Habari za Punde

‘Nyoyo za Wauguzi Zifanane na Sare zao'


Na Salum Vuai, MAELEZO

WAHITIMU wa Chuo cha Afya kilichoko Mbweni, wametakiwa kufanyakazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma zao pindipo wanapoajiriwa, na kwamba lazima nyoyo zao ziwe nyeupe kwa wagonjwa kama zilizvyo sare zao.

Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Dk. Malik Abdallah Juma alieleza hayo akiwamukilisha waziri wa wizara hiyo kwenye mahafali ya 19 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika viwanja vya chuo hicho huko Mbweni.

Wahitimu kwenye mahafali hayo wa kati ya miaka miwili na minne katika fani za uuguzi/ukunga, afya ya akili na wakunga wa vijijini ambapo walitunukiwa vyeti na stashahada.


Dk. Malik alisema haitakuwa busara kuwaona wahitimu wao wakinga'ra kwa sare nyeupe wakifurahia kumaliza mafunzo, au wanapoajiriwa, lakini wakashindwa kufuata maadili yanayoongoza taaluma zao.

Aidha alieleza wananchi wamekuwa wakiwalalamikia kutokana na tabia mbaya walizonazo baadhi ya wauguzi, kwa kukiuka maadili, na kuwatolea ujeuri, ujuvi wagonjwa wanaowahudumia, hivyo kuipaka matope fani hiyo.

"Mimi nakerwa sana na kauli iliyozoeleka kwamba mtu akitaka kushuhudia ujeuri 'first class' (daraja la kwanza), basi aende hospitali ya Mnazimmoja. Nafahamu wauguzi wengi wanatelekeza vyema majukumu yao, hawa wachache wenye tabia mbaya wasipewe nafasi kutuharibia", alisema Mkurugenzi huyo.

Aliwataka wahitimu watakaobahatika kuajiriwa katika hospitali kuu ya Mnazimmoja na nyengine nchini, kuleta mapinduzi kwa kuwa waadilifu na kutoiga tabia mbaya za wauguzi wachache wanaotajwa kuwa ni wakorofi.

Mkurugenzi huyo alisisitiza kwamba viapo walivyotoa wahitimu hao visiwe kauli za midomoni bali vitoke nyoyoni, ili kuipa taaluma yao hadhi na heshima inayostahili mbele ya jamii na pia kumridhisha Mwenyezi Mungu. 

Kwa upande mwengine, aliwashauri kuwa kuhitimu kwao chuoni hapo kusiwe mwisho na kujiona wamemaliza elimu, bali wajiendeleze kwani kumekuwa na mabadiliko ya kisayansi na kila siku kuna kitu kipya cha kujifunza.

Aliahidi kuwa, serikali kupitia wizara ya Afya kwa kushirikiana na Baraza la Chuo hicho, watachukua juhudi kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazokikabili chuo na wanafunzi ili kuwajengea mazingira mazuri ya kufanya kazi na kushughulikia masomo yao.  

Mapema, Kaimu Mkuu wa Chuo hicho Rukia Rajab, alisema wahitimu hao ni mchango wa chuo kwa serikali, na hivyo kuiomba ihakikishe inawatumia ipasavyo kwa kuwaajiri kwenye hospitali na vituo mbalimbali vya afya Unguja na Pemba.

Alifahamisha kuwa, mwaka huu utakuwa wa mwisho kwa Chuo hicho kutoa taaluma kwa miaka minne, na kitaanza kufuata mtaala wa miaka mitatu, mpango ambao unatambuliwa na umeridhiwa na nchi za Afrika Mashariki.

Aliishukuru serikali ya Zanzibar kwa kuendelea kukisaidia chuo, sambamba na ile ya Oman ambayo inaendelea kukiimarisha kwa mambo mbalimbali baada ya kufadhili ujenzi wake.

Alitaja miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana, ni pamoja na ukarabati wa ukumbi wa mikutano, kufungua tovuti, kukamilika kwa ujenzi wa dakhalia na nyumba ya walimu kutoka Norway, walimu wanne kwa msaada wa Benki ya Maendeleo Afrika (ADB).

Katika risala yao wahitimu, walisema ulinzi chuoni hapo hautoshi kulingana na ukubwa wa eneo hilo, ukuaji wa ongezeko la wanafunzi kutoka ndani na nje ya Zanzibar, na kutaka nguvu zaidi ziongezwe katika ili ujenzi wa ukuta unaozunguka chuo hicho umalizike kwa haraka na kuwahakikishia usalama wao.    
 
Jumla ya wahitimu 173 walikabidhiwa vyeti na stashahada zao, ambapo 66 wanakwenda kuwa wauguzi/ wakunga, 33 wamesomea fani ya afya ya akili na 74 ni wakunga wa vijijini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.