Habari za Punde

Vyama Vyaanza Harakati Uchaguzi Mdogo Bububu


Na Mwantanga Ame 
WAKATI Tume ya Uchaguzi Zanzibar, ikiwa imepuliza kipenga cha kuanza kwa uchaguzi mdogo wa Jimbo la Bububu, Vyama vya Siasa Zanzibar, vimeanza kujitapa kushinda uchaguzi huo huku Chama Cha CCM kikisema hakitakuwa tayari kulitoa jimbo hilo mikononi mwake.

CCM imeeleza hakitakuwa tayari kuliachia Jimbo hilo kuingia katika mikono ya upinzani na kinakusudia kulinyakuwa tena Jimbo hilo ili kuona linarudi katika mikono ya CCM.

Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Bububu unafanyika baada ya aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo hilo Mohammed Ali Mtondoo, kupitia tiketi ya CCM kufariki dunia mapema mwaka huu baada ya kuuguwa maradhi ya kupooza mwili.

Kutokana na kifo hicho Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), tayari imetangaza kufanyika kwa uchaguzi mdogo Septemba 16, mwaka huu ambapo wananchi wa Jimbo hilo watapiga kura.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai,  akizungumza na Zanzibar Leo, jana Mjini Zanzibar alisema uchaguzi huo utakuwa ni wa aina yake kwani CCM itahakikisha jimbo hilo linabakia katika mikono yake.

Alisema tayari hivi sasa Chama hicho kimeanza kufanya maandalizi ya kushinda uchaguzi huo, ikiwa pamoja na kuandaa mazingira bora kupata wagombea ambao wataingia katika kinyang’anyiro hicho kitapoanza.

Akifafanua kauli hiyo, Naibu huyo alisema mazingira hayo yatakuwa mapya ndani ya Chama cha Mapinduzi, kwa lengo la kuepusha kutokea kwa vurugu, chuki na hasama katika upatikanaji wa mgombea katika kura za maoni za ndani ya Chama.

Akifafanua zaidi alisema utaratibu wanaokusudia kuutumia ni majina ya wagombea yatayojitokeza kuomba nafasi hiyo kabla ya kuwasilishwa kwa wananchi kupigiwa kura za maoni, yatafikishwa katika vikao vya Mkutano Mkuu wa Majimbo ambao utawashirikisha mabalozi wa matawi na watapiga kura kutoa majina matatu.

Alisema baada ya kutoa majina hayo matatu Mkutano huo utayashusha kwa wanachama kuweza kuyapigia kura ya maoni ili kupata chagua lao badala ya mfumo wa zamani wa majina hayo kuwasilishwa yote kwa wananchi.

Aidha, alisema kwa vile jimbo hilo lilikuwa chini ya CCM, hawatakubali kuona linawatoka mikononi mwao na hivi sasa tayari wameanza maandalizi ya kushinda.

Alisema huo ni mmoja wa mkakati uliouweka Chama cha Mapinduzi, kuona majimbo yote yaliokuwa ngome ya CCM na  yaliochukuliwa na upinzani yanarudi mikononi mwa Chama hicho.

Hata hivyo, alisema Chama hicho kitahakikisha mchakato mzima wa uchaguzi huo unaendeshwa katika mazingira bora kwa kufanya kampeni za kistaarabu hadi kupatikana mshindi.

Kuhusu suala la kupata mgombea alisema tayari hivi sasa kuna wanachama wengi wa CCM katika Jimbo hilo wameanza kuonesha nia ya kutaka kuwania nafasi hiyo.

Nae Katibu wa Chama cha TADEA Zanzibar, Juma Ali Khatib, akizungumzia juu ya suala hilo alisema hawana sababu ya kutoshiriki uchaguzi huo kwani tayari kuna wanachama wengi wanaotaka kuwania nafasi hiyo na kushinda.

Alisema ndani ya Chama hicho tayari kuna wanachama zaidi ya watano wakiwemo wanawake wawili ambao wameonesha nia kutaka kuwania nafasi hiyo.

Alisema hivi sasa bado hakuna vikao vilivyokaa kwa ajili ya kutoa ratiba ya Chama hicho katika namna ya kupata mgombea huyo.

Hata hivyo, Katibu huyo, alisema Chama hicho kinajiandaa kufanya vikao vya chama kuweza kutoa mgombea huyo ndani ya mwezi ujao.

Mkurugenzi wa Sera wa Chama cha Wakulima na Wafanyabishara Zanzibar (AFP), Rashid Yussuf Mchenga, akizungumzia msimamo wa Chama hicho juu ya hilo, alisema  tayari Chama chao kimeshafanya uteuzi wa Mgombea ataewania nafasi hiyo na wanahakikisha kuwa atashinda.

Alisema aliyeteuliwa kuwania nafasi hiyo kwa Chama hicho ni Mussa Ali Mussa, na hivi sasa wameanza maandalizi ya kukamilisha taratibu za Tume ya Uchaguzi.

Upande wa Chama cha CUF kupitia msemaji wake Mkurugenzi Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma, Salum Bimani, akizungumza na Zanzibar Leo, alisema chama chao kitahakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na haki na chama chao kitaibuka na ushindi.

Alisema Chama chao tayari hivi sasa kimeshaanza mchakato wa kupata mgombea wa kuwania kiti hicho na kitahakikisha kinaenda katika uchaguzi huo kwa kushirikiana na vyama vyengine katika hatua zote.

Hata hivyo, Bimani alisema watachohakikisha wanakizingatia katika uchaguzi huo ni kuwahimiza wanachama wao kushiriki uchaguzi huo kwa amani.

Kwa mujibu wa ratiba ya Chama cha Mapinduzi iliyotolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa Itikadi na Uenezi, Nape Moses Nnauye, imeeleza kuwa kazi ya uchukuaji wa fomu na urejeshaji kwa ajili ya kuomba nafasi hiyo ya uongozi zinatarajiwa kuaanza Julai 26, 2012 na Julai 30 mwaka huu na utafanyika mkutano Mkuu wa Jimbo ambao utaweza kupendekeza majina matatu.

Kampeni ya matawini kwa Chama hicho inatarajiwa kufanyika Julai 31, mwaka huu na kura ya maoni itafanyika matawini Agosti 5, mwaka huu.

Baada ya kupatikana kwa jina la mgombea kutoka matawini jina lake  litafikishwa katika Kamati ya siasa ya Wilaya ya Magharibi Unguja Agosti 6, 2012 itakutana na Kamati ya siasa ya Mkoa huo inatarajiwa kukaa Agosti 7, mwaka huu.

Agosti 9, mwaka huu ratiba hiyo imefahamisha kuwa kutafanyika kikao cha Sekretarieti ya Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa na Agosti 11, 2012, Kamati Maalum  ya halmashauri Kuu ya Taifa, Agosti 13,2012 ni kikao cha Sekreterieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa itakaa na Agosti 15, mwa mwaka huo kamati Kuu ya CCM itakutana kufanya uteuzi wa mgombea.

Tume ya Uchaguzi Zanzibar imepanga kazi za uchukuaji na urejeshai wa fomu zitaanza Agosti 22, 2012 hadi Agosti 30, mwaka huu na uteuzi wa wagombea utafanyika Agosti 30, mwaka huu huku kampeni zinatarajiwa kuanza Agosti 31, 2012 hadi Septemba 15, 2012 na uchaguzi utafanyika Septemba 16, 2012.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.