zaidi katika biashara na nchi za nje katika kipindi hicho. Kwa upande mwengine kila nchi huweka jitihada katika kuongeza usafirishaji kwa kadri inavyowezekana na kupunguza uagiziaji. Kwa upande wetu, kwa miaka mitano iliyopita wakati thamani ya uingizaji kimsingi haikuongezeka kutoka kiwango cha T.Shs. 120.7 bilioni mwaka 2005 na kufikia T.Shs. 120.9 bilioni mwaka 2009, usafirishaji nje umeongezeka zaidi ya maradufu kutoka T.Shs. 12.7 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 29.7 bilioni mwaka 2009. Mwenendo huo mzuri wa biashara umesaidia kupunguza nakisi ya biashara na nchi za nje kutoka T.Shs. 108 bilioni hadi T.Shs. 91.1 bilioni baina ya mwaka 2005 na 2009. Aidha, Serikali, pia, imekamilisha uandaaji wa Mkakati wa Usafirishaji (Zanzibar Export Strategy) ambao utekelezaji wake unatarajiwa kuimarisha zaidi usafirishaji wa bidhaa kutoka nchini kwetu na hivyo kuimarisha urari wa biashara. Hatua hiyo ni ya kupongezwa na kuimarishwa.
Ukusanyaji wa Mapato:
Mheshimiwa Spika, Ili serikali iweze kuhudumia mipango yake yote ya kuleta ustawi mzuri na maendeleo ya wananchi, ilihitaji pia, kuongeza uwezo wake wa mapato. Serikali ilihitaji kusimamia vyema vianzio vilivyopo na kubuni vianzio vipya pamoja na kuangalia mfumo na uwezo wa kitaasisi na kisheria, ili uendane na nia yake ya kujitegemea. Nina furaha kutamka kwamba kwa jumla tumefanikiwa sana katika kuinua uwezo wa serikali kimapato katika kipindi chote cha Awamu ya Sita. Kama ilivyo kwa maeneo mengine, mapato ya ndani yameongezeka kwa kiasi kikubwa katika kipindi hicho. Mwaka 2005/06 serikali ilikusanya jumla ya T.Shs. 68.5 bilioni kutokana na vyanzo vya ndani kupitia Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato ya Tanzania (TRA). Mwaka 2009/10 taasisi hizi zilikusanya jumla ya T.Shs. 146.2 bilioni. Ongezeko hilo la mapato ni sawa na ukuaji wa asilimia 113. Takwimu hizi zinamaanisha kuwa mapato yetu ya ndani yamekua kutoka wastani wa T.Shs. 5.7 bilioni kwa mwezi mwaka 2005/06 hadi kufikia T.Shs. 12.2 bilioni kwa mwezi mwaka 2009/2010.
Kwa upande mmoja, mafanikio haya ni matokeo ya juhudi za serikali za kuimarisha uchumi kutokana na utekelezaji wa sera za uwekezaji. Kuimarika huko kwa uchumi kumesaidia kuongeza pia wigo wa mapato. Tunamaliza muda wa uongozi wetu tukifurahia mafanikio haya na hasa kuweza kubadilisha utegemezi wa mapato yetu kutoka yanayotegemea biashara ya kimataifa na forodha na kuwa yanayotegemea zaidi vianzio vyetu vya ndani. Huu ni msingi muhimu wa kuhakikisha kuwa mapato yetu yanakuwa endelevu.
Kwa upande mwengine, mafanikio haya ni matokeo ya kuimarika kwa utendaji wa ZRB na TRA. Naomba nitumie fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza viongozi na watendaji wote wa ZRB na TRA kwa juhudi zao. Sehemu ya juhudi zetu za kurekebisha sheria pia, zimechangia katika mafanikio haya. Zaidi ya hayo, tumesimamia vyema pale palipokuwa na dalili za udokozi. Haya yote yamewezekana kutokana na ushirikiano wa pamoja baina ya Serikali na Kamati ya Kudumu ya Uchumi na Fedha ya Baraza la Wawakilishi. Hatuna budi kwa pamoja kujivunia mafanikio haya makubwa.
Usimamizi wa Fedha Za Umma:
Mheshimiwa Spika, Ukusanyaji wa mapato pekee bila usimamizi bora wa matumizi ya serikali hauwezi kuleta maendeleo ya wananchi. Kwa kutambua hili, serikali katika kipindi cha miaka mitano iliyopita iliendelea kuimarisha usimamizi wa fedha za umma. Mfumo wa sheria uliimarishwa kwa kutungwa Sheria mpya ya Fedha na ile ya Ununuzi na Uondoshaji wa mali za Serikali hapo mwaka 2005. Utekelezaji wa sheria hizo na Kanuni zake umefanyika katika kipindi cha miaka mitano hii inayomalizika. Serikali, pia, imechukua hatua maalumu za kujenga uwezo wa wahasibu na kuimarisha huduma za uhasibu serikalini. Aidha, kwa kutambua fursa muhimu ya kuimarisha usimamizi kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano, tumeanza kutumia mfumo wa Kompyuta (Integrated Financial Management System - IFMS) unaounganisha Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali (Hazina) na Wahasibu Wakuu wote wa Wizara na Taasisi zinazojitegemea, Unguja na Pemba. Mfumo huu umesaidia kuongeza udhibiti, kuimarisha ufanisi, na kurahisisha upatikanaji wa taarifa za fedha za serikali. Hali hii imesaidia kuwezesha ulipaji wa mishahara ya wafanyakazi serikalini kwa wakati.
Itakumbukwa kuwa moja kati ya kilio kikubwa kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza hili na wananchi kwa jumla ilikuwa ni ucheleweshaji mkubwa wa mafao ya wastaafu, yakiwemo kiinua mgongo na pencheni. Serikali ilikuwa inakerwa na tatizo hili. Katika kipindi cha miaka mitano inayomalizika, kufuatia kuimarika kwa hali ya fedha serikalini, juhudi ziliongezwa kulipa deni la wastaafu lililokuwepo na kuhakikisha kuwa malimbikizo mapya yanaepukwa. Serikali imefanikiwa kulipa deni lote la wastaafu hao na kuendelea kulipa wastaafu wapya mafao yao kwa wakati kadri taratibu zinapokamilika. Pamoja na Wajumbe wa Baraza lako, naomba nichukue fursa hii kuwapongeza kwa dhati watendaji wa Wizara yetu ya Fedha na Uchumi kwa utendaji wao mahiri katika kipindi hicho chote.
Mfumko wa Bei:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo ya uchumi yanahitaji utulivu wa bei za bidhaa, bei za huduma na thamani ya sarafu. Mfumko mkubwa wa bei, unaathiri imani ya wawekezaji, unapoteza thamani ya sarafu na unaathiri kipato cha wananchi wenye kipato cha kudumu kama vile wastaafu wanaoishi kwa pencheni. Serikali imechukua juhudi kubwa kudhibiti mfumko wa bei katika kipindi cha miaka mitano inayomalizika. Hata hivyo, lazima nikiri kuwa pamoja na juhudi mbalimbali zilizochukuliwa, kasi ya mfumko wa bei imekuwa ya juu kuliko ilivyotarajiwa. Mfumko wa bei kwa mwaka 2005 ulikuwa wa asilimia 9.7, mwaka 2006 asilimia 11.4, na kupanda hadi kufikia asilimia 20.6 mwaka 2008. Sababu ya kasi hiyo kubwa ya Mfumko wa bei imeendelea kuwa ni utegemezi wetu wa chakula tunachoagiza kutoka nje ya nchi hasa mchele, mwenendo wa bei za mafuta katika soko la dunia, na kwa kipindi hicho, ujenzi wa bandari ya Malindi ambayo ndio mlango mkuu wa uingizaji na usafirishaji wa bidhaa nchini.
Mheshimiwa Spika, Kwa bahati nzuri hali hiyo ilitengemaa mwaka 2009, na bei za chakula na zile za mafuta katika soko la dunia zilishuka. Kushuka huko kulisaidia kupunguza kasi ya mfumko wa bei kutoka asilimia 20.6 ya mwaka 2008 hadi asilimia 8.9 mwaka 2009. Katika kipindi cha kupanda sana kwa kasi ya mfumko wa bei, serikali ilitumia mchanganyiko wa sera zake za mapato (fiscal policies), juhudi za kuimarisha uzalishaji wa ndani wa mazao ya chakula na kuharakisha ukamilishaji wa ujenzi wa bandari ya Malindi ili kupunguza athari ya mfumko huo. Kwa upande wa sera za mapato, serikali ilitoa unafuu maalum wa kodi za uingizaji kama ushuru wa forodha na kodi ya ongezeko la thamani kwa bidhaa za vyakula muhimu zinazoingia nchini. Serikali ilibidi kusamehe mapato yake ilimradi makali ya maisha kwa mwananchi yadhibitiwe.
Ni muhimu kutambua kuwa njia hizo zote ni za muda tu. Ili kudhibiti mfumko wa bei kwa muda mrefu, tunahitaji kuimarisha uzalishaji wa ndani wa chakula na kuimarisha kipato cha mwananchi ili kupunguza sehemu ya pato linalotumiwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya chakula. Lengo ni kupunguza mchango wa bei za chakula hasa mchele katika faharisi ya bei (Consumer Price Index). Aidha, tunapswa pia kuendelea kufuatilia mwenendo wa ujazi (Liquidity) wa fedha nchini ili kuudhibiti bila ya kuathiri juhudi za maendeleo.
Huduma za Fedha:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo ya huduma za fedha ni ishara ya maendeleo ya nchi. Sekta ya huduma za fedha inajumuisha huduma za benki, maduka ya fedha za kigeni, vyama vya kuweka na kukopa na mifuko ya huduma za mikopo midogo midogo. Sekta hii, pia, hujumuisha na huduma za Bima, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na soko la mitaji. Katika kipindi hiki, huduma za benki zimekuwa sana hapa Zanzibar. Mwaka 2005 tulikuwa na Benki sita zilizokuwa zikitoa huduma na hivi sasa zimeongezeka na kufikia Benki kumi. Ongezeko hilo la benki limepelekea mchango wa huduma za kibenki katika Pato la Taifa kuongezeka kutoka asilimia 7.8 mwaka 2005 hadi asilimia 15.3 mwaka 2009.
Miongoni mwa mafanikio makubwa na ya kujivunia zaidi katika eneo hili ni yale ya kuigeuza na kuiimarisha Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ). Mwaka 2000, wakati tunaingia madarakani, PBZ haikuwa na mtaji; ilikuwa ikipata hasara mwaka hadi mwaka na haikuwa na matumaini. Hivi sasa hali imebadilika; tulitumia awamu ya kwanza ya miaka mitano kuiimarisha (Stabilize) benki hiyo na miaka mitano inayomalizika kuigeuza kimuundo, kiutumishi, na kimtaji. Maamuzi mengine yalikuwa magumu lakini yalipaswa kufanyika, mfano ni kupunguza idadi ya Wafanyakazi; uamuzi ambao ulikuwa na athari kijamii lakini ulikuwa wa lazima.
Tulihimili, pia, msukumo mkubwa wa kuibinafsisha PBZ kutokana na ushauri wa Benki ya Dunia na Benki Kuu ya Tanzania. Wataalam wao hawakutufahamu tulipoamua kutoibinafsisha benki yetu. Kwa hivyo tulishirikiana kwa pamoja kuimarisha Benki yetu na hivi leo PBZ ina mtaji maradufu ya kiwango cha chini kinachotakiwa na msimamizi wa mabenki yaani Benki Kuu. Wakati tunaingia mwaka 2006, PBZ haikuweza kutimiza mtaji wa T.Shs. 5.0 bilioni unaohitajiwa na Benki Kuu, leo hii mtaji wa PBZ ni zaidi ya T.Shs. 11 bilioni. Kutokana na hatua madhubuti tulizochukua, tumeweza kubadilisha kabisa muundo wa mtaji wa Benki ya Watu wa Zanzibar, kutoka benki iliyokuwa ikipata hasara kila mwaka, hadi benki yenye kupata faida kwa mwaka wa nne mfululizo na ilipofika mwezi huu wa Agosti 2010, kwa mara ya kwanza katika historia yake, PBZ imeweza kutoa gawio la jumla ya T.Shs. 300 milioni kwa mmiliki wake, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Hatuna budi tujipongeze kwa mafanikio hayo.
Miundombinu:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo niliyoyataja ya mwananchi na uchumi hayawezi kupatikana bila ya kuwepo kwa miundombinu bora. Sehemu za kuingilia na kutokea nchini kama vile bandari na viwanja vya ndege, mtandao bora wa barabara, upatikanaji wa uhakika na wa bei nafuu wa nishati na mtandao bora wa mawasiliano ni nyenzo za msingi kwa nchi kupiga hatua katika maendeleo. Wakati tunaingia madarakani, nchi yetu ilikua na hali duni sana ya miundombinu yote hii. Kwa sababu hiyo, katika kipindi cha uongozi wetu, tulichukuwa jukumu la kuiimarisha miundombinu hiyo ili kushajiisha na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Naomba sasa nigusie baadhi tu ya mafanikio yaliyopatikana katika maeneo hayo hapa nchini katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Mawasiliano na uchukuzi:
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu ni visiwa na sehemu za kuingilia na kutokea za bandari na viwanja vya ndege zina umuhimu mkubwa sana. Kutokana na matatizo ya ujenzi, Bandari kuu ya Malindi ilikuwa katika hali mbaya sana mwanzoni mwa miaka ya 2000. Ushauri wa kitaalam ulionesha kuwa pengine Bandari hiyo isingeweza kutumika tena baada ya mwezi Juni mwaka 2001. Matengenezo yake, kwa hivyo, yalikuwa ni jambo la lazima. Serikali imefanikiwa kuijenga upya Bandari hiyo kwa msaada wa Jumuiya ya Ulaya na fedha kutoka SMZ. Bandari za Mkoani, Wesha na Wete huko Pemba nazo zimeimarishwa. Kwa upande wa viwanja vya ndege, Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar ambao kwa sasa unajulikana kwa jina la “Abeid Karume International Airport” nao umefanyiwa matengenezo makubwa yakiwemo ya kuijenga upya njia ya kutua na kurukia ndege tuliyoizindua siku chache zilizopita pamoja na kuiongeza urefu kutoka mita 2,600 za awali hadi mita 3,022 hivi sasa na hivyo kuwezesha ndege kubwa zaidi za aina zote duniani kutua na kuruka. Hatua hii itasaidia sana katika kukuza usafiri wa ndege pamoja na utalii nchini.
Eneo jengine muhimu na lililokuwa likilalamikiwa sana na wahusika mbalimbali ni udogo wa jengo la abiria katika kiwanja hicho, lakini kwa bahati nzuri tatizo hilo tumeshalipatia ufumbuzi. Na hivi sasa Mkandarasi, Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group Company Limited” kutoka China inakusanya zana tayari kuanza ujenzi wa jengo jipya na la kisasa katika kiwanja hicho. Ujenzi huo utachukua miezi 36 na unagharamiwa kwa mkopo nafuu wa Serikali ya China kupitia Benki yake ya Exim. Juhudi za kukiimarisha kiwanja cha Karume Pemba kupitia mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika chini ya miradi ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki nazo zinaendelea. Mawasiliano, pia, yanaendelea baina ya Serikali na Benki ya Dunia juu ya uendelezaji wa kiwanja hicho cha Karume Pemba.
Barabara:
Mheshimiwa Spika, Ni jambo la kushukuru na kufurahia kuwa katika Awamu ya Sita nchi yetu imepata maendeleo makubwa katika ustawishaji wa miundombinu ya barabara. Wenyeji na wageni wanaotutembelea leo wanafarajika kwa hali bora ya barabara zetu Unguja na Pemba.
Nakumbusha tu kwamba mwaka 2000, Zanzibar ilikuwa na jumla ya kilomita 447 za lami. Unguja km. 323.5 na Pemba km. 123.5. Kuanzia mwaka huo mpaka mwaka 2009 tumeongeza barabara za lami za km. 753 kuzifanya zote kufikia km. 1,210. Hii ni sawa na asilimia 70.6 za mtandao wote wa barabara Unguja na Pemba.
Leo wananchi wa Donge na Mkokotoni wamefarajika kwa kujengewa barabara yao kwa kiwango cha lami. Hivyo hivyo, kwa wananchi wa Nungwi na wale wa ukanda wote wa utalii wa Matemwe, Pwani Mchangani, Kiwengwa, hadi Pongwe. Hali ndio hiyo, pia, kwa Wananchi wa Michamvi, Jambiani, Makunduchi, Kizimkazi, Fumba, Machui, Ghana, na kwengineko. Barabara zote hizi zimesaidia sana sio tu kuwarahisishia wananchi wa maeneo hayo usafiri wao na bidhaa zao, bali pia, zimekuwa chachu katika kukuza maendeleo ya kilimo na utalii endelevu.
Kwa upande wa Pemba, mindombinu ya barabara nayo imeimarika kwa kiasi kikubwa. Kazi ya ujenzi wa barabara za Wete - Konde, Wete – Gando, barabara sita za kusini Pemba inaendelea kama ilivyo kwa barabara za Mfenesini - Bumbwini na Amani – Dunga hapa Unguja. Barabara ya Bahanasa Mtambwe nayo iko katika hatua za matayarisho ya ujenzi. Ikifika mwezi wa Novemba mwaka huu, nitakabidhi uongozi wa nchi yetu kwa Rais ajae pamoja na kazi inayoendelea ya uwekaji wa miundombinu mbalimbali ya barabara.
Mawasiliano ya Simu:
Mheshimiwa Spika, Kutokana na maendeleo ya haraka yanayojitokeza katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, mawasiliano ya simu na huduma zake yameimarika sana. Jumla ya kampuni tano za mawasiliano ya simu zinatoa huduma hapa Zanzibar ambapo zaidi ya watu 500,000 wanamiliki simu. Mchango wa shughuli za mawasiliano na uchukuzi katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 8.0 mwaka 2005 hadi asilimia 11.0 mwaka 2009, ambapo thamani ya huduma za shughuli hizo imeongezeka kutoka Tshs. 31.5 bilioni mwaka 2005 hadi T.shs. 96.8 bilioni mwaka 2009.
Ilikuwa nia ya serikali kuweka njia mpya kuu ya mawasiliano ya habari (fibre optic cable) kuzunguka visiwa vyote viwili na kuunganishwa na Tanzania Bara na dunia kupitia njia za aina hiyo yenye ufanisi mkubwa wa mawasiliano na gharama nafuu. Kwa bahati mbaya, maombi yetu ya mkopo nafuu katika Benki ya Exim ya China kwa utekelezaji wa mradi huu yalichelewa kupata idhini. Hata hivyo, kwa sasa hatua kubwa imefikiwa na matarajio ni kuwa mradi huu utaidhinishwa kabla ya kumalizika kwa mwaka huu wa 2010. Ukikamilika, mradi pia utasaidia sana kuimarisha ufanisi serikalini kwa kutumia utaratibu wa e-government. Mradi pia unatarajiwa kuwa chanzo kipya na muhimu kwa mapato ya serikali. Kwa bahati nzuri Pemba tayari imeunganishwa na njia kuu ya mawasiliano kupitia chini ya bahari kwa kutumia waya wa kupelekea umeme kutoka Tanga. Unguja nayo itaunganishwa hivyo hivyo kupitia waya mpya wa umeme kutoka Dar Es Salaam.
Nishati:
Mheshimiwa Spika, Kwa nchi yetu, nishati inajumuisha huduma za umeme, gesi, petroli, kuni na makaa. Katika miaka mitano inayomalizika, tumepata mafanikio makubwa ya usambazaji wa nishati ya umeme lakini, pia, tulipata mitihani mikubwa. Mafanikio ni pamoja na kuweza kusambaza umeme katika maeneo mengi zaidi vijijini. Fursa za upatikanaji wa umeme zilizofikiwa Zanzibar ni za kiwango cha juu sana ikilinganishwa na hali iliyopo katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara. Hivi karibuni wananchi watakaofaidika na umeme wa uhakika itafikia asilimia 90 ikilinganishwa na asilimia kati ya 10 na 15 kwa mataifa mengine ya Afrika Mashariki na Kati.
Mheshimiwa Spika, Katika historia yake yote, Pemba ilikuwa haijapata umeme wa uhakika, ilikuwa ikitegemea umeme wa majenereta usioaminika na uzalishaji wake ni wa gharama kubwa. Mwaka 2005 tuliahidi kukiunganisha kisiwa cha Pemba, kama ilivyo kwa Unguja, na mtandao wa Gridi ya Taifa, kwa vile sasa teknolojia ya kufanya hivyo ipo duniani. Tunamaliza muda wetu wa uongozi kwa fakhari kubwa kwa kumudu kuitekeleza ahadi ya kuwapatia umeme wa uhakika wananchi wa Pemba. Ni matumaini yangu kuwa sasa Pemba itapiga hatua za haraka zaidi za maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Naomba niwashukuru kwa mara nyengine tena wananchi wa Pemba kwa ustahamilivu wao muda wote kabla ya kupatikana kwa huduma hiyo kwa uhakika. Naomba wajue kuwa nathamini sana uvumilivu wao huo na imani yao kwangu. Kwa niaba ya wananchi wote wa Zanzibar, naishukuru tena Serikali na wananchi wa Norway na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msaada wao uliosaidia kufanikisha mradi huo. Aidha, naishukuru Serikali ya Mapinduzi na wananchi wote wa Zanzibar kwa mchango mkubwa uliokamilisha utekelezaji wa mradi huo.
Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Unguja tarehe 29 Julai mwaka 2010 itakumbukwa kuwa ni siku nyengine muhimu kwa historia ya nchi yetu kuhusiana na nishati ya umeme. Siku hiyo tulizindua upya mradi wa majenereta ya akiba Mtoni hapa Zanzibar. Majenereta hayo yana uwezo wa kuzalisha Megawati 25 za nishati hii ya umeme. Waswahili tunasema “baada ya dhiki ni faraja” na pia “mvumilivu hula mbivu”. Vipindi vya kuzimika umeme kwa mwezi mmoja baina ya Mei 21 na Juni 18 mwaka 2008 na baadae miezi mitatu baina ya Disemba 10, 2009 na Machi 8 mwaka huu vilikuwa vya dhiki kwetu sote. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Zanzibar kwa utulivu na ustahamilivu wao katika vipindi hivyo vya shida. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kutuwezesha kuvuka salama. Aidha, naomba nitambue na kuzishukuru nchi za Norway, Sweden, na Uingereza kwa msaada wao uliotuwezesha kununua majenereta hayo mapya. Kwa utaratibu ule ule wa abebwae hujikaza, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar nayo imetoa mchango mkubwa katika mradi huo. Nawapongeza wananchi wote wa Zanzibar kwa mchango wao.
Mafanikio mengine muhimu katika upatikanaji wa nishati ya umeme, ni makubaliano yaliofikiwa na Serikali ya Marekani kwa kutusaidia kuweka waya mpya wa umeme na wenye uwezo mkubwa zaidi kati ya Ras Kiromoni Dar es Salaam hadi Ras Fumba, hapa Unguja. Mradi huu uko katika hatua za utekelezaji ambapo matengenezo ya waya huo yanaendelea. Tutaikabidhi awamu ijayo ya serikali yetu mradi huo mwengine muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Tunaishukuru sana serikali na watu wa Marekani kwa msaada wao huo kupitia Shirika lake la Changamoto za Milenia (MCC). Tunasema ahsanteni sana.
Maendeleo ya Sekta ya Kilimo:
Mheshimiwa Spika, Kilimo bado kinaendelea kuwa ni sekta muhimu kwa maendeleo ya uchumi na ustawi wa jamii. Inakadiriwa asilimia 70 ya wananchi hutegemea sekta ya kilimo katika kuendesha maisha yao ya kila siku. Kwa miaka yote serikali imehakikisha kuwa huduma muhimu kwa maendeleo ya sekta ya kilimo zinapatikana kwa wakati. Huduma hizo ni pamoja na matrekta, mbolea, mbegu bora, miche, dawa za kuzuia wadudu waharibifu wa mimea na mazao, dawa za kuzuia magugu, huduma za masoko, umwagiliaji wa maji na ushauri kwa wakulima. Mafunzo maalum kwa wakulima yameendelea kutolewa kwenye maeneo yao, kwenye kituo cha Kizimbani na kwa njia za “shamba darasa”. Aidha, tumefanikiwa kuzalisha mbegu bora za mazao mbali mbali na kuzisambaza kwa wakulima wetu ili waongeze tija. Tunalishukuru Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) kwa msaada na ushirikiano wake katika shughuli hizi.
Kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji maji, mnamo mwaka 2001-2003, kwa kushirikiana na Shirika la Japan International Cooperation Agency (JICA)” Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Mazingira, iliandaa Mpango Mkuu wa Umwagiliaji Maji (Zanzibar Irrigation Master Plan – ZIMP). Lengo la mpango huo ni kuiwezesha nchi yetu kuendeleza kilimo kwa njia ya umwagiliaji maji. Chini ya mpango huo, Zanzibar ina jumla ya Hekta 8,521 ambazo zikifanyiwa kazi zinaweza kuendelezwa kwa njia ya kilimo cha umwagiliaji. Eneo linalohusika linajumuisha mabonde 57 yakiwemo 38 ya Pemba na 19 ya Unguja.
Baada ya kukamilika kwa mpango huo, serikali kwa upande mwengine, imefanikiwa kufufua miundombinu ya umwagiliaji maji kwenye eneo la Hekta 740 linalojumuisha mabonde ya Bumbwisudi, Mtwango, Kibokwa na Cheju. Mradi wa Bumbwisudi na Kibokwa ulichangiwa kwa msaada wa serikali ya Korea Kusini. Pia, kwa kutumia fedha zetu wenyewe, tumefanikiwa kusambaza umeme kwa ajili ya matumizi ya pampu za maji katika maeneo ya Cheju, Bumbwisudi na Kibokwa kwa Unguja na Tibirinzi kwa upande wa Pemba. Aidha, maandalizi ya kusambaza umeme katika mabonde ya Saninga kisiwani Pemba yamekamilika.
Katika kukamilisha Mpango Mkuu huo wa Umwagiliaji Maji, Serikali yetu ikishirikiana na Serikali ya Korea Kusini hivi karibuni itaanza Upembuzi yakinifu katika eneo lilotengwa kwa madhumuni hayo kufuatia kupatikana kwa US$ 1.5 milioni za kazi hiyo. Matarajio ni kwamba mara baada ya kumalizika Upembuzi huo, serikali itapatiwa mkopo nafuu wa kuweka miundombinu katika eneo lote lilobakia la umwagiliaji chini ya mpango huo. Hatua zote hizo ni muhimu katika juhudi za kujitosheleza kwa chakula hasa mchele.
Aidha, katika kuongeza juhudi za kilimo cha kisasa, serikali yetu imefanikiwa kununua matrekta makubwa 40, matrekta madogo (power tillers) 40 pamoja na majembe na zana zake. Mahitaji halisi ni matrekta 54. Aidha, kupitia mradi wa MACEMP, serikali imeweza kutunza na kuhifadhi mazingira ya ukanda wa bahari na kuwapatia wavuvi vifaa mbali mbali vyenye thamani ya T.Shs. 4.8 bilioni.
Mheshimiwa Spika, Kutokana na juhudi mbali mbali za kuimarisha uzalishaji, thamani ya bidhaa zilizotokana na kilimo (mazao, misitu, uvuvi) imeongezeka kwa asilimia 192.9 kutoka thamani ya TShs. 92.5 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 271.0 bilioni mwaka 2009. Kati ya ongezeko hilo thamani ya mazao ya kilimo imepanda kwa asilimia 253.7 kutoka TShs. 51.7 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 182.9 bilioni mwaka 2009.
Thamani ya mazao ya mifugo imeongezeka kwa asilimia 141.1 kutoka TShs. 16.3 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 39.3 bilioni mwaka 2009, ambapo mazao ya misitu, thamani yake imeongezeka kwa asilimia 115.4 kutoka TShs. 1.3 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 2.8 bilioni mwaka 2009. Halikadhalika mazao ya uvuvi nayo thamani yake imepanda kwa asilimia 97.4 kutoka TShs. 23.3 bilioni hadi TShs. 46.0 bilioni mwaka 2009.
Ustawi wa Jamii:
Mheshimiwa Spika, Sasa naomba kuzungumzia hatua tulizozichukua kustawisha maisha ya wananchi kwa kukuza huduma za jamii, kama afya, elimu na maji safi na salama.
Afya:
Pamoja na juhudi zinazochukuliwa katika kuimarisha sekta ya afya kupitia chakula bora na lishe na utumiaji wa maji safi na salama, huduma bora za Afya nazo zina umuhimu wa pekee. Katika miaka mitano iliyopita, serikali ilichukua juhudi maalum kuimarisha huduma za kinga na tiba katika hospitali zake Pemba na Unguja. Vituo vya afya vimeongezeka kutoka 141 mwaka 2005 hadi vituo 167 mwaka 2009. Miongoni mwa mafanikio katika sekta ya afya ni ununuzi wa vifaa vya uchunguzi na tiba. Kati ya vifaa hivyo ni mashine za kisasa za uchunguzi, CT Scan na Fluroscopy, X-ray machines 3 (2 Pemba na 1 Unguja), Ultrasound machine 2 (1 Unguja na 1 Pemba), Image intensifier, mashine ya kuchunguza maradhi ya moyo (Echocardiogram) na X-ray ya meno.
Aidha, serikali imo katika hatua ya mwisho za uwekaji wa “lift” mpya kwa hospitali ya Mnazi mmoja, mashine za kutolea dawa za usingizi 3, (1 kwa ajili ya Pemba), viti 6 vya kisasa vya kutolea huduma ya meno na vifaa vya kufanyia upasuaji.
Katika kipindi hiki, serikali imeifanyia ukarabati hospitali ya macho pamoja na kuweka vifaa vipya vya uchunguzi na tiba.
Idadi ya madaktari, wasaidizi wa madaktari na wauguzi iliongezeka kutoka 806 mwaka 2005 na kufikia hadi 859 mwaka 2009. Katika kipindi hicho, tuliendelea kupata msaada wa madaktari wa kigeni kutoka 11 mwaka 2005 hadi madaktari 48 mwaka 2009.
Kwa kushirikiana na Shirika la Neurosurgical Education Development la Spain (NED) Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imefanya operesheni kubwa za kichwa na uti wa mgongo zaidi ya 104 kwa mara ya kwanza katika historia ya Zanzibar. Kwa kiasi kikubwa hili limewezekana baada ya kununuliwa mashine ya CT Scan.
Katika jitihada za kujitosheleza kwa madaktari Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa msaada wa serikali ya Cuba imeanzisha kwa mafanikio mafunzo ya udaktari hapa nchini. Hadi sasa wapo wanafunzi 37 Unguja na 12 Pemba. Wanafunzi 37 wanatarajiwa kumaliza mafunzo yao katika kipindi cha mwaka 2014.
Kutokana na kuimarika kwa huduma za afya nchini, pamoja na mwamko wa wananchi, idadi ya wagonjwa waliopatiwa huduma za tiba iliongezeka kutoka watu 223,351 (2006) hadi watu 348,805 mwaka 2009. Pamoja na kuwa malaria iliendelea kuathiri afya za wananchi, hata hivyo, kutokana na juhudi zilizochukuliwa, Serikali imefanikiwa kupunguza malaria kwa kiwango cha kupigiwa mfano. Kwa sasa, kiwango cha maambukizi ya malaria ni wastani wa mtu mmoja kwa kila mia moja ikilinganishwa na wastani wa watu arobaini kwa kila mia moja kwa mwaka 2005. Kwa kuwa malaria ilikuwa ni miongoni mwa maradhi yanayoongoza kwa vifo, kupungua kwa maradhi haya kutachangia sana katika kuimarisha wastani wa umri wa kuishi kwa wananchi wa Zanzibar. Nawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao na wafanyakazi wa Wizara ya Afya katika zoezi la upigaji dawa za mbu majumbani mwao, ambao umefanikisha mpango wa kupunguza malaria. Kwa sasa nchi yetu imekuwa ni chuo ambapo wataalamu kutoka nchi mbali mbali duniani huja kujifunza mikakati ya kudhibiti malaria.
Mheshimiwa Spika, Moja ya maradhi thakili yanayoathiri sehemu kubwa ya watu, Kusini mwa Jangwa la Sahara, ni UKIMWI. Maradhi haya yameendelea kuathiri kwa kiasi kikubwa rika la nguvu kazi na hivyo kurejesha nyuma juhudi za ukuzaji wa uchumi na kuongeza gharama za huduma za kijamii. UKIMWI pia umekuwa chanzo kikubwa cha kuporomoka kwa wastani wa umri wa kuishi kwa nchi nyingi katika eneo hilo. Zanzibar kwa upande wake, imeendelea kupata mafanikio katika mapambano dhidi ya maradhi hayo. Kiwango cha jumla cha maambukizi kimebakia kuwa chini ya asilimia moja. Utafiti wa mwaka 2008 unaonesha kuwa kiwango hicho cha jumla ni asilimia 0.6. Hata hivyo, maambukizi bado yamebaki kuwa ya juu kwa makundi maalum kama vile watumiaji wa madawa ya kulevya na watu wanaojihusisha na ngono za jinsia moja.
Tatizo jengine muhimu na la hatari ni kupoteza maisha watoto wachanga na kinamama wanapojifungua pamoja na watoto wenye umri chini ya miaka mitano. Sote tuna jukumu la kuhakikisha kuwa baada ya uchungu wa uzazi, watoto hawapotezi uhai kwa maradhi yanayoweza kutibika. Kwa wenzetu nchi zilizoendelea, ni nadra sana mtoto mchanga kufariki. Katika kipindi cha miaka mitano ya uhai wa Baraza hili, vifo vya watoto wa chini ya umri wa miaka mitano vimepungua kutoka wastani wa vifo 101 hadi vifo 79 kwa kila watoto 1000. Hali hii bado si ya kuridhisha.
Sambamba na upunguzaji wa vifo vya watoto wadogo, serikali pia imefanikiwa kupunguza vifo vya mama waja wazito kutoka 377 hadi vifo 280 kwa kila waja wazito 100,000. Kwa jumla, mafanikio yote haya yamesaidia kuongeza wastani wa umri wa kuishi, ingawa juhudi kubwa zaidi zinahitaji kuendelezwa.
Elimu:
Mheshimiwa Spika, Baada ya afya njema, jambo jengine muhimu kwa maendeleo ya mwanadamu ni elimu. Ni kupitia jamii yenye siha nzuri na iliyoelimika vyema ndio maendeleo hufikiwa kwa haraka.
Kwa kutambua umuhimu wa elimu, Serikali ya Awamu ya Sita iliweka mkazo maalum katika kuwapatia watoto wa Zanzibar fursa ya elimu na kuinua ubora wa elimu hiyo. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia mafanikio makubwa katika juhudi zetu hizi. Leo hii kila mtoto wa Zanzibar mwenye umri wa kwenda skuli anayo fursa ya kuandikishwa na kusoma. Bado kila mtoto anapata elimu ya lazima bila ya malipo, kutoka darasa la kwanza hadi kidato cha pili (darasa la kumi). Mipango ilio mbele yetu ni utekelezaji wa lengo la elimu ya lazima kuwa hadi kidato cha nne. Tunaishukuru sekta binafsi katika utoaji wa elimu ingawa skuli nyingi za binafsi zimeelekezwa katika elimu ya maandalizi na msingi. Mashirikiano na sekta binafsi ni makubwa, pia, katika elimu ya juu ambapo viwili kati ya vyuo vikuu vitatu vilivyopo Zanzibar ni vya binafsi.
Miongoni mwa mafanikio yaliopatikana ni kuongezeka kwa mtandao wa skuli za maandalizi, skuli za msingi na sekondari baina ya mwaka 2005 na 2009 kama ifuatavyo:
Maandalizi 205 - 232
Msingi 140 - 167
Sekondari 50 - 95
Mheshimiwa Spika, Kwa bahati nzuri wananchi nao wameitikia vyema wito wa kuwapeleka watoto skuli. Idadi ya watoto katika skuli za msingi imeongezeka kutoka 208,000 mwaka 2005 hadi 220,000 mwaka 2009. Jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba idadi ya watoto wanaume na wanawake karibuni inalingana. Kwa upande wa skuli za sekondari, idadi ya wanafunzi katika kipindi cha 2005-2010 imeongezeka kutoka 64,980 hadi 77,958. Idadi ya wanafunzi wanawake imezidi ile ya wanaume kwa asilimia 10.4. Hali ya kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi pia, imejitokeza kwa ngazi ya sekondari ya juu (form V na VI) ambapo idadi ya wanafunzi imeongezeka kwa asilimia 72 kutoka 2,818 mwaka 2005 hadi wanafunzi 4,844 mwaka 2009. Katika ngazi hii, hata hivyo, idadi ya wanafunzi wa kiume ni kubwa kwa asilimia 14.2 zaidi ya ile ya wanafunzi wa kike. Kwa upande wa elimu ya juu idadi ya wanachuo katika vyuo vikuu vitatu ni 3,624 ambapo wanaume ni 2,076 na wanawake 1,548. Ili kuhakikisha ubora wa elimu, serikali imeongeza idadi ya walimu kutoka 8,790 mwaka 2005 hadi 9,798 mwaka 2009. Pia, imempatia kila mwanafunzi dawati na vitabu vya rejea kwa masomo yote ya sayansi na hesabati kwa sekondari. Ubora wa elimu ya sekondari utaimarika zaidi baada ya kukamilika mradi wa ujenzi wa skuli 19 mpya unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi hicho cha miaka mitano, Serikali imeanzisha vituo vya elimu mbadala kwa wanafunzi ambao hawakubahatika kumaliza mkondo wa kawaida. Kwa upande mwengine, mkazo mkubwa uliwekwa katika elimu ya ufundi, sayansi na elimu ya vyuo vikuu. Serikali imeanzisha vyuo viwili vipya na vya kisasa vya mafunzo ya amali, kimoja Pemba na chengine Unguja.
Mheshimiwa Spika, Kama nilivyosema awali, elimu ni chachu kubwa ya kujenga jamii ya kisasa yenye kuishi kwa matumaini na iliyoondokana na unyonge wa umaskini. Uwekezaji wote huu uliofanywa na serikali katika kipindi cha Awamu ya Sita umelenga katika yote haya. Ni matumaini yangu kuwa uwekezaji wetu huu katika rasilimali watu utasaidia sana hapo baadae katika kuharakisha maendeleo ya Wazanzibari wote.
Maji Safi na Salama:
Upatikanaji wa maji safi na salama ni muhimu kwa afya za wananchi. Hadi mwaka 2009 asilimia 86 ya Wazanzibari wote waliweza kupata huduma ya maji safi na salama. Upatikanaji huo ulifikia asilimia 95.9 kwa maeneo ya mijini na asilimia 80.7 kwa maeneo ya vijijini. Tunataraji kukamilika kwa mradi mkubwa wa maji katika Mkoa wa Mjini Magharibi mwezi Agosti/Septemba mwaka huu unaotekelezwa kwa ushirikiano na Serikali ya Japan kutalimaliza tatizo hilo mkoani humo kwa kiasi kikubwa.
Maendeleo ya Nyumba:
Katika kustawisha maisha ya wananchi wetu, niliahidi nilipochukua madaraka mwaka 2000 kuwa tutakamilisha majenzi ya nyumba za maendeleo za Michenzani zilizoanzwa na Rais wetu wa Kwanza, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume. Kwa bahati nzuri kazi hiyo imemalizika na kilio cha wananchi wote waliovunjiwa nyumba zao zaidi ya miaka 38 iliyopita nacho kimeisha baada ya kukabidhiwa nyumba mpya mwanzoni mwa mwaka huu. Kwa kweli eneo hilo sasa lina mandhari ya kupendeza. Wakati huo huo, ujenzi wa nyumba za maendeleo Mpapa unaendelea vyema na tegemeo letu ni kwamba baada ya muda mfupi utakamilika.
Serikali ya Mapinduzi Awamu ya Sita, pamoja na kuendeleza nyumba za maendeleo za makazi ya watu, imefanikiwa pia kujenga majengo mbali mbali ya kisasa ya wizara na mashirika ya umma. Aidha, tumefanya marekebisho makubwa kwa majengo mbali mbali kama hospitali na skuli. Majengo mapya ni Jengo la Vitega Uchumi la ZSTC, Majengo ya ZSSF Unguja na Pemba, Makao Makuu ya Wizara ya Jengo la Wizara ya Fedha na Uchumi Unguja na Nyumba ya Wageni Pemba, Makao Mkuu ya Wizara ya Elimu Unguja, Vituo vya Amali Unguja na Pemba, Jengo la jipya la Chuo cha Uongozi wa Fedha Chwaka, Jengo la Makao Makuu ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Jengo la Benki ya Damu – Sebleni, Jengo la Maabara ya Afya na Jamii Pemba, Jengo la Mradi wa Malaria Mombasa na Mwanakwerekwe, Hospitali ya KMKM Kibweni, Kituo cha VCT Pemba kinaendelea, Chuo cha Afya Mbweni, Jengo la Elimu ya Afya, Nyumba za Madaktari, Radio Jamii Micheweni, Kituo cha Huduma za Upimaji Ukimwi na Ushauri Nasaha Hospitali ya Mnazi Mmoja Unguja, Jengo la Uhandisi la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Mombasa, Unguja, Nyumba ya Serikali Micheweni, Afisi ya DPP Unguja, Makao Makuu ya ZIPA Maruhubi Unguja, Jengo jipya la fahari la Baraza la Wawakilishi Mbweni, Jengo la Afisi ya Mufti – Mazizini Unguja, Majengo mbali mbali ya Shirika la Bandari Unguja na Pemba, Kituo cha Mafunzo ya Kilimo na Maabara Kizimbani.
Mengine ni Majengo ya MACEMP Unguja na Pemba, Majengo ya Afisi ya miradi ya huduma za Kilimo Maruhubi na Machomane Pemba, Jengo la ZRB Mazizini (ujenzi unakaribia kumalizika), Matengenezo ya Mental Hospital, Majengo ya Elimu na Walimu, Jengo la Zimamoto Kilimani, Majengo ya Kikosi cha Volantia Mwanyanya, Makao Makuu ya Idara ya Vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi – Mazizini, Majengo ya SUZA – Tunguu na Makao Makuu ya Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja.
Majengo yaliyofanyiwa ukarabati mkubwa ni Afisi ya Rais, Ikulu, Zanzibar, Kibweni Palace, Ikulu Ndogo Wete na Chake Chake, hospitali ya Mnazi Mmoja na Kivunge Unguja na jengo la Mahakama Kuu Unguja. Uwanja wa Michezo wa Amaan Unguja na Gombani Pemba imefanyiwa ukarabati mkubwa na kuwa na sura nyengine.
Pamoja na hayo, katika kuendeleza mandhari ya mji wa Unguja, kwa kushirikiana na Aga Khan Trust, tumeifanyia matengenezo makubwa bustani ya Forodhani na kuigeuza kuwa ni kivutio cha fakhari kwa wageni na wenyeji.
Utawala Bora:
Mheshimiwa Spika, Tokea nimeingia madarakani mwaka 2000 nimeweka mkazo maalum kuhakikisha kuwa kunakuwa na utawala bora nchini ikiwa ni msingi wa kudumisha uhuru wetu na kuendeleza demokrasi. Ninafuraha kuwa kuanzia mwaka 2001 nchi yetu imepiga hatua kubwa katika uimarishaji wa misingi ya utawala bora. Kati ya mwaka 2000 na 2005 hatua zifuatazo zimechukuliwa katika mwelekeo huo. Tumeanzisha wizara maalum ya mambo ya Katiba na Utawala Bora ambayo imesimamia uundaji wa Tume Huru ya Uchaguzi inayojumuisha wajumbe kutoka vyama vikuu vya siasa nchini. Kadhalika tumeanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambalo tulilitumia katika uchaguzi mkuu wa 2005 kwa mafanikio makubwa. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Zanzibar tumeanzisha mfumo wa kuwa na Vitambulisho vya kisasa vya Wakaazi wa Zanzibar. Aidha, kila mpiga kura halali aliomo ndani katika daftari la kudumu amepatiwa kitambulisho cha kisasa cha kupigia kura ambacho kimeanza kutumika kwa mafanikio makubwa mwezi uliopita katika kura ya maoni.
Katika kuhakikisha upatikanaji wa haki za raia, tumerekebisha mfumo wa Mahakama na kuufanya uwe bora zaidi kwa kurekebisha baadhi ya sheria na kanuni na kuzipatia Mahakama uhuru zaidi wa kuendesha kazi zake, kuongeza idadi ya Mahakimu pamoja na kuyakarabati majengo yao.
Serikali ya Awamu ya Sita, pia, imeanzisha ofisi maalum ya Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mashtaka (DPP). Tumeweza vile vile kufanya marekebisho ya sheria mbali mbali za jinai. Ofisi ya Tume ya Haki za binaadamu imefunguliwa hapa Zanzibar kushughulikia ukiukwaji wa haki za binaadamu.
Mheshimiwa Spika, Nilipoingia madarakani, nilianzisha Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto ili kusimamia na kulinda haki zao pamoja na kushajiisha jamii kuziheshimu na kuzitekeleza. Wizara imekuwa ikiendelea kutoa elimu na mafunzo kupitia vyombo vya habari na kuwasikiliza wanawake na watoto wenye matatizo na kuyapatia ufumbuzi kwa kutoa ushauri nasaha kwa kushirikiana na taasisi nyengine kwa nia ya kuleta utulivu, amani na maendeleo kwa familia.
Serikali ya Awamu ya Sita, kwa kupitia Wizara hiyo, inaendelea kuwajengea uwezo wanawake kwa kuwapa fursa ya kuanzisha na kuendeleza biashara kwa lengo la kuinua kipato chao na kuinua uchumi, kwani wakiwezeshwa, wanawake wanaweza. Mashirika ya UNICEF na ILO yametoa mashirikiano makubwa katika kuhakikisha watoto wa Zanzibar wanapata haki zao za msingi kwa kuweka sheria za kazi na kupiga vita ajira za watoto na kuwawezesha wanawake kujiunga katika vikundi ili waweze kujikimu kimaisha kwa kufanya kazi na biashara. Natoa shukurani nyingi kwao na watendaji wao waliopo Zanzibar na Tanzania Bara. Pia, tumekuwa tukiwajali watu wenye ulemavu kwa kushirikiana na kusaidia taasisi zao mbali mbali ili waweze kujimudu na kujiendesha kimaisha. Aidha, tunatoa mashirikiano makubwa kwa wafanyakazi waliostaafu na kujiunga pamoja.
Ushirikishwaji na Uwezeshaji wa Wananchi:
Mheshimiwa Spika, Misingi ya kidemokrasia inayofuatwa na nchi yetu inahitaji wananchi wenyewe kushiriki katika kupanga na kutekeleza mipango yao ya maendeleo. Ushiriki huo hufanyika kupitia vikundi mbali mbali, utoaji wa maoni kwenye vikao na warsha, na kupitia Wawakilishi wao hapa Barazani na katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa upande wa Baraza hili, juhudi za kuliimarisha zimeendelezwa kwa kupatiwa watendaji wenye ujuzi na vifaa vya kisasa vya kazi. Aidha, mafunzo mbali mbali kwa njia za semina na ziara za ndani na nje ya nchi yametolewa kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza. Mashikirikiano na Mabunge mengine ulimwenguni yameimarishwa ili kuwajengea uzoefu Wajumbe na Wafanyakazi wa Baraza.
Ili kulipa haiba na hadhi inayostahiki Baraza la Wawakilishi, tumekamilisha ujenzi wa jengo hili jipya la Baraza tunalokutania leo ambao ni mali ya wananchi wote.
Baraza la saba la Wawakilishi linamaliza muda wake kwa mafanikio makubwa. Baraza hili limepitisha jumla ya miswada ya sheria 56 na sera 12 na kujibu maswali 1,640 yalioulizwa. Baraza hili litakumbukwa kihistoria kuwa ni Baraza lililoweka misingi ya kudumu ya umoja, mshikamano, utulivu na amani ya Zanzibar. Limefanya maamuzi mazito kwa uadilifu na kujijengea heshima kubwa. Baraza hili limesimamia vyema madhumuni na malengo ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kulinda uhuru wa Zanzibar na watu wake, kulinda utu, umoja na heshima ya Wazanzibari wote ya kujiamulia mambo yao yanayohusu nchi yao na uchumi wao.
Mheshimiwa Spika, Katika kuwawezesha wananchi kiuchumi, mtakumbuka kuwa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na mimi tulianzisha mfuko maalum, maarufu kama mfuko wa JK na AK. Hadi mwezi Juni mwaka huu jumla ya wananchi 658 wamenufaika kwa kukopeshwa jumla ya T.Shs. 1,345.90 milioni kutoka Mfuko huu. Lengo la mikopo kutoka mfuko huu na ile ya PRIDE, WEDF, SELF na Mfuko wa Kujitegemea ni kuwapatia mikopo nafuu wananchi wazalishaji wadogo wadogo ili kuendeleza miradi yao mbalimbali. Uanzishaji huu wa mifuko mbalimbali unahitaji kusaidiwa na uongezaji wa elimu na utaalam kwa wajasiriamali hao ili mikopo hiyo iwe endelevu na yenye tija zaidi katika kuwaongezea wananchi wetu kipato.
Mheshimiwa Spika, Katika kuimarisha mawasiliano na ushiriki wa makundi mbalimbali katika kuleta maendeleo ya nchi, Serikali imeanzisha Baraza la Biashara la Zanzibar (ZBC) lenye wajumbe sawa kutoka serikalini na sekta binafsi kwa lengo la kusikiliza maoni ya kuimarisha mazingira ya kibiashara na kiuchumi nchini. Kwa nafasi yangu ya Urais wa nchi yetu, mimi ndie mwenyekiti wa ZBC. Hii ni ishara ya umuhimu unaowekwa na serikali juu ya mashirikiano hayo na sekta binafsi. Hadi sasa, ZBC imeshafanya kwa mafanikio makubwa vikao vinne. Mashirikiano pia yameimarika baina ya serikali na taasisi zisizo za kiserikali.
Kuimarika kwa Ushirikiano wa Kimataifa:
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu, kupitia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mwanachama wa Umoja wa Mataifa, Umoja wa nchi Huru za Afrika, Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki na Jumuiya mbali mbali za Kikanda. Mahusiano mazuri na nchi za nje ni jambo jema na lenye manufaa ya kiuchumi, kijamii na usalama. Kwa bahati mbaya, serikali ya awamu ya sita iliingia madarakani mwaka 2000 hali ya kuwa Zanzibar imesusiwa na wengi kati ya Washirika wetu wa Maendeleo kwa sababu za kisiasa. Kipindi cha miaka kumi ya 2000 hadi 2010, kimeshuhudia kuimarika sana kwa uhusiano wetu na nchi hizo pamoja na mashirika ya kimataifa. Kuimarika kwa mahusiano hayo ni kielelezo cha kukubalika kwa serikali yetu, uongozi wake na kuheshimiwa demokrasia nchini.
Hali ya Kisiasa:
Mheshimiwa Spika, Kwa miongo mingi nchi yetu ilikuwa haijashuhudia utulivu endelevu wa kisiasa. Tunahitaji utulivu wa kudumu wa kisiasa ili tuweze kuwa na maendeleo endelevu. Hakuna muwekezaji yeyote makini atakaewekeza fedha nyingi katika nchi ambayo utulivu wake ni wa kimiongo, unaingia mashakani kila baada ya miaka mitano wakati wa uchaguzi.
Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia fursa ya kupata utulivu wa kudumu nchini kwetu kupitia mazungumzo baina yangu na Maalim Seif Sharriff Hamad, Katibu Mkuu wa CUF hapo tarehe 5 Novemba mwaka jana, Ikulu, Zanzibar. Tulifanikiwa kufikia maridhiano ya kumaliza uhasama wa kisiasa Zanzibar na kusameheana. Najuwa tumeshapongezwa sana, kuhusiana na maridhiano hayo. Hata hivyo, naomba nichukue fursa hii tena kumpongeza sana Maalim Seif na chama chake kwa kufanya maamuzi hayo ya kijasiri ya kuitambua serikali yangu, kuwa tayari kuleta maridhiano, na pia kukubali kuwa wananchi wenyewe ndio wawe waamuzi wa mwisho juu ya mustakabali wa nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Inaonekana kuwa moja ya tatizo linalochangia hali ya kutofahamiana ni mwamko mkubwa wa kisiasa kwa wananchi wetu unaoongezwa nguvu na kukaribiana kwa kiasi fulani kwa matokeo katika chaguzi mbali mbali. Tulihitaji kufikira njia mpya, bora zaidi, na itakayokubalika na wananchi walio wengi ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo hilo. Najua kuwa miongoni mwetu, zilikuwapo fikra na rai tofauti juu ya namna ya kukabiliana na hali hio. Wapo wachache wanaoamini kuwa hali hiyo ingejirekebisha yenyewe na hivyo utaratibu wa sasa wa chama kinachoshinda kuunda serikali peke yake uendelee japo kuwa umetuletea matatizo mengi na kwa muda mrefu.
Wapo, pia, walioamini kuwa palihitajika njia mbadala ya kuongoza nchi. Kati ya hawa, nami nikiwemo, tuliona kuwa njia hiyo mbadala ni kuwa na serikali ya umoja wa kitaifa inayoundwa na vyama vyote vilivyopata ridhaa ya wananchi kuwawakilisha katika Baraza la Wawakilishi. Aidha, serikali hiyo iongozwe na chama kilichopata kura nyingi zaidi za urais katika Uchaguzi Mkuu. Maamuzi kama haya sio madogo kwa mustakabali wa nchi. Vyama vyetu vikuu viwili, CCM na CUF vilikubaliana juu ya haja ya maamuzi hayo kufanywa na wananchi wenyewe. Kwa utaratibu unaotumika kimataifa, mojawapo ya njia za kufanya maamuzi kama haya ni kupitia kura ya maoni (Referendum) ambapo wananchi huamua kati ya fursa zilizopo. Nasi hapa Zanzibar tukakubaliana kutumia njia hiyo kupata maamuzi ya wananchi.
Mheshimiwa Spika, Tarehe 31 Julai mwaka huu wananchi wa Zanzibar walishiriki kupiga kura ya maoni na kuchagua wanachokitaka. Matokeo ya kura hiyo yalikua wazi kwa thuluthi mbili ya waliopiga kura kuamua kuwa serikali ijayo iwe ya umoja wa kitaifa. Idadi hii inamaanisha kuwa kati ya kila Wazanzibari watatu waliopiga kura, wawili wamekubali kuanzishwa kwa mfumo wa serikali ya umoja wa kitaifa baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Hata hivyo wapo wananchi wachache waliotaka utaratibu wa sasa uendelee.
Kwa kutilia maanani namna ambavyo wananchi walielimishwa kwa muda mfupi juu ya kura ya maoni na kushiriki kwa wingi na utulivu mkubwa katika upigaji wa kura hiyo, natoa pongezi za dhati kwa Kamati ya Watu Sita ya Baraza la Wawakilishi ya Kusimamia Utekelezaji wa Azimio la Baraza kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar iliyoongozwa na Mwenyekiti wake Mheshimiwa Ali Mzee Ali kwa juhudi zao katika kufanikisha zoezi hilo.
Kwa kuzingatia hekima za wazee wetu inayosema wengi wape, sote kwa pamoja, tunapaswa kuyaheshimu maamuzi haya ya wengi. Naomba niwashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa kutoa maoni yao kwa njia ya utulivu, kistaarabu na ukomavu mkubwa wa kidemokrasia. Nawashukuru zaidi walio wengi ambao wamekubaliana na mageuzi ya namna ya kuongoza nchi yetu. Sote kwa pamoja tumeandika historia mpya nchini petu. Natumai itakuwa historia nzuri itayomnufaisha kila mmoja wetu, tuliopo sasa na vizazi vijavyo. Kwa vyama vyetu vya siasa, maamuzi haya ya wananchi ni maelekezo yao kwetu. Ni ushindi wa wananchi wote, sio wa wanasiasa wala sio wa vyama vya siasa. Aidha, hatupaswi kuyabeza maoni ya wachache waliotaka kuendelea utaratibu wa sasa. Tujue tu kuwa kwenye mabadiliko sio wote huyakubali kwa haraka. Wengine mpaka waone wenyewe faida yake. Kwa hivyo hali hiyo iwe ni changamoto kwetu tuliowengi kuhakikisha kuwa historia isiyopendeza nchini kwetu haijirejei ili tuwape moyo hao wenzetu wenye hofu ili waungane nasi katika safari hii yenye matumaini.
Mheshimiwa Spika, Baada ya mchakato wa kura ya maoni na walio wengi kuunga mkono muundo mpya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, juzi tarehe 9 Agosti, Baraza lako tukufu kwa kauli moja lilipitisha Mswada wa Marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984. Marekebisho hayo ya kihistoria yataruhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa iundwe mara baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Nataka nichukue fursa hii kwanza kukupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Spika, pamoja na wajumbe wa baraza lako tukufu kwa uamuzi wenu wa kizalendo. Bila ya shaka uamuzi wenu huo utaingia katika vitabu vya historia ya Zanzibar itakayokumbukwa kwa miaka mingi ijayo.
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu inakabiliwa tena na Uchaguzi Mkuu tarehe 31 Oktoba mwaka huu. Kwa upande wetu serikalini, tunaendelea vyema na matayarisho ya uchaguzi huo kwa kukiwezesha chombo chenye dhamana yake, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar. Ni matumaini yangu kuwa Tume, Vyama vya siasa, na wananchi wote tutaungana kuhakikisha kuwa uchaguzi wa mwaka huu unaandika historia mpya nchini kwetu inayoendana na maridhiano yaliyopo ya kisiasa. Nia yetu ni kuwa na historia ya uchaguzi wa kuaminiana, uchaguzi wa kistaarabu, na uchaguzi ulio safi na huru kwenye macho yetu sote, wapiga kura na waangalizi watakaokuwepo. Uchaguzi huu unabeba matumaini makubwa zaidi ya wananchi, kimaendeleo, kiutulivu, na kiuchumi. Naomba sote tuhuishe matumaini yao kwa salama na amani.
Mwisho:
Mheshimiwa Spika, Miaka 10 katika historia ya nchi ni kipindi kifupi sana. Kwa mujibu wa Katiba yetu, Rais ndie kiongozi wetu wa nchi lakini miaka 10 ya uongozi wa nafasi ya juu katika nchi, ni muda mrefu sana wa dhamana iliyo nzito. Dhamana hiyo inampa dhima Rais kutumia mamlaka aliyopewa kuhakikisha, (i) usalama na amani ya nchi inadumishwa, (ii) Demokrasia na haki za wananchi wote zinalindwa, (iii) Nchi inapata maendeleo na kuinua ustawi wa jamii kwa jumla, (iv) Kudumisha umoja na maslahi ya Zanzibar ndani ya Muungano pamoja na kujenga mahusiano bora na majirani, na nchi na mashirika ya nje. Zaidi ya yote, Rais ana dhamana ya kuitetea, kuilinda na kuitekeleza Katiba ya nchi. Hizo zote ni dhamana nzito.
Tarehe 8 Novemba mwaka 2000 mara baada ya kuapishwa na kukabidhiwa dhamana ya kuiongoza nchi yetu, nilitoa hotuba fupi pale Uwanja wa Amaan napenda nijinukuu mwenyewe nilisema kama ifuatavyo:
“Ndugu wananchi, leo nathubutu kusimama mbele yenu kwa sababu wananchi wa Zanzibar wametumia haki yao ya kikatiba ya kumchagua Rais wanaemtaka. Wakati napokea imani yenu kwa heshima na unyenyekevu kuwa Rais wa Zanzibar, sina budi kupokea wito wa wananchi wa kutaka mabadiliko. Nilipokuwa nafanya kampeni ya kuomba kura zenu kwa niaba yangu na niaba ya chama changu, niliendelea kusisitiza juu ya umoja, amani na utulivu. Leo nasimama tena mbele yenu kwa sababu mmekubali wito huo na kunichagua kuwa Rais. Baada ya kunichagua mimi kwa kura nyingi sana na kunipa ushindi mkubwa ni dhahiri kwamba mmechagua umoja, amani na utulivu katika nchi yetu.
Napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa kuniamini kwa kazi kubwa ya utekelezaji wa chaguo lenu la umoja, amani na utulivu. Napenda niwaombe wananchi wote ushirikiano wenu”.
Baada ya maelezo hayo sina budi kuwashukuru sana wananchi wote wa Zanzibar kwa kunikubalia ombi langu la kuchagua umoja, amani na utulivu na kuniunga mkono katika kipindi chote.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita naamini kwamba nimetumia uwezo wangu kuyatekeleza yote haya kwa kadiri Mwenyezi Mungu, Rahim, alivyonijaalia. Lakini sikufanya kazi hiyo kubwa peke yangu ila nimeshirikiana na wananchi wote wa Zanzibar, viongozi wenzangu wa chama changu, Serikalini na nje ya Serikali. Nimeshirikiana na kufanyakazi kwa karibu sana na Marais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Mstaafu Benjamin Wiliam Mkapa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Nawashukuru wote kwa dhati kwa mashirikiano, msaada wao na ushauri wao kwangu kwa muda wote. Namshukuru mzee wetu Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi. Namshukuru pia Rais Mstaafu wa Zanzibar, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi kwa kuanzisha Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. Wakati huo huo, namshukuru Rais Mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour. Nilibahatika, vile vile, kufanya kazi kwa karibu na Marehemu Dr. Omar Ali Juma akiwa Makamo wa Rais chini ya Mhe. Mkapa. Mwenyezi Mungu kamuhitaji ni wajibu kwetu kumuombea maghfira na malazi mema. Nawashukuru pia Mheshimiwa Dr. Ali Moh’d Shein, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano. Nawashukuru viongozi wengine wote wa kitaifa walio madarakani na wastaafu niliowahi kufanyakazi nao, mawaziri na watendaji wengine.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa utaratibu wa uongozi wa nchi yetu, nchi inaongozwa na mihimili mitatu: ule wa Utawala (Executive) unaoongozwa na Rais, wa kutunga sheria (legislature – yaani Baraza hili tukufu) unaoongozwa na Spika na mhimili wa kusimamia haki (Judiciary) unaoongozwa na Mheshimiwa Jaji Mkuu. Kwa mujibu wa Katiba yetu, kama nilivyosema awali Kiongozi wa nchi ni Rais. Naomba nitumie fursa hii kukushukuru wewe Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza hili linalomaliza muda wake na Mheshimiwa Hamid Mahmoud Hamid Jaji Mkuu wa Zanzibar. Nasema kutoka ndani ya moyo wangu kuwa katika kipindi chote cha uongozi wangu wa nchi nimepata bahati ya kufanya kazi kwa mashirikiano makubwa kutoka kwenu. Nimebahatika kupata maoni na ushauri wenu muhimu ulionisaidia sana katika kufanya maamuzi, mengine yakiwa magumu. Wakati wote, ukaribu wenu umekuwa ni ngao muhimu kwangu hata kwa kujua tu, wenzangu wananiunga mkono na wako pamoja nami. Nakushuruni sana.
Mheshimiwa Spika, Napenda, pia, kumshukuru Waziri Kiongozi, Mheshimiwa Shamsi Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi, Mheshimiwa Ali Juma Shamuhuna pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wote waliofanya kazi chini yangu kwa mashirikiano, utiifu, na ushauri wao kwangu uliowezesha kuivusha vyema nchi yetu katika muda wote huo. Nawashukuru sana Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu, Makamishna, Wakurugenzi na viongozi na wafanyakazi wote wa serikali kwa utendaji wao mzuri uliotufikisha hapa tulipo kwenye mafanikio makubwa. Natoa shukurani pekee kwa maafisa na wafanyakazi katika Afisi ya Rais Ikulu kwa uaminifu wao kwangu, ushirikiano na kazi nzuri wakati wote na uvumilivu wao katika kazi. Nawaambia ahsanteni sana. Shukurani zangu nyingi, pia, ni kwa wakuu wa vikosi na askari wote wa vikosi vyetu vya ulinzi na usalama kwa utiifu wao kwangu kama kiongozi wao na kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuwafanyia wananchi wenzao wa Zanzibar katika kudumisha ulinzi na usalama wetu pamoja na nchi yetu. Ahsanteni sana.
Shukurani zangu maalum zinakwenda kwa wananchi wote kwa kuniamini, kunipa fursa ya kuwatumikia, na kunistahamilia wakati nchi yetu ilipopita vipindi vigumu. Natumai neno “AHSANTE” litabeba uzito wa kutosha wa shukurani zangu kwao. Nakishukuru pia Chama changu cha CCM kwa kuniamini na kunipa fursa hii adhimu. Aidha, nawashukuru viongozi wa dini na taasisi zisizokuwa za serikali kwa kushirikiana na mimi katika kipindi changu chote kuhubiri amani na umoja. Nawashukuru wenye vyombo vya habari na waandishi wote kwa kutangaza habari zetu katika kipindi chote.
Mwisho nawashukuru mabalozi wa nchi za nje waliofanya kazi Zanzibar katika kipindi cha Awamu ya Sita na, pia, waliokuwepo Tanzania Bara kwa kushirikiana na sisi kwa urafiki na kufahamiana.
Mheshimiwa Spika, Niruhusu pia kutoa shukurani nyengine maalum kwa familia yangu ambayo imekuwa ndio muhimili wangu na chachu ya mafanikio yangu. Namshukuru sana mama yangu, Mama Fatma Karume, namshukuru kwa namna ya pekee mke wangu, Mama Shadya Karume, nawashukuru sana wanangu, wajukuu na wanafamilia wote kwa kuniunga kwao mkono bila ya ukomo wala kuchoka katika kipindi chote cha mimi kuiongoza nchi yetu. Familia yangu imenistahamilia na imevumilia mengi wakati nikitumia muda mwingi kuwatumikia wananchi wenzangu. Nataka nikiri kwamba maisha yao katika kipindi hicho hayakua mepesi hata kidogo kwa vile waliokua na joto nami wakati huo, joto lao liliishia kwa familia yangu kama ilivyo kwa wanasiasa wengine. Pamoja na yote hayo walikuwa nami katika kuitumikia nchi yetu na chama chetu kwa uwezo wao wote. ahsanteni sana. Namshukuru sana Ndugu yangu Balozi Ali Karume pamoja na ndugu zangu wakike, jamaa zangu na marafiki zangu wote kwa msaada wao kwangu. Nawashukuru tena wananchi wote wa Zanzibar na Watanzania wote.
Mheshimiwa Spika, Muda wangu wa kuitumikia nchi yetu kama Rais utafikia ukomo wake mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 31 Oktoba mwaka huu. Baada ya hapo tutapata Kiongozi mwengine. Nimeeleza mafanikio makubwa tuliyoyapata miaka kumi inayomalizika. Hata hivyo, bado nchi yetu inakabiliwa na changamoto kadhaa. Katika kukabiliana na changamoto hizo, serikali yetu imeweza kuweka misingi madhubuti ya maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Misingi hii inahitaji kutunzwa, kuimarishwa na kuendelezwa kwa kasi zaidi. Kwa kuwa uchumi wetu unahitaji kasi zaidi ya mageuzi kuelekea uchumi wa kisasa unaonufaisha walio wengi, bila ya shaka sekta binafsi itapaswa kuendelezwa kwa kulelewa na kujengewa uwezo zaidi na kuendelea kuwa mdau muhimu katika uchumi wa nchi yetu. Na kwa kuwa Chama cha Mapinduzi kina ujuzi na uzoefu mkubwa katika kuyajenga na kuyasimamia mazingira ya aina hiyo, naomba nyote mkubaliane nami kuwa Rais wetu ajae atoke CCM.
Mheshimiwa Spika, Baraza la Wawakilishi ni chombo muhimu sana katika uongozi na mustakabali wa nchi yetu. Pia, ni sehemu ya ukuzaji wa demokrasia nchini na ni taasisi yenye uzito mkubwa katika ustawi wa jamii na uchumi. Katika kuliwezesha Baraza, serikali yangu imefanikiwa kujenga jengo jipya. Napenda kumshukuru mfadhili mkubwa wa ujenzi huo, Sheikh Abdulla Al Youseif. Sasa Baraza linajivunia kuwa na jengo lake wenyewe la kisasa na kuvutia likiwa ni moja ya alama ya Mhimili wa Utungaji Sheria. Nina imani kwamba Baraza litaendelea kutimiza wajibu wake kwa umahiri na ustadi mkubwa kwa faida ya kila mmoja wetu.
Hakuna marefu yasio na mwisho. Kipindi cha miaka mitano cha uhai wa Baraza hili ni kirefu lakini sasa kimefikia mwisho. Nachukua fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa Wajumbe wote wa Baraza hili kwa kazi kubwa na nzuri ambayo mmeifanya wakati wa uhai wa Baraza hili. Mafanikio yote niliyoyataja hapo kabla yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushauri na maelekezo yenu na hata kuikosoa kwenu serikali. Pongezi za pekee ni zako wewe Mheshimiwa Spika, Naibu wako na Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza na Katibu wa Baraza kwa uongozi mzuri wa shughuli za Baraza, kwa busara wakati wa vikao na kwa ufanisi mkubwa wa kuiendesha Taasisi hii muhimu. Ninajua kwamba wengi wa Wajumbe wako wamerudi tena Majimboni kuomba ridhaa ya Wananchi wawachague tena kuwa Wawakilishi wao katika Baraza lijalo litakaloundwa baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31. Nakuombeeni kheri nyote katika uchaguzi huo.
Mwisho kabisa, Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 92 (1) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Maisha ya Baraza la Wawakilishi yataendelea kwa muda wa miaka mitano baada ya kuundwa upya mara tu baada ya Uchaguzi Mkuu. Ili kutoa nafasi ya matayarisho ya mwisho kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu hapo ifikapo tarehe 31 Oktoba 2010, kwa madaraka niliyonayo chini ya kifungu cha 91(2)(a) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, natamka kwamba kuanzia Ijumaa tarehe 13 mwezi wa Agosti 2010 Baraza la saba la Wawakilishi la Zanzibar limevunjwa rasmi.
Nakutakieni Waheshimiwa Wajumbe na wananchi nyote saumu njema na Ramadhani ya baraka na wingi wa rehema.
Mwenyezi Mungu awabariki wote,
Mungu Ibariki Zanzibar,
Mungu Ibariki Tanzania,
Mungu Ibariki Afrika.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
MHESHIMIWA DK. AMANI ABEID KARUME, WAKATI WA KUAGANA NA WAHESHIMIWA WAJUMBE WA BARAZA LA WAWAKILISHI LA SABA, KATIKA UKUMBI WA BARAZA LA WAWAKILISHI, ZANZIBAR
TAREHE 11 AGOSTI, 2010
Mheshimiwa Spika,
Mheshimiwa Waziri Kiongozi,
Mheshimiwa Jaji Mkuu,
Mheshimiwa Naibu Waziri Kiongozi,
Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Mabalozi wadogo walioko Zanzibar,
Viongozi wa vyama vya siasa,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana,
ASSALAAMU ALAYKUM,
Naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma na Mwenye Uwezo wa kila Jambo, kwa kutupa afya na uzima tukaweza kujumuika hapa leo kwa ajili ya shughuli hii adhimu. Namshukuru pia kutujaalia amani na utulivu ndani ya nchi yetu vinavyotuwezesha kuendesha mambo yetu kwa mafanikio makubwa.
Nakushukuru Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi hii ya kutumia uwezo wangu wa kikatiba kuhutubia Baraza la Wawakilishi la Saba na kutoa tathmini ya utekelezaji wa baadhi ya shughuli za Awamu ya Sita ya Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar, chini ya Uongozi wangu, kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza na wananchi wote kwa jumla. Hii ndio nafasi yangu ya mwisho kulihutubia Baraza hili nikiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Nashukuru sana kupata fursa hii ambayo, pia, nitaitumia kutangaza rasmi kuvunjwa kwa Baraza hili.
Mheshimiwa Spika,
Nchi yetu inaendelea na utaratibu tuliojiwekea wa utekelezaji wa demokrasia ya kupokezana uongozi wa nchi kwa njia ya uchaguzi. Awamu ya Sita ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliingia madarakani Novemba, mwaka 2000 kufuatia Uchaguzi Mkuu nchini kwetu. Muda wa kikatiba na kisheria wa Awamu hiyo unamalizika baada ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 31, mwaka huu.
Mheshimiwa Spika,
Ni vyema kujikumbusha tunakotoka, tokea mwaka 2000 mpaka hapa tulipo 2010. Kwanza, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa viongozi walionitangulia wa Awamu zilizopita kwa jitihada zao za kuweka misingi ya maendeleo ya nchi yetu.
Awamu ya Sita iliingia katika wakati ambao nchi yetu ilikuwa imekabiliwa na matatizo ya kisiasa ambayo yalichangia kuleta hali ya mgawanyiko wa wananchi, kuathiri maendeleo ya miundombinu, kuwepo uchumi dhaifu na uhusiano usioridhisha na baadhi ya nchi marafiki.
Takwimu zinaonesha kwamba Pato la Taifa kwa mwaka 2000 lilikuwa T.Shs. 190.5 bilioni na pato la wastani la kila mtu lilikuwa T.Shs. 207,987 sawa na US$ 260 kwa mwaka. Ukusanyaji wa mapato ya ndani ya serikali kwa mwaka 2000/2001 ulifikia T.Shs. 38,674 milioni. Huduma za jamii zikiwemo elimu, afya, maji safi na salama haikuwa ya kuridhisha kutokana na kudhoofika kwa uchumi wetu. Hali ya miundombinu, zikiwemo bandari, barabara na mawasiliamo, pia ilikuwa si ya kuridhisha. Mwaka huo kulikuwepo skuli za msingi na kati 181, sekondari 28, vyuo 3 na vyuo vikuu 2.
Kwa upande wa afya, vituo vya afya vilikuwa 106 kwa Unguja na Pemba na wananchi wetu wengi waliathirika na ugonjwa wa malaria.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Mapinduzi Awamu ya Sita haikuridhika na hali hiyo na ikaamua kufuatilia kiini cha matatizo hayo, yaliyochangiwa kwa kiasi kikubwa na hali mbaya ya siasa, na kuyatafutia ufumbuzi.
Kwa jitihada za pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chama tawala cha CCM na chama cha upinzani CUF, tulifanya mazungumzo ya pamoja na tukafanikiwa kufikia mwafaka wa mwaka 2001. Hatua hiyo ilisaidia kupunguza hali ngumu ya siasa na kuwafanya wawakilishi wa CUF kuingia Baraza la Wawakilishi na Washirika wetu wa Maendeleo kurejesha uhusiano mzuri na sisi.
Hali hiyo ilisaidia kufungua sura mpya katika kuendeleza uchumi wa nchi yetu, miundombinu na huduma za jamii.
Kwa mfano, katika mwaka 2004, pato la taifa lilipanda na kufikia T.Shs. 344.3 bilioni wakati pato la wastani la mtu lilikuwa T.Shs. 330,764 sawa na US$ 303. Makusanyo ya kodi yaliimarika na kufikia T.Shs. 59,479 milioni. Serikali kwa makusudi ilifanya mageuzi ya uchumi ambayo yaliwezesha ukuaji wa ukusanyaji kodi, kustawi kwa biashara na vianzio vya uchumi kama utalii, mawasiliano, huduma za fedha nakadhalika. Jumla ya watalii 125,522 walitembelea Zanzibar mwaka 2004 ikilinganishwa na 97,165 mwaka 2000. Idadi ya benki iliongezeka kutoka benki 5 mwaka 2000 kufikia 6 mwaka 2004, na maduka ya biashara ya fedha za kigeni kuongezeka kutoka 14 mwaka 2000 hadi kufikia 24 mwaka 2004.
Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2000-2005 ulitupa mafanikio katika sekta zote. Huduma za jamii zilipata msukumo mkubwa wa maendeleo. Kwa upande wa elimu, mwaka 2004 tulikuwa na skuli za msingi na kati 229, sekondari 49, vyuo 3 na vyuo vikuu 3, kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar - SUZA tulichokifungua mwaka 2001. Idadi ya wanafunzi katika skuli za msingi ilifikia 199,938 mwaka 2004 kutoka 163,113 mwaka 2000; na wanafunzi wa sekondari 61,002 mwaka 2004, kutoka 42,542 mwaka 2000.
Huduma za afya ziliimarika na vituo vya afya viliongezeka kufikia 122 mwaka 2004. Watoto 37,581 walipatiwa chanjo za magonjwa mbali mbali ya watoto.
Upatikanaji wa maji safi na salama uliimarika kutoka asilimia 35 kwa maeneo ya vijijini na asilimia 70 katika maeneo ya mijini Unguja na Pemba mnamo mwaka 2000 hadi asilimia 51 kwa maeneo ya vijijini na asilimia 75 kwa maeneo ya mijini Unguja na Pemba mwaka 2004.
Mheshimiwa Spika,
Mipango ya uimarishaji miundombinu iliendelea kutekelezwa na ilipofikia mwaka 2004 barabara kadhaa kuu zilijengwa au kufanyiwa matengenezo.
Kuanzia mwaka 2005 hadi 2010 utekelezaji wa mipango yetu ya kazi za maendeleo ulikwenda sambamba na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2005-2010 na katika kipindi cha uhai wa Baraza hili, serikali iliendelea kuchukua hatua mbalimbali zilizolenga kuimarisha maendeleo ya wananchi. Kuhusiana na siha, Sera ya Chakula na Lishe iliandaliwa na kuanza kutekelezwa. Lazima tukiri kuwa upatikanaji wa uhakika wa chakula na lishe bora bado ni changamoto kwa sehemu fulani ya jamii yetu. Kwa vile upatikanaji wa maji safi na salama, pia, ni nyenzo muhimu kwa kuhakikisha jamii ina siha njema miaka mitano iliyopita serikali iliendeleza juhudi za kuwafikishia huduma hiyo muhimu wananchi wengi zaidi, mijini na vijijini, Pemba na Unguja.
Mafanikio ya Kiuchumi:
Mheshimiwa Spika, Kama nilivyotangulia kusema, sambamba na juhudi za kumuendeleza Mzanzibari kiafya na kielimu, katika miaka mitano inayomalizika mkazo uliwekwa katika maendeleo ya uchumi. Wataalamu wanasema kuwa hakuna maendeleo pasipo ukuaji wa uchumi. Dira yetu ya Maendeleo ya 2020 imeweka msisitizo maalumu katika mabadiliko ya kiuchumi (economic transformation) kutoka uchumi duni unaotegemea kilimo cha asili na kuelekea kwenye uchumi wa kisasa. Dira pia ilisisitiza maeneo matatu makubwa ya kiuchumi. Mosi, Utalii endelevu; pili, Uzalishaji viwandani; na tatu, Kilimo cha kisasa. Ili kutekeleza mahitaji hayo ya Dira ya Maendeleo, na kwa kutambua hali duni ya miundombinu ya kiuchumi, serikali katika kipindi cha 2005 – 2010 iliweka mkazo katika ujenzi wa mazingira mazuri na misingi imara ya kiuchumi. Mafanikio makubwa yamepatikana katika kukuza uchumi ingawa bado kuna baadhi ya changamoto kuelekea mageuzi makubwa ya uchumi kama yanavyotarajiwa chini ya Dira yetu.
Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana ni kukua kwa thamani ya Pato la Taifa kutoka T.Shs. 394.9 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 878.4 bilioni mwaka 2009 kwa kutumia bei za kudumu za mwaka 2001. Kutokana na ukuaji huo, Wastani wa pato la mtu binafsi uliongezeka kutoka T.Shs. 368,000 mwaka 2005 sawa na dola za Marekani 327.0 hadi T.Shs. 728,000 sawa dola za Marekani 557.0 Ongezeko hilo ni la kujivunia ingawa wastani wake umeendelea kuathiriwa na kasi kubwa ya ongezeko la idadi ya watu nchini petu. Juhudi maalum zinahitajika kudhibiti kasi hii ili kuendana na ukuaji wa uchumi na kuzuia athari kubwa kwa mazingira. Kasi ya wastani wa ukuaji wa uchumi imekua kutoka asilimia 4.9 mwaka 2005 kufikia asilimia 6.7 mwaka 2009. Kasi hiyo ya ukuaji ingekuwa kubwa zaidi lakini imeathiriwa na misukosuko ya kiuchumi na fedha iliyojitokeza duniani kote.
Mchango wa Kisekta:
Mheshimiwa Spika, Kufuatia mageuzi yaliyotarajiwa katika Dira ya Maendeleo ya 2020, mafanikio ya kuridhisha yamepatikana. Sekta ya huduma ndio iliyoongoza katika mchango wa Pato la Taifa na ukuaji wa uchumi kwa kuchangia wastani wa asilimia 45 ya Pato la Taifa katika kipindi hicho. Lengo katika Dira 2020 ni kuwa, sekta hii ichukue jukumu kubwa zaidi la uchumi.
Mafanikio makubwa yamepatikana katika kuimarisha Utalii nchini, ikiwa ni mojawapo ya shughuli za kiuchumi iliyopo chini ya sekta hii. Thamani ya huduma za mahoteli na mikahawa imeongezeka maradufu kutoka T.Shs. 30.6 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 63.1 bilioni mwaka 2009. Aidha, idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu nayo imekua kutoka watalii 125,522 hadi 134,954 katika kipindi hicho. Kwa jumla, mwenendo umekuwa wa kuridhisha katika maendeleo ya shughuli za utalii nchini yanaendana na Dira yetu ya Maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Sekta ya Viwanda nayo ilitarajiwa kuchukua nafasi kubwa katika kukuza uchumi. Hata hivyo, imejitokeza kuwa hili ni eneo ambalo linahitaji msukumo wa hatua zaidi katika nusu ya pili ya Dira yetu ya Maendeleo. Sekta binafsi katika uwekezaji na uzalishaji viwandani inahitaji kuhamasishwa na kushiriki vizuri zaidi. Katika miaka mitano iliyopita, mchango wa sekta hii kwa Pato la Taifa kwa wastani ulikuwa asilimia 14.1 tu. Kwa hivyo juhudi maalum zinahitajika katika awamu ya pili ya utekelezaji wa Dira ya 2020.
Uwekezaji wa Rasilimali:
Mheshimiwa Spika, Moja ya kichocheo kikubwa cha ukuzaji uchumi ni uwekezaji wa rasilimali. Nchi yetu imeshuhudia kasi kubwa ya kuongezeka kwa thamani ya raslimali iliyowekezwa kati ya mwaka 2005 na 2010 kutoka T.Shs. 76.2 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 178.9 bilioni mwaka 2009. Maeneo yote makuu ya uwekezaji yalirikodi mafanikio makubwa yanayofanana. Uwekezaji kwenye ujenzi wa nyumba uliongezeka kwa asilimia 155 kutoka T.Shs. 20.8 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 52.8 bilioni mwaka 2009. Ujenzi wa nyumba za biashara ndio ulioongoza ndani ya kundi hili ambapo uwekezaji wake umepanda kutoka T.Shs. 13 bilioni hadi T.Shs. 32.2 bilioni. Ujenzi wa nyumba za makaazi umeongezeka kutoka T.Shs. 4.1 bilioni hadi T.Shs. 10.9 bilioni katika kipindi hicho. Ongezeko hilo ni ishara ya kutosha kuwa wananchi wetu wanaendelea kupata makaazi bora. Jambo la kufurahisha zaidi ni kuwa ujenzi wa nyumba vijijini umeongezeka kutoka T.Shs. 3.6 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 9.6 bilioni mwaka 2009. Nawapongeza wananchi wote wa Zanzibar kwa muamko wao wa kujijengea makaazi bora.
Mheshimiwa Spika, Uwekezaji mwengine muhimu kwa uchumi na maendeleo yetu ni katika ununuzi wa mashine na mitambo kwa ajili ya uzalishaji. Baina ya mwaka 2005 na 2009 uwekezaji huo uliongezeka maradufu (kwa asilimia 101) kutoka thamani ya T.Shs. 30.5 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 61.4 bilioni mwaka 2009. Aidha, thamani ya uwekezaji kwenye ardhi, ujenzi wa barabara na madaraja iliongezeka kwa asilimia 155 kutoka T.Shs. 23.1 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 58.9 bilioni mwaka 2009. Kwa jumla tunapaswa kwa pamoja kujivunia ukubwa wa ongezeko la thamani ya uwekezaji katika maeneo hayo matatu na kwa uwiano uliopatikana.
Biashara ya Kimataifa:
Mheshimiwa Spika, Uhusiano wa kibiashara na nchi za nje nao una umuhimu mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi ikiwemo uwazi wa biashara (Trade Openness) unaopimwa kwa jumla ya thamani ya uingizaji na usafirishaji. Jumla ya thamani ya biashara na nchi za nje ilifikia T.Shs. 150.6 bilioni mwaka 2009 kutoka T.Shs. 133.4 bilioni mwaka 2005. Hii ni ishara kuwa nchi yetu imeshiriki zaidi katika biashara na nchi za nje katika kipindi hicho. Kwa upande mwengine kila nchi huweka jitihada katika kuongeza usafirishaji kwa kadri inavyowezekana na kupunguza uagiziaji. Kwa upande wetu, kwa miaka mitano iliyopita wakati thamani ya uingizaji kimsingi haikuongezeka kutoka kiwango cha T.Shs. 120.7 bilioni mwaka 2005 na kufikia T.Shs. 120.9 bilioni mwaka 2009, usafirishaji nje umeongezeka zaidi ya maradufu kutoka T.Shs. 12.7 bilioni mwaka 2005 hadi T.Shs. 29.7 bilioni mwaka 2009. Mwenendo huo mzuri wa biashara umesaidia kupunguza nakisi ya biashara na nchi za nje kutoka T.Shs. 108 bilioni hadi T.Shs. 91.1 bilioni baina ya mwaka 2005 na 2009. Aidha, Serikali, pia, imekamilisha uandaaji wa Mkakati wa Usafirishaji (Zanzibar Export Strategy) ambao utekelezaji wake unatarajiwa kuimarisha zaidi usafirishaji wa bidhaa kutoka nchini kwetu na hivyo kuimarisha urari wa biashara. Hatua hiyo ni ya kupongezwa na kuimarishwa.
Ukusanyaji wa Mapato:
Mheshimiwa Spika, Ili serikali iweze kuhudumia mipango yake yote ya kuleta ustawi mzuri na maendeleo ya wananchi, ilihitaji pia, kuongeza uwezo wake wa mapato. Serikali ilihitaji kusimamia vyema vianzio vilivyopo na kubuni vianzio vipya pamoja na kuangalia mfumo na uwezo wa kitaasisi na kisheria, ili uendane na nia yake ya kujitegemea. Nina furaha kutamka kwamba kwa jumla tumefanikiwa sana katika kuinua uwezo wa serikali kimapato katika kipindi chote cha Awamu ya Sita. Kama ilivyo kwa maeneo mengine, mapato ya ndani yameongezeka kwa kiasi kikubwa katika kipindi hicho. Mwaka 2005/06 serikali ilikusanya jumla ya T.Shs. 68.5 bilioni kutokana na vyanzo vya ndani kupitia Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato ya Tanzania (TRA). Mwaka 2009/10 taasisi hizi zilikusanya jumla ya T.Shs. 146.2 bilioni. Ongezeko hilo la mapato ni sawa na ukuaji wa asilimia 113. Takwimu hizi zinamaanisha kuwa mapato yetu ya ndani yamekua kutoka wastani wa T.Shs. 5.7 bilioni kwa mwezi mwaka 2005/06 hadi kufikia T.Shs. 12.2 bilioni kwa mwezi mwaka 2009/2010.
Kwa upande mmoja, mafanikio haya ni matokeo ya juhudi za serikali za kuimarisha uchumi kutokana na utekelezaji wa sera za uwekezaji. Kuimarika huko kwa uchumi kumesaidia kuongeza pia wigo wa mapato. Tunamaliza muda wa uongozi wetu tukifurahia mafanikio haya na hasa kuweza kubadilisha utegemezi wa mapato yetu kutoka yanayotegemea biashara ya kimataifa na forodha na kuwa yanayotegemea zaidi vianzio vyetu vya ndani. Huu ni msingi muhimu wa kuhakikisha kuwa mapato yetu yanakuwa endelevu.
Kwa upande mwengine, mafanikio haya ni matokeo ya kuimarika kwa utendaji wa ZRB na TRA. Naomba nitumie fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza viongozi na watendaji wote wa ZRB na TRA kwa juhudi zao. Sehemu ya juhudi zetu za kurekebisha sheria pia, zimechangia katika mafanikio haya. Zaidi ya hayo, tumesimamia vyema pale palipokuwa na dalili za udokozi. Haya yote yamewezekana kutokana na ushirikiano wa pamoja baina ya Serikali na Kamati ya Kudumu ya Uchumi na Fedha ya Baraza la Wawakilishi. Hatuna budi kwa pamoja kujivunia mafanikio haya makubwa.
Usimamizi wa Fedha Za Umma:
Mheshimiwa Spika, Ukusanyaji wa mapato pekee bila usimamizi bora wa matumizi ya serikali hauwezi kuleta maendeleo ya wananchi. Kwa kutambua hili, serikali katika kipindi cha miaka mitano iliyopita iliendelea kuimarisha usimamizi wa fedha za umma. Mfumo wa sheria uliimarishwa kwa kutungwa Sheria mpya ya Fedha na ile ya Ununuzi na Uondoshaji wa mali za Serikali hapo mwaka 2005. Utekelezaji wa sheria hizo na Kanuni zake umefanyika katika kipindi cha miaka mitano hii inayomalizika. Serikali, pia, imechukua hatua maalumu za kujenga uwezo wa wahasibu na kuimarisha huduma za uhasibu serikalini. Aidha, kwa kutambua fursa muhimu ya kuimarisha usimamizi kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano, tumeanza kutumia mfumo wa Kompyuta (Integrated Financial Management System - IFMS) unaounganisha Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali (Hazina) na Wahasibu Wakuu wote wa Wizara na Taasisi zinazojitegemea, Unguja na Pemba. Mfumo huu umesaidia kuongeza udhibiti, kuimarisha ufanisi, na kurahisisha upatikanaji wa taarifa za fedha za serikali. Hali hii imesaidia kuwezesha ulipaji wa mishahara ya wafanyakazi serikalini kwa wakati.
Itakumbukwa kuwa moja kati ya kilio kikubwa kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza hili na wananchi kwa jumla ilikuwa ni ucheleweshaji mkubwa wa mafao ya wastaafu, yakiwemo kiinua mgongo na pencheni. Serikali ilikuwa inakerwa na tatizo hili. Katika kipindi cha miaka mitano inayomalizika, kufuatia kuimarika kwa hali ya fedha serikalini, juhudi ziliongezwa kulipa deni la wastaafu lililokuwepo na kuhakikisha kuwa malimbikizo mapya yanaepukwa. Serikali imefanikiwa kulipa deni lote la wastaafu hao na kuendelea kulipa wastaafu wapya mafao yao kwa wakati kadri taratibu zinapokamilika. Pamoja na Wajumbe wa Baraza lako, naomba nichukue fursa hii kuwapongeza kwa dhati watendaji wa Wizara yetu ya Fedha na Uchumi kwa utendaji wao mahiri katika kipindi hicho chote.
Mfumko wa Bei:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo ya uchumi yanahitaji utulivu wa bei za bidhaa, bei za huduma na thamani ya sarafu. Mfumko mkubwa wa bei, unaathiri imani ya wawekezaji, unapoteza thamani ya sarafu na unaathiri kipato cha wananchi wenye kipato cha kudumu kama vile wastaafu wanaoishi kwa pencheni. Serikali imechukua juhudi kubwa kudhibiti mfumko wa bei katika kipindi cha miaka mitano inayomalizika. Hata hivyo, lazima nikiri kuwa pamoja na juhudi mbalimbali zilizochukuliwa, kasi ya mfumko wa bei imekuwa ya juu kuliko ilivyotarajiwa. Mfumko wa bei kwa mwaka 2005 ulikuwa wa asilimia 9.7, mwaka 2006 asilimia 11.4, na kupanda hadi kufikia asilimia 20.6 mwaka 2008. Sababu ya kasi hiyo kubwa ya Mfumko wa bei imeendelea kuwa ni utegemezi wetu wa chakula tunachoagiza kutoka nje ya nchi hasa mchele, mwenendo wa bei za mafuta katika soko la dunia, na kwa kipindi hicho, ujenzi wa bandari ya Malindi ambayo ndio mlango mkuu wa uingizaji na usafirishaji wa bidhaa nchini.
Mheshimiwa Spika, Kwa bahati nzuri hali hiyo ilitengemaa mwaka 2009, na bei za chakula na zile za mafuta katika soko la dunia zilishuka. Kushuka huko kulisaidia kupunguza kasi ya mfumko wa bei kutoka asilimia 20.6 ya mwaka 2008 hadi asilimia 8.9 mwaka 2009. Katika kipindi cha kupanda sana kwa kasi ya mfumko wa bei, serikali ilitumia mchanganyiko wa sera zake za mapato (fiscal policies), juhudi za kuimarisha uzalishaji wa ndani wa mazao ya chakula na kuharakisha ukamilishaji wa ujenzi wa bandari ya Malindi ili kupunguza athari ya mfumko huo. Kwa upande wa sera za mapato, serikali ilitoa unafuu maalum wa kodi za uingizaji kama ushuru wa forodha na kodi ya ongezeko la thamani kwa bidhaa za vyakula muhimu zinazoingia nchini. Serikali ilibidi kusamehe mapato yake ilimradi makali ya maisha kwa mwananchi yadhibitiwe.
Ni muhimu kutambua kuwa njia hizo zote ni za muda tu. Ili kudhibiti mfumko wa bei kwa muda mrefu, tunahitaji kuimarisha uzalishaji wa ndani wa chakula na kuimarisha kipato cha mwananchi ili kupunguza sehemu ya pato linalotumiwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya chakula. Lengo ni kupunguza mchango wa bei za chakula hasa mchele katika faharisi ya bei (Consumer Price Index). Aidha, tunapswa pia kuendelea kufuatilia mwenendo wa ujazi (Liquidity) wa fedha nchini ili kuudhibiti bila ya kuathiri juhudi za maendeleo.
Huduma za Fedha:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo ya huduma za fedha ni ishara ya maendeleo ya nchi. Sekta ya huduma za fedha inajumuisha huduma za benki, maduka ya fedha za kigeni, vyama vya kuweka na kukopa na mifuko ya huduma za mikopo midogo midogo. Sekta hii, pia, hujumuisha na huduma za Bima, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na soko la mitaji. Katika kipindi hiki, huduma za benki zimekuwa sana hapa Zanzibar. Mwaka 2005 tulikuwa na Benki sita zilizokuwa zikitoa huduma na hivi sasa zimeongezeka na kufikia Benki kumi. Ongezeko hilo la benki limepelekea mchango wa huduma za kibenki katika Pato la Taifa kuongezeka kutoka asilimia 7.8 mwaka 2005 hadi asilimia 15.3 mwaka 2009.
Miongoni mwa mafanikio makubwa na ya kujivunia zaidi katika eneo hili ni yale ya kuigeuza na kuiimarisha Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ). Mwaka 2000, wakati tunaingia madarakani, PBZ haikuwa na mtaji; ilikuwa ikipata hasara mwaka hadi mwaka na haikuwa na matumaini. Hivi sasa hali imebadilika; tulitumia awamu ya kwanza ya miaka mitano kuiimarisha (Stabilize) benki hiyo na miaka mitano inayomalizika kuigeuza kimuundo, kiutumishi, na kimtaji. Maamuzi mengine yalikuwa magumu lakini yalipaswa kufanyika, mfano ni kupunguza idadi ya Wafanyakazi; uamuzi ambao ulikuwa na athari kijamii lakini ulikuwa wa lazima.
Tulihimili, pia, msukumo mkubwa wa kuibinafsisha PBZ kutokana na ushauri wa Benki ya Dunia na Benki Kuu ya Tanzania. Wataalam wao hawakutufahamu tulipoamua kutoibinafsisha benki yetu. Kwa hivyo tulishirikiana kwa pamoja kuimarisha Benki yetu na hivi leo PBZ ina mtaji maradufu ya kiwango cha chini kinachotakiwa na msimamizi wa mabenki yaani Benki Kuu. Wakati tunaingia mwaka 2006, PBZ haikuweza kutimiza mtaji wa T.Shs. 5.0 bilioni unaohitajiwa na Benki Kuu, leo hii mtaji wa PBZ ni zaidi ya T.Shs. 11 bilioni. Kutokana na hatua madhubuti tulizochukua, tumeweza kubadilisha kabisa muundo wa mtaji wa Benki ya Watu wa Zanzibar, kutoka benki iliyokuwa ikipata hasara kila mwaka, hadi benki yenye kupata faida kwa mwaka wa nne mfululizo na ilipofika mwezi huu wa Agosti 2010, kwa mara ya kwanza katika historia yake, PBZ imeweza kutoa gawio la jumla ya T.Shs. 300 milioni kwa mmiliki wake, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Hatuna budi tujipongeze kwa mafanikio hayo.
Miundombinu:
Mheshimiwa Spika, Maendeleo niliyoyataja ya mwananchi na uchumi hayawezi kupatikana bila ya kuwepo kwa miundombinu bora. Sehemu za kuingilia na kutokea nchini kama vile bandari na viwanja vya ndege, mtandao bora wa barabara, upatikanaji wa uhakika na wa bei nafuu wa nishati na mtandao bora wa mawasiliano ni nyenzo za msingi kwa nchi kupiga hatua katika maendeleo. Wakati tunaingia madarakani, nchi yetu ilikua na hali duni sana ya miundombinu yote hii. Kwa sababu hiyo, katika kipindi cha uongozi wetu, tulichukuwa jukumu la kuiimarisha miundombinu hiyo ili kushajiisha na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Naomba sasa nigusie baadhi tu ya mafanikio yaliyopatikana katika maeneo hayo hapa nchini katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Mawasiliano na uchukuzi:
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu ni visiwa na sehemu za kuingilia na kutokea za bandari na viwanja vya ndege zina umuhimu mkubwa sana. Kutokana na matatizo ya ujenzi, Bandari kuu ya Malindi ilikuwa katika hali mbaya sana mwanzoni mwa miaka ya 2000. Ushauri wa kitaalam ulionesha kuwa pengine Bandari hiyo isingeweza kutumika tena baada ya mwezi Juni mwaka 2001. Matengenezo yake, kwa hivyo, yalikuwa ni jambo la lazima. Serikali imefanikiwa kuijenga upya Bandari hiyo kwa msaada wa Jumuiya ya Ulaya na fedha kutoka SMZ. Bandari za Mkoani, Wesha na Wete huko Pemba nazo zimeimarishwa. Kwa upande wa viwanja vya ndege, Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar ambao kwa sasa unajulikana kwa jina la “Abeid Karume International Airport” nao umefanyiwa matengenezo makubwa yakiwemo ya kuijenga upya njia ya kutua na kurukia ndege tuliyoizindua siku chache zilizopita pamoja na kuiongeza urefu kutoka mita 2,600 za awali hadi mita 3,022 hivi sasa na hivyo kuwezesha ndege kubwa zaidi za aina zote duniani kutua na kuruka. Hatua hii itasaidia sana katika kukuza usafiri wa ndege pamoja na utalii nchini.
Eneo jengine muhimu na lililokuwa likilalamikiwa sana na wahusika mbalimbali ni udogo wa jengo la abiria katika kiwanja hicho, lakini kwa bahati nzuri tatizo hilo tumeshalipatia ufumbuzi. Na hivi sasa Mkandarasi, Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group Company Limited” kutoka China inakusanya zana tayari kuanza ujenzi wa jengo jipya na la kisasa katika kiwanja hicho. Ujenzi huo utachukua miezi 36 na unagharamiwa kwa mkopo nafuu wa Serikali ya China kupitia Benki yake ya Exim. Juhudi za kukiimarisha kiwanja cha Karume Pemba kupitia mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika chini ya miradi ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki nazo zinaendelea. Mawasiliano, pia, yanaendelea baina ya Serikali na Benki ya Dunia juu ya uendelezaji wa kiwanja hicho cha Karume Pemba.
Barabara:
Mheshimiwa Spika, Ni jambo la kushukuru na kufurahia kuwa katika Awamu ya Sita nchi yetu imepata maendeleo makubwa katika ustawishaji wa miundombinu ya barabara. Wenyeji na wageni wanaotutembelea leo wanafarajika kwa hali bora ya barabara zetu Unguja na Pemba.
Nakumbusha tu kwamba mwaka 2000, Zanzibar ilikuwa na jumla ya kilomita 447 za lami. Unguja km. 323.5 na Pemba km. 123.5. Kuanzia mwaka huo mpaka mwaka 2009 tumeongeza barabara za lami za km. 753 kuzifanya zote kufikia km. 1,210. Hii ni sawa na asilimia 70.6 za mtandao wote wa barabara Unguja na Pemba.
Leo wananchi wa Donge na Mkokotoni wamefarajika kwa kujengewa barabara yao kwa kiwango cha lami. Hivyo hivyo, kwa wananchi wa Nungwi na wale wa ukanda wote wa utalii wa Matemwe, Pwani Mchangani, Kiwengwa, hadi Pongwe. Hali ndio hiyo, pia, kwa Wananchi wa Michamvi, Jambiani, Makunduchi, Kizimkazi, Fumba, Machui, Ghana, na kwengineko. Barabara zote hizi zimesaidia sana sio tu kuwarahisishia wananchi wa maeneo hayo usafiri wao na bidhaa zao, bali pia, zimekuwa chachu katika kukuza maendeleo ya kilimo na utalii endelevu.
Kwa upande wa Pemba, mindombinu ya barabara nayo imeimarika kwa kiasi kikubwa. Kazi ya ujenzi wa barabara za Wete - Konde, Wete – Gando, barabara sita za kusini Pemba inaendelea kama ilivyo kwa barabara za Mfenesini - Bumbwini na Amani – Dunga hapa Unguja. Barabara ya Bahanasa Mtambwe nayo iko katika hatua za matayarisho ya ujenzi. Ikifika mwezi wa Novemba mwaka huu, nitakabidhi uongozi wa nchi yetu kwa Rais ajae pamoja na kazi inayoendelea ya uwekaji wa miundombinu mbalimbali ya barabara.
Mawasiliano ya Simu:
Mheshimiwa Spika, Kutokana na maendeleo ya haraka yanayojitokeza katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, mawasiliano ya simu na huduma zake yameimarika sana. Jumla ya kampuni tano za mawasiliano ya simu zinatoa huduma hapa Zanzibar ambapo zaidi ya watu 500,000 wanamiliki simu. Mchango wa shughuli za mawasiliano na uchukuzi katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 8.0 mwaka 2005 hadi asilimia 11.0 mwaka 2009, ambapo thamani ya huduma za shughuli hizo imeongezeka kutoka Tshs. 31.5 bilioni mwaka 2005 hadi T.shs. 96.8 bilioni mwaka 2009.
Ilikuwa nia ya serikali kuweka njia mpya kuu ya mawasiliano ya habari (fibre optic cable) kuzunguka visiwa vyote viwili na kuunganishwa na Tanzania Bara na dunia kupitia njia za aina hiyo yenye ufanisi mkubwa wa mawasiliano na gharama nafuu. Kwa bahati mbaya, maombi yetu ya mkopo nafuu katika Benki ya Exim ya China kwa utekelezaji wa mradi huu yalichelewa kupata idhini. Hata hivyo, kwa sasa hatua kubwa imefikiwa na matarajio ni kuwa mradi huu utaidhinishwa kabla ya kumalizika kwa mwaka huu wa 2010. Ukikamilika, mradi pia utasaidia sana kuimarisha ufanisi serikalini kwa kutumia utaratibu wa e-government. Mradi pia unatarajiwa kuwa chanzo kipya na muhimu kwa mapato ya serikali. Kwa bahati nzuri Pemba tayari imeunganishwa na njia kuu ya mawasiliano kupitia chini ya bahari kwa kutumia waya wa kupelekea umeme kutoka Tanga. Unguja nayo itaunganishwa hivyo hivyo kupitia waya mpya wa umeme kutoka Dar Es Salaam.
Nishati:
Mheshimiwa Spika, Kwa nchi yetu, nishati inajumuisha huduma za umeme, gesi, petroli, kuni na makaa. Katika miaka mitano inayomalizika, tumepata mafanikio makubwa ya usambazaji wa nishati ya umeme lakini, pia, tulipata mitihani mikubwa. Mafanikio ni pamoja na kuweza kusambaza umeme katika maeneo mengi zaidi vijijini. Fursa za upatikanaji wa umeme zilizofikiwa Zanzibar ni za kiwango cha juu sana ikilinganishwa na hali iliyopo katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara. Hivi karibuni wananchi watakaofaidika na umeme wa uhakika itafikia asilimia 90 ikilinganishwa na asilimia kati ya 10 na 15 kwa mataifa mengine ya Afrika Mashariki na Kati.
Mheshimiwa Spika, Katika historia yake yote, Pemba ilikuwa haijapata umeme wa uhakika, ilikuwa ikitegemea umeme wa majenereta usioaminika na uzalishaji wake ni wa gharama kubwa. Mwaka 2005 tuliahidi kukiunganisha kisiwa cha Pemba, kama ilivyo kwa Unguja, na mtandao wa Gridi ya Taifa, kwa vile sasa teknolojia ya kufanya hivyo ipo duniani. Tunamaliza muda wetu wa uongozi kwa fakhari kubwa kwa kumudu kuitekeleza ahadi ya kuwapatia umeme wa uhakika wananchi wa Pemba. Ni matumaini yangu kuwa sasa Pemba itapiga hatua za haraka zaidi za maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Naomba niwashukuru kwa mara nyengine tena wananchi wa Pemba kwa ustahamilivu wao muda wote kabla ya kupatikana kwa huduma hiyo kwa uhakika. Naomba wajue kuwa nathamini sana uvumilivu wao huo na imani yao kwangu. Kwa niaba ya wananchi wote wa Zanzibar, naishukuru tena Serikali na wananchi wa Norway na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msaada wao uliosaidia kufanikisha mradi huo. Aidha, naishukuru Serikali ya Mapinduzi na wananchi wote wa Zanzibar kwa mchango mkubwa uliokamilisha utekelezaji wa mradi huo.
Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Unguja tarehe 29 Julai mwaka 2010 itakumbukwa kuwa ni siku nyengine muhimu kwa historia ya nchi yetu kuhusiana na nishati ya umeme. Siku hiyo tulizindua upya mradi wa majenereta ya akiba Mtoni hapa Zanzibar. Majenereta hayo yana uwezo wa kuzalisha Megawati 25 za nishati hii ya umeme. Waswahili tunasema “baada ya dhiki ni faraja” na pia “mvumilivu hula mbivu”. Vipindi vya kuzimika umeme kwa mwezi mmoja baina ya Mei 21 na Juni 18 mwaka 2008 na baadae miezi mitatu baina ya Disemba 10, 2009 na Machi 8 mwaka huu vilikuwa vya dhiki kwetu sote. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Zanzibar kwa utulivu na ustahamilivu wao katika vipindi hivyo vya shida. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kutuwezesha kuvuka salama. Aidha, naomba nitambue na kuzishukuru nchi za Norway, Sweden, na Uingereza kwa msaada wao uliotuwezesha kununua majenereta hayo mapya. Kwa utaratibu ule ule wa abebwae hujikaza, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar nayo imetoa mchango mkubwa katika mradi huo. Nawapongeza wananchi wote wa Zanzibar kwa mchango wao.
Mafanikio mengine muhimu katika upatikanaji wa nishati ya umeme, ni makubaliano yaliofikiwa na Serikali ya Marekani kwa kutusaidia kuweka waya mpya wa umeme na wenye uwezo mkubwa zaidi kati ya Ras Kiromoni Dar es Salaam hadi Ras Fumba, hapa Unguja. Mradi huu uko katika hatua za utekelezaji ambapo matengenezo ya waya huo yanaendelea. Tutaikabidhi awamu ijayo ya serikali yetu mradi huo mwengine muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Tunaishukuru sana serikali na watu wa Marekani kwa msaada wao huo kupitia Shirika lake la Changamoto za Milenia (MCC). Tunasema ahsanteni sana.
Maendeleo ya Sekta ya Kilimo:
Mheshimiwa Spika, Kilimo bado kinaendelea kuwa ni sekta muhimu kwa maendeleo ya uchumi na ustawi wa jamii. Inakadiriwa asilimia 70 ya wananchi hutegemea sekta ya kilimo katika kuendesha maisha yao ya kila siku. Kwa miaka yote serikali imehakikisha kuwa huduma muhimu kwa maendeleo ya sekta ya kilimo zinapatikana kwa wakati. Huduma hizo ni pamoja na matrekta, mbolea, mbegu bora, miche, dawa za kuzuia wadudu waharibifu wa mimea na mazao, dawa za kuzuia magugu, huduma za masoko, umwagiliaji wa maji na ushauri kwa wakulima. Mafunzo maalum kwa wakulima yameendelea kutolewa kwenye maeneo yao, kwenye kituo cha Kizimbani na kwa njia za “shamba darasa”. Aidha, tumefanikiwa kuzalisha mbegu bora za mazao mbali mbali na kuzisambaza kwa wakulima wetu ili waongeze tija. Tunalishukuru Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) kwa msaada na ushirikiano wake katika shughuli hizi.
Kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji maji, mnamo mwaka 2001-2003, kwa kushirikiana na Shirika la Japan International Cooperation Agency (JICA)” Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Mazingira, iliandaa Mpango Mkuu wa Umwagiliaji Maji (Zanzibar Irrigation Master Plan – ZIMP). Lengo la mpango huo ni kuiwezesha nchi yetu kuendeleza kilimo kwa njia ya umwagiliaji maji. Chini ya mpango huo, Zanzibar ina jumla ya Hekta 8,521 ambazo zikifanyiwa kazi zinaweza kuendelezwa kwa njia ya kilimo cha umwagiliaji. Eneo linalohusika linajumuisha mabonde 57 yakiwemo 38 ya Pemba na 19 ya Unguja.
Baada ya kukamilika kwa mpango huo, serikali kwa upande mwengine, imefanikiwa kufufua miundombinu ya umwagiliaji maji kwenye eneo la Hekta 740 linalojumuisha mabonde ya Bumbwisudi, Mtwango, Kibokwa na Cheju. Mradi wa Bumbwisudi na Kibokwa ulichangiwa kwa msaada wa serikali ya Korea Kusini. Pia, kwa kutumia fedha zetu wenyewe, tumefanikiwa kusambaza umeme kwa ajili ya matumizi ya pampu za maji katika maeneo ya Cheju, Bumbwisudi na Kibokwa kwa Unguja na Tibirinzi kwa upande wa Pemba. Aidha, maandalizi ya kusambaza umeme katika mabonde ya Saninga kisiwani Pemba yamekamilika.
Katika kukamilisha Mpango Mkuu huo wa Umwagiliaji Maji, Serikali yetu ikishirikiana na Serikali ya Korea Kusini hivi karibuni itaanza Upembuzi yakinifu katika eneo lilotengwa kwa madhumuni hayo kufuatia kupatikana kwa US$ 1.5 milioni za kazi hiyo. Matarajio ni kwamba mara baada ya kumalizika Upembuzi huo, serikali itapatiwa mkopo nafuu wa kuweka miundombinu katika eneo lote lilobakia la umwagiliaji chini ya mpango huo. Hatua zote hizo ni muhimu katika juhudi za kujitosheleza kwa chakula hasa mchele.
Aidha, katika kuongeza juhudi za kilimo cha kisasa, serikali yetu imefanikiwa kununua matrekta makubwa 40, matrekta madogo (power tillers) 40 pamoja na majembe na zana zake. Mahitaji halisi ni matrekta 54. Aidha, kupitia mradi wa MACEMP, serikali imeweza kutunza na kuhifadhi mazingira ya ukanda wa bahari na kuwapatia wavuvi vifaa mbali mbali vyenye thamani ya T.Shs. 4.8 bilioni.
Mheshimiwa Spika, Kutokana na juhudi mbali mbali za kuimarisha uzalishaji, thamani ya bidhaa zilizotokana na kilimo (mazao, misitu, uvuvi) imeongezeka kwa asilimia 192.9 kutoka thamani ya TShs. 92.5 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 271.0 bilioni mwaka 2009. Kati ya ongezeko hilo thamani ya mazao ya kilimo imepanda kwa asilimia 253.7 kutoka TShs. 51.7 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 182.9 bilioni mwaka 2009.
Thamani ya mazao ya mifugo imeongezeka kwa asilimia 141.1 kutoka TShs. 16.3 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 39.3 bilioni mwaka 2009, ambapo mazao ya misitu, thamani yake imeongezeka kwa asilimia 115.4 kutoka TShs. 1.3 bilioni mwaka 2005 hadi TShs. 2.8 bilioni mwaka 2009. Halikadhalika mazao ya uvuvi nayo thamani yake imepanda kwa asilimia 97.4 kutoka TShs. 23.3 bilioni hadi TShs. 46.0 bilioni mwaka 2009.
Ustawi wa Jamii:
Mheshimiwa Spika, Sasa naomba kuzungumzia hatua tulizozichukua kustawisha maisha ya wananchi kwa kukuza huduma za jamii, kama afya, elimu na maji safi na salama.
Afya:
Pamoja na juhudi zinazochukuliwa katika kuimarisha sekta ya afya kupitia chakula bora na lishe na utumiaji wa maji safi na salama, huduma bora za Afya nazo zina umuhimu wa pekee. Katika miaka mitano iliyopita, serikali ilichukua juhudi maalum kuimarisha huduma za kinga na tiba katika hospitali zake Pemba na Unguja. Vituo vya afya vimeongezeka kutoka 141 mwaka 2005 hadi vituo 167 mwaka 2009. Miongoni mwa mafanikio katika sekta ya afya ni ununuzi wa vifaa vya uchunguzi na tiba. Kati ya vifaa hivyo ni mashine za kisasa za uchunguzi, CT Scan na Fluroscopy, X-ray machines 3 (2 Pemba na 1 Unguja), Ultrasound machine 2 (1 Unguja na 1 Pemba), Image intensifier, mashine ya kuchunguza maradhi ya moyo (Echocardiogram) na X-ray ya meno.
Aidha, serikali imo katika hatua ya mwisho za uwekaji wa “lift” mpya kwa hospitali ya Mnazi mmoja, mashine za kutolea dawa za usingizi 3, (1 kwa ajili ya Pemba), viti 6 vya kisasa vya kutolea huduma ya meno na vifaa vya kufanyia upasuaji.
Katika kipindi hiki, serikali imeifanyia ukarabati hospitali ya macho pamoja na kuweka vifaa vipya vya uchunguzi na tiba.
Idadi ya madaktari, wasaidizi wa madaktari na wauguzi iliongezeka kutoka 806 mwaka 2005 na kufikia hadi 859 mwaka 2009. Katika kipindi hicho, tuliendelea kupata msaada wa madaktari wa kigeni kutoka 11 mwaka 2005 hadi madaktari 48 mwaka 2009.
Kwa kushirikiana na Shirika la Neurosurgical Education Development la Spain (NED) Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imefanya operesheni kubwa za kichwa na uti wa mgongo zaidi ya 104 kwa mara ya kwanza katika historia ya Zanzibar. Kwa kiasi kikubwa hili limewezekana baada ya kununuliwa mashine ya CT Scan.
Katika jitihada za kujitosheleza kwa madaktari Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa msaada wa serikali ya Cuba imeanzisha kwa mafanikio mafunzo ya udaktari hapa nchini. Hadi sasa wapo wanafunzi 37 Unguja na 12 Pemba. Wanafunzi 37 wanatarajiwa kumaliza mafunzo yao katika kipindi cha mwaka 2014.
Kutokana na kuimarika kwa huduma za afya nchini, pamoja na mwamko wa wananchi, idadi ya wagonjwa waliopatiwa huduma za tiba iliongezeka kutoka watu 223,351 (2006) hadi watu 348,805 mwaka 2009. Pamoja na kuwa malaria iliendelea kuathiri afya za wananchi, hata hivyo, kutokana na juhudi zilizochukuliwa, Serikali imefanikiwa kupunguza malaria kwa kiwango cha kupigiwa mfano. Kwa sasa, kiwango cha maambukizi ya malaria ni wastani wa mtu mmoja kwa kila mia moja ikilinganishwa na wastani wa watu arobaini kwa kila mia moja kwa mwaka 2005. Kwa kuwa malaria ilikuwa ni miongoni mwa maradhi yanayoongoza kwa vifo, kupungua kwa maradhi haya kutachangia sana katika kuimarisha wastani wa umri wa kuishi kwa wananchi wa Zanzibar. Nawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao na wafanyakazi wa Wizara ya Afya katika zoezi la upigaji dawa za mbu majumbani mwao, ambao umefanikisha mpango wa kupunguza malaria. Kwa sasa nchi yetu imekuwa ni chuo ambapo wataalamu kutoka nchi mbali mbali duniani huja kujifunza mikakati ya kudhibiti malaria.
Mheshimiwa Spika, Moja ya maradhi thakili yanayoathiri sehemu kubwa ya watu, Kusini mwa Jangwa la Sahara, ni UKIMWI. Maradhi haya yameendelea kuathiri kwa kiasi kikubwa rika la nguvu kazi na hivyo kurejesha nyuma juhudi za ukuzaji wa uchumi na kuongeza gharama za huduma za kijamii. UKIMWI pia umekuwa chanzo kikubwa cha kuporomoka kwa wastani wa umri wa kuishi kwa nchi nyingi katika eneo hilo. Zanzibar kwa upande wake, imeendelea kupata mafanikio katika mapambano dhidi ya maradhi hayo. Kiwango cha jumla cha maambukizi kimebakia kuwa chini ya asilimia moja. Utafiti wa mwaka 2008 unaonesha kuwa kiwango hicho cha jumla ni asilimia 0.6. Hata hivyo, maambukizi bado yamebaki kuwa ya juu kwa makundi maalum kama vile watumiaji wa madawa ya kulevya na watu wanaojihusisha na ngono za jinsia moja.
Tatizo jengine muhimu na la hatari ni kupoteza maisha watoto wachanga na kinamama wanapojifungua pamoja na watoto wenye umri chini ya miaka mitano. Sote tuna jukumu la kuhakikisha kuwa baada ya uchungu wa uzazi, watoto hawapotezi uhai kwa maradhi yanayoweza kutibika. Kwa wenzetu nchi zilizoendelea, ni nadra sana mtoto mchanga kufariki. Katika kipindi cha miaka mitano ya uhai wa Baraza hili, vifo vya watoto wa chini ya umri wa miaka mitano vimepungua kutoka wastani wa vifo 101 hadi vifo 79 kwa kila watoto 1000. Hali hii bado si ya kuridhisha.
Sambamba na upunguzaji wa vifo vya watoto wadogo, serikali pia imefanikiwa kupunguza vifo vya mama waja wazito kutoka 377 hadi vifo 280 kwa kila waja wazito 100,000. Kwa jumla, mafanikio yote haya yamesaidia kuongeza wastani wa umri wa kuishi, ingawa juhudi kubwa zaidi zinahitaji kuendelezwa.
Elimu:
Mheshimiwa Spika, Baada ya afya njema, jambo jengine muhimu kwa maendeleo ya mwanadamu ni elimu. Ni kupitia jamii yenye siha nzuri na iliyoelimika vyema ndio maendeleo hufikiwa kwa haraka.
Kwa kutambua umuhimu wa elimu, Serikali ya Awamu ya Sita iliweka mkazo maalum katika kuwapatia watoto wa Zanzibar fursa ya elimu na kuinua ubora wa elimu hiyo. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia mafanikio makubwa katika juhudi zetu hizi. Leo hii kila mtoto wa Zanzibar mwenye umri wa kwenda skuli anayo fursa ya kuandikishwa na kusoma. Bado kila mtoto anapata elimu ya lazima bila ya malipo, kutoka darasa la kwanza hadi kidato cha pili (darasa la kumi). Mipango ilio mbele yetu ni utekelezaji wa lengo la elimu ya lazima kuwa hadi kidato cha nne. Tunaishukuru sekta binafsi katika utoaji wa elimu ingawa skuli nyingi za binafsi zimeelekezwa katika elimu ya maandalizi na msingi. Mashirikiano na sekta binafsi ni makubwa, pia, katika elimu ya juu ambapo viwili kati ya vyuo vikuu vitatu vilivyopo Zanzibar ni vya binafsi.
Miongoni mwa mafanikio yaliopatikana ni kuongezeka kwa mtandao wa skuli za maandalizi, skuli za msingi na sekondari baina ya mwaka 2005 na 2009 kama ifuatavyo:
Maandalizi 205 - 232
Msingi 140 - 167
Sekondari 50 - 95
Mheshimiwa Spika, Kwa bahati nzuri wananchi nao wameitikia vyema wito wa kuwapeleka watoto skuli. Idadi ya watoto katika skuli za msingi imeongezeka kutoka 208,000 mwaka 2005 hadi 220,000 mwaka 2009. Jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba idadi ya watoto wanaume na wanawake karibuni inalingana. Kwa upande wa skuli za sekondari, idadi ya wanafunzi katika kipindi cha 2005-2010 imeongezeka kutoka 64,980 hadi 77,958. Idadi ya wanafunzi wanawake imezidi ile ya wanaume kwa asilimia 10.4. Hali ya kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi pia, imejitokeza kwa ngazi ya sekondari ya juu (form V na VI) ambapo idadi ya wanafunzi imeongezeka kwa asilimia 72 kutoka 2,818 mwaka 2005 hadi wanafunzi 4,844 mwaka 2009. Katika ngazi hii, hata hivyo, idadi ya wanafunzi wa kiume ni kubwa kwa asilimia 14.2 zaidi ya ile ya wanafunzi wa kike. Kwa upande wa elimu ya juu idadi ya wanachuo katika vyuo vikuu vitatu ni 3,624 ambapo wanaume ni 2,076 na wanawake 1,548. Ili kuhakikisha ubora wa elimu, serikali imeongeza idadi ya walimu kutoka 8,790 mwaka 2005 hadi 9,798 mwaka 2009. Pia, imempatia kila mwanafunzi dawati na vitabu vya rejea kwa masomo yote ya sayansi na hesabati kwa sekondari. Ubora wa elimu ya sekondari utaimarika zaidi baada ya kukamilika mradi wa ujenzi wa skuli 19 mpya unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi hicho cha miaka mitano, Serikali imeanzisha vituo vya elimu mbadala kwa wanafunzi ambao hawakubahatika kumaliza mkondo wa kawaida. Kwa upande mwengine, mkazo mkubwa uliwekwa katika elimu ya ufundi, sayansi na elimu ya vyuo vikuu. Serikali imeanzisha vyuo viwili vipya na vya kisasa vya mafunzo ya amali, kimoja Pemba na chengine Unguja.
Mheshimiwa Spika, Kama nilivyosema awali, elimu ni chachu kubwa ya kujenga jamii ya kisasa yenye kuishi kwa matumaini na iliyoondokana na unyonge wa umaskini. Uwekezaji wote huu uliofanywa na serikali katika kipindi cha Awamu ya Sita umelenga katika yote haya. Ni matumaini yangu kuwa uwekezaji wetu huu katika rasilimali watu utasaidia sana hapo baadae katika kuharakisha maendeleo ya Wazanzibari wote.
Maji Safi na Salama:
Upatikanaji wa maji safi na salama ni muhimu kwa afya za wananchi. Hadi mwaka 2009 asilimia 86 ya Wazanzibari wote waliweza kupata huduma ya maji safi na salama. Upatikanaji huo ulifikia asilimia 95.9 kwa maeneo ya mijini na asilimia 80.7 kwa maeneo ya vijijini. Tunataraji kukamilika kwa mradi mkubwa wa maji katika Mkoa wa Mjini Magharibi mwezi Agosti/Septemba mwaka huu unaotekelezwa kwa ushirikiano na Serikali ya Japan kutalimaliza tatizo hilo mkoani humo kwa kiasi kikubwa.
Maendeleo ya Nyumba:
Katika kustawisha maisha ya wananchi wetu, niliahidi nilipochukua madaraka mwaka 2000 kuwa tutakamilisha majenzi ya nyumba za maendeleo za Michenzani zilizoanzwa na Rais wetu wa Kwanza, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume. Kwa bahati nzuri kazi hiyo imemalizika na kilio cha wananchi wote waliovunjiwa nyumba zao zaidi ya miaka 38 iliyopita nacho kimeisha baada ya kukabidhiwa nyumba mpya mwanzoni mwa mwaka huu. Kwa kweli eneo hilo sasa lina mandhari ya kupendeza. Wakati huo huo, ujenzi wa nyumba za maendeleo Mpapa unaendelea vyema na tegemeo letu ni kwamba baada ya muda mfupi utakamilika.
Serikali ya Mapinduzi Awamu ya Sita, pamoja na kuendeleza nyumba za maendeleo za makazi ya watu, imefanikiwa pia kujenga majengo mbali mbali ya kisasa ya wizara na mashirika ya umma. Aidha, tumefanya marekebisho makubwa kwa majengo mbali mbali kama hospitali na skuli. Majengo mapya ni Jengo la Vitega Uchumi la ZSTC, Majengo ya ZSSF Unguja na Pemba, Makao Makuu ya Wizara ya Jengo la Wizara ya Fedha na Uchumi Unguja na Nyumba ya Wageni Pemba, Makao Mkuu ya Wizara ya Elimu Unguja, Vituo vya Amali Unguja na Pemba, Jengo la jipya la Chuo cha Uongozi wa Fedha Chwaka, Jengo la Makao Makuu ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Jengo la Benki ya Damu – Sebleni, Jengo la Maabara ya Afya na Jamii Pemba, Jengo la Mradi wa Malaria Mombasa na Mwanakwerekwe, Hospitali ya KMKM Kibweni, Kituo cha VCT Pemba kinaendelea, Chuo cha Afya Mbweni, Jengo la Elimu ya Afya, Nyumba za Madaktari, Radio Jamii Micheweni, Kituo cha Huduma za Upimaji Ukimwi na Ushauri Nasaha Hospitali ya Mnazi Mmoja Unguja, Jengo la Uhandisi la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Mombasa, Unguja, Nyumba ya Serikali Micheweni, Afisi ya DPP Unguja, Makao Makuu ya ZIPA Maruhubi Unguja, Jengo jipya la fahari la Baraza la Wawakilishi Mbweni, Jengo la Afisi ya Mufti – Mazizini Unguja, Majengo mbali mbali ya Shirika la Bandari Unguja na Pemba, Kituo cha Mafunzo ya Kilimo na Maabara Kizimbani.
Mengine ni Majengo ya MACEMP Unguja na Pemba, Majengo ya Afisi ya miradi ya huduma za Kilimo Maruhubi na Machomane Pemba, Jengo la ZRB Mazizini (ujenzi unakaribia kumalizika), Matengenezo ya Mental Hospital, Majengo ya Elimu na Walimu, Jengo la Zimamoto Kilimani, Majengo ya Kikosi cha Volantia Mwanyanya, Makao Makuu ya Idara ya Vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi – Mazizini, Majengo ya SUZA – Tunguu na Makao Makuu ya Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja.
Majengo yaliyofanyiwa ukarabati mkubwa ni Afisi ya Rais, Ikulu, Zanzibar, Kibweni Palace, Ikulu Ndogo Wete na Chake Chake, hospitali ya Mnazi Mmoja na Kivunge Unguja na jengo la Mahakama Kuu Unguja. Uwanja wa Michezo wa Amaan Unguja na Gombani Pemba imefanyiwa ukarabati mkubwa na kuwa na sura nyengine.
Pamoja na hayo, katika kuendeleza mandhari ya mji wa Unguja, kwa kushirikiana na Aga Khan Trust, tumeifanyia matengenezo makubwa bustani ya Forodhani na kuigeuza kuwa ni kivutio cha fakhari kwa wageni na wenyeji.
Utawala Bora:
Mheshimiwa Spika, Tokea nimeingia madarakani mwaka 2000 nimeweka mkazo maalum kuhakikisha kuwa kunakuwa na utawala bora nchini ikiwa ni msingi wa kudumisha uhuru wetu na kuendeleza demokrasi. Ninafuraha kuwa kuanzia mwaka 2001 nchi yetu imepiga hatua kubwa katika uimarishaji wa misingi ya utawala bora. Kati ya mwaka 2000 na 2005 hatua zifuatazo zimechukuliwa katika mwelekeo huo. Tumeanzisha wizara maalum ya mambo ya Katiba na Utawala Bora ambayo imesimamia uundaji wa Tume Huru ya Uchaguzi inayojumuisha wajumbe kutoka vyama vikuu vya siasa nchini. Kadhalika tumeanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambalo tulilitumia katika uchaguzi mkuu wa 2005 kwa mafanikio makubwa. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Zanzibar tumeanzisha mfumo wa kuwa na Vitambulisho vya kisasa vya Wakaazi wa Zanzibar. Aidha, kila mpiga kura halali aliomo ndani katika daftari la kudumu amepatiwa kitambulisho cha kisasa cha kupigia kura ambacho kimeanza kutumika kwa mafanikio makubwa mwezi uliopita katika kura ya maoni.
Katika kuhakikisha upatikanaji wa haki za raia, tumerekebisha mfumo wa Mahakama na kuufanya uwe bora zaidi kwa kurekebisha baadhi ya sheria na kanuni na kuzipatia Mahakama uhuru zaidi wa kuendesha kazi zake, kuongeza idadi ya Mahakimu pamoja na kuyakarabati majengo yao.
Serikali ya Awamu ya Sita, pia, imeanzisha ofisi maalum ya Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mashtaka (DPP). Tumeweza vile vile kufanya marekebisho ya sheria mbali mbali za jinai. Ofisi ya Tume ya Haki za binaadamu imefunguliwa hapa Zanzibar kushughulikia ukiukwaji wa haki za binaadamu.
Mheshimiwa Spika, Nilipoingia madarakani, nilianzisha Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto ili kusimamia na kulinda haki zao pamoja na kushajiisha jamii kuziheshimu na kuzitekeleza. Wizara imekuwa ikiendelea kutoa elimu na mafunzo kupitia vyombo vya habari na kuwasikiliza wanawake na watoto wenye matatizo na kuyapatia ufumbuzi kwa kutoa ushauri nasaha kwa kushirikiana na taasisi nyengine kwa nia ya kuleta utulivu, amani na maendeleo kwa familia.
Serikali ya Awamu ya Sita, kwa kupitia Wizara hiyo, inaendelea kuwajengea uwezo wanawake kwa kuwapa fursa ya kuanzisha na kuendeleza biashara kwa lengo la kuinua kipato chao na kuinua uchumi, kwani wakiwezeshwa, wanawake wanaweza. Mashirika ya UNICEF na ILO yametoa mashirikiano makubwa katika kuhakikisha watoto wa Zanzibar wanapata haki zao za msingi kwa kuweka sheria za kazi na kupiga vita ajira za watoto na kuwawezesha wanawake kujiunga katika vikundi ili waweze kujikimu kimaisha kwa kufanya kazi na biashara. Natoa shukurani nyingi kwao na watendaji wao waliopo Zanzibar na Tanzania Bara. Pia, tumekuwa tukiwajali watu wenye ulemavu kwa kushirikiana na kusaidia taasisi zao mbali mbali ili waweze kujimudu na kujiendesha kimaisha. Aidha, tunatoa mashirikiano makubwa kwa wafanyakazi waliostaafu na kujiunga pamoja.
Ushirikishwaji na Uwezeshaji wa Wananchi:
Mheshimiwa Spika, Misingi ya kidemokrasia inayofuatwa na nchi yetu inahitaji wananchi wenyewe kushiriki katika kupanga na kutekeleza mipango yao ya maendeleo. Ushiriki huo hufanyika kupitia vikundi mbali mbali, utoaji wa maoni kwenye vikao na warsha, na kupitia Wawakilishi wao hapa Barazani na katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa upande wa Baraza hili, juhudi za kuliimarisha zimeendelezwa kwa kupatiwa watendaji wenye ujuzi na vifaa vya kisasa vya kazi. Aidha, mafunzo mbali mbali kwa njia za semina na ziara za ndani na nje ya nchi yametolewa kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza. Mashikirikiano na Mabunge mengine ulimwenguni yameimarishwa ili kuwajengea uzoefu Wajumbe na Wafanyakazi wa Baraza.
Ili kulipa haiba na hadhi inayostahiki Baraza la Wawakilishi, tumekamilisha ujenzi wa jengo hili jipya la Baraza tunalokutania leo ambao ni mali ya wananchi wote.
Baraza la saba la Wawakilishi linamaliza muda wake kwa mafanikio makubwa. Baraza hili limepitisha jumla ya miswada ya sheria 56 na sera 12 na kujibu maswali 1,640 yalioulizwa. Baraza hili litakumbukwa kihistoria kuwa ni Baraza lililoweka misingi ya kudumu ya umoja, mshikamano, utulivu na amani ya Zanzibar. Limefanya maamuzi mazito kwa uadilifu na kujijengea heshima kubwa. Baraza hili limesimamia vyema madhumuni na malengo ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kulinda uhuru wa Zanzibar na watu wake, kulinda utu, umoja na heshima ya Wazanzibari wote ya kujiamulia mambo yao yanayohusu nchi yao na uchumi wao.
Mheshimiwa Spika, Katika kuwawezesha wananchi kiuchumi, mtakumbuka kuwa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na mimi tulianzisha mfuko maalum, maarufu kama mfuko wa JK na AK. Hadi mwezi Juni mwaka huu jumla ya wananchi 658 wamenufaika kwa kukopeshwa jumla ya T.Shs. 1,345.90 milioni kutoka Mfuko huu. Lengo la mikopo kutoka mfuko huu na ile ya PRIDE, WEDF, SELF na Mfuko wa Kujitegemea ni kuwapatia mikopo nafuu wananchi wazalishaji wadogo wadogo ili kuendeleza miradi yao mbalimbali. Uanzishaji huu wa mifuko mbalimbali unahitaji kusaidiwa na uongezaji wa elimu na utaalam kwa wajasiriamali hao ili mikopo hiyo iwe endelevu na yenye tija zaidi katika kuwaongezea wananchi wetu kipato.
Mheshimiwa Spika, Katika kuimarisha mawasiliano na ushiriki wa makundi mbalimbali katika kuleta maendeleo ya nchi, Serikali imeanzisha Baraza la Biashara la Zanzibar (ZBC) lenye wajumbe sawa kutoka serikalini na sekta binafsi kwa lengo la kusikiliza maoni ya kuimarisha mazingira ya kibiashara na kiuchumi nchini. Kwa nafasi yangu ya Urais wa nchi yetu, mimi ndie mwenyekiti wa ZBC. Hii ni ishara ya umuhimu unaowekwa na serikali juu ya mashirikiano hayo na sekta binafsi. Hadi sasa, ZBC imeshafanya kwa mafanikio makubwa vikao vinne. Mashirikiano pia yameimarika baina ya serikali na taasisi zisizo za kiserikali.
Kuimarika kwa Ushirikiano wa Kimataifa:
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu, kupitia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mwanachama wa Umoja wa Mataifa, Umoja wa nchi Huru za Afrika, Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki na Jumuiya mbali mbali za Kikanda. Mahusiano mazuri na nchi za nje ni jambo jema na lenye manufaa ya kiuchumi, kijamii na usalama. Kwa bahati mbaya, serikali ya awamu ya sita iliingia madarakani mwaka 2000 hali ya kuwa Zanzibar imesusiwa na wengi kati ya Washirika wetu wa Maendeleo kwa sababu za kisiasa. Kipindi cha miaka kumi ya 2000 hadi 2010, kimeshuhudia kuimarika sana kwa uhusiano wetu na nchi hizo pamoja na mashirika ya kimataifa. Kuimarika kwa mahusiano hayo ni kielelezo cha kukubalika kwa serikali yetu, uongozi wake na kuheshimiwa demokrasia nchini.
Hali ya Kisiasa:
Mheshimiwa Spika, Kwa miongo mingi nchi yetu ilikuwa haijashuhudia utulivu endelevu wa kisiasa. Tunahitaji utulivu wa kudumu wa kisiasa ili tuweze kuwa na maendeleo endelevu. Hakuna muwekezaji yeyote makini atakaewekeza fedha nyingi katika nchi ambayo utulivu wake ni wa kimiongo, unaingia mashakani kila baada ya miaka mitano wakati wa uchaguzi.
Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia fursa ya kupata utulivu wa kudumu nchini kwetu kupitia mazungumzo baina yangu na Maalim Seif Sharriff Hamad, Katibu Mkuu wa CUF hapo tarehe 5 Novemba mwaka jana, Ikulu, Zanzibar. Tulifanikiwa kufikia maridhiano ya kumaliza uhasama wa kisiasa Zanzibar na kusameheana. Najuwa tumeshapongezwa sana, kuhusiana na maridhiano hayo. Hata hivyo, naomba nichukue fursa hii tena kumpongeza sana Maalim Seif na chama chake kwa kufanya maamuzi hayo ya kijasiri ya kuitambua serikali yangu, kuwa tayari kuleta maridhiano, na pia kukubali kuwa wananchi wenyewe ndio wawe waamuzi wa mwisho juu ya mustakabali wa nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Inaonekana kuwa moja ya tatizo linalochangia hali ya kutofahamiana ni mwamko mkubwa wa kisiasa kwa wananchi wetu unaoongezwa nguvu na kukaribiana kwa kiasi fulani kwa matokeo katika chaguzi mbali mbali. Tulihitaji kufikira njia mpya, bora zaidi, na itakayokubalika na wananchi walio wengi ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo hilo. Najua kuwa miongoni mwetu, zilikuwapo fikra na rai tofauti juu ya namna ya kukabiliana na hali hio. Wapo wachache wanaoamini kuwa hali hiyo ingejirekebisha yenyewe na hivyo utaratibu wa sasa wa chama kinachoshinda kuunda serikali peke yake uendelee japo kuwa umetuletea matatizo mengi na kwa muda mrefu.
Wapo, pia, walioamini kuwa palihitajika njia mbadala ya kuongoza nchi. Kati ya hawa, nami nikiwemo, tuliona kuwa njia hiyo mbadala ni kuwa na serikali ya umoja wa kitaifa inayoundwa na vyama vyote vilivyopata ridhaa ya wananchi kuwawakilisha katika Baraza la Wawakilishi. Aidha, serikali hiyo iongozwe na chama kilichopata kura nyingi zaidi za urais katika Uchaguzi Mkuu. Maamuzi kama haya sio madogo kwa mustakabali wa nchi. Vyama vyetu vikuu viwili, CCM na CUF vilikubaliana juu ya haja ya maamuzi hayo kufanywa na wananchi wenyewe. Kwa utaratibu unaotumika kimataifa, mojawapo ya njia za kufanya maamuzi kama haya ni kupitia kura ya maoni (Referendum) ambapo wananchi huamua kati ya fursa zilizopo. Nasi hapa Zanzibar tukakubaliana kutumia njia hiyo kupata maamuzi ya wananchi.
Mheshimiwa Spika, Tarehe 31 Julai mwaka huu wananchi wa Zanzibar walishiriki kupiga kura ya maoni na kuchagua wanachokitaka. Matokeo ya kura hiyo yalikua wazi kwa thuluthi mbili ya waliopiga kura kuamua kuwa serikali ijayo iwe ya umoja wa kitaifa. Idadi hii inamaanisha kuwa kati ya kila Wazanzibari watatu waliopiga kura, wawili wamekubali kuanzishwa kwa mfumo wa serikali ya umoja wa kitaifa baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Hata hivyo wapo wananchi wachache waliotaka utaratibu wa sasa uendelee.
Kwa kutilia maanani namna ambavyo wananchi walielimishwa kwa muda mfupi juu ya kura ya maoni na kushiriki kwa wingi na utulivu mkubwa katika upigaji wa kura hiyo, natoa pongezi za dhati kwa Kamati ya Watu Sita ya Baraza la Wawakilishi ya Kusimamia Utekelezaji wa Azimio la Baraza kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar iliyoongozwa na Mwenyekiti wake Mheshimiwa Ali Mzee Ali kwa juhudi zao katika kufanikisha zoezi hilo.
Kwa kuzingatia hekima za wazee wetu inayosema wengi wape, sote kwa pamoja, tunapaswa kuyaheshimu maamuzi haya ya wengi. Naomba niwashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa kutoa maoni yao kwa njia ya utulivu, kistaarabu na ukomavu mkubwa wa kidemokrasia. Nawashukuru zaidi walio wengi ambao wamekubaliana na mageuzi ya namna ya kuongoza nchi yetu. Sote kwa pamoja tumeandika historia mpya nchini petu. Natumai itakuwa historia nzuri itayomnufaisha kila mmoja wetu, tuliopo sasa na vizazi vijavyo. Kwa vyama vyetu vya siasa, maamuzi haya ya wananchi ni maelekezo yao kwetu. Ni ushindi wa wananchi wote, sio wa wanasiasa wala sio wa vyama vya siasa. Aidha, hatupaswi kuyabeza maoni ya wachache waliotaka kuendelea utaratibu wa sasa. Tujue tu kuwa kwenye mabadiliko sio wote huyakubali kwa haraka. Wengine mpaka waone wenyewe faida yake. Kwa hivyo hali hiyo iwe ni changamoto kwetu tuliowengi kuhakikisha kuwa historia isiyopendeza nchini kwetu haijirejei ili tuwape moyo hao wenzetu wenye hofu ili waungane nasi katika safari hii yenye matumaini.
Mheshimiwa Spika, Baada ya mchakato wa kura ya maoni na walio wengi kuunga mkono muundo mpya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, juzi tarehe 9 Agosti, Baraza lako tukufu kwa kauli moja lilipitisha Mswada wa Marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984. Marekebisho hayo ya kihistoria yataruhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa iundwe mara baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Nataka nichukue fursa hii kwanza kukupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Spika, pamoja na wajumbe wa baraza lako tukufu kwa uamuzi wenu wa kizalendo. Bila ya shaka uamuzi wenu huo utaingia katika vitabu vya historia ya Zanzibar itakayokumbukwa kwa miaka mingi ijayo.
Mheshimiwa Spika, Nchi yetu inakabiliwa tena na Uchaguzi Mkuu tarehe 31 Oktoba mwaka huu. Kwa upande wetu serikalini, tunaendelea vyema na matayarisho ya uchaguzi huo kwa kukiwezesha chombo chenye dhamana yake, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar. Ni matumaini yangu kuwa Tume, Vyama vya siasa, na wananchi wote tutaungana kuhakikisha kuwa uchaguzi wa mwaka huu unaandika historia mpya nchini kwetu inayoendana na maridhiano yaliyopo ya kisiasa. Nia yetu ni kuwa na historia ya uchaguzi wa kuaminiana, uchaguzi wa kistaarabu, na uchaguzi ulio safi na huru kwenye macho yetu sote, wapiga kura na waangalizi watakaokuwepo. Uchaguzi huu unabeba matumaini makubwa zaidi ya wananchi, kimaendeleo, kiutulivu, na kiuchumi. Naomba sote tuhuishe matumaini yao kwa salama na amani.
Mwisho:
Mheshimiwa Spika, Miaka 10 katika historia ya nchi ni kipindi kifupi sana. Kwa mujibu wa Katiba yetu, Rais ndie kiongozi wetu wa nchi lakini miaka 10 ya uongozi wa nafasi ya juu katika nchi, ni muda mrefu sana wa dhamana iliyo nzito. Dhamana hiyo inampa dhima Rais kutumia mamlaka aliyopewa kuhakikisha, (i) usalama na amani ya nchi inadumishwa, (ii) Demokrasia na haki za wananchi wote zinalindwa, (iii) Nchi inapata maendeleo na kuinua ustawi wa jamii kwa jumla, (iv) Kudumisha umoja na maslahi ya Zanzibar ndani ya Muungano pamoja na kujenga mahusiano bora na majirani, na nchi na mashirika ya nje. Zaidi ya yote, Rais ana dhamana ya kuitetea, kuilinda na kuitekeleza Katiba ya nchi. Hizo zote ni dhamana nzito.
Tarehe 8 Novemba mwaka 2000 mara baada ya kuapishwa na kukabidhiwa dhamana ya kuiongoza nchi yetu, nilitoa hotuba fupi pale Uwanja wa Amaan napenda nijinukuu mwenyewe nilisema kama ifuatavyo:
“Ndugu wananchi, leo nathubutu kusimama mbele yenu kwa sababu wananchi wa Zanzibar wametumia haki yao ya kikatiba ya kumchagua Rais wanaemtaka. Wakati napokea imani yenu kwa heshima na unyenyekevu kuwa Rais wa Zanzibar, sina budi kupokea wito wa wananchi wa kutaka mabadiliko. Nilipokuwa nafanya kampeni ya kuomba kura zenu kwa niaba yangu na niaba ya chama changu, niliendelea kusisitiza juu ya umoja, amani na utulivu. Leo nasimama tena mbele yenu kwa sababu mmekubali wito huo na kunichagua kuwa Rais. Baada ya kunichagua mimi kwa kura nyingi sana na kunipa ushindi mkubwa ni dhahiri kwamba mmechagua umoja, amani na utulivu katika nchi yetu.
Napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru wananchi wote wa Zanzibar kwa kuniamini kwa kazi kubwa ya utekelezaji wa chaguo lenu la umoja, amani na utulivu. Napenda niwaombe wananchi wote ushirikiano wenu”.
Baada ya maelezo hayo sina budi kuwashukuru sana wananchi wote wa Zanzibar kwa kunikubalia ombi langu la kuchagua umoja, amani na utulivu na kuniunga mkono katika kipindi chote.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita naamini kwamba nimetumia uwezo wangu kuyatekeleza yote haya kwa kadiri Mwenyezi Mungu, Rahim, alivyonijaalia. Lakini sikufanya kazi hiyo kubwa peke yangu ila nimeshirikiana na wananchi wote wa Zanzibar, viongozi wenzangu wa chama changu, Serikalini na nje ya Serikali. Nimeshirikiana na kufanyakazi kwa karibu sana na Marais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Mstaafu Benjamin Wiliam Mkapa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Nawashukuru wote kwa dhati kwa mashirikiano, msaada wao na ushauri wao kwangu kwa muda wote. Namshukuru mzee wetu Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi. Namshukuru pia Rais Mstaafu wa Zanzibar, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi kwa kuanzisha Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. Wakati huo huo, namshukuru Rais Mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour. Nilibahatika, vile vile, kufanya kazi kwa karibu na Marehemu Dr. Omar Ali Juma akiwa Makamo wa Rais chini ya Mhe. Mkapa. Mwenyezi Mungu kamuhitaji ni wajibu kwetu kumuombea maghfira na malazi mema. Nawashukuru pia Mheshimiwa Dr. Ali Moh’d Shein, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano. Nawashukuru viongozi wengine wote wa kitaifa walio madarakani na wastaafu niliowahi kufanyakazi nao, mawaziri na watendaji wengine.
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa utaratibu wa uongozi wa nchi yetu, nchi inaongozwa na mihimili mitatu: ule wa Utawala (Executive) unaoongozwa na Rais, wa kutunga sheria (legislature – yaani Baraza hili tukufu) unaoongozwa na Spika na mhimili wa kusimamia haki (Judiciary) unaoongozwa na Mheshimiwa Jaji Mkuu. Kwa mujibu wa Katiba yetu, kama nilivyosema awali Kiongozi wa nchi ni Rais. Naomba nitumie fursa hii kukushukuru wewe Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza hili linalomaliza muda wake na Mheshimiwa Hamid Mahmoud Hamid Jaji Mkuu wa Zanzibar. Nasema kutoka ndani ya moyo wangu kuwa katika kipindi chote cha uongozi wangu wa nchi nimepata bahati ya kufanya kazi kwa mashirikiano makubwa kutoka kwenu. Nimebahatika kupata maoni na ushauri wenu muhimu ulionisaidia sana katika kufanya maamuzi, mengine yakiwa magumu. Wakati wote, ukaribu wenu umekuwa ni ngao muhimu kwangu hata kwa kujua tu, wenzangu wananiunga mkono na wako pamoja nami. Nakushuruni sana.
Mheshimiwa Spika, Napenda, pia, kumshukuru Waziri Kiongozi, Mheshimiwa Shamsi Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi, Mheshimiwa Ali Juma Shamuhuna pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wote waliofanya kazi chini yangu kwa mashirikiano, utiifu, na ushauri wao kwangu uliowezesha kuivusha vyema nchi yetu katika muda wote huo. Nawashukuru sana Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu, Makamishna, Wakurugenzi na viongozi na wafanyakazi wote wa serikali kwa utendaji wao mzuri uliotufikisha hapa tulipo kwenye mafanikio makubwa. Natoa shukurani pekee kwa maafisa na wafanyakazi katika Afisi ya Rais Ikulu kwa uaminifu wao kwangu, ushirikiano na kazi nzuri wakati wote na uvumilivu wao katika kazi. Nawaambia ahsanteni sana. Shukurani zangu nyingi, pia, ni kwa wakuu wa vikosi na askari wote wa vikosi vyetu vya ulinzi na usalama kwa utiifu wao kwangu kama kiongozi wao na kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuwafanyia wananchi wenzao wa Zanzibar katika kudumisha ulinzi na usalama wetu pamoja na nchi yetu. Ahsanteni sana.
Shukurani zangu maalum zinakwenda kwa wananchi wote kwa kuniamini, kunipa fursa ya kuwatumikia, na kunistahamilia wakati nchi yetu ilipopita vipindi vigumu. Natumai neno “AHSANTE” litabeba uzito wa kutosha wa shukurani zangu kwao. Nakishukuru pia Chama changu cha CCM kwa kuniamini na kunipa fursa hii adhimu. Aidha, nawashukuru viongozi wa dini na taasisi zisizokuwa za serikali kwa kushirikiana na mimi katika kipindi changu chote kuhubiri amani na umoja. Nawashukuru wenye vyombo vya habari na waandishi wote kwa kutangaza habari zetu katika kipindi chote.
Mwisho nawashukuru mabalozi wa nchi za nje waliofanya kazi Zanzibar katika kipindi cha Awamu ya Sita na, pia, waliokuwepo Tanzania Bara kwa kushirikiana na sisi kwa urafiki na kufahamiana.
Mheshimiwa Spika, Niruhusu pia kutoa shukurani nyengine maalum kwa familia yangu ambayo imekuwa ndio muhimili wangu na chachu ya mafanikio yangu. Namshukuru sana mama yangu, Mama Fatma Karume, namshukuru kwa namna ya pekee mke wangu, Mama Shadya Karume, nawashukuru sana wanangu, wajukuu na wanafamilia wote kwa kuniunga kwao mkono bila ya ukomo wala kuchoka katika kipindi chote cha mimi kuiongoza nchi yetu. Familia yangu imenistahamilia na imevumilia mengi wakati nikitumia muda mwingi kuwatumikia wananchi wenzangu. Nataka nikiri kwamba maisha yao katika kipindi hicho hayakua mepesi hata kidogo kwa vile waliokua na joto nami wakati huo, joto lao liliishia kwa familia yangu kama ilivyo kwa wanasiasa wengine. Pamoja na yote hayo walikuwa nami katika kuitumikia nchi yetu na chama chetu kwa uwezo wao wote. ahsanteni sana. Namshukuru sana Ndugu yangu Balozi Ali Karume pamoja na ndugu zangu wakike, jamaa zangu na marafiki zangu wote kwa msaada wao kwangu. Nawashukuru tena wananchi wote wa Zanzibar na Watanzania wote.
Mheshimiwa Spika, Muda wangu wa kuitumikia nchi yetu kama Rais utafikia ukomo wake mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 31 Oktoba mwaka huu. Baada ya hapo tutapata Kiongozi mwengine. Nimeeleza mafanikio makubwa tuliyoyapata miaka kumi inayomalizika. Hata hivyo, bado nchi yetu inakabiliwa na changamoto kadhaa. Katika kukabiliana na changamoto hizo, serikali yetu imeweza kuweka misingi madhubuti ya maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Misingi hii inahitaji kutunzwa, kuimarishwa na kuendelezwa kwa kasi zaidi. Kwa kuwa uchumi wetu unahitaji kasi zaidi ya mageuzi kuelekea uchumi wa kisasa unaonufaisha walio wengi, bila ya shaka sekta binafsi itapaswa kuendelezwa kwa kulelewa na kujengewa uwezo zaidi na kuendelea kuwa mdau muhimu katika uchumi wa nchi yetu. Na kwa kuwa Chama cha Mapinduzi kina ujuzi na uzoefu mkubwa katika kuyajenga na kuyasimamia mazingira ya aina hiyo, naomba nyote mkubaliane nami kuwa Rais wetu ajae atoke CCM.
Mheshimiwa Spika, Baraza la Wawakilishi ni chombo muhimu sana katika uongozi na mustakabali wa nchi yetu. Pia, ni sehemu ya ukuzaji wa demokrasia nchini na ni taasisi yenye uzito mkubwa katika ustawi wa jamii na uchumi. Katika kuliwezesha Baraza, serikali yangu imefanikiwa kujenga jengo jipya. Napenda kumshukuru mfadhili mkubwa wa ujenzi huo, Sheikh Abdulla Al Youseif. Sasa Baraza linajivunia kuwa na jengo lake wenyewe la kisasa na kuvutia likiwa ni moja ya alama ya Mhimili wa Utungaji Sheria. Nina imani kwamba Baraza litaendelea kutimiza wajibu wake kwa umahiri na ustadi mkubwa kwa faida ya kila mmoja wetu.
Hakuna marefu yasio na mwisho. Kipindi cha miaka mitano cha uhai wa Baraza hili ni kirefu lakini sasa kimefikia mwisho. Nachukua fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa Wajumbe wote wa Baraza hili kwa kazi kubwa na nzuri ambayo mmeifanya wakati wa uhai wa Baraza hili. Mafanikio yote niliyoyataja hapo kabla yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushauri na maelekezo yenu na hata kuikosoa kwenu serikali. Pongezi za pekee ni zako wewe Mheshimiwa Spika, Naibu wako na Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza na Katibu wa Baraza kwa uongozi mzuri wa shughuli za Baraza, kwa busara wakati wa vikao na kwa ufanisi mkubwa wa kuiendesha Taasisi hii muhimu. Ninajua kwamba wengi wa Wajumbe wako wamerudi tena Majimboni kuomba ridhaa ya Wananchi wawachague tena kuwa Wawakilishi wao katika Baraza lijalo litakaloundwa baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31. Nakuombeeni kheri nyote katika uchaguzi huo.
Mwisho kabisa, Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 92 (1) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Maisha ya Baraza la Wawakilishi yataendelea kwa muda wa miaka mitano baada ya kuundwa upya mara tu baada ya Uchaguzi Mkuu. Ili kutoa nafasi ya matayarisho ya mwisho kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu hapo ifikapo tarehe 31 Oktoba 2010, kwa madaraka niliyonayo chini ya kifungu cha 91(2)(a) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, natamka kwamba kuanzia Ijumaa tarehe 13 mwezi wa Agosti 2010 Baraza la saba la Wawakilishi la Zanzibar limevunjwa rasmi.
Nakutakieni Waheshimiwa Wajumbe na wananchi nyote saumu njema na Ramadhani ya baraka na wingi wa rehema.
Mwenyezi Mungu awabariki wote,
Mungu Ibariki Zanzibar,
Mungu Ibariki Tanzania,
Mungu Ibariki Afrika.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment