Na Mwajuma Juma, Zanzibar
KAMPUNI ya Future Century kwa kushirikiana na Kampuni ya Vannedrick zote za Dar es Salaam, zinatarajia kudhamini Ligi Kuu ya Zanzibar msimu ujao.Lengo la kudhamini ni kuweza kuendeleza na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa soka, ambaounaonekana kudidimia visiwani Zanzibar na kuleta hamasa kwa mashabiki wa soka.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Zanzibar, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Vennedrick Tanzania Limited, Fredrick Mwakalebela, alisema katika udhamini huo, wataangalia mambo muhimu ili kuweza kufanikisha mpango huo.
Alisema miongoni mwa mambo watakayoangalia katika udhamini huo, kutoa vifaa kwa klabu zitakazoshiriki ligi hiyo, usafiri, zawadi na kuiwezesha ZFA kuendeleza ligi hiyo. "Tuna nia nzuri ya kusaidia Zanzibar kisoka, kuanzia tunadhamini ligi na ikiwezekana, tutaweza kuzishawishi kampuni nyingine ili ziweze kudhamini," alisema Mwakalebela.
Naye, Rais wa ZFA Taifa, Ali Fereji Tamim, alisema kupatikana kwa wadhamini katika ligi hiyo itapendeza na vipaji vya vijana vitaonekana.
Chanzo: Majira
No comments:
Post a Comment